Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mikono Yenu na Iwe na Nguvu

Mikono Yenu na Iwe na Nguvu

Mikono Yenu na Iwe na Nguvu

“Mikono yenu na iwe na nguvu, ninyi ambao siku hizi mnayasikia maneno haya kutoka katika kinywa cha manabii.”—ZEKARIA 8:9.

1, 2. Kwa nini tunapaswa kuchunguza vitabu vya Hagai na Zekaria?

INGAWA unabii wa Hagai na Zekaria uliandikwa yapata miaka 2,500 iliyopita, bado una mafunzo muhimu kwetu. Masimulizi ya Biblia yaliyo katika vitabu hivyo viwili si historia tu. Masimulizi hayo ni sehemu ya “mambo yote yaliyoandikwa zamani . . . ili kutufundisha sisi.” (Waroma 15:4) Mambo mengi yaliyo katika vitabu hivyo hutufanya tufikirie hali halisi ambazo zimekuwa zikitukia tangu Ufalme uliposimamishwa mbinguni mwaka wa 1914.

2 Akirejelea matukio na hali zilizowapata watu wa Mungu wa kale, mtume Paulo alisema hivi: “Basi mambo hayo yaliendelea kuwapata kuwa vielelezo, nayo yaliandikwa ili kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.” (1 Wakorintho 10:11) Huenda basi ukauliza, ‘Vitabu vya Hagai na Zekaria vinatufunza mambo gani muhimu?’

3. Hagai na Zekaria walikazia nini?

3 Kama vile makala iliyotangulia ilivyosema, unabii wa Hagai na Zekaria ulihusu wakati ambapo Wayahudi walirudi katika nchi waliyopewa na Mungu baada ya kuachiliwa huru kutoka utekwani huko Babiloni. Manabii hao wawili walikazia kujengwa upya kwa hekalu. Wayahudi waliweka msingi wa hekalu mwaka wa 536 K.W.K. Ingawa Wayahudi fulani wazee walikumbuka hekalu la zamani, kwa ujumla, watu ‘walipaaza sauti kwa shangwe.’ Hata hivyo, jambo muhimu hata zaidi limetukia katika siku zetu. Jambo gani?—Ezra 3:3-13.

4. Ni nini kilichotokea muda mfupi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu?

4 Muda mfupi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, watiwa-mafuta wa Yehova waliachiliwa huru kutoka katika utekwa wa Babiloni Mkubwa. Jambo hilo lilionyesha wazi kwamba Yehova anawategemeza. Mwanzoni ilidhaniwa kwamba viongozi wa kidini na washiriki wao wa kisiasa walikuwa wamekomesha kazi ya kuhubiri na ya kufundisha ya Wanafunzi wa Biblia. (Ezra 4:8, 13, 21-24) Lakini, Yehova Mungu aliondoa mambo yaliyozuia kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Kwa makumi ya miaka tangu 1919, kazi ya Ufalme imeongezeka na hakuna kitu ambacho kimeweza kuikomesha.

5, 6. Andiko la Zekaria 4:7 linatabiri utimizo wa jambo gani muhimu?

5 Tuna uhakika kwamba kazi ya kuhubiri na kufundisha inayofanywa na watumishi wa Yehova watiifu wa wakati wetu itaendelea kwa msaada wake. Tunasoma hivi kwenye Zekaria 4:7: “Ataleta jiwe la juu kabisa. Nalo litapaaziwa sauti: ‘Linavutia kama nini! Linavutia kama nini!’” Unabii huo unahusu jambo gani muhimu ambalo limetimizwa katika siku zetu?

6 Andiko la Zekaria 4:7 linatabiri wakati ambapo ibada ya kweli ya Bwana Mwenye Enzi Kuu ingefanywa kuwa kamilifu katika ua wa kidunia wa hekalu lake la kiroho. Hekalu hilo ni mpango wa Yehova wa kumfikia katika ibada kwa msingi wa dhabihu ya upatanisho ya Kristo Yesu. Ni kweli kwamba hekalu hilo kubwa la kiroho limekuwapo tangu karne ya kwanza W.K. Hata hivyo, bado ibada ya kweli duniani haijafanywa kuwa kamilifu. Sasa mamilioni ya waabudu wanatumikia katika ua wa kidunia wa hekalu hilo la kiroho. Watu hao pamoja na umati wa wale watakaofufuliwa watafanywa kuwa wakamilifu wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo. Mwishoni mwa hiyo miaka elfu, ni waabudu wa kweli wa Mungu tu ndio watakaobaki katika dunia iliyosafishwa.

7. Yesu ana jukumu gani katika kufanya ibada ya kweli iwe kamilifu katika siku zetu, na kwa nini hilo linatutia moyo?

7 Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua waliona ujenzi wa hekalu ukikamilishwa mwaka wa 515 K.W.K. Vivyo hivyo, andiko la Zekaria 6:12, 13 lilitabiri jukumu la Yesu la kufanya ibada ya kweli ifikie hali yake kamilifu: “Yehova wa majeshi amesema hivi: ‘Tazama, mtu ambaye jina lake ni Chipukizi. Naye atachipuka kutoka mahali pake mwenyewe, naye atalijenga hekalu la Yehova. Naye . . . atachukua heshima; ataketi na kutawala juu ya kiti chake cha ufalme, naye atakuwa kuhani juu ya kiti chake cha ufalme.’” Kwa kuwa Yesu, aliye mbinguni na anayesababisha wafalme wa ukoo wa Daudi kuchipuka, anategemeza kazi ya Ufalme kwenye hekalu la kiroho, je, kuna mtu yeyote anayeweza kuizuia kazi hiyo? La hasha! Je, hilo halipaswi kututia moyo tuendelee na utumishi wetu, bila kukengeushwa na mahangaiko ya kila siku?

Mambo ya Kutanguliza

8. Kwa nini ni lazima tutangulize kazi inayofanywa katika hekalu la kiroho?

8 Ili tupate msaada na baraka za Yehova, lazima tuendelee kutanguliza kazi inayofanywa katika hekalu la kiroho. Tofauti na Wayahudi waliosema, “Wakati haujaja,” tunapaswa kukumbuka kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (Hagai 1:2; 2 Timotheo 3:1) Yesu alitabiri kwamba wanafunzi wake washikamanifu wangehubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi. Tunapaswa kuwa waangalifu tusipuuze huduma yetu ya pekee. Kazi ya kuhubiri na kufundisha iliyokuwa imekomeshwa kwa muda mfupi kwa sababu ya upinzani kutoka kwa ulimwengu ilianza tena mwaka wa 1919, lakini bado haijakamilishwa. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba kazi hiyo itakamilishwa!

9, 10. Baraka za Yehova zinategemea nini, na hilo linatuhusuje?

9 Kadiri tunavyofanya kazi hiyo kwa bidii, ndivyo tutakavyobarikiwa, tukiwa kikundi na tukiwa mtu mmoja-mmoja. Ona ahadi ya Yehova inayotupa uhakikisho. Wayahudi waliporudia ibada safi kwa nafsi yote na kuanza tena kujenga msingi wa hekalu kwa bidii, Yehova alisema hivi: “Kuanzia leo hii nitatoa baraka.” (Hagai 2:19) Wayahudi wangepata tena kibali cha Yehova kwa ukamili. Sasa ona baraka zinazotajwa katika ahadi hii ya Mungu: “Kutakuwa na mbegu ya amani; mzabibu utazaa matunda yake, na dunia itatoa mazao yake, na mbingu zitatoa umande wake; nami nitawafanya mabaki ya watu hawa warithi vitu hivyo vyote.”—Zekaria 8:9-13.

10 Kama vile Yehova alivyowabariki Wayahudi hao kiroho na kimwili, ndivyo atakavyotubariki tukifanya kazi aliyotupa kwa bidii na kwa mioyo yenye furaha. Baraka hizo zinatia ndani amani kati yetu wenyewe, usalama, ufanisi, na ukuzi wa kiroho. Lakini Mungu ataendelea kutubariki maadamu tunaendelea kufanya kazi katika hekalu la kiroho jinsi anavyotaka tuifanye.

11. Tunaweza kujichunguzaje?

11 Sasa ndio wakati wa ‘kuweka moyo wetu juu ya njia zetu.’ (Hagai 1:5, 7) Tunapaswa kuchanganua mambo tunayotanguliza maishani. Baraka ambazo Yehova anatupa leo zinategemea jinsi tunavyolitukuza jina lake na kuendelea kufanya kazi yetu katika hekalu lake la kiroho. Unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, nimeacha kutanguliza mambo niliyoyatanguliza zamani? Je, bidii yangu kwa ajili ya Yehova, kweli yake, na kazi yake ni sawa na bidii niliyokuwa nayo nilipobatizwa? Je, tamaa ya kuishi maisha ya starehe inaathiri maoni yangu kuhusu Yehova na Ufalme wake? Je, ninakosa kumtukuza Yehova kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu au kuhangaikia maoni yao?’—Ufunuo 2:2-4.

12. Andiko la Hagai 1:6, 9 linazungumzia hali gani iliyokuwapo miongoni mwa Wayahudi?

12 Hatutaki kukosa baraka za Mungu kwa sababu ya kupuuza kazi ya kulitukuza jina lake. Kumbuka kwamba baada ya kuanza kazi kwa bidii, Wayahudi waliorudishwa walikuwa “mbioni, kila mmoja kwa ajili ya nyumba yake mwenyewe,” kama andiko la Hagai 1:9 linavyosema. Walijishughulisha tu na mahitaji yao na maisha yao. Hivyo, kukawa na ‘mavuno kidogo,’ uhaba wa chakula kizuri na vinywaji, na ukosefu wa nguo za kuwapasha joto. (Hagai 1:6) Yehova aliacha kuwabariki. Je, kuna mambo tunayojifunza kutokana na hali hiyo?

13, 14. Tunaweza kutumiaje jambo tunalojifunza katika Hagai 1:6, 9, na kwa nini hilo ni muhimu?

13 Naam, ili tuendelee kupata baraka za Yehova, ni lazima tuepuke kuhangaikia masilahi yetu wenyewe huku tukipuuza kumtukuza Yehova. Tunahitaji kuepuka kufanya hivyo iwe tunakengeushwa na kutafuta pesa, miradi ya kujitajirisha upesi, miradi ya kufuatia elimu ya juu ili kuwa na kazi nzuri katika mfumo huu, au miradi ya kujitakia makuu.

14 Mambo hayo si dhambi. Hata hivyo, unapofikiria uzima wa milele, je, huoni kwamba hayo ni “matendo yaliyokufa”? (Waebrania 9:14) Kwa njia gani? Yamekufa kiroho, ni ya ubatili, na hayana faida yoyote. Mtu akiendelea kuyafuatilia, matendo hayo yatamfanya afe kiroho. Ndivyo ilivyokuwa kwa Wakristo fulani watiwa-mafuta katika siku za mitume. (Wafilipi 3:17-19) Hali hiyo pia imewapata wengine katika siku zetu. Huenda unajua baadhi ya watu ambao walikengeushwa pole kwa pole kutoka kwenye utendaji wa Kikristo na kutoka kutanikoni na sasa hawaonyeshi kwamba wangependa kurudia utumishi wa Yehova. Ni matumaini yetu kwamba watu hao watamrudia Yehova, lakini ukweli ni kwamba kufuatia “matendo yaliyokufa” kunaweza kumfanya mtu apoteze kibali na baraka za Yehova. Hilo ni jambo lenye kusikitisha sana. Linamfanya mtu apoteze shangwe na amani inayotokana na roho ya Mungu. Isitoshe, hebu wazia kile ambacho mtu hupoteza asiposhirikiana na undugu wa Kikristo wenye upendo!—Wagalatia 1:6; 5:7, 13, 22-24.

15. Andiko la Hagai 2:14 linaonyeshaje uzito wa ibada yetu?

15 Hilo ni jambo zito sana. Ona kwenye Hagai 2:14 jinsi Yehova alivyowaona Wayahudi ambao waliipuuza nyumba yake ya ibada ili wajenge nyumba zao wenyewe, kihalisi au kwa njia ya mfano. “‘Hivyo ndivyo kikundi hiki cha watu kilivyo, na hivyo ndivyo taifa hili lilivyo mbele zangu,’ asema Yehova, ‘na hivyo ndivyo kazi yote ya mikono yao ilivyo, na chochote wanachotoa huko, ni najisi.’” Dhabihu zozote ambazo Wayahudi walitoa kwa moyo nusu-nusu kwenye madhabahu ya muda huko Yerusalemu hazingekubaliwa ikiwa wangeendelea kupuuza ibada ya kweli.—Ezra 3:3.

Uhakikisho wa Kupata Msaada

16. Wayahudi walipata uhakikisho gani kutokana na maono ambayo Zekaria alipokea?

16 Kupitia maono manane ambayo Zekaria aliona, Mungu aliwahakikishia Wayahudi watiifu ambao walifanya kazi ya kujenga upya hekalu kwamba angewategemeza. Maono ya kwanza yalitoa uhakikisho wa kwamba hekalu lingekamilishwa na Yerusalemu na Yuda zingebarikiwa ikiwa Wayahudi wangeendelea kuwa watiifu na kufanya kazi waliyopewa. (Zekaria 1:8-17) Maono ya pili yalionyesha mwisho wa serikali zote zinazoipinga ibada ya kweli. (Zekaria 1:18-21) Maono mengine yaliwahakikishia kwamba Mungu angewalinda wakati wa ujenzi wa hekalu, kwamba watu wa mataifa mengi wangemiminika kwenye nyumba ya Yehova ya ibada iliyokamilishwa, kwamba kungekuwa na amani na usalama wa kweli, kwamba vizuizi vikubwa vya kazi ya ujenzi iliyoagizwa na Mungu vingeondolewa, kwamba uovu ungeondolewa, na kwamba malaika wangesimamia mambo na kuandaa ulinzi. (Zekaria 2:5, 11; 3:10; 4:7; 5:6-11; 6:1-8) Kwa sababu ya uhakikisho huo wa kwamba Mungu angewategemeza, unaweza kutambua sababu iliyofanya watu watiifu warekebishe maisha yao na kutilia maanani kazi ambayo Mungu alitaka waifanye alipowakomboa.

17. Kwa kuwa tumepewa uhakikisho, tunapaswa kujiuliza maswali gani?

17 Vivyo hivyo, kwa kuwa tumehakikishiwa kwamba mwishowe ibada ya kweli itashinda, tunapaswa kuchochewa kutenda na kuifikiria kwa uzito nyumba ya Yehova ya ibada. Jiulize hivi: ‘Ikiwa ninasadiki kwamba huu ndio wakati wa kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi, je, miradi yangu na maisha yangu yanapatana na usadikisho huo? Je, ninatenga wakati wa kutosha ili kujifunza Neno la Mungu la kinabii, kulitanguliza maishani mwangu, na kuzungumza juu yake pamoja na Wakristo wenzangu na vilevile wale ninaowahubiria?’

18. Kulingana na Zekaria sura ya 14, ni mambo gani yatakayotukia wakati ujao?

18 Zekaria alirejelea uharibifu wa Babiloni Mkubwa unaofuatiwa na vita vya Har–Magedoni. Tunasoma hivi: “Itakuwa siku moja inayojulikana kuwa ni ya Yehova. Haitakuwa mchana, wala haitakuwa usiku; na itatukia kwamba wakati wa jioni kutakuwa na nuru.” Naam, siku ya Yehova itakuwa yenye giza kwelikweli, siku isiyopendeza kwa adui zake duniani! Lakini itakuwa siku nzuri na yenye nuru kwa waabudu waaminifu wa Yehova. Zekaria pia alieleza jinsi kila kitu katika ulimwengu mpya kitakavyoutangaza utakatifu wa Yehova. Ibada ya kweli kwenye hekalu kubwa la kiroho la Mungu ndiyo itakayokuwa ibada pekee duniani. (Zekaria 14:7, 16-19) Huo ni uhakikisho ulioje! Tutaona utimizo wa mambo yaliyotabiriwa, nasi tutaona pia enzi kuu ya Yehova ikitetewa. Kwelikweli, hiyo itakuwa siku ya Yehova isiyo na kifani!

Baraka za Kudumu

19, 20. Ni nini kinachokutia moyo katika andiko la Zekaria 14:8, 9?

19 Baada ya utimizo huo mkuu, Shetani na roho wake waovu watawekwa katika hali ya kutotenda, ambayo inafananishwa na abiso. (Ufunuo 20:1-3, 7) Kisha, baraka zitamiminika wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu. Andiko la Zekaria 14:8, 9 linasema hivi: “Itatukia siku hiyo kwamba maji yaliyo hai yatatoka katika Yerusalemu, nusu yake kuelekea upande wa bahari ya mashariki na nusu yake kuelekea upande wa bahari ya magharibi. Itakuwa hivi wakati wa kiangazi na wa majira ya baridi kali. Na Yehova atakuwa mfalme juu ya dunia yote. Katika siku hiyo Yehova atakuwa mmoja, na jina lake litakuwa moja.”

20 “Maji yaliyo hai,” au “mto wa maji ya uzima,” yanayowakilisha maandalizi ya Yehova ya uzima, yataendelea kutiririka kutoka kwenye kiti cha Ufalme wa Kimasihi. (Ufunuo 22:1, 2) Umati mkubwa wa waabudu wa Yehova ambao wataokoka Har–Magedoni, watafaidika kwa kuwekwa huru kutokana na laana ya kifo kilichotokana na Adamu. Hata wafu watafaidika kupitia ufufuo. Huo utakuwa mwanzo wa kipindi kipya cha utawala wa Yehova juu ya dunia. Wanadamu wote duniani watamtambua Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote na kwamba ni yeye pekee anayepaswa kuabudiwa.

21. Tunapaswa kuwa na usadikisho gani?

21 Kutokana na mambo yote ambayo Hagai na Zekaria walitabiri na yote ambayo yametimizwa, tuna sababu nzuri za kuendelea kufanya kazi ambayo Mungu ametupa katika ua wa kidunia wa hekalu lake la kiroho. Hadi wakati ambapo ibada ya kweli itafanywa kuwa kamilifu, acheni sote tujitahidi sana kutanguliza mambo ya Ufalme. Andiko la Zekaria 8:9 linatuhimiza hivi: “Mikono yenu na iwe na nguvu, ninyi ambao siku hizi mnayasikia maneno haya kutoka katika kinywa cha manabii.”

Je, Unakumbuka?

• Ni mambo gani yaliyotukia wakati wa Hagai na Zekaria ambayo yanafanya vitabu hivyo vihusu nyakati zetu?

• Vitabu vya Hagai na Zekaria vinatufunza nini kuhusu mambo ya kutanguliza?

• Kwa nini kuchunguza vitabu vya Hagai na Zekaria kunatupa uhakika kuhusu wakati ujao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Hagai na Zekaria waliwahimiza Wayahudi wafanye kazi kwa nafsi yote na kupata baraka

[Picha katika ukurasa wa 27]

Je, umo ‘mbioni kwa ajili ya nyumba yako mwenyewe’?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Yehova aliahidi baraka, naye amezileta