Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fuata Kielelezo Cha Yesu Kwa Kuwahangaikia Maskini

Fuata Kielelezo Cha Yesu Kwa Kuwahangaikia Maskini

Fuata Kielelezo Cha Yesu Kwa Kuwahangaikia Maskini

UMASKINI na uonevu umekuwapo karibu katika historia yote ya mwanadamu. Ingawa Sheria ya Mungu kwa Waisraeli iliwalinda maskini na kupunguza matatizo yao, Sheria hiyo ilipuuzwa mara nyingi. (Amosi 2:6) Nabii Ezekieli alishutumu njia ambayo maskini walitendewa. Alisema hivi: “Watu wa nchi wenyewe wameendesha mbinu ya kupunja nao wamenyakua katika unyang’anyi, nao wamemtendea vibaya anayeteseka na aliye maskini, na kumpunja bila haki mkaaji mgeni.”—Ezekieli 22:29.

Hivyo ndivyo hali ilivyokuwa hata Yesu alipokuwa duniani. Viongozi wa kidini hawakuwahangaikia hata kidogo maskini na wenye uhitaji. Viongozi wa kidini waliitwa “wapenda-pesa” ambao “humeza nyumba za wajane” na ambao walihangaikia sana desturi zao badala ya kuwajali wazee na wenye uhitaji. (Luka 16:14; 20:47; Mathayo 15:5, 6) Katika mfano wa Yesu wa Msamaria mwema, baada ya kuhani na Mlawi kumwona mtu aliyekuwa amejeruhiwa, walimpita na kwenda upande ule mwingine wa barabara badala ya kumsaidia.—Luka 10:30-37.

Yesu Aliwahangaikia Maskini

Masimulizi ya Injili kuhusu maisha ya Yesu yanaonyesha kwamba alielewa kabisa matatizo ya maskini na kujali mahitaji yao. Ingawa Yesu alikuwa ameishi mbinguni, alijiondolea mwenyewe hali yake, akawa mwanadamu, na ‘maskini kwa ajili yetu.’ (2 Wakorintho 8:9) Alipouona umati Yesu ‘aliwasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36) Lile simulizi kuhusu mjane mwenye uhitaji linaonyesha kwamba Yesu alipendezwa na mchango wenye thamani ndogo wa yule mjane maskini wala si zawadi kubwa za matajiri ambao walitoa “kutokana na ziada yao.” Kile ambacho mjane huyo alifanya kiligusa moyo wa Yesu kwa sababu “kutokana na uhitaji wake alitumbukiza ndani riziki yote aliyokuwa nayo.”—Luka 21:4.

Mbali na kuwahurumia maskini, Yesu alihangaikia mahitaji yao pia. Yeye pamoja na mitume wake walikuwa na hazina ya pekee ili kuwasaidia Waisraeli wenye uhitaji. (Mathayo 26:6-9; Yohana 12:5-8; 13:29) Yesu aliwahimiza wale waliotaka kuwa wafuasi wake kutambua daraka lao la kuwasaidia wenye uhitaji. Alimwambia hivi mtawala fulani kijana aliyekuwa tajiri: “Uza vitu vyote ulivyo navyo uwagawie maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.” Kwa kuwa mtu huyo hakutaka kuacha mali zake hilo linaonyesha kwamba alipenda mali kuliko Mungu na kuliko mwanadamu mwenzake. Hivyo, hakuwa na sifa zinazohitajiwa ili kuwa mfuasi wa Yesu.—Luka 18:22, 23.

Wafuasi wa Kristo Huwahangaikia Maskini

Baada ya Yesu kufa, mitume na wafuasi wengine wa Kristo waliendelea kuwahangaikia wale waliokuwa maskini kati yao. Katika mwaka wa 49 W.K. hivi, mtume Paulo alikutana na Yakobo, Petro, na Yohana na akazungumza nao kuhusu kazi ya kuhubiri habari njema ambayo alikuwa amepewa na Bwana Yesu Kristo. Walikubaliana kwamba Paulo na Barnaba waende kwa “mataifa” ili kuwahubiria hasa watu wasio Wayahudi. Hata hivyo, Yakobo na wenzake waliwahimiza Paulo na Barnaba ‘wawakumbuke walio maskini.’ Paulo ‘alijitahidi sana kufanya’ jambo hilo.—Wagalatia 2:7-10.

Wakati wa utawala wa Maliki Klaudio, kulikuwa na njaa kali sana katika sehemu mbalimbali za Milki ya Roma. Hivyo, Wakristo huko Antiokia “wakaamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa, wafanye huduma ya kupeleka misaada kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea; nao wakafanya hivyo, wakaipeleka kwa wanaume wazee kwa mkono wa Barnaba na Sauli.”—Matendo 11:28-30.

Wakristo wa kweli leo wanaelewa pia kwamba wafuasi wa Yesu wanapaswa kuwahangaikia maskini na wenye uhitaji, hasa waamini wenzao. (Wagalatia 6:10) Hivyo, wanawahangaikia kikweli wale wanaohitaji msaada wa kimwili. Kwa mfano, mnamo 1998, kulikuwa na ukame ulioharibu sehemu kubwa ya kaskazini-mashariki mwa Brazili. Ukame huo uliharibu mashamba ya mpunga, maharagwe, na mahindi, na hivyo kusababisha njaa kali. Hakujawahi kamwe kuwa na njaa kali hivyo kwa muda wa miaka 15. Katika sehemu nyingine, hata maji ya kunywa yalipungua. Bila kukawia, Mashahidi wa Yehova katika maeneo mengine ya nchi hiyo walipanga halmashauri za kutoa misaada, na baada ya muda mfupi, walikuwa wamekusanya chakula kingi na kulipia gharama ya kukisafirisha.

Mashahidi waliotoa misaada hiyo waliandika hivi: “Tunafurahi sana kwamba tumeweza kuwasaidia ndugu zetu, hasa kwa sababu tuna hakika kwamba tumefanya moyo wa Yehova ushangilie. Hatusahau kamwe maneno ya Yakobo 2:15, 16.” Mistari hiyo ya Biblia inasema: “Ikiwa ndugu au dada yuko uchi naye hana chakula cha kutosha kwa ajili ya siku, na mmoja wenu amwambie: ‘Nenda kwa amani, jipashe moto na kula vizuri,’ lakini ninyi mkose kumpa mahitaji ya mwili wake, ina faida gani?”

Katika kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova katika jiji la São Paulo, Shahidi mmoja mnyenyekevu na mwenye bidii ambaye ni maskini kimwili, mara nyingi hujikakamua kupata riziki. Anasema: “Ingawa mimi ni maskini, ujumbe wa Biblia umenipa kusudi maishani. Sijui ningekuwa wapi kama singepata msaada wa Mashahidi wenzangu.” Wakati fulani uliopita, mwanamke huyo Mkristo mwenye bidii alihitaji kufanyiwa upasuaji lakini akashindwa kulipia gharama za hospitali. Baadaye, ndugu na dada Wakristo kutanikoni walilipia gharama za upasuaji huo. Wakristo wa kweli huwasaidia waamini wenzao ulimwenguni pote.

Hata masimulizi hayo yawe yenye kutia moyo jinsi gani, ni wazi kwamba jitihada hizo za unyoofu haziwezi kumaliza umaskini. Hata serikali zenye uwezo na mashirika makubwa ya kimataifa ya kutoa misaada, hayajaweza kumaliza tatizo hilo la muda mrefu, ingawa yamefanikiwa kwa kiasi fulani. Kwa hiyo, swali ni, Ni nini suluhisho la kudumu la umaskini na matatizo mengine yanayowakumba wanadamu?

Mafundisho ya Biblia Huandaa Msaada wa Kudumu

Masimulizi ya Injili yanaonyesha kwamba kwa kawaida Yesu Kristo aliwatendea mema wale waliokuwa maskini au waliokuwa na mahitaji mengine. (Mathayo 14:14-21) Hata hivyo, Yesu alitanguliza kazi gani? Pindi moja, baada ya kuwasaidia wenye uhitaji, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Twendeni mahali pengine, katika miji ya vijiji iliyo karibu, ili nipate kuhubiri huko pia.” Kwa nini Yesu aliacha kazi ya kuwasaidia wagonjwa na wenye uhitaji ili arudie kazi yake ya kuhubiri? Alisema: “Kwa maana nilitoka kwa kusudi hilo [yaani, kuhubiri].” (Marko 1:38, 39; Luka 4:43) Ingawa Yesu aliona ni muhimu kuwafanyia mema watu waliokuwa na uhitaji, kazi iliyokuwa muhimu zaidi kwake ni kuhubiri Ufalme wa Mungu.—Marko 1:14.

Kwa kuwa Biblia inawahimiza Wakristo ‘wafuate hatua za Yesu kwa ukaribu,’ leo wao wana mwongozo ulio wazi kuhusu mambo wanayopaswa kutanguliza wanapojitahidi kuwasaidia wengine. (1 Petro 2:21) Kama Yesu, wao huwasaidia watu walio na uhitaji. Hata hivyo, kama Yesu, wao pia huona kazi ya kufundisha ujumbe wa Biblia kuhusu Ufalme wa Mungu kuwa muhimu zaidi. (Mathayo 5:14-16; 24:14; 28:19, 20) Lakini, kwa nini tunapaswa kuona kazi ya kuhubiri ujumbe unaopatikana katika Neno la Mungu kuwa muhimu zaidi kuliko njia nyingine za kuwasaidia watu?

Visa mbalimbali ulimwenguni pote vinaonyesha kwamba watu wanapoelewa na kufuata mashauri ya Biblia, wanaweza kushughulikia matatizo ya maisha kutia ndani umaskini. Isitoshe, ujumbe wa Biblia kuhusu Ufalme wa Mungu unaohubiriwa na Mashahidi wa Yehova leo, huwapa watu tumaini la wakati ujao, yaani, tumaini linalofanya maisha yawe na kusudi hata chini ya hali ngumu zaidi. (1 Timotheo 4:8) Hilo ni tumaini gani?

Neno la Mungu linatuhakikishia hivi kuhusu wakati wetu ujao: “Kulingana na ahadi yake [Mungu] tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Wakati mwingine Biblia inapotaja “dunia,” inarejelea watu wanaoishi duniani. (Mwanzo 11:1) Hivyo, “dunia mpya” yenye uadilifu ambayo inaahidiwa ni jamii ya wanadamu ambao wana kibali cha Mungu. Pia, Neno la Mungu linaahidi kwamba chini ya utawala wa Kristo, wale walio na kibali cha Mungu watapata zawadi ya uzima wa milele na wataishi maisha yenye kuridhisha katika dunia paradiso. (Marko 10:30) Kila mtu anaweza kuishi wakati huo mzuri, kutia ndani walio maskini. Katika ‘dunia hiyo mpya’ tatizo la umaskini litasuluhishwa milele.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

YESU ‘ATAMKOMBOAJE MASKINI’?—Zaburi 72:12

HAKI: “Na ahukumu wenye kuteseka katikati ya watu, na awaokoe wana wa maskini, na amponde mpunjaji.” (Zaburi 72:4) Kristo atakapotawala dunia, kutakuwa na haki kwa wote. Ufisadi, ambao ndio uovu unaosababisha umaskini katika nchi nyingi zilizo na uwezo wa kutajirika, hautakuwapo.

AMANI: “Katika siku zake aliye mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena.” (Zaburi 72:7) Umaskini uliopo duniani mara nyingi husababishwa na mapambano na vita vya wanadamu. Kristo ataleta amani kamilifu duniani, na hivyo kumaliza vita na mapambano ambayo ndiyo hasa yanayosababisha umaskini.

HURUMA: “Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri, nayo damu yao itakuwa na thamani machoni pake.” (Zaburi 72:12-14) Watu wa hali ya chini, maskini, na wanaokandamizwa watakuwa familia moja ya kibinadamu yenye furaha, iliyoungana chini ya utawala wa Mfalme Yesu Kristo.

UFANISI: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani.” (Zaburi 72:16) Wakati wa utawala wa Kristo, kutakuwa na wingi wa vitu vya kimwili. Watu hawatateseka kutokana na upungufu wa chakula na njaa ambazo mara nyingi husababisha umaskini leo.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yesu alihangaikia mahitaji ya maskini

[Picha katika ukurasa wa 6]

Ujumbe wa Biblia hutupa tumaini halisi