Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujua Kwa Nini Mungu Huruhusu Kuteseka Kulibadili Maisha Yangu

Kujua Kwa Nini Mungu Huruhusu Kuteseka Kulibadili Maisha Yangu

Simulizi la Maisha

Kujua Kwa Nini Mungu Huruhusu Kuteseka Kulibadili Maisha Yangu

SIMULIZI LA HARRY PELOYAN

Kwa nini Mungu huruhusu kuteseka? Nilisumbuliwa na swali hilo tangu nilipokuwa mvulana mdogo. Wazazi wangu walifanya kazi kwa bidii, walikuwa wanyoofu, na walipendezwa na familia yao. Lakini baba yangu hakupendezwa na mambo ya dini, na mama yangu alipendezwa kidogo tu. Hivyo, hawangeweza kunipa jibu la swali hilo.

NILIFIKIRIA swali hilo hata zaidi wakati na baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, nilipofanya kazi katika Jeshi la Marekani la Wanamaji kwa zaidi ya miaka mitatu. Baada ya vita, nilipewa kazi katika meli iliyopeleka misaada China. Nilikuwa huko kwa karibu mwaka mmoja na nilijionea watu wakiteseka sana.

Wachina ni watu wenye akili na bidii. Lakini wengi walikuwa na matatizo kwa sababu ya umaskini na jeuri iliyosababishwa na Vita vya Pili vya Ulimwengu. Tulipokuwa ufuoni, nilisikitika hasa kuona watoto wenye sura nzuri ambao hawakuwa na chakula cha kutosha na waliovalia matambara huku wakiomba-omba.

Kwa Nini Watu Wanateseka?

Nilizaliwa mnamo 1925 na kulelewa huko California, Marekani. Sikuwa nimewahi kuona mambo kama hayo. Hivyo, mara nyingi nilijiuliza, ‘Ikiwa kuna Muumba mweza-yote, kwa nini anaruhusu mambo hayo yawapate wanadamu wengi, hasa watoto wasio na hatia?’

Pia, nilijiuliza, ikiwa kuna Mungu, kwa nini anaruhusu uharibifu kama huo, mauaji makubwa, kifo, na kuteseka ambako kumewakumba wanadamu katika historia yote, hasa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, wakati zaidi ya watu milioni 50 walipokufa? Isitoshe, wakati wa vita hivyo, kwa nini makasisi waliwachochea watu wa dini moja wauane eti kwa sababu tu wao ni wa mataifa tofauti?

Darubini

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza mwaka wa 1939 na watu wengi kuuawa duniani, nilihisi kwamba haiwezekani kuwa kuna Mungu. Kisha, katika somo la sayansi katika shule ya sekondari, sote darasani tuliombwa tutengeneze chombo fulani cha kisayansi. Kwa kuwa nilipendezwa na elimu ya nyota, niliamua kutengeneza darubini kubwa yenye kioo chenye kipenyo cha [sentimeta 20].

Ili kutengeneza darubini hiyo, nilinunua kipande cha kioo chenye unene wa zaidi ya [sentimeta 2.5] na upana wa [sentimeta 20] kisha nikakipeleka kikatwe ili kiwe na umbo la mviringo. Halafu nikaanza kukisugua kwa mkono ili kibonyee. Nilifanya kazi hiyo muhula mzima nilipopata nafasi. Kioo hicho kilipokamilika nilikitia ndani ya chuma kirefu chenye tundu. Kisha nikatia lenzi zenye nguvu mbalimbali.

Baada ya kumaliza kutengeneza darubini, niliipeleka nje kwa mara ya kwanza wakati wa usiku usio na mbalamwezi na nikaielekeza kwenye nyota na sayari za mfumo wetu wa jua. Nilishangaa kuona nyota nyingi na sayari, na jinsi zilivyopangwa vizuri. Nilishangaa hata zaidi nilipojua kwamba zile nilizodhani kuwa nyota ni vikundi vya nyota kama vile Kilimia, na kila kikundi kina mabilioni ya nyota.

Kisha nikafikiria, ‘Kwa kweli mambo hayo yote hayawezi kuwa yalijitokeza yenyewe. Vitu haviwezi kujipanga vyenyewe kwa utaratibu. Sayari na nyota zimepangwa kwa utaratibu sana hivi kwamba zinaonekana kuwa zilifanyizwa na mtu mwenye akili nyingi. Je, kweli Mungu yuko?’ Kutumia darubini hiyo kulinisaidia niache kuamini kwamba hakuna Mungu.

Kisha nikajiuliza: ‘Ikiwa kwa kweli kuna Mungu mwenye nguvu na mwenye hekima ya kuumba sayari na nyota hizi zenye kustaajabisha, je, hawezi kurekebisha hali iliyopo duniani? Kwanza kabisa, kwa nini ameruhusu ubaya?’ Nilipowauliza watu wa dini maswali hayo, hawakunijibu kwa njia yenye kuridhisha.

Baada ya kumaliza shule ya sekondari na kwenda chuoni kwa miaka kadhaa, nilijiunga na Jeshi la Marekani la Wanamaji. Lakini, hata makasisi wa kijeshi hawakuweza kujibu maswali yangu. Mara nyingi wale waliokuwa na ujuzi wa kidini walisema, “Bwana hufanya mambo kwa njia ambazo haziwezi kueleweka.”

Naendelea Kutafuta Majibu

Hata baada ya kutoka China, nilitaka kujua kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka. Maswali hayo yaliendelea kunisumbua, hasa baada ya kuona makaburi ya kijeshi katika visiwa mbalimbali tulipokuwa tukirudi nyumbani kupitia Pasifiki. Karibu makaburi yote hayo yalikuwa ya vijana waliouawa.

Nilipofika Marekani, niliacha kazi ya Jeshi la Wanamaji. Nilikuwa nimebaki na mwaka mmoja wa masomo katika Chuo Kikuu cha Harvard huko Cambridge, Massachusetts. Nilihitimu baada ya mwaka mmoja na kupata shahada, hata hivyo, sikurudi nyumbani, California. Niliamua kukaa katika Pwani ya Mashariki ya Marekani kwa muda ili kujaribu kupata majibu kwa maswali yangu. Nilikusudia kwenda New York City, ambako kuna dini nyingi nilizotaka kuhudhuria ili kujua mafundisho yao.

Huko New York, shangazi yangu Isabel Kapigian, alinikaribisha niishi kwake. Yeye na binti zake wawili, Rose na Ruth, walikuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa sikufikiri kwamba ningependezwa na imani yao, nilianza kuhudhuria dini nyingine, nikizungumza na watu wa dini hizo na kusoma vitabu vyao. Niliwauliza kwa nini Mungu ameruhusu uovu, lakini hata wao hawakujua jibu. Nilikata kauli kwamba huenda hakuna Mungu.

Kupata Majibu

Baadaye, nilimuuliza shangazi yangu na binti zake ikiwa ningeweza kusoma baadhi ya vitabu vyao ili kujua maoni ya Mashahidi wa Yehova. Niliposoma vitabu vyao, nilitambua mara moja kwamba Mashahidi walikuwa tofauti sana na dini nyinginezo. Majibu yao yalitegemea Biblia na yaliridhisha sana. Kwa muda mfupi, maswali yangu kuhusu kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka yalijibiwa.

Si hayo tu, bali pia niliona kwamba majibu ya Mashahidi wa Yehova yanategemea Biblia nao wanaishi kulingana na imani yao. Kwa mfano, nilimuuliza shangazi yangu kile ambacho vijana Mashahidi wa Yehova walifanya nchini Ujerumani wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Je, walijiunga na jeshi la Ujerumani? Je, walisema “Heil Hitler!,” na kupigia bendera ya swastika saluti? Alijibu la, hawakufanya hivyo. Na kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote, walipelekwa katika kambi za mateso ambako wengi wao waliuawa. Alinieleza kwamba msimamo wa Mashahidi wa Yehova ni uleule kila mahali wakati wa vita, yaani, msimamo wa kutounga mkono upande wowote. Hata katika nchi za kidemokrasia, vijana Mashahidi wa Yehova walifungwa gerezani kwa sababu ya msimamo huo.

Kisha, shangazi yangu akaniomba nisome andiko la Yohana 13:35, linalosema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” Lazima Wakristo wa kweli wawe na upendo ambao ndio huwatambulisha duniani pote. Kamwe hawajiungi na upande wowote wa vita wala hawauani eti kwa sababu wao ni wa mataifa tofauti! Shangazi aliniuliza: “Je, unaweza kuwazia Yesu na wanafunzi wake wakiunga mkono upande fulani wa vita huko Roma, wakiuana wao kwa wao?”

Pia, aliniomba nisome 1 Yohana 3:10-12. Andiko hilo linasema: “Watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi ni wazi kwa jambo hili: Kila mtu ambaye haendelei kufanya uadilifu hatokani na Mungu, wala yeye ambaye hampendi ndugu yake. . . . Tunapaswa kupendana; si kama Kaini, aliyetokana na yule mwovu akamuua ndugu yake.”

Biblia iko wazi kabisa. Wakristo wa kweli wanapendana, haidhuru wanaishi katika taifa gani. Hivyo, hawangeweza kuwaua ndugu zao wa kiroho au mtu mwingine yeyote. Ndiyo sababu Yesu angeweza kusema hivi kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:16.

Sababu ya Mungu Kuruhusu Kuteseka

Baada ya muda mfupi nilijifunza kwamba Biblia hutuambia kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka. Inaeleza kwamba Mungu alipowaumba wazazi wetu wa kwanza, walikuwa wakamilifu na aliwaweka katika bustani iliyokuwa paradiso. (Mwanzo 1:26; 2:15) Pia, aliwapa zawadi yenye kutamanika, yaani, uhuru wa kufanya maamuzi. Lakini walipaswa kutumia uhuru huo vizuri. Kama wangemtii Mungu na kutii sheria zake, wangeendelea kuishi kwa ukamilifu katika paradiso. Wangepanua mipaka ya paradiso mpaka ienee dunia yote. Watoto wao pia wangekuwa wakamilifu hivi kwamba baada ya muda, dunia ingekuwa paradiso yenye utukufu inayokaliwa na wanadamu wakamilifu na wenye furaha.—Mwanzo 1:28.

Hata hivyo, kwa kuwa Adamu na Hawa walichagua kujitegemea badala ya kumtegemea Mungu, Mungu hangewaruhusu waendelee kuwa wakamilifu. (Mwanzo 2:16, 17) Inasikitisha kwamba wazazi wetu wa kwanza walitumia uhuru wao vibaya na wakachagua kutomtegemea Mungu. Walichochewa na kiumbe wa roho mwasi aliyekuja kuitwa Shetani Ibilisi. Alitamani kujitegemea badala ya kumtegemea Mungu na akatamani ibada ambayo kihalali ni ya Mungu.—Mwanzo 3:1-19; Ufunuo 4:11.

Hivyo, Shetani akawa “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4) Biblia inasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30) Kwa kuwa Shetani na wazazi wetu wa kwanza hawakutii, hilo lilisababisha kutokamilika, jeuri, kifo, huzuni, na kuteseka kwa wanadamu wote.—Waroma 5:12.

“Mwanadamu Hana Uwezo wa Kuongoza Hatua Yake”

Ili kuonyesha jinsi familia ya kibinadamu ingeathiriwa kwa sababu ya kupuuza sheria za Muumba, kwa miaka mingi, Mungu ameruhusu wanadamu wapatwe na matokeo ya kutotii. Kipindi hicho cha wakati kimewapa wanadamu wote nafasi ya kuthibitisha ukweli huu wa Biblia: “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake. . . . Ee Yehova, nirekebishe mimi.”—Yeremia 10:23, 24.

Sasa, baada ya karne nyingi, tunaweza kuona kwamba kujitawala badala ya kutawaliwa na Mungu hakujaleta mafanikio. Hivyo, Mungu hataruhusu wanadamu waendelee kujitegemea badala ya kumtegemea yeye na sheria zake.

Wakati Ujao Ulio Bora

Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba hivi karibuni, Mungu atakomesha mfumo huu wa mambo ulio mkatili: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena . . . Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.

Unabii wa Danieli 2:44 unasema: “Katika siku za wafalme hao [aina yote ya utawala uliopo], Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” Utawala wa kibinadamu hautaruhusiwa tena kamwe. Ufalme wa Mungu utatawala dunia yote. Chini ya usimamizi wa Ufalme huo, dunia yote itafanywa kuwa paradiso na wanadamu watakuwa wakamilifu ili waishi milele kwa furaha. Biblia inaahidi: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Mungu ameahidi wakati ujao mzuri ajabu!

Maisha Tofauti

Kupata majibu yenye kuridhisha kulibadili maisha yangu. Kuanzia wakati huo na kuendelea, nilitaka kumtumikia Mungu na kuwasaidia wengine kupata majibu hayo. Nilielewa uzito wa maneno haya ya 1 Yohana 2:17: “Ulimwengu [mfumo huu wa mambo unaotawaliwa na Shetani] unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” Nilitaka sana kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Niliamua kuishi New York na nikaanza kushirikiana na kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova. Nilifurahia kuwasaidia wengine kujua mambo niliyokuwa nimejifunza.

Mwaka wa 1949, nilikutana na Rose Marie Lewis. Yeye pamoja na mama yake, Sadie, na dada zake sita walikuwa Mashahidi wa Yehova. Rose alimtumikia Mungu akiwa mhubiri wa wakati wote. Alikuwa na sifa nyingi nzuri, nami nilivutiwa naye mara moja. Tulifunga ndoa mnamo Juni 1950 na tukaishi New York. Tulifurahia mambo tuliyofanya na kushangilia katika tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu.

Mwaka wa 1957, mimi na Rose Marie tulipata mgawo wa utumishi wa wakati wote katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, huko Brooklyn, New York. Kufikia Juni 2004, tulikuwa tumeoana kwa miaka 54 na kutumia miaka 47 kati ya hiyo katika makao makuu huko Brooklyn. Ilikuwa miaka yenye shangwe ya kumtumikia Yehova na kufanya kazi pamoja na maelfu ya waamini wenzetu.

Pigo Kubwa Zaidi

Kwa kusikitisha, mnamo Desemba 2004, Rose Marie alipimwa na ikapatikana kwamba ana uvimbe wa kansa katika pafu lake. Madaktari walisema kwamba uvimbe huo ulikua haraka na ulipaswa kuondolewa. Upasuaji ulifanywa mwishoni mwa mwezi wa Desemba, na juma moja baadaye, nikiwa katika chumba cha Rose hospitalini, daktari-mpasuaji alikuja na kusema: “Rose Marie, nenda nyumbani! Umepona!”

Hata hivyo, muda mfupi baada ya kurudi nyumbani, Rose Marie alianza kuwa na maumivu makali ya tumbo na sehemu nyinginezo. Maumivu hayo yalizidi, hivyo akarudi hospitali kwa uchunguzi zaidi. Ilipatikana kwamba viungo vyake vingi muhimu vilitoa damu iliyoganda na hivyo havikuweza kupata oksijeni. Madaktari walifanya kila walichoweza ili kuzuia hali hiyo lakini hawakufanikiwa. Majuma machache baadaye, mnamo Januari 30, 2005, nilipata pigo kubwa zaidi maishani mwangu. Mpendwa wangu Rose Marie alikufa.

Wakati huo, nilikuwa na umri wa miaka 80 hivi, na nilikuwa nimeona watu wakiteseka maishani mwangu, lakini pigo hilo lilikuwa tofauti. Mimi na Rose Marie tulikuwa “mwili mmoja” kama Biblia inavyosema. (Mwanzo 2:24) Nilikuwa nimeona watu wengine wakiteseka na niliwahi kuhuzunika wakati marafiki na watu wa ukoo walipokufa. Lakini pigo nililopata mke wangu alipokufa, limekuwa kubwa sana na la kudumu. Sasa ninaelewa vizuri zaidi huzuni ambayo familia ya kibinadamu imekuwa nayo kwa muda mrefu kwa sababu ya kifo cha wapendwa.

Hata hivyo, kuelewa chanzo cha kuteseka na jinsi kutakavyokoma kumenisaidia kuvumilia. Andiko la Zaburi 34:18 linasema: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” Jambo hasa linalotusaidia kuvumilia ni kujua kwamba Biblia hufundisha kutakuwa na ufufuo na kwamba wale walio makaburini watarudi na kupata nafasi ya kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Andiko la Matendo 24:15 linasema: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Rose Marie alimpenda Mungu sana. Nina hakika kwamba Mungu alimpenda pia na kwamba atamkumbuka na kumfufua kwa wakati wake unaofaa, nami natumaini itakuwa hivi karibuni.—Luka 20:38; Yohana 11:25.

Ingawa huzuni inayosababishwa na kufa kwa mpendwa ni kubwa, shangwe ya kumpokea tena mpendwa wakati wa ufufuo itakuwa kubwa hata zaidi. (Marko 5:42) Neno la Mungu linaahidi hivi: “Wafu wako wataishi. . . . Dunia itawaacha hata wale wasiojiweza katika kifo waanguke katika kuzaliwa.” (Isaya 26:19) Wengi kati ya “waadilifu” wanaotajwa kwenye Matendo 24:15 huenda wakafufuliwa kwanza. Huo utakuwa wakati mzuri kama nini! Rose Marie atakuwa kati ya wale watakaofufuliwa. Bila shaka, atakaribishwa kwa uchangamfu na wapendwa wake! Itapendeza sana kuishi wakati ambapo kuteseka hakutakuwapo!

[Picha katika ukurasa wa 9]

Niliona watu wakiteseka nilipokuwa China

[Picha katika ukurasa wa 10]

Tangu mwaka wa 1957, nimetumikia katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nilimwoa Rose Marie mwaka wa 1950

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tulipokumbuka mwaka wa 50 wa ndoa yetu mwaka wa 2000