Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtumikia Kristo Mfalme Kwa Ushikamanifu

Kumtumikia Kristo Mfalme Kwa Ushikamanifu

Kumtumikia Kristo Mfalme Kwa Ushikamanifu

“Akapewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.” —DANIELI 7:14.

1, 2. Tunajuaje kwamba Kristo hakupata mamlaka kamili ya Ufalme mwaka wa 33 W.K.?

NI MFALME gani anayeweza kufa kwa ajili ya raia wake kisha aishi tena na kutawala akiwa mfalme? Ni mfalme gani anayeweza kuishi duniani akiwachochea raia wake wamwamini na kuwa washikamanifu kwake, kisha atawale kutoka mbinguni? Yesu Kristo peke yake ndiye anayeweza kufanya hivyo, na kufanya mengi zaidi. (Luka 1:32, 33) Wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., baada ya Kristo kufa, kufufuliwa, na kupaa mbinguni, Mungu ‘alimfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko.’ (Waefeso 1:20-22; Matendo 2:32-36) Hivyo, Kristo alianza kutawala kwa kiwango kidogo. Raia wake wa kwanza walikuwa Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho, ambao wanafanyiza Israeli wa kiroho, yaani, “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:16; Wakolosai 1:13.

2 Miaka 30 hivi baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mtume Paulo alisema kwamba Kristo hakuwa amepata mamlaka kamili ya Ufalme, lakini alikuwa “kwenye mkono wa kuume wa Mungu, tangu wakati huo na kuendelea akingojea mpaka adui zake wawekwe kuwa kiti cha miguu yake.” (Waebrania 10:12, 13) Kisha, karibu na mwisho wa karne ya kwanza W.K., mtume Yohana ambaye alikuwa mzee sana aliona kimbele katika maono Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, Yehova, akimweka Kristo Yesu kuwa Mfalme wa Ufalme wa mbinguni uliokuwa umeanzishwa. (Ufunuo 11:15; 12:1-5) Kufikia mahali ambapo tumefika katika historia, tunaweza kuchunguza uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba Kristo alianza kutawala mbinguni akiwa Mfalme wa Kimasihi mwaka wa 1914. *

3. (a) Habari njema ya Ufalme wa Mungu imekuwa na jambo gani jipya tangu mwaka wa 1914? (b) Tunaweza kujiuliza maswali gani?

3 Naam, tangu mwaka wa 1914 habari njema ya Ufalme imekuwa na jambo jipya lenye kusisimua. Kristo amekuwa akitawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu wa mbinguni, ingawa anafanya hivyo “katikati ya adui [zake].” (Zaburi 110:1, 2; Mathayo 24:14; Ufunuo 12:7-12) Isitoshe, duniani pote, raia wake washikamanifu wananyenyekea kwa hiari mamlaka yake kwa kushiriki katika kazi ya elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote ambayo haina kifani. (Danieli 7:13, 14; Mathayo 28:18) Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho, wale “wana wa ufalme,” wanatumikia wakiwa “mabalozi walio badala ya Kristo.” Wanaungwa mkono kwa ushikamanifu na umati unaozidi kuongezeka wa “kondoo wengine” wa Kristo, ambao ni wajumbe wa Ufalme wa Mungu. (Mathayo 13:38; 2 Wakorintho 5:20; Yohana 10:16) Hata hivyo, tunahitaji kuchunguza ikiwa sisi binafsi tunatambua mamlaka ya Kristo. Je, sisi ni washikamanifu kabisa kwake? Tunaweza kuonyeshaje ushikamanifu kwa Mfalme anayetawala mbinguni? Acheni kwanza tuchunguze sababu zinazotufanya tuwe washikamanifu kwa Kristo.

Mfalme Anayewavutia Raia Wake Kuwa Washikamanifu

4. Yesu alitimiza nini wakati wa huduma yake duniani akiwa Mfalme Aliyechaguliwa?

4 Ushikamanifu wetu kwa Kristo unategemea kuthamini yale aliyotenda na sifa zake kuu. (1 Petro 1:8) Alipokuwa duniani akiwa Mfalme Aliyechaguliwa, Yesu alionyesha kwa kiwango kidogo yale ambayo angefanya duniani pote kwa wakati wa Mungu unaofaa, wakati ambapo angekuwa Mfalme anayetawala. Aliwalisha wenye njaa. Aliwaponya wagonjwa, vipofu, walemavu, viziwi, na mabubu. Pia, aliwafufua wafu. (Mathayo 15:30, 31; Luka 7:11-16; Yohana 6:5-13) Isitoshe, kujua maisha ya Yesu hapa duniani hutuwezesha kujua sifa zake akiwa Mtawala wa dunia wa wakati ujao, hasa upendo wake wa kujidhabihu. (Marko 1:40-45) Kuhusiana na hilo, inasemekana kwamba Napoléon Bonaparte alisema hivi: ‘Aleksanda, Kaisari, Charlemagne, na mimi mwenyewe tulianzisha milki mbalimbali, lakini kazi zetu kuu zilitegemea nini? Kutumia mabavu. Yesu Kristo peke yake ndiye aliyeanzisha ufalme wake kwa msingi wa upendo, na hadi leo mamilioni ya watu wanaweza kufa kwa ajili yake.’

5. Kwa nini utu wa Yesu ulivutia sana?

5 Kwa sababu Yesu alikuwa mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, wale waliolemewa na mikazo na mizigo waliburudishwa na mafundisho yake yenye kujenga na utu wake wenye fadhili. (Mathayo 11:28-30) Watoto walistarehe walipokuwa na Yesu. Watu wanyenyekevu na wenye utambuzi walikubali kwa hiari kuwa wanafunzi wake. (Mathayo 4:18-22; Marko 10:13-16) Kwa kuwa aliwajali na kuwaheshimu watu, wanawake wengi wanaomwogopa Mungu walikuwa washikamanifu kwake, na baadhi yao wakatumia wakati, jitihada, na mali zao kumhudumia alipokuwa akitimiza huduma yake.—Luka 8:1-3.

6. Yesu alionyesha hisia gani nyororo wakati Lazaro alipokufa?

6 Kristo alionyesha hisia zake nyororo zaidi wakati Lazaro, rafiki yake mpendwa, alipokufa. Yesu aliguswa sana na huzuni ya Maria na Martha hivi kwamba hangeweza kujizuia asipige kite kwa sababu ya huzuni na ‘kutokwa na machozi.’ ‘Alitaabishwa’ na huzuni nyingi na majonzi, hata ingawa alijua kwamba angemfufua Lazaro baada ya muda usio mrefu. Kisha, akichochewa na upendo na huruma, Yesu alitumia mamlaka aliyopewa na Mungu kumfufua Lazaro.—Yohana 11:11-15, 33-35, 38-44.

7. Kwa nini Yesu anastahili ushikamanifu wetu? (Ona pia sanduku kwenye ukurasa wa 31.)

7 Sisi hustaajabia jinsi Yesu alivyopenda sana mema na kuchukia unafiki na uovu. Alichukua hatua mara mbili kuondoa wafanyabiashara wenye pupa hekaluni. (Mathayo 21:12, 13; Yohana 2:14-17) Isitoshe, akiwa mwanadamu duniani, alipatwa na matatizo ya kila aina, na hilo lilimwezesha kujionea mikazo na matatizo tunayopata. (Waebrania 5:7-9) Pia, Yesu alijua jinsi watu wanavyohisi wanapochukiwa na kudhulumiwa. (Yohana 5:15-18; 11:53, 54; 18:38–19:16) Mwishowe, alikubali kwa ujasiri kufa kifo kikatili ili atimize mapenzi ya Baba yake na kuwapa raia wake uzima wa milele. (Yohana 3:16) Je, sifa hizo za Kristo hazikuchochei kuendelea kumtumikia kwa ushikamanifu? (Waebrania 13:8; Ufunuo 5:6-10) Lakini ni nini kinachohitajiwa ili kuwa raia wa Kristo Mfalme?

Kustahili Kuwa Raia

8. Raia wa Kristo wanatakiwa kuwa na nini?

8 Fikiria mfano huu: Kwa kawaida, ili mtu awe raia wa nchi nyingine anahitaji kutimiza matakwa fulani ya msingi. Huenda akatakiwa kuwa na mwenendo mzuri na kutimiza viwango fulani vya afya. Vivyo hivyo, raia wa Kristo wanahitaji kudumisha viwango vya juu vya maadili na afya nzuri ya kiroho.—1 Wakorintho 6:9-11; Wagalatia 5:19-23.

9. Tunaweza kuonyeshaje kwamba sisi ni washikamanifu kwa Kristo?

9 Pia, Yesu Kristo anawataka raia wake wawe washikamanifu kwake na kwa Ufalme wake. Wanaonyesha ushikamanifu huo kwa kutenda mambo ambayo Yesu alifundisha alipokuwa duniani akiwa Mfalme Aliyechaguliwa. Kwa mfano, badala ya kutanguliza vitu vya kimwili, wanatanguliza masilahi ya Ufalme na mapenzi ya Mungu. (Mathayo 6:31-34) Pia, wanajitahidi sana kuwa na utu kama wa Kristo, hata wanapokabili hali ngumu sana. (1 Petro 2:21-23) Isitoshe, raia wa Kristo hufuata mfano wake kwa kuwatendea wengine mema kwa hiari.—Mathayo 7:12; Yohana 13:3-17.

10. Tunaweza kuonyeshaje ushikamanifu kwa Kristo (a) katika familia na (b) katika kutaniko?

10 Pia, wafuasi wa Yesu huonyesha kwamba wao ni washikamanifu kwake kwa kuiga sifa zake katika familia. Kwa mfano, waume huonyesha ushikamanifu kwa Mfalme wao wa mbinguni kwa kuwatendea wake zao na watoto wao kupatana na sifa za Kristo. (Waefeso 5:25, 28-30; 6:4; 1 Petro 3:7) Wake huonyesha ushikamanifu kwa Kristo kupitia mwenendo wao safi na “roho ya utulivu na ya upole.” (1 Petro 3:1-4; Waefeso 5:22-24) Watoto huonyesha ushikamanifu kwa Kristo wanapoiga mfano wake wa kutii. Yesu alipokuwa kijana, alijitiisha kwa wazazi wake, hata ingawa hawakuwa wakamilifu. (Luka 2:51, 52; Waefeso 6:1) Raia wa Kristo hujitahidi kumwiga kwa ushikamanifu kwa ‘kuonyesha hisia-mwenzi, kuwa na upendo wa kindugu,’ na kuwa “wenye huruma nyororo.” Wao hujitahidi kuwa kama Kristo, kwa kuonyesha ‘unyenyekevu katika akili, kutolipa ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano.’—1 Petro 3:8, 9; 1 Wakorintho 11:1.

Raia Wanaotii Sheria

11. Raia wa Kristo hujitiisha kwa sheria gani?

11 Kama vile watu wanaotaka kuwa raia wa nchi nyingine hutii sheria za nchi hiyo, raia wa Kristo hujitiisha kwa “sheria ya Kristo” kwa kufuata mambo yote ambayo Yesu alifundisha na kuamuru. (Wagalatia 6:2) Wao hufuata kwa ushikamanifu hasa ile “sheria ya kifalme” ya upendo. (Yakobo 2:8) Sheria hizo zinahusisha nini?

12, 13. Tunajitiishaje kwa ushikamanifu kwa “sheria ya Kristo”?

12 Raia wa Kristo si wakamilifu, nao hukosea. (Waroma 3:23) Hivyo, wanahitaji kuendelea kusitawisha “upendo wa kindugu usio na unafiki” ili ‘wapendane sana kutoka moyoni.’ (1 Petro 1:22) “Ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine,” Wakristo hufuata kwa ushikamanifu sheria ya Kristo kwa “kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.” Kutii sheria hiyo huwasaidia wasikazie fikira hali ya kutokamilika na badala yake watafute sababu za kupendana. Je, wewe unathamini kushirikiana pamoja na watu wanaojitiisha kwa ushikamanifu kwa Mfalme wetu mwenye upendo kwa kujivika upendo, “kifungo kikamilifu cha muungano”?—Wakolosai 3:13, 14.

13 Isitoshe, Yesu alieleza kwamba upendo wake ulizidi ule ambao kwa kawaida watu huonyeshana. (Yohana 13:34, 35) Tukiwapenda wale tu wanaotupenda, hatutakuwa tukifanya jambo “linalozidi lile la kawaida.” Hivyo, upendo wetu hautakuwa kamili, badala yake utakuwa na kasoro. Yesu alituhimiza tuige upendo wa Baba yake kwa kusitawisha upendo unaoongozwa na kanuni hata kwa ajili ya maadui wanaotuchukia na kututesa. (Mathayo 5:46-48) Upendo huo pia huwachochea raia wa Ufalme kuvumilia kwa ushikamanifu wanapofanya kazi yao kuu. Hiyo ni kazi gani?

Ushikamanifu Unajaribiwa

14. Kwa nini kazi ya kuhubiri ni muhimu sana?

14 Raia wa Ufalme wa Mungu wana kazi muhimu ya “kutoa ushahidi kamili kuhusiana na ufalme wa Mungu.” (Matendo 28:23) Ni muhimu kufanya hivyo kwa sababu Ufalme wa Kimasihi utatetea enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote. (1 Wakorintho 15:24-28) Tunapohubiri habari njema, wale wanaosikia wanapata nafasi ya kuwa raia wa Ufalme wa Mungu. Isitoshe, jinsi watu wanavyoitikia ujumbe huo ni kipimo kinachomwezesha Kristo Mfalme kuwahukumu wanadamu. (Mathayo 24:14; 2 Wathesalonike 1:6-10) Hivyo, njia kuu ya kuonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kwa Kristo ni kutii amri yake ya kuwaeleza wengine kuhusu Ufalme.—Mathayo 28:18-20.

15. Kwa nini ushikamanifu wa Wakristo unajaribiwa?

15 Bila shaka, Shetani hupinga kazi ya kuhubiri kwa njia yoyote ile, na watawala wa kibinadamu hawatambui mamlaka ambayo Kristo amepewa na Mungu. (Zaburi 2:1-3, 6-8) Hivyo, Yesu aliwaonya wanafunzi wake hivi: “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yohana 15:20) Hivyo, wafuasi wa Kristo wamo katika pigano la kiroho linalojaribu ushikamanifu wao.—2 Wakorintho 10:3-5; Waefeso 6:10-12.

16. Raia wa Ufalme humlipaje “Mungu vitu vya Mungu”?

16 Hata hivyo, raia wa Ufalme wa Mungu hubaki wakiwa washikamanifu kwa Mfalme wao asiyeonekana bila kuwadharau watawala wa kibinadamu. (Tito 3:1, 2) Yesu alisema hivi: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:13-17) Hivyo, raia wa Kristo hutii sheria za serikali ambazo hazipingi sheria za Mungu. (Waroma 13:1-7) Hata hivyo, wakati mahakama kuu ya Kiyahudi ilipokiuka sheria za Mungu kwa kuwaagiza wanafunzi wa Yesu waache kuhubiri, wanafunzi hao walisema kwa ujasiri na kwa heshima kwamba ni lazima ‘wamtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Matendo 1:8; 5:27-32.

17. Kwa nini tunaweza kukabili majaribu ya ushikamanifu kwa ujasiri?

17 Raia wa Kristo wanahitaji ujasiri mwingi ili waendelee kuwa washikamanifu kwa Mfalme wao wanapokabili mateso. Hata hivyo, Yesu alisema: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.” (Mathayo 5:11, 12) Wafuasi wa Kristo wa mapema waliona maneno hayo yakitimia. Hata walipopigwa kwa sababu ya kuendelea kuhubiri kuhusu Ufalme, walishangilia “kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake. Na kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.” (Matendo 5:41, 42) Mnahitaji kupongezwa kwa kuwa mnaonyesha ushikamanifu kama huo wakati mnapovumilia hali ngumu, ugonjwa, kifo cha mpendwa, au upinzani.—Waroma 5:3-5; Waebrania 13:6.

18. Maneno ya Yesu kwa Pontio Pilato yanaonyesha nini?

18 Wakati ambapo Yesu hakuwa ametawazwa kuwa Mfalme, alimweleza hivi Gavana Mroma Pontio Pilato: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Hivyo, raia wa Ufalme wa mbinguni hawashiriki katika vita vyovyote wala kuunga mkono mapambano yoyote ya wanadamu. Kwa sababu ya ushikamanifu wao kwa “Mkuu wa Amani,” wao hawajihusishi hata kidogo na shughuli za ulimwengu zinazosababisha migawanyiko.—Isaya 2:2-4; 9:6, 7.

Raia Washikamanifu Watapata Baraka Zinazodumu Milele

19. Kwa nini raia wa Kristo wanaweza kutarajia wakati ujao wakiwa na uhakika?

19 Raia washikamanifu wa Kristo, “Mfalme wa wafalme,” wanaweza kutarajia wakati ujao wakiwa na uhakika. Wanasubiri kwa hamu kuona Yesu akionyesha mamlaka yake kuu ya kifalme. (Ufunuo 19:11–20:3; Mathayo 24:30) Mabaki ya “wana wa ufalme” washikamanifu, ambao wametiwa mafuta kwa roho, wanatazamia urithi wao wenye thamani wakiwa wafalme pamoja na Kristo mbinguni. (Mathayo 13:38; Luka 12:32) “Kondoo wengine” washikamanifu wa Kristo wanasubiri kwa hamu kupata kibali cha Mfalme wao, wakati atakapotangaza hivi: “Njooni, ninyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, urithini [dunia Paradiso ambayo ni eneo la] ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.” (Yohana 10:16; Mathayo 25:34) Basi, acheni raia wote wa Ufalme waazimie kuendelea kumtumikia Kristo Mfalme kwa ushikamanifu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Ona kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, “Kwa nini Mashahidi wa Yehova husema kwamba Ufalme wa Mungu ulianzishwa mwaka wa 1914?” ukurasa wa 397-399, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini Kristo anastahili ushikamanifu wetu?

• Raia wa Kristo huonyeshaje kwamba wao ni washikamanifu kwake?

• Kwa nini tunataka kuwa washikamanifu kwa Kristo Mfalme?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 31]

SIFA NYINGINE MUHIMU ZA KRISTO

Hana ubaguziYohana 4:7-30.

HurumaMathayo 9:35-38; 12:18-21; Marko 6:30-34.

Upendo wa kujidhabihuYohana 13:1; 15:12-15.

UshikamanifuMathayo 4:1-11; 28:20; Marko 11:15-18.

Hisia-mwenziMarko 7:32-35; Luka 7:11-15; Waebrania 4:15, 16.

Kukubali sababuMathayo 15:21-28.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kwa kupendana, tunatii kwa ushikamanifu “sheria ya Kristo”

[Picha katika ukurasa wa 31]

Je, sifa za Kristo hukuchochea kumtumikia kwa ushikamanifu?