Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msiogope Yehova Yuko Pamoja Nanyi!

Msiogope Yehova Yuko Pamoja Nanyi!

Msiogope Yehova Yuko Pamoja Nanyi!

ZAIDI ya miaka 50 iliyopita, muda mfupi tu baada ya milipuko ya mabomu ya kwanza ya nyukilia, Harold C. Urey, mwanasayansi wa atomi na mshindi wa Tuzo ya Nobeli, alisema hivi kuhusu wakati ujao: “Tutakula kwa woga, tutalala kwa woga, tutaishi kwa woga na tutakufa kwa woga.” Leo, haishangazi kwamba ulimwengu umejaa woga! Kila siku, magazeti yanatangaza visa vya ugaidi vyenye kuogopesha, uhalifu wenye jeuri, na magonjwa yenye kutisha.

Tukiwa Wakristo, tunajua hali hizo zinamaanisha nini. Zinaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo ambazo Biblia ilitabiri zingekuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Kwa hiyo, uhakika wetu unaimarishwa kwa kujua kwamba hivi karibuni Yehova Mungu ataleta ulimwengu mpya ambamo uadilifu utakaa. (2 Petro 3:13) Hata hivyo, je, sisi Wakristo huogopa?

Maoni ya Watumishi wa Mungu Kuhusu Woga

Yakobo, Daudi, na Eliya walikuwa miongoni mwa watumishi wa Yehova ambao waliogopa kwa kiasi fulani walipokabili hatari. (Mwanzo 32:6, 7; 1 Samweli 21:11, 12; 1 Wafalme 19:2, 3) Si kwamba watu hao hawakuwa na imani. Badala yake, walithibitisha kabisa kwamba walimtegemea Yehova. Hata hivyo, Yakobo, Daudi, na Eliya walikuwa wanadamu tu, na kwa hiyo walihisi woga. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Eliya alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu.”—Yakobo 5:17.

Huenda sisi pia tukaogopa tunapofikiria tatizo tunalokabili au tunaloweza kukabili wakati ujao. Woga wa aina hiyo unaeleweka. Biblia inasema kwamba Shetani Ibilisi ameazimia “kupigana vita” na wale “wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 12:17) Ingawa maneno hayo yanawahusu hasa Wakristo watiwa-mafuta, Paulo aliandika hivi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Hata hivyo, hatupaswi kujihisi hoi tunapokabili matatizo. Kwa nini?

“Mungu wa Matendo ya Kuokoa”

Mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Kwetu, Mungu wa kweli ni Mungu wa matendo ya kuokoa.” (Zaburi 68:20) Yehova amethibitisha tena na tena kwamba ana uwezo wa kuwaokoa watu wake, iwe kwa kuwakomboa kutokana na hali zenye hatari au kwa kuwaimarisha ili wavumilie hali hizo. (Zaburi 34:17; Danieli 6:22; 1 Wakorintho 10:13) Kutokana na jinsi ambavyo umejifunza Biblia, ni ‘matendo mangapi ya kuokoa’ kama hayo ambayo unaweza kukumbuka?

Kwa kutumia Watch Tower Publications Index * (Index de Publications de la Société), kwa nini usifanye utafiti kuhusu matukio halisi kama vile Gharika ya ulimwenguni pote ya siku za Noa, kukombolewa kwa Loti na binti zake kutoka Sodoma na Gomora, Kutoka kwa Waisraeli Misri na kuvuka Bahari Nyekundu, au kukomeshwa kwa njama ya Hamani ya kuwaangamiza Wayahudi? Kusoma na kutafakari masimulizi hayo yenye kuchochea kutaimarisha imani yako kwamba Yehova ni Mungu wa matendo ya kuokoa. Kufanya hivyo kutakusaidia kuyakabili majaribu ya imani yako bila woga.

Mifano ya Leo

Je, unaweza kufikiria mifano ya watu ambao wameonyesha uvumilivu katika eneo lenu? Huenda ni mtu ambaye amefungwa gerezani kwa sababu ya kuwa mwaminifu kwa Mungu. Huenda unamjua Mkristo mwenye umri mkubwa anayemtumikia Yehova licha ya matatizo ya afya. Au fikiria vijana wanaojitenga na ulimwengu licha ya mikazo mingi kutoka kwa wanafunzi wenzao. Kisha, kuna wazazi wasio na wenzi ambao wanalea watoto bila kusaidiwa na mwenzi wa ndoa, au waseja ambao wanamtumikia Yehova licha ya kuhisi upweke. Unajifunza nini kutokana na mifano hiyo? Kufikiria uaminifu wao kunaweza kukusaidia kuvumilia na kutoogopa licha ya majaribu unayokabili.

Tunahitaji kuwa wenye ujasiri si wakati tu tunapokabili upinzani na mateso, lakini pia wakati tunapoanza kutilia shaka kwamba Yehova anatupenda. Tunapaswa kuwa na uhakika kwamba fidia ya Kristo inatuhusu tukiwa mtu mmoja-mmoja. (Wagalatia 2:20) Kisha, tunaweza kumkaribia Yehova bila woga wowote au hofu. Ikiwa tunajihisi kwamba hatustahili kupendwa na Yehova, tunaweza kutafakari maneno haya ya Yesu kwa wafuasi wake: “Je, shomoro wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiogope: Ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.”—Mathayo 10:29-31.

Mara nyingi magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanachapisha visa mbalimbali vya Mashahidi wa Yehova wa siku hizi ambao wamekabili matatizo bila woga. Hilo halimaanishi kwamba hawakuwahi kuwa na hisia zisizofaa kuhusiana na matatizo yao. Hata hivyo, hawakuacha hisia hizo ziwazuie wasimtumikie Yehova. Masimulizi yao yaliyochapishwa yanaweza kukusaidia pia kuvumilia bila woga. Fikiria mifano hii miwili.

Maisha Yake Yalibadilika Alipojeruhiwa

Gazeti la Amkeni! la Aprili 22, 2003, lilikuwa na makala “Jinsi Maisha Yangu Yalivyobadilika Nilipojeruhiwa.” Katika gazeti hilo, Stanley Ombeva, ambaye ni Shahidi wa Yehova nchini Kenya, anaonyesha matatizo aliyokabili alipogongwa na gari lililokuwa likienda kasi. Afya yake ilipodhoofika, alipoteza kazi yake na marupurupu yote. Katika simulizi lake, Ndugu Ombeva anasema hivi: “Hali ilipozidi kuwa mbaya, nilianza kuwa na hisia zisizofaa, nikawa mbinafsi, na niliudhika upesi. Nyakati nyingine niliudhika na kukasirishwa.” Licha ya kuteseka, Mkristo huyo hakuogopa. Hakuruhusu hali yake imvunje moyo na kumkatisha tamaa. Badala yake, alimtegemea Yehova. Ndugu Ombeva anasema hivi: “Daima [Yehova] alinitegemeza sana katika matatizo yangu yote hivi kwamba niliona haya wakati mwingine. Niliazimia kabisa kusoma na kutafakari kuhusu maandiko niliyojua yangenifariji.”

Maelezo ya unyoofu ya Ndugu Ombeva yaliwasaidia wengi kuvumilia majaribu bila kuogopa. Dada mmoja Mkristo aliandika hivi: “Nililia niliposoma makala hiyo. Nilihisi kwamba kupitia makala hiyo Yehova alikuwa akinionyesha upendo mchangamfu na kunifariji.” Shahidi mwingine aliandika hivi: “Makala kama hizi zinatutia moyo sana sisi tunaopatwa na hali kama hizo na ambao huteseka bila kulalamika.”

Kukabiliana na Matatizo ya Kihisia

Kisa kingine chenye kugusa moyo ni kile cha Herbert Jennings, kilichosimuliwa katika makala “Hamjui Uhai Wenu Utakuwa Nini Kesho.” * Ndugu Jennings anakabiliana na ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia. Akikumbuka wakati alipoanza kuwa mgonjwa, anasema hivi: “Nilihitaji kujikakamua sana kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hata hivyo, nilijua kabisa manufaa ya ushirika wa kiroho. Ili kukabiliana na hali hiyo, nilikuwa ninaingia katika Jumba la Ufalme baada ya watu kuketi na kutulia kisha kuondoka muda mfupi tu kabla hawajaanza kuondoka baada ya programu.”

Pia, ilikuwa vigumu kwake kuhubiri. Ndugu Jennings anasema hivi: “Mara nyingine, singeweza hata kupiga kengele ya mlango hata baada ya kufika kwenye nyumba. Hata hivyo, niliendelea kuhubiri kwa sababu niling’amua kwamba huduma yetu yamaanisha wokovu kwetu wenyewe na kwa yeyote anayeitikia ifaavyo. (1 Timotheo 4:16) Baada ya muda mfupi, ningeweza kudhibiti hisia zangu, kwenda kwenye mlango mwingine, na kujaribu tena kupiga kengele. Kwa kuendelea kushiriki katika huduma, nilidumisha afya ya kiroho ifaayo nayo ikaongeza uwezo wangu wa kuvumilia.”

Simulizi la Ndugu Jennings linalosema mambo waziwazi liliwasaidia wasomaji wengi kukabiliana pia na taabu zao bila woga. Kwa mfano, dada mmoja Mkristo aliandika hivi: “Kwa muda wa miaka 28 ambayo nimekuwa nikisoma magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, sijawahi kuguswa moyo kama wakati nilipokuwa nikisoma makala hii. Niliacha utumishi wa wakati wote na kujihisi kuwa mwenye hatia sana. Nilihisi kwamba kama ningekuwa na imani zaidi ningeendelea na utumishi wangu. Niliposoma jinsi Ndugu Jennings alivyoacha mgawo wake ili ashughulikie afya yake, ilinisaidia kuwa na maoni yenye kusawazika kuhusu hali yangu. Simulizi hilo lilikuwa jibu kwa sala zangu!”

Vivyo hivyo, ndugu mmoja Mkristo aliandika hivi: “Baada ya kutumika kutanikoni nikiwa mzee kwa miaka kumi, niliacha pendeleo hilo la uzee kwa sababu ya ugonjwa fulani wa akili. Kwa sababu ya kushindwa kuendelea kuwa mzee, mara nyingi nilisikitika sana niliposoma makala za masimulizi ya maisha ambazo mara nyingi hueleza mambo ya ajabu yanayotimizwa na watu wa Yehova. Hata hivyo, ustahimilivu wa Ndugu Jennings ulinitia moyo. Nilisoma tena na tena makala hiyo.”

Kusonga Mbele Tukiwa na Uhakika

Kama Ndugu Ombeva na Ndugu Jennings, Mashahidi wa Yehova wengi wanaendelea bila woga kumwabudu Yehova Mungu licha ya vizuizi vikubwa. Ikiwa wewe ni mmoja wao, unastahili pongezi. Uwe na hakika kwamba: ‘Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa umewahudumia watakatifu nawe unaendelea kuhudumu.’—Waebrania 6:10.

Kama vile Yehova alivyowasaidia watu wake waaminifu wa nyakati za kale kushinda maadui wao, anaweza kukusaidia kushinda kizuizi chochote ambacho huenda ukakabili. Basi, fikiria maneno haya ambayo Yehova alisema kupitia nabii Isaya: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.”—Isaya 41:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 18 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 2000, ukurasa wa 24-28.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kama Stanley Ombeva (juu) na Herbert Jennings (kulia), wengi wanamtumikia Yehova bila woga

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 14]

USAF photo