Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wachungaji Ambao Ni “Vielelezo Kwa Kundi”

Wachungaji Ambao Ni “Vielelezo Kwa Kundi”

Wachungaji Ambao Ni “Vielelezo Kwa Kundi”

“Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu . . . kwa kupenda . . . , kwa hamu . . . , [na] kuwa vielelezo kwa kundi.”—1 PETRO 5:2, 3.

1, 2. (a) Yesu alimpa mtume Petro pendeleo gani, na kwa nini alikuwa na sababu nzuri ya kumwamini Petro? (b) Yehova anawaonaje wachungaji waliowekwa rasmi?

MUDA fulani kabla ya Pentekoste 33 W.K., Petro na wanafunzi wengine sita walikuwa wakila kiamsha-kinywa ambacho Yesu alitayarisha kwenye ufuo wa Bahari ya Galilaya. Hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa Petro kumwona Yesu baada ya kufufuliwa, na hapana shaka kwamba alisisimuka kujua kwamba Yesu alikuwa hai. Lakini huenda Petro alikuwa na wasiwasi pia kwa sababu siku chache mapema, alikuwa amemkana Yesu hadharani. (Luka 22:55-60; 24:34; Yohana 18:25-27; 21:1-14) Je, Yesu alimkemea Petro aliyetubu kwa sababu ya kukosa imani? Hapana. Badala yake, Yesu alimpa Petro pendeleo la kulisha na kuchunga ‘kondoo wake wadogo.’ (Yohana 21:15-17) Kama vile simulizi la Biblia kuhusu kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza linavyoonyesha, Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kumwamini Petro. Akiwa pamoja na mitume wengine na wanaume wazee wa Yerusalemu, Petro alilichunga kutaniko la Kikristo kulipokuwa na majaribu makali na ongezeko la haraka.—Matendo 1:15-26; 2:14; 15:6-9.

2 Leo, Yehova kupitia Yesu Kristo amewaweka rasmi wanaume wanaostahili ili wawe wachungaji wa kiroho ambao wanaongoza kondoo Zake katika nyakati hizi za hatari zaidi katika historia ya wanadamu. (Waefeso 4:11, 12; 2 Timotheo 3:1) Je, Yehova ana sababu nzuri ya kuwaamini wanaume hao? Undugu wa Kikristo wenye amani ulimwenguni pote unaonyesha hivyo. Naam, kama Petro, wachungaji hao ni wanadamu wanaofanya makosa. (Wagalatia 2:11-14; Yakobo 3:2) Hata hivyo, Yehova anaamini kwamba watatunza kondoo ambao ‘aliwanunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.’ (Matendo 20:28) Yehova anawapenda sana wanaume hao na anaona kwamba ‘wanastahili heshima mara mbili.’—1 Timotheo 5:17.

3. Ni nini kinachowawezesha wachungaji wa kiroho waendelee kutimiza madaraka yao kwa kupenda na kwa hamu?

3 Ni nini kinachowawezesha wachungaji wa kiroho waendelee kutimiza madaraka yao kwa kupenda na kwa hamu, na hivyo kuwa vielelezo kwa kundi? Kama Petro na wachungaji wengine wa karne ya kwanza, wanategemea roho takatifu ya Mungu, ambayo inawapa nguvu wanazohitaji ili watimize wajibu wao. (2 Wakorintho 4:7) Pia, roho takatifu inawasaidia kusitawisha matunda ya roho, yaani, upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujizuia. (Wagalatia 5:22, 23) Acheni tuchunguze jinsi wachungaji wanavyoweza kuweka mfano katika kuonyesha matunda hayo wanapolichunga kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao.

Lipendeni Kundi na Kila Kondoo

4, 5. (a) Yehova na Yesu huonyeshaje kwamba wanalipenda kundi? (b) Ni baadhi ya mambo gani yanayoonyesha kwamba wachungaji wa kiroho wanalipenda kundi?

4 Upendo ndio sifa kuu zaidi inayotokezwa na roho ya Mungu. Yehova huonyesha kwamba analipenda kundi lote kwa kuliandalia chakula tele cha kiroho. (Isaya 65:13, 14; Mathayo 24:45-47) Hata hivyo, yeye hufanya mengi zaidi ya kulilisha kundi. Anajali kila kondoo. (1 Petro 5:6, 7) Yesu pia analipenda kundi. Alitoa uhai wake kwa ajili ya kundi, naye anajua kila kondoo “kwa jina.”—Yohana 10:3, 14-16.

5 Wachungaji wa kiroho humwiga Yehova na Yesu. Wao huonyesha kwamba wanalipenda kundi lote la Mungu kwa ‘kufanya bidii katika kufundisha’ kutaniko. Hotuba zao za Biblia hulisha na kulinda kundi, na wote kutanikoni huona bidii yao katika jambo hilo. (1 Timotheo 4:13, 16) Lakini kuna mambo wanayofanya ambayo hayaonwi sana na wengine kutanikoni, kama vile kushughulikia rekodi za kutaniko, kushughulikia barua, kutayarisha ratiba za migawo, na kushughulikia mambo mengine mengi ambayo huwezesha mikutano ya kutaniko na shughuli nyingine zitendeke “kwa adabu na kwa mpango.” (1 Wakorintho 14:40) Wao hufanya mengi ya mambo hayo bila wengine kutanikoni kujua, na huenda mambo wanayofanya yasitambuliwe. Naam, wanafanya kazi ngumu kwa upendo.—Wagalatia 5:13.

6, 7. (a) Ni njia gani moja inayowawezesha wachungaji kuwajua kondoo? (b) Kwa nini inafaa nyakati nyingine kumweleza mzee jinsi tunavyohisi?

6 Wachungaji Wakristo wenye upendo hupendezwa na kila kondoo kutanikoni. (Wafilipi 2:4) Njia moja inayowawezesha wachungaji kumfahamu vizuri kila kondoo ni kushiriki pamoja nao katika kazi ya kuhubiri. Mara nyingi Yesu alienda kuhubiri pamoja na wafuasi wake, naye alitumia pindi hizo kuwatia moyo. (Luka 8:1) Mchungaji mmoja Mkristo mwenye uzoefu anasema hivi: “Mimi huona kwamba njia moja nzuri ya kumjua na kumtia moyo ndugu au dada ni kushiriki huduma ya shambani pamoja naye.” Ikiwa hujashiriki huduma ya shambani pamoja na mzee yeyote hivi karibuni, kwa nini usipange kufanya hivyo bila kukawia?

7 Upendo ulimchochea Yesu kushangilia na kuhuzunika pamoja na wafuasi wake. Kwa mfano, wanafunzi wake 70 waliporudi wakiwa na shangwe baada ya kuhubiri, Yesu alijawa na “shangwe sana.” (Luka 10:17-21) Hata hivyo, alipoona jinsi kifo cha Lazaro kilivyomwathiri Maria na watu wa familia yao na marafiki wao, ‘Yesu alitokwa na machozi.’ (Yohana 11:33-35) Vivyo hivyo, leo wachungaji wanaojali huhangaikia hisia za kondoo. Upendo huwachochea ‘kushangilia pamoja na watu wanaoshangilia’ na ‘kulia pamoja na watu wanaolia.’ (Waroma 12:15) Ukiwa na shangwe au huzuni maishani mwako, usiogope kuwaeleza wachungaji Wakristo jinsi unavyohisi. Watatiwa moyo kujua jambo linalofanya uwe na shangwe. (Waroma 1:11, 12) Ukiwaeleza majaribu unayokabili, watakuimarisha na kukufariji.—1 Wathesalonike 1:6; 3:1-3.

8, 9. (a) Mzee mmoja alionyeshaje kwamba anampenda mke wake? (b) Kwa nini ni muhimu mchungaji aipende familia yake?

8 Upendo wa mchungaji kwa kundi unaonyeshwa hasa na vile anavyoitendea familia yake. (1 Timotheo 3:1, 4) Ikiwa ameoa, upendo na heshima yake kwa mke wake ni mfano wa kuigwa na waume wengine. (Waefeso 5:25; 1 Petro 3:7) Hebu ona maelezo haya ya mwanamke mmoja Mkristo anayeitwa Linda. Mume wake alikuwa mwangalizi kwa zaidi ya miaka 20 kabla ya kifo chake. Linda anasema: “Sikuzote mume wangu alikuwa na shughuli nyingi za kutaniko. Lakini alinifanya nihisi kwamba tuko pamoja. Mara nyingi alionyesha kwamba anathamini msaada wangu, naye alipopata nafasi tulifanya mambo pamoja. Hivyo, nilihisi kwamba ananipenda, nami sikuona wivu alipotumia wakati kutumikia kutaniko.”

9 Ikiwa mchungaji Mkristo ana watoto, jinsi anavyowatia nidhamu kwa upendo na kuwapongeza kwa ukawaida ni mfano wa kuigwa na wazazi wengine. (Waefeso 6:4) Upendo wake kwa familia yake huonyesha kwamba anastahili daraka alilopewa alipowekwa rasmi kwa mwongozo wa roho takatifu.—1 Timotheo 3:4, 5.

Dumisheni Shangwe na Amani kwa Kuwasiliana

10. (a) Ni nini kinachoweza kuathiri shangwe na amani ya kutaniko? (b) Ni suala gani lililohatarisha amani ya kutaniko la karne ya kwanza, nalo lilisuluhishwaje?

10 Roho takatifu inaweza kutokeza shangwe na amani katika moyo wa kila Mkristo, katika baraza la wazee, na katika kutaniko lote. Hata hivyo, kutowasiliana waziwazi kunaweza kuathiri shangwe na amani hiyo. Sulemani alisema hivi: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.” (Methali 15:22) Kwa upande mwingine, kuwasiliana waziwazi na kwa heshima hudumisha shangwe na amani. Kwa mfano, wakati suala la tohara lilipokuwa karibu kuvuruga amani ya kutaniko la karne ya kwanza, baraza linaloongoza huko Yerusalemu lilitafuta mwongozo wa roho takatifu. Pia, walieleza maoni yao tofauti-tofauti kuhusu jambo hilo. Baada ya mazungumzo yenye kusisimua, walifanya uamuzi. Walipoyajulisha makutaniko uamuzi wao usiopingwa, akina ndugu “walishangilia juu ya kitia-moyo hicho.” (Matendo 15:6-23, 25, 31; 16:4, 5) Shangwe na amani zilidumishwa.

11. Wazee wanaweza kudumishaje shangwe na amani kutanikoni?

11 Vivyo hivyo leo, wachungaji hudumisha shangwe na amani kutanikoni kwa kuwasiliana waziwazi. Matatizo yanapotishia kuvuruga amani ya kutaniko, wao hukutana na kueleza hisia zao waziwazi. Wao husikiliza kwa heshima maelezo ya wachungaji wenzao. (Methali 13:10; 18:13) Baada ya kusali ili wapate roho takatifu, wao hutegemeza maamuzi yao juu ya kanuni za Biblia na miongozo iliyochapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47; 1 Wakorintho 4:6) Uamuzi unaopatana na Maandiko unapofanywa na baraza la wazee, kila mzee hukubali mwongozo wa roho takatifu kwa kuunga mkono uamuzi huo hata ikiwa maoni yake hayakukubaliwa na wengi katika baraza. Kuonyesha sifa ya kiasi kwa njia hiyo hudumisha shangwe na amani na ni mfano mzuri kwa kondoo kuhusu jinsi ya kutembea na Mungu. (Mika 6:8) Je, wewe huonyesha kiasi kwa kuunga mkono maamuzi yanayotegemea Biblia ambayo yanafanywa na wachungaji kutanikoni?

Iweni Wastahimilivu na Wenye Fadhili

12. Kwa nini Yesu alihitaji kuonyesha ustahimilivu na fadhili aliposhughulika na mitume?

12 Ingawa mitume walikosea mara nyingi, Yesu alionyesha ustahimilivu na fadhili aliposhughulika nao. Kwa mfano, Yesu alijitahidi tena na tena kuwaonyesha umuhimu wa unyenyekevu. (Mathayo 18:1-4; 20:25-27) Lakini, usiku wa mwisho wa maisha ya Yesu duniani, baada ya kuwafundisha unyenyekevu kwa kuwaosha miguu, ‘kulitokea pia bishano kali kati yao juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote.’ (Luka 22:24; Yohana 13:1-5) Je, Yesu aliwakemea mitume? Hapana, alizungumza nao kwa fadhili, na kusema: “Ni nani aliye mkuu zaidi, yule anayeketi mezani au yule anayehudumu? Je, si yule anayeketi mezani? Lakini mimi nimo katikati yenu kama yule anayehudumu.” (Luka 22:27) Hatimaye, ustahimilivu wa Yesu, fadhili zake, na mfano wake mwema, uligusa mioyo ya mitume hao.

13, 14. Ni wakati gani ambapo ni lazima wachungaji watende kwa fadhili?

13 Vivyo hivyo, huenda mchungaji akahitaji kumshauri mtu tena na tena kuhusu udhaifu fulani. Huenda mchungaji huyo akamkasirikia mtu huyo. Lakini, mchungaji akikumbuka udhaifu wake mwenyewe ‘anapomwonya yule asiye na utaratibu,’ atamtendea ndugu yake kwa ustahimilivu na fadhili. Kwa njia hiyo anawaiga Yesu na Yehova ambao wanaonyesha sifa hizo wanaposhughulika na Wakristo wote, kutia ndani wachungaji.—1 Wathesalonike 5:14; Yakobo 2:13.

14 Nyakati nyingine, huenda wachungaji wakalazimika kumshauri vikali mtu aliyefanya dhambi nzito. Mtu huyo asipotubu, lazima wachungaji wamwondoe mkosaji huyo kutanikoni. (1 Wakorintho 5:11-13) Hata hivyo, jinsi wanavyoshughulika na mtu huyo huonyesha kwamba wanachukia dhambi, bali si mkosaji. (Yuda 23) Wachungaji wanapoonyesha fadhili, huenda ikawa rahisi kwa kondoo aliyepotea kurudi kundini.—Luka 15:11-24.

Matendo Mema Yanachochewa na Imani

15. Wachungaji huiga wema wa Yehova katika njia gani moja, na ni nini kinachowachochea kufanya hivyo?

15 “Yehova ni mwema kwa wote,” hata kwa wale wasiothamini mambo anayowafanyia. (Zaburi 145:9; Mathayo 5:45) Yehova huonyesha wema wake kwa kuwatuma watu wake wahubiri “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Wachungaji huonyesha wema wa Mungu kwa kuongoza katika kazi hiyo ya kuhubiri. Ni nini ambacho huchochea bidii yao nyingi? Ni imani thabiti katika Yehova na ahadi zake.—Waroma 10:10, 13, 14.

16. Wachungaji wanaweza ‘kuwatendeaje mema’ kondoo?

16 Zaidi ya kuwatendea “wote mema” kwa kuhubiri, wachungaji wana daraka la kuwatendea mema “hasa wale ambao katika imani ni jamaa [zao].” (Wagalatia 6:10) Mojawapo ya njia ambazo wanatumia kufanya hivyo ni kufanya ziara za uchungaji zenye kutia moyo. Mzee mmoja anasema hivi: “Mimi hufurahia kufanya ziara za uchungaji. Ziara hizo huniwezesha kuwapongeza ndugu na dada kwa jitihada zao na zinawawezesha kujua kwamba bidii yao inathaminiwa.” Nyakati nyingine, wachungaji wanaweza kumpendekezea mtu njia za kuboresha utumishi wake kwa Yehova. Kwa kufanya hivyo, wachungaji wenye hekima humwiga mtume Paulo. Ona jinsi alivyowasihi akina ndugu huko Thesalonike: “Tuna uhakika katika Bwana kuwahusu ninyi, kwamba mnafanya nanyi mtaendelea kufanya mambo tunayoagiza.” (2 Wathesalonike 3:4) Maelezo kama hayo yanayoonyesha kwamba wachungaji wanawatumaini kondoo huwavutia kondoo hao na kufanya iwe rahisi kwao ‘kuwatii wale wanaoongoza.’ (Waebrania 13:17) Ukifanyiwa ziara ya uchungaji yenye kutia moyo, je, utaonyesha kwamba unathamini ziara hiyo?

Ili Muwe Wapole Mnahitaji Kujizuia

17. Petro alijifunza nini kutoka kwa Yesu?

17 Yesu alikuwa mwenye tabia-pole, hata alipochokozwa. (Mathayo 11:29) Aliposalitiwa na kukamatwa, Yesu alitenda kwa upole na alijizuia sana. Bila kufikiri, Petro alichomoa upanga na kulipiza kisasi. Lakini Yesu alimkumbusha hivi: “Unafikiri kwamba siwezi kumwomba Baba yangu anipe sasa hivi vikosi zaidi ya kumi na viwili vya malaika?” (Mathayo 26:51-53; Yohana 18:10) Petro alijifunza kutokana na kisa hicho, na baadaye aliwakumbusha Wakristo hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu. . . . Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho.”—1 Petro 2:21-23.

18, 19. (a) Ni wakati gani hasa ambapo ni lazima wachungaji watende kwa upole na kujizuia? (b) Tutazungumzia maswali gani katika makala inayofuata?

18 Vivyo hivyo, wachungaji wenye mafanikio huwa wapole hata wanapotendewa isivyo haki. Kwa mfano, huenda wengine wasiitikie vizuri wakati wachungaji wanapojaribu kuwasaidia. Ikiwa mtu anayehitaji msaada ni dhaifu kiroho au ni mgonjwa kiroho, huenda akaitikia mashauri kwa ‘kusema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma.’ (Methali 12:18) Hata hivyo, kama Yesu, wachungaji hawajibu kwa maneno makali wala kulipiza kisasi. Badala yake, wao hujizuia na kuonyesha hisia-mwenzi, na hilo linaweza kumsaidia yule anayehitaji msaada. (1 Petro 3:8, 9) Je, wewe hujifunza kutokana na mfano wa wazee kwa kutenda kwa upole na kujizuia unaposhauriwa?

19 Hapana shaka kwamba Yehova na Yesu huthamini sana jitihada za maelfu ya wachungaji wanaolichunga kundi ulimwenguni pote kwa kupenda. Yehova na Mwana wake wanawapenda pia maelfu ya watumishi wa huduma wanaowasaidia wazee ‘kuwahudumia watakatifu.’ (Waebrania 6:10) Basi, kwa nini ndugu wengine waliobatizwa husita kufikia ‘kazi hiyo njema’? (1 Timotheo 3:1) Na Yehova huwazoezaje wale anaowaweka rasmi kuwa wachungaji? Tutazungumzia maswali hayo katika makala inayofuata.

Je, Unakumbuka?

• Ni baadhi ya mambo gani yanayoonyesha kwamba wachungaji wanalipenda kundi?

• Wote kutanikoni wanaweza kudumishaje shangwe na amani?

• Kwa nini wachungaji huonyesha ustahimilivu na fadhili wanapotoa mashauri?

• Wazee huonyeshaje wema na imani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wazee huchochewa na upendo kulitumikia kutaniko

[Picha katika ukurasa wa 18]

Pia wao hutumia wakati pamoja na familia zao katika tafrija . . .

. . . na katika huduma

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wazee wanapowasiliana waziwazi wao hudumisha shangwe na amani kutanikoni