Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwazoeza Wachungaji kwa Ajili ya Kundi Lake

Yehova Huwazoeza Wachungaji kwa Ajili ya Kundi Lake

Yehova Huwazoeza Wachungaji kwa Ajili ya Kundi Lake

“Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi.” —METHALI 2:6.

1, 2. Kwa nini wanaume waliobatizwa hujitahidi kufikia madaraka zaidi kutanikoni?

“NILIFURAHI sana nilipowekwa rasmi kuwa mzee,” asema Nick, ambaye ametumikia akiwa mzee kwa miaka saba. “Niliona pendeleo hilo kuwa njia ya kuongeza utumishi wangu kwa Yehova. Nilihisi kwamba ninapaswa kumshukuru kwa mambo yote ambayo amenifanyia. Nilitaka pia kuwasaidia washiriki wa kutaniko kwa kadiri niwezavyo, kama vile wazee wengine walivyonisaidia.” Hata hivyo, ijapokuwa Nick alikuwa na shangwe, alikuwa pia na wasiwasi. Nick anaendelea kusema hivi: “Kwa sababu sikuwa nimefikisha umri wa miaka 30 nilipowekwa rasmi, nilihisi kwamba sina ustadi unaohitajiwa, yaani, utambuzi na hekima ya kulichunga kundi vizuri.”

2 Wale ambao Yehova anawaweka ili kulichunga kundi lake wana sababu nyingi za kufurahi. Mtume Paulo aliwakumbusha wazee wa Efeso sababu moja aliponukuu maneno haya ya Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Wanaume waliobatizwa ambao wanatumikia wakiwa watumishi wa huduma au wazee hupata nafasi nyingi zaidi za kumtumikia Yehova na kutaniko. Kwa mfano, watumishi wa huduma huwasaidia wazee. Watumishi hao hushughulikia pia migawo mingi muhimu inayohitaji wakati mwingi. Ndugu hao wanachochewa na upendo kwa Mungu na kwa jirani wanapotoa utumishi huo muhimu.—Marko 12:30, 31.

3. Kwa nini huenda wengine wakasita kufikia mapendeleo kutanikoni?

3 Namna gani ikiwa mwanamume Mkristo anasita kufikia pendeleo la kuwa mtumishi wa huduma au mzee kwa sababu ya kuhisi kwamba hastahili? Kama Nick, huenda akahisi kwamba hana ustadi unaohitajiwa ili kuwa mchungaji stadi. Je, wewe ni mmoja wa ndugu waliobatizwa ambao wanahisi hivyo? Inaeleweka mtu anapokuwa na mahangaiko hayo. Yehova atawatoza hesabu wachungaji waliowekwa rasmi kulingana na jinsi wanavyolitendea kundi. Yesu alisema hivi: “Kila mtu ambaye alipewa mengi, atadaiwa mengi; na yule ambaye watu wamemweka asimamie mengi, watamdai mengi zaidi kutoka kwake kuliko ilivyo kawaida.”—Luka 12:48.

4. Yehova huwasaidiaje wale anaowaweka rasmi kutunza kondoo zake?

4 Je, Yehova anatazamia wale anaowaweka kuwa watumishi wa huduma na wazee kutimiza madaraka yao bila msaada wowote? Hapana, yeye huwapa msaada unaowawezesha kutimiza madaraka yao na kufanikiwa. Kama makala iliyotangulia ilivyoonyesha, Yehova huwapa roho yake takatifu, na matunda ya roho hiyo huwasaidia kulitunza kundi kwa wororo. (Matendo 20:28; Wagalatia 5:22, 23) Pia, Yehova huwapa hekima, ujuzi, na utambuzi. (Methali 2:6) Anafanyaje hivyo? Acheni tuzungumzie njia tatu ambazo Yehova anatumia kuwazoeza wale ambao anawaweka rasmi kutunza kondoo zake.

Kuzoezwa na Wachungaji Wenye Uzoefu

5. Kwa nini Petro na Yohana walikuwa wachungaji stadi?

5 Mitume Petro na Yohana waliposimama mbele ya Sanhedrini, waamuzi wenye elimu nyingi ya kilimwengu wa mahakama hiyo waliwaona kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” Naam, wangeweza kusoma na kuandika, lakini hawakuwa wameelimishwa kuhusu Maandiko katika shule za kirabi. Hata hivyo, Petro na Yohana pamoja na wale wanafunzi wengine walikuwa walimu stadi, nao waliwachochea watu wengi waliowasikiliza kuwa waamini. Watu hao wa kawaida walipataje kuwa walimu stadi? Baada ya kuwasikiliza Petro na Yohana, mahakama ‘ilianza kutambua juu yao kwamba walikuwa pamoja na Yesu.’ (Matendo 4:1-4, 13) Naam, walikuwa wamepokea roho takatifu. (Matendo 1:8) Lakini pia ilikuwa wazi, hata kwa waamuzi hao vipofu kiroho, kwamba Yesu alikuwa amewazoeza wanafunzi wake. Yesu alipokuwa pamoja na mitume wake duniani, hakuwafundisha tu kukusanya watu walio kama kondoo bali aliwafundisha pia jinsi ya kuwachunga watu hao baada ya kuingia ndani ya kundi.—Mathayo 11:29; 20:24-28; 1 Petro 5:4.

6. Yesu na Paulo waliweka mfano gani katika kuwazoeza wengine?

6 Baada ya Yesu kufufuliwa, aliendelea kuwazoeza wale waliowekwa rasmi kuwa wachungaji. (Ufunuo 1:1; 2:1–3:22) Kwa mfano, yeye mwenyewe ndiye aliyemchagua Paulo na kusimamia mazoezi aliyopata. (Matendo 22:6-10) Paulo alithamini mazoezi aliyoyapata, naye akatumia mambo aliyojifunza kuwazoeza wazee wengine. (Matendo 20:17-35) Kwa mfano, alitumia wakati mwingi na alijitahidi sana kumzoeza Timotheo awe “mfanyakazi” katika utumishi wa Mungu, bila “lolote la kuonea aibu.” (2 Timotheo 2:15) Watu hao wawili wakawa na uhusiano wa karibu. Mapema, Paulo aliandika hivi kumhusu Timotheo: “Kama mtoto na baba yake yeye alitumika pamoja nami katika kuendeleza habari njema.” (Wafilipi 2:22) Paulo hakukusudia kumfanya Timotheo au mtu mwingine kuwa mwanafunzi wake. Badala yake, aliwahimiza waamini wenzake wawe ‘waigaji wake, kama vile yeye alivyo mwigaji wa Kristo.’—1 Wakorintho 11:1.

7, 8. (a) Simulia kisa kinachoonyesha faida zinazotokea wakati wazee wanapomwiga Yesu na Paulo. (b) Ni wakati gani ambapo wazee wanapaswa kuanza kuwazoeza ndugu ambao watakuwa watumishi wa huduma na wazee?

7 Wachungaji wenye uzoefu humwiga Yesu na Paulo kwa kuwazoeza akina ndugu waliobatizwa, nao wanapata matokeo mazuri pia. Fikiria kisa cha Chad. Alilelewa katika familia iliyogawanyika kidini, lakini hivi majuzi aliwekwa kuwa mzee. Chad anasema hivi: “Kwa miaka mingi, wazee kadhaa wenye uzoefu walinisaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Kwa kuwa baba yangu hakuwa mwamini, wazee hao walipendezwa nami nao wakawa kama baba zangu wa kiroho. Walinizoeza katika huduma, na baadaye, mzee mmoja alinizoeza kushughulikia migawo niliyopewa kutanikoni.”

8 Kama kisa cha Chad kinavyoonyesha, wachungaji wenye utambuzi huanza mapema kuwazoeza akina ndugu ambao watakuwa watumishi wa huduma na wazee kabla hawajastahili kupata mapendeleo hayo. Kwa nini? Kwa sababu Biblia inaamuru kwamba watumishi wa huduma na wazee wawe na viwango vya juu vya maadili na vya kiroho kabla hawajawekwa rasmi kutumikia. Wanapaswa “wajaribiwe juu ya kufaa kwanza.”—1 Timotheo 3:1-10.

9. Wachungaji waliokomaa wana daraka gani, na kwa nini?

9 Ili ndugu waliobatizwa wajaribiwe, inafaa kwanza wazoezwe. Kwa mfano: Ikiwa mwanafunzi wa shule angeambiwa afanye mtihani mgumu kuhusu somo ambalo hajawahi kufundishwa na walimu, je, angepita mtihani huo? Kuna uwezekano mkubwa kwamba angeanguka. Hivyo, mazoezi yanahitajiwa. Walimu wanaojali huwazoeza wanafunzi si ili wapite mtihani tu bali pia ili watumie ujuzi ambao wamepata. Vivyo hivyo, wazee wenye bidii huwasaidia akina ndugu waliobatizwa wasitawishe sifa ambazo wanaume waliowekwa rasmi wanahitaji kuwa nazo kwa kuwapa mazoezi hususa. Wanafanya hivyo si tu ili kuwasaidia ndugu hao wawekwe rasmi kutumikia, bali pia ili wawe na sifa za kustahili vya kutosha kulitunza kundi. (2 Timotheo 2:2) Bila shaka, lazima akina ndugu waliobatizwa wafanye sehemu yao na kujitahidi kufikia sifa za mtumishi wa huduma au mzee. (Tito 1:5-9) Hata hivyo, wachungaji wenye uzoefu wanaweza kuwasaidia kufanya maendeleo haraka zaidi kwa kuwazoeza kwa hiari wale wanaojitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko.

10, 11. Wachungaji wanaweza kuwazoezaje wengine kwa ajili ya mapendeleo zaidi?

10 Wachungaji wenye uzoefu wanaweza kuwazoezaje wengine kushughulikia migawo kutanikoni? Kwanza, ni kwa kupendezwa na akina ndugu kutanikoni. Hiyo inamaanisha kwenda pamoja nao kwa ukawaida katika huduma ya shambani na kuwasaidia kuboresha uwezo wao wa kulitumia “sawasawa neno la kweli.” (2 Timotheo 2:15) Wachungaji waliokomaa huwaeleza ndugu hao shangwe inayotokana na kuwatumikia wengine na uradhi ambao wao wenyewe wanapata wanapojiwekea miradi ya kiroho na kuifikia. Pia wachungaji huwapa ndugu hao madokezo hususa kwa fadhili ili kuwaonyesha jinsi wanavyoweza kuwa “vielelezo kwa kundi.”—1 Petro 5:3, 5.

11 Ndugu anapowekwa kuwa mtumishi wa huduma, wachungaji wenye hekima huendelea kumzoeza. Bruce, ambaye ametumikia akiwa mzee kwa makumi ya miaka, anasema hivi: “Ninapenda kuketi pamoja na mtumishi wa huduma aliyewekwa rasmi hivi karibuni ili kupitia pamoja naye maagizo yaliyochapishwa na mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Pia, sisi husoma miongozo inayozungumzia mgawo wake hususa, kisha mimi hufanya kazi pamoja naye mpaka anapofahamu majukumu yake.” Mtumishi wa huduma anapopata uzoefu, anaweza pia kuzoezwa kufanya kazi ya uchungaji. Bruce anaendelea kusema hivi: “Ninapoandamana na mtumishi wa huduma kwenye ziara ya uchungaji, mimi humsaidia kuchagua maandiko hususa ambayo yatamtia moyo na kumchochea mtu tunayemtembelea au familia tunayoitembelea. Kujifunza kutumia Maandiko kwa njia inayofikia moyo ni muhimu ili mtumishi wa huduma awe mchungaji stadi.”—Waebrania 4:12; 5:14.

12. Wachungaji wenye uzoefu wanaweza kuwazoezaje wazee waliowekwa rasmi hivi karibuni?

12 Pia, wachungaji waliowekwa rasmi hivi karibuni hufaidika sana wanapopata mazoezi zaidi. Nick, aliyetajwa mwanzoni, anasema: “Mazoezi niliyopata hasa kutoka kwa waangalizi wawili wenye umri mkubwa yalinisaidia sana. Kwa kawaida, ndugu hao walielewa jinsi mambo fulani yanavyopaswa kushughulikiwa. Sikuzote walinisikiliza kwa subira na kufikiria kwa uzito maoni yangu, hata ikiwa hawakukubaliana nayo. Nilijifunza mengi kwa kuona jinsi walivyoshughulika na akina ndugu na dada kutanikoni kwa unyenyekevu na heshima. Wazee hao walinionyesha kwamba ninahitaji kutumia Biblia kwa ustadi ninaposhughulikia matatizo au ninapowatia wengine moyo.”

Kuzoezwa na Neno la Mungu

13. (a) Ndugu anahitaji nini ili awe mchungaji stadi? (b) Kwa nini Yesu alisema hivi: “Yale ninayofundisha si yangu”?

13 Naam, Neno la Mungu, Biblia, lina sheria, kanuni, na mifano ambayo mchungaji anahitaji ili awe ‘na uwezo kamili na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Timotheo 3:16, 17) Huenda ndugu akawa na elimu nyingi, lakini ujuzi wake wa Maandiko na jinsi anavyoyatumia ndio utakaomsaidia kuwa mchungaji stadi. Fikiria mfano wa Yesu. Yeye ndiye mchungaji wa kiroho mwenye ujuzi zaidi, mwenye utambuzi zaidi, na mwenye hekima zaidi kuwahi kuishi duniani. Hata hivyo, hakutegemea hekima yake mwenyewe alipofundisha kondoo za Yehova. Alisema hivi: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” Kwa nini Yesu alielekeza sifa kwa Baba yake wa mbinguni? Alieleza hivi: “Yule ambaye husema mambo aliyotunga yeye mwenyewe anatafuta utukufu wake mwenyewe.”—Yohana 7:16, 18.

14. Wachungaji huepukaje kujitafutia utukufu?

14 Wachungaji washikamanifu huepuka kujitafutia utukufu. Wanapotoa mashauri na wanapowatia wengine moyo, wao hawatumii hekima yao wenyewe bali Neno la Mungu. Wanajua kwamba mgawo wa mchungaji ni kuwasaidia kondoo kupata “akili ya Kristo,” si akili ya wazee. (1 Wakorintho 2:14-16) Kwa mfano, namna gani ikiwa mzee anayewasaidia wenzi fulani kushughulikia matatizo yao ya ndoa anategemeza mashauri yake juu ya mambo aliyojionea maishani badala ya kutumia kanuni za Biblia na habari zilizochapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (Mathayo 24:45) Mashauri yake yanaweza kuathiriwa sana na mila za kwao na ujuzi wake wenye mipaka. Ni kweli kwamba mila nyingine si mbaya, na huenda mzee huyo amejionea mengi maishani. Lakini kondoo hufaidika zaidi wakati wachungaji wanapowatia moyo kusikiliza sauti ya Yesu na maneno ya Yehova badala ya kusikiliza mawazo ya wanadamu au mila.—Zaburi 12:6; Methali 3:5, 6.

Kuzoezwa na “Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara”

15. Yesu alimpa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kazi gani, na ni sababu gani moja ambayo imefanya jamii hiyo ifanikiwe?

15 Wachungaji kama vile mitume Petro, Yohana, na Paulo walikuwa washiriki wa kikundi ambacho Yesu alikitaja kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Jamii hiyo ya mtumwa imefanyizwa na ndugu za Yesu waliotiwa mafuta kwa roho ambao wako duniani, na wana tumaini la kutawala pamoja na Kristo mbinguni. (Ufunuo 5:9, 10) Katika siku hizi za mwisho za mfumo huu, si ajabu kwamba idadi ya ndugu za Kristo waliobaki duniani imepungua. Hata hivyo, kazi ambayo Yesu aliwapa, ya kuhubiri habari njema ya Ufalme kabla mwisho uje, imeongezeka kuliko wakati mwingine wowote. Hata hivyo, jamii ya mtumwa imefanikiwa sana! Kwa nini? Sababu moja ni kwamba wamewazoeza washiriki wa “kondoo wengine” wawasaidie katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. (Yohana 10:16; Mathayo 24:14; 25:40) Leo, sehemu kubwa ya kazi hiyo inafanywa na kikundi hicho chenye ushikamanifu.

16. Jamii ya mtumwa huwazoezaje wanaume waliowekwa rasmi?

16 Jamii ya mtumwa huandaaje mazoezi hayo? Katika karne ya kwanza, wawakilishi wa jamii ya mtumwa waliagizwa wawazoeze na kuwaweka rasmi waangalizi katika makutaniko, kisha waangalizi hao walipaswa kuwazoeza kondoo. (1 Wakorintho 4:17) Utaratibu huo unafuatwa hata leo. Baraza Linaloongoza, yaani, kile kikundi kidogo cha wazee watiwa-mafuta ambao wanawakilisha jamii ya mtumwa, huagiza wawakilishi wake kuwazoeza na kuwaweka rasmi watumishi wa huduma na wazee katika makumi ya maelfu ya makutaniko ulimwenguni pote. Isitoshe, Baraza Linaloongoza hupanga shule za kuwazoeza washiriki wa Halmashauri za Tawi, waangalizi wanaosafiri, wazee, na watumishi wa huduma ili washughulikie kondoo kwa njia bora. Miongozo mingine huandaliwa kupitia barua, makala za Mnara wa Mlinzi, na habari nyingine zinazochapishwa, kama vile kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova. *

17. (a) Yesu ameonyeshaje kwamba anaamini jamii ya mtumwa? (b) Wachungaji wa kiroho wanaweza kuonyeshaje kwamba wanaamini jamii ya mtumwa?

17 Yesu aliiamini sana jamii ya mtumwa hivi kwamba aliiweka juu ya “mali zake zote,” yaani, masilahi yake yote ya kiroho duniani. (Mathayo 24:47) Wachungaji waliowekwa rasmi huonyesha pia kwamba wanaamini jamii ya mtumwa kwa kufuata miongozo inayotolewa na Baraza lake Linaloongoza. Naam, wachungaji wanapowazoeza wengine, wanapokubali kuzoezwa na Neno la Mungu, na wanapotumia mazoezi yanayoandaliwa na jamii ya mtumwa, wanadumisha umoja katika kundi. Tunashukuru kama nini kwamba Yehova amewazoeza wanaume wanaojali sana kila mshiriki wa kutaniko la Kikristo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungejibuje?

• Wachungaji wa kiroho waliokomaa huwazoezaje wengine?

• Kwa nini wachungaji hawafundishi kwa kutegemea maoni yao wenyewe?

• Wachungaji huonyeshaje kwamba wanaamini jamii ya mtumwa, na kwa nini wanafanya hivyo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Wazee Wakristo huwazoeza vijana kutanikoni

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huwaandalia wazee mazoezi kwa njia nyingi