Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uko Tayari Kwa Ajili ya Wokovu?

Je, Uko Tayari Kwa Ajili ya Wokovu?

Je, Uko Tayari Kwa Ajili ya Wokovu?

“Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na nyumba yako yote, kwa maana nimekuona wewe kuwa mwadilifu mbele zangu kati ya kizazi hiki.”—MWANZO 7:1.

1. Katika siku za Noa, Yehova alifanya maandalizi gani ya wokovu?

KATIKA siku za Noa, Yehova ‘alileta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa,’ na pia aliandaa wokovu. (2 Petro 2:5) Mungu wa kweli alimpa Noa aliyekuwa mwadilifu maagizo yaliyo wazi kuhusu jinsi angejenga safina ili kuhifadhi viumbe wakati wa gharika ya ulimwenguni pote. (Mwanzo 6:14-16) Kama vile ambavyo tungetazamia kutoka kwa mtumishi mtiifu wa Yehova, “Noa a[li]fanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru.” Kwa kweli, “alifanya vivyo hivyo.” Utii wa Noa ni mojawapo ya sababu za kuwa kwetu hai leo.—Mwanzo 6:22.

2, 3. (a) Watu walioishi siku za Noa waliitikiaje utendaji wa Noa? (b) Noa aliingia katika safina akiwa na uhakika gani?

2 Kujenga safina hakukuwa kazi rahisi. Inaelekea kwamba watu wengi walishangazwa na mambo ambayo Noa na familia yake walikuwa wakifanya. Hata hivyo, hilo halikutosha kuwasadikisha kwamba wangeweza kuokoka iwapo tu wangeingia katika safina hiyo. Hatimaye, subira ya Mungu kuelekea ulimwengu huo mwovu ikakoma.—Mwanzo 6:3; 1 Petro 3:20.

3 Baada ya Noa na familia yake kufanya kazi ngumu kwa makumi ya miaka, Yehova alimwambia Noa hivi: “Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na nyumba yako yote, kwa maana nimekuona wewe kuwa mwadilifu mbele zangu kati ya kizazi hiki.” Akiwa na imani na uhakika katika neno la Yehova, “Noa akaingia ndani ya safina, yeye na wanawe na mke wake na wake za wanawe pamoja naye.” Yehova aliufunga mlango ili kuwalinda waabudu wake. Maji ya Gharika yalipokuja juu ya dunia, safina hiyo ikawa uandalizi wenye kutegemeka wa Mungu kwa ajili ya wokovu.—Mwanzo 7:1, 7, 10, 16.

Ulinganifu Kati ya Siku za Noa na Leo

4, 5. (a) Yesu alilinganisha wakati wa kuwapo kwake na nini? (b) Siku za Noa zinalingana na siku zetu jinsi gani?

4 “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:37) Yesu alitumia maneno hayo kuonyesha kwamba wakati wa kuwapo kwake kusikoonekana hali zingekuwa kama zilivyokuwa siku za Noa, na kwa kweli ndivyo zilivyo leo. Hasa kuanzia mwaka wa 1919, ujumbe wenye kuonya kama ule uliotolewa na Noa, umekuwa ukitangazwa kwa watu wa mataifa yote. Kwa ujumla, itikio lao limekuwa kama la watu wa siku za Noa.

5 Yehova alitumia Furiko kuchukua hatua dhidi ya ulimwengu ambao ulikuwa ‘umejaa jeuri.’ (Mwanzo 6:13) Kila mtu aliona kwamba Noa na familia yake hawakushiriki jeuri hiyo, badala yake waliendelea kujenga safina kwa amani. Hivyo ndivyo ilivyo leo. Watu wanyoofu wanaweza ‘kuona tofauti kati ya mwadilifu na mwovu, kati ya mtu anayemtumikia Mungu na mtu ambaye hajamtumikia.’ (Malaki 3:18) Unyoofu, fadhili, amani, na bidii ya Mashahidi wa Yehova huwavutia watu wasio na ubaguzi nazo sifa hizo huonyesha tofauti iliyopo kati ya watu wa Mungu na ulimwengu kwa ujumla. Mashahidi hukataa katakata kujihusisha na jeuri ya aina yoyote. Wao huongozwa na roho ya Yehova na hivyo wana amani na wanafuatia uadilifu.—Isaya 60:17.

6, 7. (a) Watu wa siku za Noa walikosa kutambua nini, na hali hiyo inalinganaje na hali ya leo? (b) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba kwa ujumla Mashahidi wa Yehova huonwa kuwa tofauti?

6 Watu walioishi katika siku za Noa hawakutambua kwamba Noa alikuwa akitegemezwa na Mungu naye alifuata mwongozo wake. Kwa hiyo walipuuza ujumbe wake na kukosa kutii onyo lake. Namna gani leo? Ingawa wengi huvutiwa na utendaji na mwenendo wa Mashahidi wa Yehova, wengi wao hupuuza tu habari njema na maonyo ya Biblia. Huenda majirani, waajiri, au watu wa ukoo wakawasifu sana Wakristo wa kweli kwa sababu ya sifa zao nzuri, hata hivyo wao husema, “Inasikitisha tu kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova!” Watu hao hawatambui kwamba Mashahidi huonyesha sifa kama vile upendo, amani, fadhili, wema, upole, na kujizuia kwa sababu wanaongozwa na roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22-25) Sifa nzuri za Mashahidi wa Yehova zinapaswa kuwafanya watu wathamini ujumbe wao.

7 Kwa mfano, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakijenga Jumba la Ufalme nchini Urusi. Mpita-njia mmoja akasimama hapo na kumwambia hivi mjenzi mmoja: “Huu ni mjengo wa ajabu sana—hakuna mtu anayevuta sigara, wala anayewatusi wengine, wala mlevi! Kwani ninyi ni Mashahidi wa Yehova?” Mjenzi huyo akamwuliza, “Nikisema la, utaniamini?” Mtu huyo akamjibu mara moja, “Siwezi.” Katika jiji lingine nchini Urusi, meya wa jiji hilo alivutiwa sana alipowaona Mashahidi wakijenga Jumba lao jipya la Ufalme. Alisema kwamba ingawa awali alikuwa na maoni ya kwamba dini zote ni sawa, baada ya kuona roho ya kujitolea ya Mashahidi wa Yehova, alibadili maoni yake. Hiyo ni mifano miwili tu inayoonyesha kwamba watu wa Yehova ni tofauti na wale ambao hawaishi kulingana na viwango vya Biblia.

8. Ili tuokoke mwisho wa ulimwengu huu mbovu tunapaswa kufanya nini?

8 Kabla “ulimwengu wa kale” haujaharibiwa katika Furiko, Noa alikuwa “mhubiri [mwaminifu] wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Katika hizi siku za mwisho za ulimwengu huu, watu wa Yehova wanawafundisha watu viwango vya Mungu vya uadilifu na kutangaza habari njema za tumaini la kuokolewa kuingia katika ulimwengu mpya. (2 Petro 3:9-13) Noa na familia yake yenye kumwogopa Mungu waliokolewa katika safina. Vivyo hivyo, wokovu leo unategemea kuwa na imani na kushirikiana kwa ushikamanifu na sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova la ulimwenguni pote.

Tunahitaji Imani Ili Kuokolewa

9, 10. Kwa nini tunahitaji kuwa na imani ili tuokoke uharibifu wa ulimwengu huu wa Shetani?

9 Mtu anapaswa kufanya nini ili aokoke uharibifu unaokuja wa ulimwengu huu ulio katika nguvu za Shetani? (1 Yohana 5:19) Lazima atambue kwamba anahitaji ulinzi. Kisha lazima atafute ulinzi huo. Watu wa siku za Noa waliendelea na maisha yao ya kila siku kama kawaida nao hawakuona uhitaji wa ulinzi kutokana na msiba uliokuwa karibu. Walikosa kitu kingine pia—imani katika Mungu.

10 Kwa upande mwingine, Noa na familia yake walitambua kwamba walihitaji kulindwa na kuokolewa. Walikuwa pia na imani katika Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu, Yehova Mungu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Yehova] vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” Paulo aliongezea hivi: “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake; na kupitia imani hiyo aliuhukumu ulimwengu kuwa wenye hatia, naye akawa mrithi wa uadilifu unaolingana na imani.”—Waebrania 11:6, 7.

11. Tunajifunza nini kutokana na ulinzi ambao Yehova aliandaa katika nyakati za kale?

11 Ili tuokoke uharibifu wa ulimwengu huu mbovu, haitoshi tu kuamini kwamba utaharibiwa. Ni lazima tuwe na imani na kutumia kwa hekima maandalizi yote ya Mungu ya kutuokoa. Bila shaka, tunahitaji kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. (Yohana 3:16, 36) Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba ni wale tu waliokuwa ndani ya safina ya Noa ndio waliookoka Gharika. Vivyo hivyo, majiji ya makimbilio katika Israeli la kale yaliandaa ulinzi kwa mtu aliyeua bila kukusudia maadamu tu alikimbilia katika majiji hayo na kuendelea kukaa humo hadi kifo cha kuhani mkuu. (Hesabu 35:11-32) Wakati wa pigo la kumi juu ya Misri katika siku za Musa, wazaliwa wa kwanza wa Wamisri waliuawa, lakini wazaliwa wa Waisraeli waliokoka. Kwa nini? Yehova alikuwa amemwagiza hivi Musa: “Nao [Waisraeli] watachukua sehemu ya damu [ya kondoo wa Pasaka] na kuipaka juu ya miimo miwili ya mlango na sehemu ya juu ya mlango wa nyumba ambamo watamla. . . . Na yeyote kati yenu asitoke nje ya mlango wa nyumba yake mpaka asubuhi.” (Kutoka 12:7, 22) Ni mzaliwa yupi wa kwanza wa Waisraeli angethubutu kupuuza maagizo hayo ya Mungu na kutoka katika nyumba iliyopakwa damu juu ya miimo miwili ya malango na sehemu ya juu ya mlango?

12. Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza swali gani, na kwa nini?

12 Kwa hiyo tuna sababu ya kufikiria kwa uangalifu kuhusu hali yetu. Je, kweli tuko ndani ya mpango wa Yehova wa kutulinda kiroho? Dhiki kuu itakapozuka, wale walio chini ya ulinzi huo watatiririkwa na machozi ya shangwe na shukrani. Wengine watalia machozi ya huzuni na majuto.

Marekebisho ya Hatua kwa Hatua Yatatuwezesha Kuokoka

13. (a) Marekebisho ya kitengenezo yametimiza nini? (b) Eleza baadhi ya marekebisho ya hatua kwa hatua.

13 Yehova amefanya marekebisho ya hatua kwa hatua katika sehemu ya kidunia ya tengenezo lake. Marekebisho hayo yameboresha, yameimarisha, na kufanya mpango wake wa kutulinda kiroho uwe thabiti. Tangu miaka ya 1870 na kitu hadi mwaka wa 1932, wazee na mashemasi walikuwa wakipigiwa kura na washiriki wa kutaniko. Mwaka wa 1932, badala ya kuwa na wazee waliopigiwa kura kukawa na halmashauri ya utumishi iliyopigiwa kura na kutaniko ili kumsaidia mkurugenzi wa utumishi aliyewekwa rasmi. Mwaka wa 1938, mipango ikafanywa ili watumishi wote wa kutaniko wawekwe rasmi kitheokrasi. Chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, tangu mwaka wa 1972, mapendekezo hufanywa na yakikubaliwa, makutaniko hupokea barua zinazowaweka rasmi kitheokrasi waangalizi na watumishi wa huduma. Kadiri ambavyo miaka imepita, kazi ya Baraza Linaloongoza imeongezeka na mabadiliko kadhaa yamefanywa ili kurahisisha kazi yao.

14. Ni programu gani ya mazoezi iliyoanza mwaka wa 1959?

14 Mwaka wa 1950, baada ya kuchunguza kwa makini Zaburi 45:16, programu ya mazoezi ya kuendelea ilianzishwa. Andiko hilo lasema hivi: “Mahali pa mababu zako patachukuliwa na wana wako, ambao utawaweka kuwa wakuu katika dunia yote.” Wazee wanaoongoza makutaniko leo wanazoezwa kwa ajili ya majukumu mbalimbali ya kitheokrasi ya leo na baada ya Har-magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Shule ya Huduma ya Ufalme ilianzishwa mwaka wa 1959. Wakati huo, ilikuwa shule ya mwezi mzima kwa ajili ya watumishi wa kutaniko, ambao leo huitwa waangalizi-wasimamizi. Leo, shule hiyo huwafundisha waangalizi wote na watumishi wa huduma. Ndugu hao nao huwafundisha Mashahidi wa Yehova mmoja-mmoja katika makutaniko yao. Hivyo, wote husaidiwa kiroho kuongeza ustadi katika huduma yao wakiwa watangazaji wa habari njema ya Ufalme.—Marko 13:10.

15. Usafi wa kutaniko la Kikristo hudumishwa katika njia gani mbili?

15 Watu wanaotaka kuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo wanapaswa kutimiza matakwa fulani. Hivyo, wadhihaki wa leo hufungiwa nje, kama vile wadhihaki wa siku za Noa walivyozuiwa kuingia ndani ya safina. (2 Petro 3:3-7) Hasa tangu mwaka wa 1952, Mashahidi wa Yehova wameunga mkono mpango unaosaidia kulinda kutaniko, yaani, kuwatenga na ushirika watenda-dhambi wasiotubu. Bila shaka, wakosaji wanaotubu kikweli husaidiwa kwa upendo ‘kuifanyia miguu yao mapito yaliyonyooka.’—Waebrania 12:12, 13; Methali 28:13; Wagalatia 6:1.

16. Hali ya kiroho ya watu wa Yehova ikoje?

16 Haishangazi kwamba watu wa Yehova wamepata ufanisi wa kiroho. Ufanisi huo haukutokea wenyewe tu. Kupitia nabii Isaya, Yehova alisema hivi: “Tazama! Watumishi wangu watakula, lakini ninyi mtakuwa na njaa. Tazama! Watumishi wangu watakunywa, lakini ninyi mtakuwa na kiu. Tazama! Watumishi wangu watashangilia, lakini ninyi mtaona aibu. Tazama! Watumishi wangu watapiga vigelegele kwa shangwe kwa sababu ya hali nzuri ya moyo, lakini ninyi mtalia kwa sababu ya maumivu ya moyo nanyi mtapiga mayowe kwa sababu ya mvunjiko kabisa wa roho.” (Isaya 65:13, 14) Yehova anaendelea kutupa chakula tele cha kiroho, chenye lishe na cha wakati unaofaa, ambacho hutupa nguvu kiroho.—Mathayo 24:45.

Uwe Tayari kwa Ajili ya Wokovu

17. Ni nini kitakachotusaidia kujitayarisha kwa ajili ya wokovu?

17 Kuliko wakati mwingine wowote, huu ndio wakati wa ‘kufikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo.’ (Waebrania 10:23-25) Kushirikiana sana na mojawapo ya makutaniko zaidi ya 98,000 ya Mashahidi wa Yehova na kuendelea kuwa watendaji, kutatusaidia kujitayarisha kwa ajili ya wokovu. Tutategemezwa na waamini wenzetu tunapojitahidi kuonyesha “utu mpya” na kufanya kila tuwezalo ili kuwasaidia wengine wajifunze juu ya maandalizi ya Yehova ya wokovu.—Waefeso 4:22-24; Wakolosai 3:9, 10; 1 Timotheo 4:16.

18. Kwa nini umeazimia kukaa karibu na kutaniko la Kikristo?

18 Shetani na ulimwengu wake mbovu hutamani sana kutushawishi tuliache kutaniko la Kikristo. Hata hivyo, tunaweza kuendelea kuwa sehemu ya kutaniko hilo na kuokoka mwisho wa ulimwengu huu mbovu. Upendo wetu kwa Yehova na kuthamini maandalizi yake yenye upendo na vituchochee kuazimia hata zaidi kuzipinga jitihada za Shetani. Kutafakari baraka tulizo nazo leo kutaimarisha azimio letu. Baadhi ya baraka hizo zitazungumziwa katika makala inayofuata.

Ungejibuje?

• Nyakati zetu zinalinganaje na siku za Noa?

• Ni sifa gani inayohitajiwa ili kuokoka?

• Ni marekebisho gani ya hatua kwa hatua yameimarisha mpango wa Yehova wa kutulinda?

• Sisi binafsi tunaweza kujitayarishaje kwa ajili ya wokovu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Watu walioishi siku za Noa hawakutilia maanani ujumbe wake

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kuna faida ya kuchukua kwa uzito maonyo ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Shule ya Huduma ya Ufalme hutimiza nini?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Huu ndio wakati wa kukaa karibu na kutaniko la Kikristo