Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Una “Uhuru wa Kusema”?

Je, Wewe Una “Uhuru wa Kusema”?

Je, Wewe Una “Uhuru wa Kusema”?

ZAIDI ya watu milioni sita katika nchi 235 wana kile kinachoitwa katika Biblia “uhuru wa kusema.” Maneno hayo yanapatikana mara 16 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. (Wafilipi 1:20; 1 Timotheo 3:13; Waebrania 3:6; 1 Yohana 3:21) “Uhuru wa kusema” unahusisha nini? Tunaweza kuupataje? Tunaweza kuwa na uhuru wa kusema katika mambo gani?

Kulingana na Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uhuru wa kusema” linamaanisha “uhuru wa usemi, kuongea bila woga, . . . kusema kwa ujasiri; humaanisha pia, uhakika, ujasiri mchangamfu, uhodari, na neno hilo halihusiani kila mara na usemi.” Hata hivyo, hatupaswi kufikiri kimakosa kwamba uhuru wa kusema humaanisha kusema bila kufikiri au kusema kwa ukaidi. Biblia inatuambia: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote.” (Wakolosai 4:6) Uhuru wa kusema unahusisha kutumia busara bila kuruhusu hali zenye kuvunja moyo au woga wa mwanadamu utuzuie tusizungumze.

Je, mtu huzaliwa akiwa na uhuru wa kusema? Fikiria maneno ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo huko Efeso. Alisema hivi: “Mimi, niliye mtu mdogo kuliko aliye mdogo zaidi kati ya watakatifu wote, nilipewa fadhili hizi zisizostahiliwa, ili niwatangazie mataifa habari njema juu ya utajiri usiopimika wa Kristo.” Paulo aliongeza kusema kwamba kupitia Yesu Kristo “tuna uhuru huu wa kusema na tuna uwezo wa kukaribia tukiwa na uhakika kupitia imani yetu katika yeye.” (Waefeso 3:8-12) Uhuru wa kusema hutokana na uhusiano wa mtu na Yehova Mungu unaotegemea imani katika Yesu Kristo, wala mtu hazaliwi akiwa nao. Na tuone kinachoweza kutusaidia kupata uhuru huo na jinsi tunavyoweza kuutumia tunapohubiri, tunapofundisha, na tunaposali.

Ni Nini Kinachotusaidia Kuhubiri kwa Ujasiri?

Yesu Kristo ndiye kielelezo bora zaidi cha mtu aliyetumia uhuru wake wa kusema. Bidii yake ilimchochea kutumia nafasi alizopata ili kuhubiri. Iwe alikuwa akipumzika, akila nyumbani kwa mtu fulani, au akitembea barabarani, hakukosa kamwe kutumia nafasi alizopata kuzungumza kuhusu Ufalme wa Mungu. Yesu hakunyamazishwa na dhihaka wala upinzani wa moja kwa moja. Badala yake, aliwashutumu kwa ujasiri viongozi wa dini za uwongo. (Mathayo 23:13-36) Hata alipokamatwa na kushtakiwa, Yesu alisema bila woga.—Yohana 18:6, 19, 20, 37.

Mitume wa Yesu pia walijifunza kusema kwa uhuru. Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., Petro alisema kwa uhuru mbele ya umati wa watu zaidi ya 3,000. Muda mfupi mapema, aliogopa alipotambuliwa na kijakazi. (Marko 14:66-71; Matendo 2:14, 29, 41) Walipoburutwa mbele ya viongozi wa kidini, Petro na Yohana hawakujikunyata kwa woga. Hawakusita kutoa ushahidi kwa ujasiri kumhusu Yesu Kristo aliyefufuliwa. Viongozi wa kidini walitambua kwamba Petro na Yohana walikuwa pamoja na Yesu kwa sababu ya maneno yao ya waziwazi. (Matendo 4:5-13) Ni nini kilichowawezesha kuongea kwa ujasiri?

Yesu alikuwa amewaahidi hivi mitume wake: “Watakapowapeleka ninyi, msihangaike juu ya jambo mtakalosema au jinsi mtakavyolisema; kwa maana mtapewa jambo la kusema katika saa hiyo; kwa maana wanaosema si ninyi tu, bali ni roho ya Baba yenu inayosema kupitia ninyi.” (Mathayo 10:19, 20) Roho takatifu ilimsaidia Petro na wengine kushinda haya au woga wowote ambao ungewazuia kusema kwa uhuru. Roho hiyo yenye nguvu nyingi inaweza kutusaidia sisi pia.

Zaidi ya hayo, Yesu aliwapa wafuasi wake utume wa kufanya wanafunzi. Alikuwa na haki ya kufanya hivyo kwa sababu Yeye ndiye ambaye amepewa “mamlaka yote mbinguni na duniani.” Naye angekuwa ‘pamoja nao.’ (Mathayo 28:18-20) Kwa kuwa walijua kwamba Yesu alikuwa pamoja nao, wanafunzi wa karne ya kwanza walikuwa na ujasiri wa kukabiliana na wenye mamlaka waliojaribu kuzuia kazi yao ya kuhubiri. (Matendo 4:18-20; 5:28, 29) Kujua hivyo kunaweza kuwa na matokeo yaleyale kwetu.

Paulo alitaja sababu nyingine ya kuwa na uhuru wa kusema alipohusianisha tumaini na “uhuru mkubwa wa kusema.” (2 Wakorintho 3:12; Wafilipi 1:20) Kwa kuwa ujumbe wa tumaini ulikuwa mzuri sana, Wakristo walihitaji kuwajulisha wengine. Kwa kweli, tumaini letu linatuchochea kuwa na uhuru wa kusema.—Waebrania 3:6.

Kuhubiri kwa Ujasiri

Tunaweza kuhubirije kwa ujasiri hata tunapokabili hali ngumu? Fikiria mfano wa mtume Paulo. Alipokuwa mfungwa huko Roma, aliwaomba waamini wenzake wasali ili ‘apewe uwezo wa kusema kwa kufungua kinywa chake, ili aweze kusema kuhusiana nayo kwa ujasiri kama anavyopaswa kusema.’ (Waefeso 6:19, 20) Je, sala hizo zilijibiwa? Ndiyo! Alipokuwa gerezani, Paulo aliendelea ‘kuhubiri ufalme wa Mungu . . . kwa uhuru wa kusema ulio mkubwa zaidi, bila kizuizi.’—Matendo 28:30, 31.

Kutumia nafasi tunazopata kutoa ushahidi kazini, shuleni, au tunaposafiri kwaweza kupima uhuru wetu wa kusema. Huenda tukanyamaza kwa sababu ya haya au kuogopa jinsi wengine watakavyoitikia, au kwa sababu tunatilia shaka uwezo wetu. Tena, mtume Paulo anatuwekea kielelezo kizuri. Alisema hivi: “Tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu ili kuwaambia ninyi habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.” (1 Wathesalonike 2:2) Kwa kuwa alimtegemea Yehova, Paulo alifanya mambo ambayo hangeweza kufanya kwa uwezo wake mwenyewe.

Sala ilimsaidia Sherry kuwa na ujasiri wa kutoa ushahidi nafasi ilipojitokeza. Siku moja alipokuwa akimsubiri mume wake arudi kutoka katika shughuli fulani, alimwona mwanamke mwingine akiwa anasubiri pia. “Nikiwa na wasiwasi mwingi,” asema Sherry, “nilimwomba Yehova anipe ujasiri.” Sherry alipomkaribia mwanamke huyo, kasisi Mbaptisti akafika. Sherry hakutarajia kukutana na kasisi. Hata hivyo, alisali tena naye akapata ujasiri wa kutoa ushahidi. Alimwachia mwanamke huyo vichapo na kupanga ziara ya kurudia. Tunapotumia nafasi zinazojitokeza ili kutoa ushahidi, tunaweza kuwa na hakika kwamba kumtegemea Yehova kutatusaidia kusema kwa uhuru.

Tunapofundisha

Uhuru wa kusema unahusiana sana na kufundisha. Kuhusu “wanaume wanaohudumu kwa njia nzuri” kutanikoni, Biblia inasema hivi: “Wanajipatia wenyewe msimamo mzuri na uhuru mwingi wa kusema katika imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (1 Timotheo 3:13) Wanajipatia uhuru huo wa kusema kwa kutumia maishani mwao wenyewe mambo wanayowafundisha wengine. Kufanya hivyo hulinda na kuimarisha kutaniko.

Tunapokuwa na uhuru wa kusema kwa njia hiyo, shauri letu linakuwa na matokeo zaidi na yaelekea kwamba litafuatwa. Badala ya kukengeushwa na mfano mbaya, wasikilizaji wanatiwa moyo wanapoona faida za mambo wanayofundishwa. Uhuru huo huwawezesha wale walio na sifa za kiroho ‘kumrekebisha upya ndugu yao’ kabla tatizo halijatia mizizi. (Wagalatia 6:1) Kwa upande mwingine, mtu anayeweka mfano mbaya huenda akasita kusema, akihisi kwamba hana haki ya kuzungumza. Kuchelewa kutoa shauri linalohitajiwa kwaweza kuleta msiba.

Kusema kwa ujasiri hakumaanishi tuwe wachambuzi, wenye kushikilia au kusisitiza maoni yetu. Paulo alimhimiza Filemoni “kwa msingi wa upendo.” (Filemoni 8, 9) Nayo maneno ya mtume huyo yalikuwa na matokeo mazuri. Kwa kweli, shauri lolote ambalo mzee atatoa, lapaswa kuchochewa na upendo!

Bila shaka, uhuru wa kusema ni muhimu wakati shauri linapotolewa. Ni muhimu pia nyakati nyinginezo. Paulo aliliandikia hivi kutaniko la Korintho: “Nina uhuru mkubwa wa kusema kuwaelekea ninyi. Ninajisifu kwa njia kubwa kuhusiana nanyi.” (2 Wakorintho 7:4) Paulo hakusita kuwapongeza ndugu na dada zake walipostahili pongezi. Upendo ulimchochea akazie sifa nzuri za waabudu wenzake, ingawa alijua udhaifu wao. Vivyo hivyo, kutaniko la Kikristo leo hujengwa wazee wanapowapongeza na kuwatia moyo sana ndugu na dada zao.

Ili kufundisha kwa matokeo, Wakristo wote wanahitaji kuwa na uhuru wa kusema. Sherry, aliyetajwa awali, alitaka kuwatia moyo watoto wake watoe ushahidi shuleni. “Hata ingawa nililelewa katika kweli,” anakiri, “sikuwa na mazoea ya kutoa ushahidi shuleni. Na kwa kawaida sihubiri isivyo rasmi. Nilijiuliza hivi, ‘Ni kielelezo cha aina gani ninachowawekea watoto wangu?’” Jambo hilo lilimchochea Sherry kujitahidi zaidi kuhubiri isivyo rasmi.

Naam, wengine wanatutazama nao huona tukikosa kutenda yale tunayofundisha. Basi, na tujipatie uhuru wa kusema kwa kujitahidi kutenda yale tunayofundisha.

Katika Sala

Uhuru wa kusema ni muhimu hasa tunaposali kwa Yehova. Tunaweza kwa uhuru kumweleza Yehova mambo yote yaliyo moyoni mwetu tukiwa na uhakika kwamba anasikiliza sala zetu naye atazijibu. Tukifanya hivyo tunakuwa na uhusiano mzuri na wa karibu pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Hatupaswi kamwe kusita kusali kwa Yehova, huku tukifikiri kwamba sisi ni watu duni. Tufanye nini ikiwa kosa au dhambi fulani inatufanya tuhisi hatia na kushindwa kusali kutoka moyoni? Je, bado tunaweza kusali kwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu kwa uhuru?

Sababu nyingine inayotufanya tuwe na uhakika tunaposali ni cheo cha juu cha Yesu akiwa Kuhani Mkuu. Andiko la Waebrania 4:15, 16 lasema hivi: “Tuna kuhani mkuu, si mtu ambaye hawezi kuusikitikia udhaifu wetu, bali yeye ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na dhambi. Basi na tukikaribie, tukiwa na uhuru wa kusema, kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa, ili tupokee rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa.” Kifo cha Yesu na jukumu lake akiwa Kuhani Mkuu hutuwezesha kuwa na uhuru wa kusema.

Tukijitahidi kwa moyo wote kumtii Yehova, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atajibu sala zetu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Wapendwa, ikiwa mioyo yetu haituhukumu kuwa na hatia, tuna uhuru wa kusema kwa Mungu; na chochote kile tunachoomba tunapokea kutoka kwake, kwa sababu tunazishika amri zake na tunafanya mambo yanayopendeza machoni pake.”—1 Yohana 3:21, 22.

Kumfikia Yehova kwa uhuru katika sala humaanisha kwamba tunaweza kumwambia chochote. Tunaweza kumweleza Yehova mambo yoyote yanayotutia wasiwasi, yanayotuhangaisha, au yanayotuogopesha, tukiwa na hakika kwamba hatakosa kamwe kusikiliza sala zetu za kutoka moyoni. Hata ikiwa tumefanya dhambi nzito, tukitubu kikweli, hisia za hatia hazipaswi kutuzuia kusali.

Zawadi isiyostahiliwa ya uhuru wa kusema ni yenye thamani sana. Tunaweza kuitumia kumtukuza Mungu tunapohubiri na kufundisha na tunapomkaribia zaidi katika sala. ‘Tusitupilie mbali uhuru wetu wa kusema, ulio na thawabu kubwa ya kulipwa’—thawabu ya uzima wa milele.—Waebrania 10:35.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mtume Paulo alisema kwa ujasiri

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ili kufundisha kwa matokeo tunahitaji kuwa na uhuru wa kusema

[Picha katika ukurasa wa 16]

Uhuru wa kusema katika sala ni muhimu