Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusudi la Mungu Kuelekea Dunia Litatimizwa Karibuni

Kusudi la Mungu Kuelekea Dunia Litatimizwa Karibuni

Kusudi la Mungu Kuelekea Dunia Litatimizwa Karibuni

WAKATI Adamu na Hawa walipokuwa katika paradiso, walipewa agizo hili: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.”—Mwanzo 1:28.

Kuitiisha dunia kulimaanisha mengi zaidi ya kulima au kutunza sehemu ndogo. Adamu na Hawa na watoto wao walipaswa kuifanya dunia nzima iwe Paradiso. Hata hivyo, wenzi hao wawili wa kwanza walifanya dhambi nao wakafukuzwa kutoka katika bustani ya Edeni. (Mwanzo 3:23, 24) Lakini hilo halikumaanisha kwamba dunia haitapata kutiishwa.

Kwa kuwa watabarikiwa na Mungu, wanadamu watiifu wataweza kuitiisha dunia. Waisraeli wa kale walipokuwa na kibali cha Mungu, mashamba yao yalizaa chakula na matunda mazuri kwa wingi. Ndivyo itakavyokuwa wakati ambapo dunia nzima itakuwa paradiso. Kama inavyoahidiwa katika Neno la Mungu, Biblia, “hakika dunia itatoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.” (Zaburi 67:6) Hivyo, malisho ya wanyama na milima, miti na maua, mito na bahari, zitashangilia. (Zaburi 96:11-13; 98:7-9) Dunia yetu itajawa na mimea inayonawiri, ndege maridadi, wanyama wenye kupendeza, na watu wachangamfu.

Ulimwengu Mpya Uko Karibu!

Tunakaribia sana kuingia katika ulimwengu mpya ulioahidiwa na Yehova Mungu. Mtume Petro aliandika hivi: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Baada ya kusoma maneno hayo ya Petro, huenda watu fulani wakakata kauli kwamba dunia hii haitapata kamwe kuwa paradiso. Huenda wakafikiri kwamba Mungu ataumba mbingu na dunia nyingine. Je, ndivyo itakavyokuwa?

“Mbingu mpya” ni nini? Si mbingu halisi zilizoumbwa na Mungu. (Zaburi 19:1, 2) Petro alikuwa ametangulia kutaja “mbingu” za mfano, yaani, serikali za wanadamu ambazo zimekwezwa au kuinuliwa juu ya raia zake. (2 Petro 3:10-12) “Mbingu” hizo zimewakatisha tamaa wanadamu nazo zitapitilia mbali. (Yeremia 10:23; Danieli 2:44) “Mbingu mpya” zitakazochukua mahali pake ni Ufalme wa Mungu. Mfalme Yesu Kristo na wale 144,000 ambao ni warithi pamoja naye waliofufuliwa wakaishi mbinguni, ndio watakaokuwa wafalme katika Ufalme huo.—Waroma 8:16, 17; Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3.

“Dunia mpya” ambayo Petro anataja si sayari mpya. Yehova aliumba dunia kwa njia ambayo wanadamu wanaweza kuishi humo milele. (Zaburi 104:5) Wakati mwingine, Biblia hutumia neno “dunia” inapozungumza kuhusu wanadamu. (Mwanzo 11:1) Dunia itakayoharibiwa hivi karibuni, ni watu ambao wamejifanya wenyewe kuwa sehemu ya ulimwengu huu mbovu. Vivyo hivyo, ulimwengu mbovu au watu wasiomwogopa Mungu waliharibiwa wakati wa Gharika ya siku za Noa. (2 Petro 3:5-7) Basi “dunia mpya” ni nini? Ni jamii mpya ya watu, yaani, waabudu wa kweli wa Mungu walio “wanyoofu mioyoni mwao.” (Zaburi 125:4; 1 Yohana 2:17) Sheria zote za “dunia mpya” zitatoka katika “mbingu mpya.” Wanaume waaminifu duniani watahakikisha kwamba sheria hizo zinafuatwa.

Mabadiliko Mapya na ya Ajabu!

Hapana shaka kwamba Yehova alitupa makao maridadi alipoiumba dunia ili ikaliwe na wanadamu. Yeye mwenyewe alisema kwamba kila kitu alichoumba duniani “kilikuwa chema sana.” (Mwanzo 1:31) Shetani Ibilisi aliwaongoza Adamu na Hawa waasi. (Mwanzo 3:1-5; Ufunuo 12:9) Hata hivyo, karibuni Mungu atachukua hatua kuhakikisha kwamba wanyoofu wanapata “uzima ulio wa kweli.” Huo ni, “uzima wa milele” chini ya hali kamilifu katika Paradiso. (1 Timotheo 6:12, 19) Hebu sasa tuchunguze baadhi ya baraka ambazo watu watafurahia wakati huo.

Wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu, Shetani atafungwa naye hataweza kuwasababishia wanadamu ole. Mtume Yohana anasema: “Nami nikamwona malaika [Mikaeli, yule malaika mkuu au Yesu Kristo] akishuka kutoka mbinguni mwenye ufunguo wa abiso na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Naye akamkamata yule joka mkubwa, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, na kumfunga kwa miaka elfu. Naye akamtupa ndani ya abiso na kuifunga na kuitia muhuri juu yake, ili asipotoshe mataifa tena mpaka ile miaka elfu itakapokwisha.” (Ufunuo 20:1-3; 12:12) Mbali na kufurahia uhuru kutokana na uvutano wa Shetani akiwa abiso, wanadamu watafurahia baraka nyingine nyingi chini ya utawala wa Ufalme.

Uovu, jeuri, na vita havitakuwapo tena. Biblia inaahidi hivi: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani. Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:10, 11, 29) Yehova Mungu ‘atakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9) Bila shaka, kutakuwa na usalama na amani!

Tutakuwa na chakula tele kitamu na chenye afya. Mtunga-zaburi alisema hivi katika wimbo: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Wakati huo, hakuna mtu atakayekuwa na maumivu makali ya njaa.

Hakuna mtu atakayekuwa mgonjwa. Bila shaka, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24; 35:5, 6) Yesu Kristo alipokuwa duniani, aliwaponya wenye ukoma, walemavu, na vipofu. (Mathayo 9:35; Marko 1:40-42; Yohana 5:5-9) Bila shaka, atafanya mengi zaidi katika ulimwengu mpya! Hebu wazia shangwe itakayokuwapo wakati ambapo vipofu, viziwi, walemavu, na mabubu watakapoponywa.

Matatizo yanayosababishwa na uzee yataondolewa hatua kwa hatua kadiri wanadamu watiifu watakavyokuwa wakamilifu. Hakutakuwa tena na miwani, mikongojo, magongo ya kutembelea, viti vya magurudumu, hospitali, wala madawa. Mwili wetu utabadilika sana nguvu zetu za ujanani zitakaporudishwa! (Ayubu 33:25) Kila asubuhi tutaamka tukiwa tumeburudika na tayari kuanza siku nyingine ya utendaji wenye shangwe.

Ufufuo wa wapendwa wetu na watu wengine utatuletea shangwe moyoni. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Itasisimua kama nini kuwakaribisha Abeli, Noa, Abrahamu, Sara, Ayubu, Musa, Ruthu, Daudi, Eliya, Esta, na wengine wengi! Mamilioni ya wengine watafufuliwa pia. Wengi wao hawakujifunza kumhusu Yehova, lakini watakaribishwa na watu wenye hamu ya kuwafundisha kumhusu Mungu, makusudi yake, na kumhusu Mwana wake, Yesu Kristo. Ujuzi kumhusu Yehova utaijaza dunia kabisa kadiri watu watakaofufuliwa watakavyomjua Muumba wao.

Jambo bora kabisa ni kwamba tutaweza kumwabudu Mungu wa pekee wa kweli milele. Tutapata pendeleo la ‘kumtumikia Yehova kwa kushangilia,’ na tutashirikiana kujenga nyumba maridadi, kulima, na hatimaye kuitiisha dunia nzima. (Zaburi 100:1-3; Isaya 65:21-24) Kuishi milele katika paradiso yenye kuvutia, yenye kusitawi, na yenye amani ambayo inaleta utukufu kwa jina takatifu la Yehova kutakuwa jambo lenye kupendeza kama nini!—Zaburi 145:21; Yohana 17:3.

Jaribu la Mwisho kwa Wanadamu

Wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu, Yesu atatumia faida za dhabihu yake ya fidia kwa wanadamu watiifu. Mwishowe, dhambi yote itakuwa imeondolewa na wanadamu watakuwa wakamilifu. (1 Yohana 2:2; Ufunuo 21:1-4) Baada ya matokeo ya dhambi ya Adamu kuondolewa kabisa, wanadamu wakamilifu watatimiza viwango vya Mungu, kimwili, kihisia, kiadili, na kiroho. Hivyo, ‘watakuwa hai’ kikamili wanapofikia hali ya ukamilifu isiyo na dhambi. (Ufunuo 20:5) Ukamilifu huo na dunia Paradiso zitamletea Mungu utukufu ulioje!

Baada ya Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu, Shetani Ibilisi pamoja na roho wake waovu, au malaika waovu, watafunguliwa kwa muda mfupi kutoka katika abiso ambamo walitupwa mwanzoni mwa miaka hiyo elfu. (Ufunuo 20:1-3) Wataruhusiwa kujaribu kwa mara ya mwisho kuwageuza watu waache kumwabudu Mungu. Ingawa baadhi ya watu watashindwa na tamaa mbaya, uasi huo hautafaulu. Yehova atawaangamiza watu wenye ubinafsi pamoja na Shetani na roho wake wote waovu. Uovu hautakuwapo tena kamwe. Watenda-maovu wote wataangamizwa milele, na waadilifu watapokea uzima wa milele.—Ufunuo 20:7-10.

Je, Utakuwapo?

Wale wanaompenda Yehova Mungu wana tumaini la kuishi milele kwa furaha. Maisha katika Paradiso hayatakuwa yenye kuchosha kamwe. Badala yake, maisha yatazidi kuwa yenye kupendeza siku baada ya siku, kwa kuwa hakutakuwa na mwisho wa kujifunza kumhusu Yehova Mungu. (Waroma 11:33) Sikuzote utajifunza jambo jipya, nawe utakuwa na wakati wa kutosha wa kujifunza. Kwa nini? Kwa sababu utaishi, si kwa miaka 70 au 80 tu, bali milele.—Zaburi 22:26; 90:10; Mhubiri 3:11.

Ikiwa unampenda Mungu, sikuzote utafurahia kufanya mapenzi yake. Mtume Yohana aliandika: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Kwa hiyo, usiruhusu chochote kikuzuie kuishi maisha ya uadilifu na hivyo kumpendeza Yehova Mungu. Usisahau kamwe tumaini zuri ajabu linaloahidiwa katika Neno la Mungu, Biblia. Amua kutoka moyoni kufanya mapenzi ya Yehova, nawe usiache kamwe kufanya hivyo. Ukifanya hivyo, utakuwapo wakati ambapo kusudi la Mungu kuelekea dunia litatimizwa nayo makao yetu yawe paradiso milele.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Waisraeli wa kale walipokuwa na kibali cha Mungu, mashamba yao yalizaa chakula na matunda kwa wingi

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ni mambo gani unayotazamia kufurahia katika Paradiso?