Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kwanza cha Zaburi

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kwanza cha Zaburi

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kwanza cha Zaburi

UNGEKIPA jina gani kitabu cha Biblia ambacho kimejaa sifa kwa Muumba wetu, Yehova Mungu? Hakuna jina linalofaa zaidi kuliko Zaburi, au Sifa. Kitabu hicho ambacho ndicho kirefu zaidi katika Biblia kina nyimbo zilizotungwa kwa ustadi ambazo husimulia sifa za ajabu za Mungu na matendo yake yenye nguvu, hali kadhalika unabii mbalimbali. Nyingi kati ya nyimbo hizo huonyesha hisia walizokuwa nazo waandikaji walipokabili matatizo. Maneno hayo yanahusisha kipindi cha wakati cha miaka elfu moja hivi, tangu siku za nabii Musa hadi nyakati za baada ya uhamisho. Kiliandikwa na Musa, Mfalme Daudi, na wengine. Yasemekana kwamba kuhani Ezra ndiye aliyepanga kitabu hicho jinsi kilivyo leo.

Tangu nyakati za kale, kitabu cha Zaburi kiligawanywa katika mikusanyo mitano au sehemu, za nyimbo: (1) Zaburi 1-41; (2) Zaburi 42-72; (3) Zaburi 73-89; (4) Zaburi 90-106; na (5) Zaburi 107-150. Makala hii itazungumzia mkusanyo wa kwanza. Isipokuwa zaburi tatu, nyingine zote katika sehemu hii yasemekana kwamba ziliandikwa na Mfalme Daudi wa Israeli la kale. Waliotunga Zaburi 1, 10, na 33 hawajulikani.

“MUNGU WANGU NI MWAMBA WANGU”

(Zaburi 1:1–24:10)

Baada ya zaburi ya kwanza kutangaza kwamba mwenye furaha ni mtu anayependezwa na sheria ya Yehova, zaburi ya pili huingia moja kwa moja katika suala la Ufalme. * Zaburi hizi zina sihi nyingi kwa Mungu. Kwa mfano, Zaburi ya 3-5, 7, 12, 13, na 17, ni sihi za kuomba ukombozi dhidi ya adui. Zaburi ya 8 hukazia ukuu wa Yehova ukilinganishwa na uduni wa mwanadamu.

Akimfafanua Yehova kuwa Mlinzi wa watu wake, Daudi aimba hivi: “Mungu wangu ni mwamba wangu. Nitamkimbilia.” (Zaburi 18:2) Yehova anasifiwa akiwa Muumba na Mpaji-Sheria katika Zaburi ya 19, akiwa Mwokozi katika Zaburi ya 20, na akiwa Mwokozi wa Mfalme wake aliyetiwa mafuta katika Zaburi ya 21. Zaburi ya 23 inamfafanua kuwa Mchungaji Mkuu, nayo Zaburi ya 24 inamwonyesha akiwa Mfalme mtukufu.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:1, 2—Ni ‘jambo gani la upuuzi’ ambalo mataifa yanaendelea kusema? “Jambo la upuuzi” ni kwamba serikali za kibinadamu zimehangaikia daima kuendeleza mamlaka yao. Huo ni upuuzi kwa sababu kusudi lao halitafua dafu. Je, kweli vikundi vya mataifa vyaweza kutazamia kufanikiwa vinapochukua msimamo “dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake”?

2:7—“Agizo la Yehova” ni nini? Agizo hilo ni agano la Ufalme, ambalo Yehova amefanya pamoja na Mwana wake mpendwa, Yesu Kristo.—Luka 22:28, 29.

2:12—Watawala wa mataifa wanaweza ‘kumbusu mwana’ jinsi gani? Katika nyakati za Biblia, kubusu kulikuwa ishara ya urafiki na uaminifu. Kulikuwa njia ya kuwakaribisha wageni. Wafalme wa dunia wanaagizwa wambusu Mwana, yaani, wamkaribishe akiwa Mfalme wa Kimasihi.

3:utangulizi—Utangulizi katika baadhi ya zaburi una kusudi gani? Nyakati nyingine utangulizi humtambulisha mwandikaji na/au hutoa habari kuhusu hali ilivyokuwa wakati wa kutungwa kwa zaburi hiyo, kama ilivyo katika Zaburi ya 3. Utangulizi waweza pia kueleza kusudi au matumizi ya wimbo fulani hususa (Zaburi ya 4 na ya 5) na pia kutoa maagizo ya wimbo (Zaburi ya 6).

3:2“Sela” ni nini? Kwa ujumla inadhaniwa kwamba neno hilo huwakilisha kituo katika uimbaji peke yake au kutia ndani vyombo vya muziki, ili kutafakari kimya. Kituo hicho kilitumiwa ili kukazia wazo au hisia zilizotoka tu kuimbwa. Hakuna haja ya kulisoma neno hilo kwa sauti Zaburi zinaposomwa hadharani.

11:3—Ni misingi gani inayobomolewa? Ni misingi inayotegemeza jamii ya wanadamu, yaani, sheria, utengamano, na haki. Misingi hiyo inapovurugwa, kunakuwa na misukosuko ya kijamii na ukosefu wa haki. Katika hali hizo, “yeyote aliye mwadilifu” anapaswa kumtumaini Mungu kabisa.—Zaburi 11:4-7.

21:3—“Taji la dhahabu safi” lina umuhimu gani? Biblia haitaji ikiwa taji hilo lilikuwa halisi au liliwakilisha utukufu zaidi aliopata Daudi baada ya ushindi mwingi vitani. Hata hivyo, mstari huo ni unabii unaohusu taji la ufalme ambalo Yesu alipokea kutoka kwa Yehova mwaka wa 1914. Taji hilo ni la dhahabu ili kuonyesha kwamba utawala wake ndio utawala bora zaidi.

22:1, 2—Kwa nini Daudi alihisi kwamba Yehova amemwacha? Daudi alikuwa na mikazo mingi sana kutoka kwa adui zake hivi kwamba ‘moyo wake ulikuwa kama nta na uliyeyuka ndani katika sehemu zake za ndani.’ (Zaburi 22:14) Huenda aliona ni kana kwamba Yehova amemwacha. Alipotundikwa mtini, Yesu pia alihisi hivyohivyo. (Mathayo 27:46) Maneno ya Daudi yanaonyesha hisia zake kuelekea hali ngumu aliyokabili. Hata hivyo, katika sala yake iliyoandikwa katika Zaburi 22:16-21, ni wazi kwamba Daudi hakupoteza imani katika Mungu.

Mambo Tunayojifunza:

1:1. Tunapaswa kuepuka kushirikiana na wale wasiompenda Yehova.—1 Wakorintho 15:33.

1:2. Kila siku tunapaswa kuchunguza mambo ya kiroho.—Mathayo 4:4.

4:4. Tunapokasirika au kuwa na ghadhabu, tunapaswa kuuzuia ulimi wetu usije ukasema jambo tutakalojuta baadaye.—Waefeso 4:26.

4:5. Dhabihu zetu za kiroho zitakuwa “dhabihu za uadilifu” iwapo tu zinatokana na nia nzuri na mwenendo wetu unapatana na matakwa ya Yehova.

6:5. Kusudi kuu la maisha yetu ni kumsifu Yehova.—Zaburi 115:17.

9:12. Yehova hutafuta umwagikaji wa damu ili kuwaadhibu wenye hatia ya damu, lakini hukumbuka “kilio cha wenye kuteseka.”

15:2, 3; 24:3-5. Lazima waabudu wa kweli waseme kweli na kuepuka viapo vya uwongo na uchongezi.

15:4. Tunapaswa kufanya yote tuwezayo ili kutimiza ahadi zetu, hata ikiwa ni vigumu sana kufanya hivyo, isipokuwa iwe tumegundua kwamba tulitoa ahadi isiyopatana na maandiko.

15:5. Tukiwa waabudu wa Yehova, tunapaswa kuepuka kutumia pesa vibaya.

17:14, 15. “Watu wa mfumo huu wa mambo” hujitahidi kufa na kupona ili kuishi maisha ya starehe, kuwa na familia, na kuwaachia watoto wao urithi. Hangaiko kuu la Daudi maishani lilikuwa kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu ili ‘auone uso wake,’ au apate kibali cha Yehova. ‘Alipoamka’ na kuona ahadi na uhakikishio wa Yehova, Daudi ‘alitosheka kuliona umbo Lake,’ au alishangilia kwamba Yehova alikuwa pamoja naye. Kama Daudi, je, hatupaswi kuzingatia moyoni hazina za kiroho?

19:1-6. Ikiwa uumbaji ambao hauwezi kuongea wala kufikiri, unampa Yehova utukufu, je, sisi ambao tunaweza kufikiri, kuongea, na kumwabudu hatupaswi kumtukuza hata zaidi?—Ufunuo 4:11.

19:7-11. Matakwa ya Yehova—yanatufaidi sana!

19:12, 13. Makosa na matendo ya kimbelembele ni dhambi ambazo tunapaswa kuepuka.

19:14. Mbali na kuhangaikia mambo tunayofanya, tunapaswa pia kuhangaikia yale tunayosema na kufikiri.

“UMENITEGEMEZA KWA SABABU YA UTIMILIFU WANGU”

(Zaburi 25:1–41:13)

Jinsi Daudi alivyoonyesha tamaa ya kutoka moyoni na azimio thabiti la kushikilia utimilifu wake katika zaburi mbili za kwanza za sehemu hii! “Mimi nami nitatembea katika utimilifu wangu,” anaimba. (Zaburi 26:11) Katika sala yake ya kuomba msamaha wa dhambi, anakiri hivi: “Nilipokaa kimya mifupa yangu ilichakaa kwa sababu ya kuugua kwangu mchana kutwa.” (Zaburi 32:3) Daudi anawahakikishia hivi washikamanifu wa Yehova: “Macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.”—Zaburi 34:15.

Mashauri ya Zaburi 37 yalikuwa yenye thamani kama nini kwa Waisraeli na kwetu sisi tunaoishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo! (2 Timotheo 3:1-5) Ikitabiri kumhusu Yesu Kristo, Zaburi 40:7, 8 inasema: “Tazama nimekuja, katika kitabu cha kukunjwa imeandikwa juu yangu. Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” Zaburi ya mwisho katika mkusanyo huo inazungumzia Daudi akimwomba Yehova msaada wakati wa taabu baada ya dhambi yake na Bath-sheba. Anaimba hivi: “Umenitegemeza kwa sababu ya utimilifu wangu.”—Zaburi 41:12.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

26:6—Tunaweza kutembeaje tukizunguka madhabahu ya Yehova, kama alivyofanya Daudi? Madhabahu huwakilisha nia ya Yehova ya kukubali dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo iliyotolewa ili wanadamu wakombolewe. (Waebrania 8:5; 10:5-10) Sisi hutembea tukizunguka madhabahu ya Yehova kwa kuonyesha imani yetu katika dhabihu hiyo.

29:3-9—Kwa nini sauti ya Yehova inalinganishwa na ngurumo inayotisha? Ili kuonyesha kwamba Yehova ana nguvu zisizo na kifani!

31:23—Mtu mwenye majivuno hupataje malipo tele? Malipo yanayozungumziwa hapa ni adhabu. Mtu mwadilifu hupata malipo yake anapotiwa nidhamu na Yehova kwa sababu ya makosa ambayo amefanya bila kukusudia. Kwa kuwa mtu mwenye majivuno haachi mwenendo wake mbaya, yeye hupata malipo tele kwa kuadhibiwa vikali.—Methali 11:31; 1 Petro 4:18.

33:6—“Roho,” ya kinywa cha Yehova ni nini? Roho hiyo ni nguvu za utendaji za Mungu au roho takatifu aliyotumia kuumba mbingu halisi. (Mwanzo 1:1, 2) Inaitwa roho ya kinywa chake, kwa kuwa kama vile pumzi yenye nguvu, inaweza kutumwa itimize mambo yaliyo mbali.

35:19—Kwa nini Daudi aliomba kwamba wale wanaomchukia wasikonyeze jicho? Kukonyeza jicho kungemaanisha kwamba adui za Daudi wanafurahia mafanikio ya hila zao dhidi yake. Daudi aliomba isiwe hivyo.

Mambo Tunayojifunza:

26:4. Tunapaswa kuepuka kushirikana na wale wanaoficha jinsi walivyo katika Intaneti, wanafunzi au wafanyakazi wenzetu wanaojifanya rafiki zetu wakiwa na nia mbaya, waasi imani wanaojifanya kuwa wanyoofu, na wale wanaoishi maisha maradufu.

26:7, 12; 35:18; 40:9. Lazima tumsifu Yehova hadharani katika mikutano ya Kikristo.

26:8; 27:4. Je, tunapenda kuhudhuria mikutano ya Kikristo?

26:11. Daudi aliomba akombolewe, huku akiwa ameazimia kudumisha utimilifu wake. Sisi nasi tunaweza kudumisha utimilifu wetu licha ya kutokamilika.

29:10. Kwa kuketi juu ya “gharika,” Yehova huonyesha kwamba anadhibiti kikamili nguvu zake.

30:5. Sifa kuu ya Yehova ni upendo wala si hasira.

32:9. Yehova hataki tuwe kama punda au nyumbu anayetii kwa sababu ya lijamu au fimbo. Badala yake, angependa tuamue kumtii kwa sababu tunaelewa mapenzi yake.

33:17-19. Hakuna mifumo yoyote ya mwanadamu inaweza kuokoa, hata iwe yenye nguvu namna gani. Lazima tumtegemee Yehova na Ufalme wake.

34:10. Huo ni uhakikishio ulioje kwa wale wanaotanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao!

39:1, 2Waovu wanapotafuta habari ili kuwadhuru waamini wenzetu, tunapaswa ‘kuweka lijamu kama mlinzi wa kinywa chetu’ na kutosema chochote.

40:1, 2Kumtumaini Yehova kunaweza kutusaidia kukabiliana na mshuko wa moyo na kututoa “katika shimo lenye kunguruma, kutoka katika matope ya nchi.”

40:5, 12. Tukikumbuka kwamba baraka zetu ‘ni nyingi kuliko tunavyoweza kusimulia,’ hatutalemewa na misiba wala kasoro zetu, hata ziwe nyingi kadiri gani.

‘Yehova na Abarikiwe’

Zaburi hizo 41 za sehemu ya kwanza ni zenye kufariji na kutia moyo kama nini! Iwe tunakumbwa na majaribu au tuna dhamiri mbaya, tunaweza kupata nguvu na kutiwa moyo kutokana na sehemu hii ya Neno la Mungu lenye Nguvu. (Waebrania 4:12) Zaburi hizo zina habari inayotoa mwongozo mzuri maishani. Tunahakikishiwa tena na tena kwamba licha ya matatizo tunayokabili, Yehova hatatuacha.

Mkusanyo wa kwanza wa zaburi wamalizika kwa maneno haya: “Yehova Mungu wa Israeli na abarikiwe tangu wakati usio na kipimo mpaka wakati usio na kipimo. Amina na Amina.” (Zaburi 41:13) Baada ya kuchunguza zaburi hizo, je, hatuchochewi kumbariki, au kumsifu Yehova?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Zaburi ya 2 ilitimizwa kwanza katika siku za Daudi.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Ikiwa uumbaji usio na uhai unamtukuza Yehova, sisi hatuna budi kumtukuza hata zaidi!

[Picha katika ukurasa wa 17]

Daudi alitunga sehemu kubwa ya zile zaburi 41 za kwanza

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unajua ni zaburi gani inayomfafanua Yehova kuwa Mchungaji Mkuu?

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kila siku unapaswa kuchunguza mambo ya kiroho

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 17]

Stars: Courtesy United States Naval Observatory

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

Stars, pages 18 and 19: Courtesy United States Naval Observatory

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]

Stars: Courtesy United States Naval Observatory