Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni nini kinachosababisha “vitu vyenye kutamanika vya mataifa” viingie katika “nyumba” ya ibada ya kweli?—Hagai 2:7.

Yehova alitabiri hivi kupitia nabii Hagai: “Nitayatikisa mataifa yote, navyo vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote vitaingia; nami nitaijaza nyumba hii utukufu.” (Hagai 2:7) Je, kutikiswa “kwa mataifa yote” ndiko kunakosababisha “vitu vyenye kutamanika” vya mataifa, au watu wanyoofu, waikubali ibada ya kweli? Jibu ni la.

Zingatia kile kinachotikisa, au kutetemesha mataifa, na matokeo yake. Biblia inasema kwamba “mataifa yamekuwa na fujo na vikundi vya mataifa vimeendelea kusema jambo la upuuzi.” (Zaburi 2:1) “Jambo la upuuzi” wanaloendelea “kusema,” au kutafakari, ni kuendeleza mamlaka yao wenyewe. Tisho dhidi ya utawala wao linawatikisa kuliko kitu kingine chochote.

Kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu uliosimamishwa inayofanywa na Mashahidi wa Yehova imekuwa tisho kwelikweli kwa mataifa. Kwani, Ufalme wa Kimasihi wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote” za wanadamu. (Danieli 2:44) Ujumbe wa hukumu tunaohubiri unayatetemesha mataifa. (Isaya 61:2) Nayo mataifa hutikiswa hata zaidi kadiri kazi ya kuhubiri inavyozidi kufanywa kwa mapana na marefu. Kule kutikiswa kunakotabiriwa katika Hagai 2:7 ni ishara ya nini?

Andiko la Hagai 2:6 lasema hivi: “Yehova wa majeshi amesema hivi, ‘Bado mara moja—ni kitambo kidogo—nami nitatikisa mbingu na dunia na bahari na nchi kavu.’” Akinukuu mstari huu, mtume Paulo aliandika hivi: “Ameahidi, akisema: ‘Bado mara moja tena nitaitikisa, si dunia peke yake, bali pia na mbingu.’ Sasa maneno ‘Bado mara moja tena’ yanatoa ishara ya kuondolewa kwa vitu vinavyotikiswa kuwa vitu ambavyo vimefanywa, ili vitu ambavyo havitikiswi [Ufalme] vibaki.” (Waebrania 12:26, 27) Ndiyo, mfumo wote wa mambo utatikiswa usiwepo tena ili ulimwengu mpya wa Mungu uchukue mahali pake.

Watu wanyoofu wanavutwa waingie katika ibada ya kweli lakini si kwa sababu mataifa yanatikiswa au kutetemeshwa. Kile kinachowavuta kwa Yehova na ibada yake ni kilekile kinachoyatikisa mataifa, yaani kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Kutangazwa kwa ‘habari za furaha kuhusu habari njema ya milele’ huwavuta watu wenye mwelekeo unaofaa wajiunge na ibada ya Mungu wa kweli.—Ufunuo 14:6, 7.

Ujumbe wa ufalme ni ujumbe wa hukumu na wokovu. (Isaya 61:1, 2) Matokeo ya kuhubiriwa kwa ujumbe huo ulimwenguni pote ni mawili: kutikiswa kwa mataifa na kuingia kwa vitu vyenye kutamanika vya mataifa, jambo linalomletea Yehova utukufu.