Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shangwe za Kutembea kwa Utimilifu

Shangwe za Kutembea kwa Utimilifu

Shangwe za Kutembea kwa Utimilifu

“Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—METHALI 10:22.

1, 2. Kwa nini twapaswa kujihadhari tusije tukajishughulisha mno na wakati ujao?

“KUJISHUGHULISHA mno na siku za usoni . . . hutuzuia kuona hali zilivyo leo,” akasema mwanafalsafa mmoja Mmarekani. Ndivyo walivyo watoto wanaojishughulisha na majukumu ya watu wazima hivi kwamba wanakosa kuona faida za utoto hadi inapokuwa kuchelewa mno.

2 Hata waabudu wa Yehova huwa na maoni kama hayo. Hebu fikiria hali hii. Sisi hutazamia sana kutimizwa kwa ahadi ya Mungu ya kuleta paradiso duniani. Tunasubiri kwa hamu maisha yasiyo na magonjwa, uzee, maumivu, na mateso. Ingawa ni vizuri kutazamia yote hayo, itakuwaje ikiwa tunajishughulisha mno na baraka za kimwili za wakati ujao hivi kwamba hatuoni baraka za kiroho tulizo nazo leo? Itakuwa hali yenye kusikitisha kama nini! Huenda tukavunjika moyo kwa urahisi na ‘mioyo yetu iwe migonjwa kwa sababu matarajio yetu yamechelewa’ kuliko tulivyotazamia. (Methali 13:12) Matatizo na hali ngumu maishani zaweza kutufanya tushuke moyo au kuanza kujisikitikia. Badala ya kukabiliana na hali mbaya, huenda tukaanza kuwa walalamikaji. Twaweza kuepuka yote hayo kwa kutafakari na kuthamini baraka tulizo nazo leo.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Andiko la Methali 10:22 lasema hivi: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.” Je, ufanisi wa kiroho wa watumishi wa Yehova leo si baraka tunayoweza kushangilia? Na tuchunguze nyanja mbalimbali za ufanisi wetu wa kiroho na kuona jinsi tunavyohusika sisi binafsi. Kutafakari mambo yote ambayo Yehova amemfanyia ‘mwadilifu anayetembea katika utimilifu wake’ kutaimarisha kwelikweli azimio letu la kuendelea kumtumikia Baba yetu wa mbinguni kwa shangwe.—Methali 20:7.

‘Baraka Zinazotutajirisha’ Leo

4, 5. Ni fundisho gani la Biblia linalokupendeza sana, na kwa nini?

4 Ujuzi sahihi wa mafundisho ya Biblia. Kwa ujumla, dini zinazodai kuwa za Kikristo hudai kwamba zinaiamini Biblia. Hata hivyo, hazikubali mafundisho yake. Hata washiriki wa dini ileile huwa na maoni tofauti kuhusu mambo ambayo Biblia hufundisha hasa. Hali yao ni tofauti kabisa na hali ya watumishi wa Yehova! Haidhuru taifa, utamaduni, au malezi yetu, tunamwabudu Mungu tunayemjua kwa jina. Yeye si mungu wa kifumbo wa utatu. (Kumbukumbu la Torati 6:4; Zaburi 83:18; Marko 12:29) Pia, tunajua kwamba suala muhimu la enzi kuu ya Mungu litatatuliwa hivi karibuni na kwamba kwa kuendelea kuwa watimilifu kwake, kila mmoja wetu anahusika kibinafsi katika suala hilo. Tunajua ukweli kuhusu hali ya wafu nasi hatuna hofu isiyofaa kumwelekea Mungu ambaye wengine husema kwamba huwatesa wanadamu katika moto wa mateso au kuwatupa toharani.—Mhubiri 9:5, 10.

5 Isitoshe, ni shangwe iliyoje kujua kwamba hatukutokana na mageuzi ya kiholela! Badala yake, tuliumbwa na Mungu, kwa mfano wake mwenyewe. (Mwanzo 1:26; Malaki 2:10) Mtunga-zaburi alimwimbia hivi Mungu wake: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.”—Zaburi 139:14.

6, 7. Ni mabadiliko gani maishani mwako au katika maisha ya wengine unaowajua ambayo ni baraka kwelikweli?

6 Kuwa huru kutokana na mazoea na matendo yenye kudhuru. Vyombo vya habari hutoa maonyo mengi kuhusu hatari za kuvuta sigara, kunywa pombe kupita kiasi, na upotovu katika ngono. Hata hivyo, ni wachache sana wanaotii. Inakuwaje basi mtu mnyoofu anapojifunza kwamba Mungu wa kweli hushutumu mambo hayo na huhuzunishwa na wale wanaoyatenda? Mtu huyo huyaondolea mbali kabisa mambo hayo maishani mwake! (Isaya 63:10; 1 Wakorintho 6:9, 10; 2 Wakorintho 7:1; Waefeso 4:30) Ingawa anafanya hivyo ili kumpendeza Yehova Mungu, yeye hupata baraka zaidi—afya nzuri na amani ya akili.

7 Ni vigumu sana kuacha mazoea mabaya. Hata hivyo, kila mwaka makumi ya maelfu ya watu hufanya hivyo. Wao hujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa kwa maji, wakionyesha waziwazi kwamba wameondolea mbali maishani mwao mazoea yasiyompendeza Mungu. Hilo ni jambo lenye kutia moyo kama nini! Azimio letu la kuendelea kuwa huru kutokana na utumwa na dhambi na mwenendo wenye kuumiza huimarika.

8. Ni shauri gani la Biblia huchangia furaha ya familia?

8 Maisha ya familia yenye furaha. Katika nchi nyingi, familia zinavunjika. Ndoa nyingi huishia katika talaka na kuwaacha watoto wakiwa na makovu mabaya ya kihisia. Katika nchi fulani za Ulaya, karibu asilimia 20 ya familia ni familia za mzazi mmoja. Yehova ametusaidiaje kutembea katika njia ya utimilifu katika maisha ya familia? Tafadhali soma Waefeso 5:22–6:4 uone shauri zuri ambalo Neno la Mungu huwapa waume, wake, na watoto. Bila shaka, kufuata shauri hilo na mashauri mengine ya Maandiko huimarisha vifungo vya ndoa, husaidia wazazi kuwalea watoto ifaavyo, na huchangia furaha katika maisha ya familia. Je, hizo si baraka tunazoweza kufurahia kupata?

9, 10. Maoni yetu kuhusu wakati ujao yanatofautianaje na maoni ya ulimwengu?

9 Kuwa na hakika kwamba matatizo ya ulimwengu yatatatuliwa hivi karibuni. Licha ya ujuzi wa sayansi na teknolojia na pia jitihada za kutoka moyoni za baadhi ya viongozi, bado maisha ya leo yamejaa matatizo mazito. Klaus Schwab, mwanzilishi wa shirika la World Economic Forum, hivi karibuni alisema kwamba “msururu wa matatizo yanayoukumba ulimwengu unazidi kuwa mrefu, nao wakati wa kuyatatua unazidi kuwa mfupi.” Alitaja “hatari zinazokumba mataifa yote kama vile ugaidi, kuzorota kwa mazingira na misukosuko ya kiuchumi.” Schwab alikata kauli hii: “Leo, kuliko wakati mwingine wowote, watu wanahitaji kushirikiana na kufanya maamuzi haraka ili kutatua matatizo yanayoukumba ulimwengu.” Karne ya 21 inapozidi kusonga mbele, matumaini ya mwanadamu yangali gizani.

10 Inaridhisha kama nini kujua kwamba Yehova alipanga kuwe na Ufalme wa Kimasihi unaoweza kutatua matatizo yote ya mwanadamu! Kupitia Ufalme huo, Mungu wa kweli ‘atakomesha vita’ na kuleta “wingi wa amani.” (Zaburi 46:9; 72:7) Yesu Kristo, akiwa Mfalme aliyetiwa mafuta, ‘atamkomboa maskini, mwenye kuteseka, na mtu wa hali ya chini kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.’ (Zaburi 72:12-14) Chini ya utawala wa Ufalme, hakutakuwa na upungufu wa chakula. (Zaburi 72:16) Yehova “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Tayari Ufalme huo umesimamishwa mbinguni na hivi karibuni utachukua hatua inayohitajika ili kutatua matatizo yote duniani.—Danieli 2:44; Ufunuo 11:15.

11, 12. (a) Je, kufuatia raha maishani huleta furaha ya kudumu? Eleza. (b) Furaha ya kweli hutokana na nini?

11 Kujua chanzo cha furaha ya kweli. Furaha ya kweli inatokana na nini? Mtaalamu mmoja wa mambo ya akili alisema kwamba furaha hutokana na mambo matatu—raha, shughuli (kujishughulisha katika kazi na familia), na kusudi (kujitahidi kufikia mradi au lengo kubwa zaidi kwa faida ya wengine). Kati ya mambo hayo matatu, aliorodhesha raha kuwa la mwisho katika umuhimu kisha akasema: “Hilo litawashangaza wengi kwa sababu watu wengi hutanguliza raha maishani mwao.” Biblia ina maoni gani kuhusu jambo hilo?

12 Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alisema hivi: “Nilisema, naam mimi, moyoni mwangu: ‘Njoo basi, nikujaribu kwa kushangilia. Pia, uone mema.’ Na tazama! hilo pia lilikuwa ubatili. Nikasema juu ya kicheko: ‘Ni wazimu!’ na juu ya shangwe: ‘Hii inafanya nini?’” (Mhubiri 2:1, 2) Kulingana na Maandiko, shangwe yoyote inayotokana na raha ni ya muda tu. Vipi kuhusu kazi? Tuna kazi muhimu zaidi ya kufanya—kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Tunapowahubiria wengine ujumbe wa wokovu ulio katika Biblia, tunashiriki katika kazi inayoweza kutuokoa sisi wenyewe na kuwaokoa wale wanaotusikiliza. (1 Timotheo 4:16) Tukiwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu,” tumeona kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (1 Wakorintho 3:9; Matendo 20:35) Kazi hiyo hufanya maisha yetu yawe na kusudi na humwezesha Muumba kumjibu mdhihaki wake, Shetani Ibilisi. (Methali 27:11) Kwa kweli, Yehova ameonyesha kwamba ujitoaji-kimungu huleta furaha ya kweli na yenye kudumu.—1 Timotheo 4:8.

13. (a) Ni katika njia gani Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni baraka inayotuletea shangwe? (b) Umefaidikaje kutokana na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?

13 Programu ya mazoezi muhimu na yenye matokeo. Gerhard ni mzee katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Akikumbuka siku zake za ujanani, anasema hivi: “Nilipokuwa kijana, singeweza kusema maneno waziwazi na hivyo nikaanza kuwa na kigugumizi. Nilishuka moyo na kujiona kuwa sifai. Wazazi wangu walipanga nipate mazoezi ya kuzungumza, lakini jitihada zao hazikufaulu. Sikuwa na tatizo la kimwili bali la kiakili. Hata hivyo, kulikuwa na uandalizi wa pekee kutoka kwa Yehova—Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kujiandikisha katika shule hiyo kulinipa ujasiri mpya. Nilijitahidi niwezavyo kufanyia mazoezi mambo niliyojifunza. Nilifaulu! Nilianza kusema waziwazi zaidi, nikaacha kushuka moyo, nami nikawa na ujasiri zaidi katika huduma. Sasa, mimi hutoa hata hotuba za watu wote. Namshukuru Yehova kwelikweli, aliyeniwezesha kuwa na furaha tena maishani, kupitia shule hiyo.” Je, hatupati shangwe kutokana na jinsi Yehova anavyotuzoeza kufanya kazi yake?

14, 15. Nyakati za taabu, ni msaada gani tunaoweza kupata? Toa mfano.

14 Uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova na utegemezo wa undugu wa kimataifa wenye umoja. Katrin, anayeishi Ujerumani, alikuwa na wasiwasi sana baada ya kusikia kuhusu tetemeko la ardhi na kisha tsunami iliyofuata huko kusini-mashariki mwa Asia. Binti yake alikuwa amezuru Thailand msiba huo ulipotokea. Kwa saa 32 mama huyo hakujua iwapo binti yake alikuwa hai au alikuwa miongoni mwa wale waliokufa ambao idadi yao ilikuwa ikiongezeka. Katrin alipata faraja kama nini hatimaye alipopokea simu iliyomhakikishia kwamba binti yake alikuwa salama!

15 Ni nini kilichomsaidia Katrin muda wote huo alipokuwa na wasiwasi? Anaandika hivi: “Kwa karibu muda wote huo nilikuwa nikisali kwa Yehova. Kila mara nilipofanya hivyo nilipata nguvu na amani ya akili. Isitoshe, ndugu zangu wa kiroho wenye upendo walinitembelea na kunitia moyo.” (Wafilipi 4:6, 7) Hali yake ingekuwa mbaya kama nini ikiwa angelazimika kukaa muda wote huo pasipo kusali kwa Yehova au faraja kutoka kwa ndugu wa kiroho wenye upendo! Uhusiano wetu wa karibu na Yehova na Mwana wake pamoja na ushirika wetu na ndugu zetu Wakristo ni baraka ya pekee, yenye thamani sana hivi kwamba hatuwezi kuipuuza kamwe.

16. Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha thamani ya tumaini la ufufuo.

16 Tumaini la kuwaona tena wapendwa wetu waliokufa. (Yohana 5:28, 29) Kijana anayeitwa Matthias alilelewa na wazazi Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, hakuthamini baraka hizo, naye akapeperuka na kuliacha kutaniko la Kikristo alipokuwa tineja. Sasa anaandika hivi: “Kwa kweli sikuwa kamwe na mazungumzo mazito pamoja na baba yangu. Tulibishana kwa miaka mingi. Hata hivyo, sikuzote baba yangu alinitakia mema. Alinipenda sana, ingawa sikutambua wakati huo. Mwaka wa 1996, niliketi kando ya kitanda chake nikiwa nimeushika mkono wake na kulia kwelikweli, nilimweleza jinsi nilivyosikitika kwa yote niliyokuwa nimefanya na kwamba ninampenda sana. Hata hivyo hangeweza kunisikia. Baada ya kuugua kwa muda mfupi, alikufa. Ikiwa nitamwona baba yangu atakapofufuliwa, nitalipia mambo niliyokosa kufanya wakati uliopita. Naye hakika atafurahi kusikia kuwa mimi ni mzee kutanikoni na kwamba mimi na mke wangu tuna pendeleo la kuwa mapainia.” Tumaini la ufufuo ni baraka iliyoje kwetu!

“Haongezi Maumivu Pamoja Nayo”

17. Kutafakari baraka za Yehova hutusaidiaje?

17 Kuhusu Baba yake wa mbinguni, Yesu Kristo alisema hivi: “Yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:45) Ikiwa Yehova Mungu huwamiminia baraka zake wasio waadilifu na waovu, bila shaka atafanya hivyo hata zaidi kwa wale wanaotembea kwa utimilifu! Andiko la Zaburi 84:11 lasema hivi: “Yehova mwenyewe hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea bila kosa.” Tunapotafakari jinsi Yehova anavyowatunza na kuwahangaikia kwa njia ya pekee wale wanaompenda, mioyo yetu inafurikwa na shukrani na shangwe iliyoje!

18. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova haongezi maumivu katika baraka zake? (b) Kwa nini watumishi wengi washikamanifu wa Mungu huteseka?

18 “Baraka ya Yehova”—hiyo ndiyo imewapa watu wake ufanisi wa kiroho. Nasi tuna hakika kwamba “haongezi maumivu pamoja nayo.” (Methali 10:22) Kwa nini basi watumishi wengi washikamanifu wa Mungu hukumbwa na majaribu ambayo huwafanya wawe na maumivu mengi na kuteseka sana? Sisi hupata matatizo na taabu kwa sababu tatu kuu. (1) Mwelekeo wetu wa dhambi. (Mwanzo 6:5; 8:21; Yakobo 1:14, 15) (2) Shetani na roho wake waovu. (Waefeso 6:11, 12) (3) Ulimwengu mbovu. (Yohana 15:19) Ingawa Yehova huacha mambo mabaya yatupate, si yeye anayeyasababisha. “Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.” (Yakobo 1:17) Yehova haongezi maumivu katika baraka zake.

19. Wale wanaoendelea kutembea katika utimilifu watapata nini?

19 Sikuzote, ufanisi wa kiroho hutia ndani kukuza uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Tunapomkaribia Mungu, ‘tunajiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili tuushike imara uzima ulio wa kweli’—uzima wa milele. (1 Timotheo 6:12, 17-19) Katika ulimwengu ujao wa Mungu, tutakuwa na ufanisi wa kiroho pamoja na baraka za kimwili. Wale wote ‘wanaoendelea kuisikiliza sauti ya Yehova’ watapata uzima ulio wa kweli kutoka kwa Yehova. (Kumbukumbu la Torati 28:2) Na tuazimie hata zaidi kwamba tutaendelea kutembea kwa shangwe katika utimilifu.

Umejifunza Nini?

• Kwa nini haifai kujishughulisha kupita kiasi na mambo ya wakati ujao?

• Ni baraka gani tulizo nazo leo?

• Kwa nini watumishi waaminifu wa Mungu huteseka?

[Maswali ya Funzo]