Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Chagua Uzima Ili Uendelee Kuwa Hai’

‘Chagua Uzima Ili Uendelee Kuwa Hai’

‘Chagua Uzima Ili Uendelee Kuwa Hai’

“Nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 30:19.

1, 2. Ni kwa njia gani mwanadamu aliumbwa kwa mfano wa Mungu?

“NA TUFANYE mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” Maneno hayo yaliyoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu yanapatikana katika sura ya kwanza ya Biblia. Andiko la Mwanzo 1:26, 27 linasema hivi: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba.” Naam, mwanadamu wa kwanza alikuwa tofauti na viumbe wote duniani. Alifanana na Muumba wake, kwa sababu angeweza kuiga jinsi Mungu anavyofikiri, upendo wake, haki yake, hekima yake, na nguvu zake. Alikuwa na dhamiri ya kumsaidia kufanya maamuzi ambayo yangemfaidi na kumpendeza Mzazi wake aliye mbinguni. (Waroma 2:15) Kwa ufupi, Adamu alikuwa na uhuru wa kuchagua. Yehova alipochunguza jinsi alivyomuumba mwana wake wa kidunia, alisema hivi kuhusu kazi yake: ‘Tazama! ni njema sana.’—Mwanzo 1:31; Zaburi 95:6.

2 Kwa kuwa sisi ni wazao wa Adamu, tumeumbwa pia kwa mfano na sura ya Mungu. Lakini, je, tuna uhuru wa kuchagua mambo tunayotaka kufanya? Ingawa Yehova anaweza kujua kimbele mambo yatakayotukia wakati ujao, yeye haamui kimbele matendo ya mtu mmoja-mmoja wala matokeo ya matendo hayo. Yeye hapangi kimbele mambo yatakayowapata watoto wake walio duniani. Ili tuweze kuelewa umuhimu wa kutumia uhuru wetu wa kuchagua kufanya uchaguzi unaofaa, acheni kwanza tujifunze jambo fulani kutokana na taifa la Israeli.—Waroma 15:4.

Waisraeli Walikuwa na Uhuru wa Kuchagua

3. Ni amri gani iliyo ya kwanza kati ya zile Amri Kumi, na Waisraeli waaminifu walitii amri hiyo jinsi gani?

3 Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Mimi ni Yehova Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, kutoka katika nyumba ya watumwa.” (Kumbukumbu la Torati 5:6) Katika mwaka wa 1513 K.W.K., taifa la Israeli lilikombolewa kimuujiza kutoka utekwani huko Misri, na hivyo lilipaswa kuamini kabisa maneno hayo. Katika amri ya kwanza kati ya zile Amri Kumi, Yehova alitangaza hivi kupitia Musa msemaji wake: “Usiwe na miungu mingine yoyote dhidi ya uso wangu.” (Kutoka 20:1, 3) Wakati huo, taifa la Israeli lilichagua kutii. Kwa hiari, walijitoa kikamili kwa Yehova.—Kutoka 20:5; Hesabu 25:11.

4. (a) Musa aliwaambia Waisraeli nini kuhusu uchaguzi waliopaswa kufanya? (b) Tunaweza kuchagua nini leo?

4 Miaka 40 hivi baadaye, Musa aliwakumbusha Waisraeli wa kizazi kingine kuhusu uchaguzi waliopaswa kufanya. Alitangaza hivi: “Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako.” (Kumbukumbu la Torati 30:19) Leo, hata sisi tunaweza kuchagua. Naam, tunaweza kuchagua kumtumikia Yehova kwa uaminifu na kupata uzima wa milele, au tunaweza kuchagua kumwasi na kupata matokeo mabaya. Ona mifano miwili ya watu waliofanya uchaguzi uliotofautiana.

5, 6. Yoshua alichagua kufanya nini, na matokeo yakawaje?

5 Katika mwaka wa 1473 K.W.K., Yoshua aliwaongoza Waisraeli kuingia Nchi ya Ahadi. Katika himizo lenye kuchochea ambalo alitoa kabla ya kifo chake, Yoshua alilisihi taifa lote hivi: “Sasa ikiwa mnaona ni vibaya machoni penu kumtumikia Yehova, jichagulieni leo yule mtakayemtumikia, kama ni miungu ambayo waliitumikia mababu zenu waliokuwa ng’ambo ile nyingine ya Mto au kama ni miungu ya Waamori ambao mnakaa katika nchi yao.” Kisha akizungumza kuhusu familia yake, Yoshua aliongeza hivi: “Mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.”—Yoshua 24:15.

6 Kabla ya wakati huo, Yehova alikuwa amemsihi Yoshua awe hodari na mwenye nguvu, na kumwagiza asiache kutii Sheria ya Mungu. Badala yake, kwa kusoma kitabu cha Sheria kwa sauti ya chini mchana na usiku, Yoshua angeifanikisha njia yake. (Yoshua 1:7, 8) Yoshua alitii mashauri hayo naye akafanikiwa. Chaguo lake lilimwezesha kupata baraka. Yoshua alitangaza hivi: “Hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia katika ahadi zote nzuri ambazo Yehova alikuwa ameipa nyumba ya Israeli; mambo yote yalitimia.”—Yoshua 21:45.

7. Katika siku za Isaya, Waisraeli fulani walichagua nini, na matokeo yakawaje?

7 Kwa upande mwingine, ona jinsi hali ilivyokuwa katika Israeli yapata miaka 700 baadaye. Kufikia wakati huo, Waisraeli wengi walikuwa wakifuata desturi za kipagani. Kwa mfano, siku ya mwisho wa mwaka, watu walikusanyika kuzunguka meza iliyotandazwa vyakula vitamu vya aina mbalimbali na divai tamu. Hiyo haikuwa karamu ya kawaida tu. Ilikuwa sherehe ya kidini iliyofanywa ili kutukuza miungu miwili ya kipagani. Nabii Isaya aliandika maoni ya Mungu kuhusu ukosefu huo wa uaminifu: “Ninyi ndio wale watu wanaomwacha Yehova, wale wanaousahau mlima wangu mtakatifu, wale wanaoandaa meza kwa ajili ya mungu wa Bahati Njema na wale wanaojaza divai iliyochanganywa kwa ajili ya mungu wa Majaliwa.” Waliamini kwamba mavuno ya kila mwaka hayakutegemea baraka za Yehova, bali yalitegemea kutuliza “mungu wa Bahati Njema” na “mungu wa Majaliwa.” Hata hivyo, uasi wao na uchaguzi wao wa ukaidi ulionyesha yale ambayo yangewapata. Yehova alitangaza hivi: “Nitawaandikia ninyi upanga, nanyi nyote mtainama ili kuuawa; kwa sababu niliita, lakini hamkuitika; nilisema, lakini hamkusikiliza; nanyi mliendelea kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pangu, mlichagua jambo ambalo halikunipendeza.” (Isaya 65:11, 12) Kwa sababu ya uchaguzi wao usio wa hekima waliharibiwa, na miungu ya Bahati Njema na Majaliwa haingeweza kuzuia uharibifu huo.

Kufanya Uchaguzi Unaofaa

8. Kulingana na Kumbukumbu la Torati 30:20, ni mambo gani yanayohusika katika kufanya uchaguzi unaofaa?

8 Musa alipowahimiza Waisraeli wachague uzima, alitaja hatua tatu ambazo walipaswa kuchukua: “Kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye.” (Kumbukumbu la Torati 30:20) Acheni tuchunguze kila moja ya hatua hizo ili tufanye uchaguzi unaofaa.

9. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunampenda Yehova?

9 Kwa kumpenda Yehova Mungu wetu: Sisi huchagua kumtumikia Yehova kwa sababu tunampenda. Kwa kutii vielelezo vyenye kuonya vya siku za Waisraeli, sisi hupinga vishawishi vyote vya kujihusisha katika ukosefu wa adili na kuepuka kuishi kwa njia itakayotufanya tunaswe na mtego wa ulimwengu wa kufuatia mali. (1 Wakorintho 10:11; 1 Timotheo 6:6-10) Sisi hushikamana na Yehova na kushika masharti yake. (Yoshua 23:8; Zaburi 119:5, 8) Kabla ya Waisraeli kuingia Nchi ya Ahadi, Musa aliwahimiza hivi: “Tazama! nimewafundisha masharti na maamuzi ya hukumu, kama vile ambavyo Yehova Mungu wangu ameniamuru mimi, ili ninyi mfanye hivyo katikati ya nchi ambayo mnaenda kuimiliki. Nanyi mtazishika na kuzifanya, kwa sababu hiyo ni hekima kwenu na uelewaji kwenu mbele ya macho ya vikundi vya watu watakaosikia juu ya masharti yote haya.” (Kumbukumbu la Torati 4:5, 6) Sasa ndio wakati wa kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa kutanguliza mapenzi yake maishani mwetu. Tutabarikiwa sana tukichagua kufanya hivyo.—Mathayo 6:33.

10-12. Tunajifunza nini kwa kuchunguza mambo yaliyotukia siku za Noa?

10 Kwa kuisikiliza sauti ya Mungu: Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Karibu watu wote walioishi kabla ya Gharika walikengeushwa na “hawakujali” maonyo ya Noa. Matokeo? “Gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” Yesu alionya kwamba siku zetu, wakati wa “kuwapo kwa Mwana wa binadamu,” zingefanana na wakati huo. Mambo yaliyotukia siku za Noa ni onyo kali kwa watu wanaochagua kupuuza ujumbe wa Mungu.—Mathayo 24:39.

11 Wale wanaodhihaki maonyo ya Mungu ambayo yanatolewa na watumishi wake wa leo wanapaswa kutambua matokeo ya kupuuza maonyo hayo. Mtume Petro alisema hivi kuhusu wadhihaki hao: “Kulingana na kupenda kwao, wao hawalioni jambo hili, kwamba mbingu zilikuwapo tangu zamani za kale na dunia ikisimama imara kutoka katika maji na katikati ya maji kwa neno la Mungu; na kwa njia hizo ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji. Lakini kwa neno hilohilo mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 3:3-7.

12 Hebu ona tofauti kati ya uchaguzi wa watu hao na uchaguzi wa Noa na familia yake. “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina.” Kwa kuwa Noa alitii onyo hilo, familia yake iliokolewa. (Waebrania 11:7) Acheni tuwe wepesi kusikia ujumbe wa Mungu na kutii.—Yakobo 1:19, 22-25.

13, 14. (a) Kwa nini ni muhimu ‘kushikamana na Yehova’? (b) Tunapaswa kufanya nini ili kumruhusu Yehova, “Mfinyanzi wetu,” atufinyange?

13 Kwa kushikamana na Yehova: Ili ‘tuchague uzima na kuendelea kuwa hai,’ hatupaswi tu kumpenda Yehova na kumsikiliza bali tunapaswa pia “kushikamana naye,” yaani, kuendelea kufanya mapenzi yake. Yesu alisema hivi: “Nanyi kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.” (Luka 21:19) Uchaguzi wetu kuhusu jambo hilo huonyesha yaliyo moyoni mwetu. Andiko la Methali 28:14 linasema: “Mwenye furaha ni mtu anayehofu sikuzote, lakini yeye anayeufanya moyo wake kuwa mgumu ataanguka katika msiba.” Farao wa Misri ya kale ni mfano wa mtu aliyefanya moyo wake kuwa mgumu. Wakati yale Mapigo Kumi yalipoletwa juu ya Misri, Farao alifanya moyo wake kuwa mgumu badala ya kumwogopa Mungu. Yehova hakumlazimisha Farao asitii, lakini alimwacha mtawala huyo mwenye kiburi afanye uchaguzi. Kama vile mtume Paulo anavyoeleza maoni ya Yehova kuhusu Farao, mapenzi ya Yehova yalitimia: “Kwa sababu hii nimekuacha ubaki, ili kuhusiana na wewe nionyeshe nguvu zangu, na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.”—Waroma 9:17.

14 Karne nyingi baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka kwa Farao, nabii Isaya alitangaza hivi: “Ee Yehova, wewe ni Baba yetu. Sisi ni udongo, nawe ni Mfinyanzi wetu; nasi sote ni kazi ya mkono wako.” (Isaya 64:8) Tunapomruhusu Yehova atufinyange kupitia funzo la kibinafsi na kutii Neno lake, sisi hujivika utu mpya pole kwa pole. Tunakuwa wapole zaidi na tunakubali kufinyangwa, na hivyo inakuwa rahisi kwetu kushikamana kabisa na Yehova kwa sababu tunataka sana kumpendeza.—Waefeso 4:23, 24; Wakolosai 3:8-10.

“Utawajulisha”

15. Kulingana na Kumbukumbu la Torati 4:9, Musa aliwakumbusha Waisraeli matakwa gani mawili?

15 Musa aliliambia hivi taifa la Israeli kabla halijaingia Nchi ya Ahadi: “Ila jiangalie na kuitunza vema nafsi yako, ili usisahau mambo ambayo macho yako yameona, nayo yasiondoke moyoni mwako siku zote za maisha yako; nawe utawajulisha mambo hayo wana wako na wajukuu wako.” (Kumbukumbu la Torati 4:9) Ili kupata baraka za Yehova na kufanikiwa katika nchi ambayo wangeirithi, watu hao walipaswa kutimiza matakwa mawili ya Yehova Mungu wao. Hawakupaswa kusahau mambo mazuri ambayo waliona Yehova akiwafanyia, nao walipaswa kufundisha vizazi vya baadaye mambo hayo. Ni lazima sisi watu wa Mungu leo tufanye vivyo hivyo ikiwa tunataka ‘kuchagua uzima na kuendelea kuwa hai.’ Ni mambo gani ambayo tumeona Yehova akitutendea?

16, 17. (a) Wamishonari waliozoezwa katika Shule ya Gileadi wametimiza nini katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme? (b) Ni mifano gani unayojua ya watu ambao wamedumisha bidii yao?

16 Tunasisimuka kuona jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi yetu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Tangu Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) ilipoanzishwa mwaka wa 1943, wamishonari wamekuwa mstari wa mbele katika kazi ya kufanya wanafunzi katika nchi nyingi. Mpaka leo hii, wahitimu wa mapema wa shule hiyo wamedumisha bidii ya kuhubiri kuhusu Ufalme hata ingawa umri wao umesonga sana na baadhi yao hawawezi kutimiza mengi kwa sababu ya udhaifu wa kimwili. Mfano mmoja bora ni wa Mary Olson, ambaye alihitimu Shule ya Gileadi mwaka wa 1944. Dada huyo alianza kutumikia akiwa mmishonari huko Uruguai, kisha Kolombia, na sasa yuko Puerto Riko. Ingawa hawezi kutimiza mengi kwa sababu ya matatizo ya kimwili yanayosababishwa na uzee, Dada Olson angali na shangwe ya kuhubiri. Kwa kuwa anajua Kihispania, kila juma yeye hujiunga na wahubiri wenyeji katika huduma ya shambani.

17 Nancy Porter, ambaye sasa ni mjane, alihitimu Shule ya Gileadi mwaka wa 1947, naye bado anatumikia huko Bahamas. Yeye pia ni mmishonari mwenye bidii nyingi ya kuhubiri. Katika simulizi lake la maisha, Dada Porter anasema hivi: “Kuwafundisha wengine kweli ya Biblia kumeniletea furaha ya kipekee. Shughuli hizo zote zimenisaidia kuwa na taratibu ya kiroho ambayo imeimarisha maisha yangu.” * Dada Porter na watumishi wengine waaminifu wanapokumbuka yaliyopita, hawasahau mambo ambayo Yehova amefanya. Namna gani sisi? Je, sisi hufurahia jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi ya Ufalme katika eneo letu?—Zaburi 68:11.

18. Tunaweza kujifunza nini tunaposoma masimulizi ya maisha ya wamishonari?

18 Tunafurahi sana kuona yale ambayo watumishi hao wa muda mrefu wametimiza na bado wanatimiza. Tunatiwa moyo tunaposoma masimulizi yao ya maisha, kwa sababu tunapoona mambo ambayo Yehova amewafanyia waaminifu hao, azimio letu la kumtumikia Yehova linaimarishwa. Je, wewe husoma na kutafakari kwa ukawaida masimulizi hayo yenye kusisimua yanayochapishwa katika Mnara wa Mlinzi?

19. Wazazi Wakristo wanaweza kutumiaje vizuri masimulizi ya maisha yanayochapishwa katika Mnara wa Mlinzi?

19 Musa aliwakumbusha Waisraeli kwamba hawakupaswa kusahau mambo yote ambayo Yehova alikuwa amewafanyia wala hawakupaswa kuyaondoa moyoni mwao siku zote za maisha yao. Kisha Musa akataja hatua nyingine: “Utawajulisha mambo hayo wana wako na wajukuu wako.” (Kumbukumbu la Torati 4:9) Masimulizi ya maisha yanachochea sana. Vijana wanaokua wanahitaji vielelezo vizuri. Akina dada waseja wanaweza kujifunza kutokana na mifano ya uaminifu ya akina dada wenye umri mkubwa ambao masimulizi yao ya maisha yamechapishwa katika Mnara wa Mlinzi. Akina ndugu na dada hupata nafasi nyingi zaidi za kuhubiri habari njema kwa bidii wanapoamua kutumikia katika eneo la lugha ya kigeni katika nchi ya kwao. Enyi wazazi Wakristo, kwa nini msitumie masimulizi ya wamishonari waaminifu waliohitimu Shule ya Gileadi na masimulizi ya wengine ili kuwachochea watoto wenu kuchagua utumishi wa wakati wote?

20. Tunapaswa kufanya nini ili ‘kuchagua uzima’?

20 Basi, kila mmoja wetu anaweza ‘kuchaguaje uzima’? Kwa kutumia zawadi ya uhuru wa kuchagua kumwonyesha Yehova kwamba tunampenda na kwa kuendelea kufanya yote tunayoweza katika utumishi wake maadamu ametupa pendeleo hilo. “Kwa maana,” kama Musa alivyotangaza, Yehova “ni uhai wako na urefu wa siku zako.”—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Ona makala yenye kichwa, “Mwenye Furaha na Shukrani Licha ya Kufiwa na Mpendwa,” iliyochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 2001, ukurasa wa 23-27.

Je, Unakumbuka?

• Umejifunza nini kupitia mifano ambayo tumechunguza kuhusu watu waliofanya uchaguzi uliotofautiana?

• Tunapaswa kuchukua hatua gani ili ‘kuchagua uzima’?

• Tunasihiwa tutimize matakwa gani mawili?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Nimeweka uzima na kifo mbele yako”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Noa na familia yake waliokolewa kwa sababu ya kusikiliza sauti ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 30]

Mary Olson

[Picha katika ukurasa wa 30]

Nancy Porter