Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutumikia Kwa Shangwe Licha ya Magonjwa

Kutumikia Kwa Shangwe Licha ya Magonjwa

Simulizi la Maisha

Kutumikia Kwa Shangwe Licha ya Magonjwa

SIMULIZI LA VARNAVAS SPETSIOTIS

Katika mwaka wa 1990, nikiwa na umri wa miaka 68, nilipooza kabisa. Hata hivyo, kwa karibu miaka 15 sasa, nimetumikia kwa shangwe nikiwa mhudumu wa wakati wote katika kisiwa cha Saiprasi. Ni nini ambacho kimenisaidia kuendelea katika utumishi wa Yehova licha ya magonjwa?

NILIZALIWA mnamo Oktoba 11, 1922, katika familia yenye watoto tisa, wavulana wanne na wasichana watano. Tuliishi katika kijiji cha Xylophagou, huko Saiprasi. Ingawa familia yetu ilikuwa na mali, bidii nyingi ilihitajiwa kufanya kazi shambani ili kutunza familia kubwa hivyo.

Baba yangu, Antonis, alipenda kusoma na alikuwa mdadisi. Muda mfupi baada ya mimi kuzaliwa, Baba alipokuwa akimtembelea mwalimu mmoja kijijini, aliona trakti Peoples Pulpit, iliyochapishwa na Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo). Alianza kuisoma, na baada ya muda, alipendezwa na ujumbe wake. Baba na Andreas Christou, mmoja wa rafiki zake, wakawa wa kwanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova katika kisiwa hicho.

Ongezeko Licha ya Upinzani

Baadaye, wote wawili walipata vitabu vingine vinavyofafanua Biblia kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Punde si punde, Baba na Andreas walichochewa kuwaambia wanakijiji wenzao kweli za Biblia walizokuwa wakijifunza. Kwa sababu ya kuhubiri, walipingwa vikali na makasisi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki na watu wengine waliofikiri kwamba Mashahidi wa Yehova ni hatari.

Wanakijiji wengi waliwaheshimu walimu hao wawili wa Biblia. Baba yangu alijulikana kuwa mwenye fadhili na mkarimu. Mara nyingi alisaidia familia maskini. Nyakati nyingine angeondoka nyumbani kisiri wakati wa usiku na kupeleka ngano au mkate milangoni mwa familia zenye uhitaji. Ujumbe wa wahudumu hao wawili uliwavutia watu kwa sababu ya mwenendo wao wa Kikristo usio na ubinafsi.—Mathayo 5:16.

Hivyo, karibu watu 12 walipendezwa na ujumbe wa Biblia. Walipoendelea kuelewa kweli, waliona uhitaji wa kukutana katika nyumba mbalimbali wakiwa kikundi ili kujifunza Biblia. Karibu mwaka wa 1934, Nikos Matheakis, mhudumu wa wakati wote kutoka Ugiriki alifika Saiprasi na akakutana na kikundi cha Xylophagou. Akiwa mwenye subira na bidii, Ndugu Matheakis alikipanga kikundi hicho na kukisaidia kuelewa Maandiko vizuri. Kikundi hicho ndicho kilichokuwa kutaniko la kwanza la Mashahidi wa Yehova huko Saiprasi.

Kazi ya Kikristo ilipoendelea na watu wengi kukubali kweli ya Biblia, akina ndugu waliona uhitaji wa kuwa na mahali pa kufanyia mikutano. Ndugu yangu mkubwa George, na mke wake, Eleni, walikubali chumba walichotumia kama ghala kitumiwe kwa ajili ya mikutano. Ghala hiyo iliyokuwa karibu na nyumba yao, ilifanyiwa marekebisho na kuwa mahali panapofaa kufanyia mikutano. Hivyo, akina ndugu wakawa na Jumba la Ufalme la kwanza kisiwani. Walifurahi kama nini! Nacho kilikuwa kichocheo kilichoje cha ongezeko zaidi!

Kuuthamini Ukweli

Mnamo 1938, nikiwa na umri wa miaka 16, niliamua kuwa seremala. Hivyo, Baba akanipeleka Nicosia, jiji kuu la Saiprasi. Kwa sababu alikuwa na utambuzi, alipanga niishi na Nikos Matheakis. Ndugu huyo mwaminifu angali anakumbukwa na watu wengi kisiwani kwa sababu ya bidii na ukarimu wake. Shauku na ujasiri wake ni sifa zilizohitajiwa na Mkristo yeyote huko Saiprasi siku hizo.

Ndugu Matheakis alinisaidia sana kuwa na msingi mzuri wa ujuzi wa Biblia na kufanya maendeleo ya kiroho. Nilipoishi naye, nilihudhuria mikutano yote iliyofanywa nyumbani kwake. Kwa mara ya kwanza nilihisi kwamba upendo wangu kwa Yehova ulikuwa unaongezeka. Niliazimia kusitawisha uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Baada ya miezi michache, nilimuuliza Ndugu Matheakis ikiwa ninaweza kujiunga naye katika kazi ya kuhubiri. Huo ulikuwa mwaka wa 1939.

Baada ya muda, nilirudi nyumbani kutembelea familia yetu. Kuwa pamoja na baba yangu kwa muda kulizidisha usadikisho wangu kwamba nilikuwa nimeupata ukweli na kusudi la maisha. Mnamo Septemba 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza. Vijana wengi wa umri wangu walijitolea kwenda vitani, lakini kwa kufuata mwongozo wa Biblia, niliamua kutounga mkono upande wowote. (Isaya 2:4; Yohana 15:19) Mwaka huohuo, nikajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa mnamo 1940. Kwa mara ya kwanza nilihisi kwamba siogopi wanadamu!

Mnamo 1948, nilimwoa Efprepia. Tulipata watoto wanne. Baadaye tulitambua kwamba tulihitaji kujitahidi sana ili kuwalea “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Tulisali na kujitahidi kuwasaidia watoto wetu kumpenda Yehova sana na kuheshimu sheria na kanuni zake.

Matatizo ya Afya

Katika mwaka wa 1964, nilipokuwa na umri wa miaka 42, nilianza kufa ganzi mkono na mguu wangu wa kulia. Pole kwa pole, hali hiyo ikaenea upande wa kushoto. Iligunduliwa kwamba nina ugonjwa unaoharibu misuli. Ugonjwa huo hauna tiba na unasababisha kupooza. Habari hizo zilinihuzunisha sana. Ugonjwa huo ulitokea haraka na ghafula sana! Nilikuwa na hasira na ghadhabu, nami nilijiuliza hivi: ‘Kwa nini hali hii imenipata? Kwani nimefanya nini ili niteseke hivi?’ Hata hivyo, baada ya muda niliweza kushinda mshtuko niliopata nilipojua nina ugonjwa huo. Lakini baadaye nililemewa na wasiwasi nami sikujua litakalonipata. Nilikuwa na maswali mengi akilini. Je, nitapooza kabisa hivi kwamba nilazimike kuwategemea wengine? Nitaikabilije hali hiyo? Je, nitaweza kutosheleza mahitaji ya familia yangu, yaani, mke na watoto wangu? Kwa kweli, mawazo hayo yalinitia uchungu.

Wakati huo mgumu zaidi maishani mwangu, nilisali sana kwa Yehova kuliko wakati mwingine wowote, na kumweleza kwa unyoofu wasiwasi na mahangaiko yangu yote. Nilisali usiku na mchana nikitokwa machozi. Baada ya muda nilifarijika. Niliona maneno haya yenye kufariji ya Wafilipi 4:6, 7 yakitimia katika kisa changu: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”

Kukabiliana na Ugonjwa wa Kupooza

Afya yangu iliendelea kudhoofika, nami nikalazimika kubadili maisha yangu. Kwa kuwa singeendelea kufanya kazi ya useremala, niliamua kufanya kazi ambayo haikuhitaji nguvu nyingi na ambayo ilifaana na hali yangu ya kimwili na iliyoniwezesha kupata riziki kwa ajili ya familia yangu. Mwanzoni, nilitumia gari dogo kusafirisha na kuuza aiskrimu. Nilifanya kazi hiyo kwa miaka sita hivi mpaka nilipolazimika kutumia kiti cha magurudumu. Kisha, nikaanza kufanya kazi mbalimbali ambazo ningeweza.

Tangu mwaka wa 1990, afya yangu imezorota sana hivi kwamba siwezi kufanya kazi yoyote. Sasa ninategemea wengine wanisaidie hata kufanya mambo ambayo ni ya kawaida kwa mtu mwenye afya. Mimi husaidiwa kupanda kitandani, kuoga, na kuvaa. Ili nihudhurie mikutano ya Kikristo, ninasukumwa kwa kiti cha magurudumu, kisha kuingizwa ndani ya gari. Tunapofika kwenye Jumba la Ufalme, inabidi nitolewe ndani ya gari na kuwekwa kwenye kiti cha magurudumu ili nisukumwe. Wakati wa mikutano, mimi hutumia kifaa fulani kupasha joto miguu yangu.

Hata hivyo, licha ya kupooza, ninahudhuria mikutano yote kwa ukawaida. Ninaelewa kwamba Yehova hutufundisha mikutanoni, na kwamba kuwa pamoja na ndugu na dada zangu wa kiroho ni ulinzi hakika na chanzo cha msaada na utegemezo. (Waebrania 10:24, 25) Nimefaidika kwa kutembelewa kwa ukawaida na waamini wenzangu walio wakomavu kiroho. Kwa hakika ninahisi kama alivyohisi Daudi: “Kikombe changu kimejazwa vizuri.”—Zaburi 23:5.

Mke wangu mpendwa amekuwa msaada mkubwa katika miaka yote hiyo. Watoto wangu pia wamenisaidia sana. Kwa miaka mingi sasa, wameshughulikia mahitaji yangu ya kila siku. Kazi wanayofanya si rahisi, na kadiri miaka inavyosonga ndivyo inavyokuwa vigumu zaidi kunishughulikia. Kwa kweli wameonyesha subira na kujitolea, nami namwomba Yehova aendelee kuwabariki.

Sala ni msaada mwingine mkubwa kutoka kwa Yehova wa kuwaimarisha watumishi wake. (Zaburi 65:2) Yehova amejibu sala zangu kwa kunipa nguvu za kuendelea katika imani kwa miaka yote hiyo. Hasa ninapohisi nimevunjika moyo, sala hunituliza na kunisaidia kudumisha shangwe. Kuwasiliana na Yehova kwa ukawaida hunichangamsha na kunichochea kuendelea kusonga mbele. Ninasadiki kabisa kwamba Yehova husikia sala za watumishi wake na kuwapa amani ya akili wanayohitaji.—Zaburi 51:17; 1 Petro 5:7.

Zaidi ya yote, ninaimarishwa kila wakati ninapokumbuka kwamba mwishowe Mungu atawaponya wote watakaopata zawadi ya uzima katika Paradiso chini ya utawala wa Ufalme wa Mwana wake, Yesu Kristo. Mara nyingi nimedondokwa na machozi ya shangwe ninapotafakari tumaini hilo zuri ajabu.—Zaburi 37:11, 29; Luka 23:43; Ufunuo 21:3, 4.

Kutumikia Nikiwa Mhudumu wa Wakati Wote

Mwaka wa 1991 hivi, baada ya kuchanganua hali yangu, niligundua kwamba njia bora zaidi ya kuepuka kujisikitikia ni kuendelea kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme. Mwaka huohuo, nikaanza utumishi wa wakati wote.

Kwa sababu ya ulemavu, mara nyingi ninahubiri sana kwa barua. Hata hivyo, siwezi kuandika kwa urahisi; inanibidi kujitahidi sana ili niweze kuandika. Inakuwa vigumu kushika kalamu kwa nguvu kwa kuwa mkono wangu umedhoofishwa na ugonjwa huo unaoharibu misuli. Hata hivyo, kupitia sala na kuvumilia, nimekuwa nikihubiri kwa zaidi ya miaka 15 kwa barua. Mimi hutumia pia simu kuhubiri. Ninatumia kila nafasi kuzungumza na watu wa ukoo, marafiki, na majirani ambao hunitembelea nyumbani kuhusu tumaini langu la ulimwengu mpya na dunia Paradiso.

Kwa kufanya hivyo, nimefurahia mambo mengi yenye kutia moyo. Nilifurahi sana kuona mmoja wa wajukuu wangu ambaye nilimfunza Biblia miaka 12 hivi iliyopita akifanya maendeleo ya kiroho na kuthamini kweli ya Biblia. Akichochewa na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia, amekuwa mshikamanifu na imara katika msimamo wa Kikristo wa kutokuwamo.

Ninapendezwa hasa wakati watu ninaowaandikia wanapowasiliana nami wakitaka habari zaidi kuhusu Biblia. Nyakati nyingine, baadhi yao huomba vichapo zaidi vya Biblia. Kwa mfano, mwanamke mmoja alinipigia simu na kunishukuru kwa barua yenye kutia moyo niliyomtumia mume wake. Barua hiyo ilimpendeza sana. Hivyo, nikawa na mazungumzo mengi ya Biblia pamoja naye na mume wake nyumbani kwangu.

Matumaini

Kwa miaka mingi, nimeona idadi ya watangazaji wa Ufalme ikiongezeka katika sehemu hii ya ulimwengu. Lile Jumba dogo la Ufalme karibu na nyumba ya ndugu yangu George, limepanuliwa na kufanyiwa marekebisho mara kadhaa. Ni mahali maridadi pa ibada panapotumiwa na makutaniko mawili ya Mashahidi wa Yehova.

Baba alikufa mnamo 1943, akiwa na umri wa miaka 52. Lakini aliacha urithi wenye thamani wa kiroho! Watoto wake wanane walipenda kweli na bado wanamtumikia Yehova. Sasa kuna makutaniko matatu yakiwa na jumla ya wahubiri wa Ufalme 230 katika kijiji cha Xylophagou, ambapo Baba alizaliwa, na katika kijiji kingine cha karibu!

Matokeo hayo mazuri yameniletea shangwe kubwa sana. Sasa, nikiwa na umri wa miaka 83, ninaweza kusema kwa uhakika maneno haya ya mtunga-zaburi: “Wana-simba wenye manyoya shingoni wamekuwa na vichache na kukaa njaa; lakini kwa wale wanaomtafuta Yehova, hawatakosa chochote chema.” (Zaburi 34:10) Ninangoja kwa hamu wakati ambapo unabii huu wa Isaya 35:6 utakapotimizwa: “Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya.” Licha ya kuwa mlemavu, nimeazimia kuendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe mpaka wakati huo.

[Ramani katika ukurasa wa 17]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

UTURUKI

SIRIA

LEBANONI

SAIPRASI

Nicosia

Xylophagou

Bahari ya Mediterania

[Picha katika ukurasa wa 17]

Jumba la Ufalme la kwanza huko Xylophagou linalotumiwa mpaka leo

[Picha katika ukurasa wa 18]

Nikiwa na Efprepia mwaka wa 1946, na leo

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mimi hufurahia kuhubiri kwa simu na kwa barua