Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika Sheria ya Musa, kwa nini mahusiano fulani ya ngono yalionwa kuwa yanamfanya mtu kuwa “asiye safi”?

Mungu alikusudia kuwe na ngono ili wanadamu waweze kuzaana na ili ifurahiwe na wenzi wa ndoa. (Mwanzo 1:28; Methali 5:15-18) Hata hivyo, katika sura ya 12 na 15 ya Mambo ya Walawi, tunapata amri zinazohusu uchafu unaohusianishwa na shahawa, hedhi, na kuzaa. (Mambo ya Walawi 12:1-6; 15:16-24) Amri hizo zilizopewa Waisraeli wa kale zilisaidia kuboresha afya, kudumisha viwango vya juu vya maadili, na kukazia utakatifu wa damu, na uhitaji wa upatanisho kwa ajili ya dhambi.

Mbali na mambo mengine, matakwa ya Sheria ya Musa kuhusu ngono yaliboresha afya ya Waisraeli kwa ujumla. Kitabu kimoja (The Bible and Modern Medicine) kinasema: “Amri iliyokataza ngono wakati wa hedhi ilithibitika kuwa njia bora ya kuzuia magonjwa fulani ya zinaa . . . na kansa ya mlango wa tumbo la uzazi.” Sheria hizo ziliwalinda watu wa Mungu kutokana na magonjwa ambayo huenda hawangeyajua wala kuyagundua. Mahusiano safi ya ngono yalisaidia taifa hilo liongezeke, na Mungu alikuwa ameliahidi ongezeko na ufanisi. (Mwanzo 15:5; 22:17) Sheria hizo pia zilijali hisia za watu wa Mungu. Kupitia sheria hizo, waume na wake walijifunza kudhibiti tamaa zao za ngono.

Hata hivyo, mambo yaliyohusianishwa hasa na uchafu unaotokana na ngono, ni kumwagika kwa damu. Sheria za Yehova kuhusu damu ziliwaonyesha Waisraeli umuhimu wa utakatifu wa damu na pia sehemu muhimu ya damu katika ibada ya Yehova, hasa kuhusu dhabihu na upatanisho kwa ajili ya dhambi.—Mambo ya Walawi 17:11; Kumbukumbu la Torati 12:23, 24, 27.

Hivyo, mambo hayo yaliyoelezwa kwa kina katika Sheria kuhusu damu yanahusiana sana na kutokamilika kwa wanadamu. Waisraeli walijua kwamba baada ya Adamu na Hawa kutenda dhambi, hawangeweza kuzaa watoto wakamilifu. Watoto wao wote wangeathiriwa na matokeo ya dhambi yao, yaani, kutokamilika na kufa. (Waroma 5:12) Kwa sababu hiyo, wazazi wangeweza tu kupitisha kutokamilika na dhambi kwa watoto wao, ingawa viungo vya uzazi vya kibinadamu vilikusudiwa kupitisha uhai mkamilifu kupitia mpango wa ndoa.

Hivyo, matakwa ya Sheria kuhusu utakaso hayangewakumbusha Waisraeli kuhusu dhambi waliyorithi tu bali pia uhitaji wa dhabihu ya fidia ili kufunika dhambi na kurudisha ukamilifu wa kibinadamu. Ni wazi kwamba dhabihu za wanyama walizotoa hazikutimiza hayo. (Waebrania 10:3, 4) Sheria ya Musa ilikusudiwa iwaongoze kwa Kristo na kuwasaidia kuelewa kwamba ni kupitia dhabihu ya uhai mkamilifu wa Yesu tu ndio wanadamu wanaweza kupata msamaha wa dhambi, na kuwawezesha walio waaminifu kupata uzima wa milele.—Wagalatia 3:24; Waebrania 9:13, 14.