Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Anawajali Waliozeeka

Mungu Anawajali Waliozeeka

Mungu Anawajali Waliozeeka

LEO, haishangazi kwamba ulimwenguni pote wazee huteswa. Tangu zamani, Biblia ilitabiri kwamba katika “siku za mwisho” za mfumo huu usiomwogopa Mungu, watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na upendo wa asili.” (2 Timotheo 3:1-3) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “upendo wa asili” linaweza kutia ndani upendo ambao kwa kawaida uko kati ya watu wa familia. Kulingana na unabii wa Biblia, leo upendo kama huo umepotea kabisa.

Tofauti na wale wanaowatesa wazee, Yehova Mungu anawathamini na kuwajali sana watu wenye umri mkubwa. Ona jinsi jambo hilo linavyoonyeshwa katika Biblia.

“Mwamuzi wa Wajane”

Maandiko ya Kiebrania yanathibitisha jinsi Yehova Mungu anavyowajali wazee. Kwa mfano, kwenye Zaburi 68:5, Daudi anamtaja Mungu kuwa “mwamuzi wa wajane,” ambao kwa kawaida ni wazee. * Katika tafsiri nyingine za Biblia, neno “mwamuzi” linatafsiriwa “mteteaji” na “mlinzi.” Ni wazi kwamba Yehova huwajali wajane. Hiyo ndiyo sababu Biblia inasema kwamba wakiteswa, hasira ya Yehova huwaka. (Kutoka 22:22-24) Mungu na watumishi wake wanawathamini sana wajane na waaminifu wote waliozeeka. Andiko la Methali 16:31 linaonyesha maoni ya Yehova Mungu na ya watu wake linaposema hivi: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.”

Haishangazi kwamba kuwaheshimu waliozeeka kulikuwa sehemu kuu ya Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli. Waisraeli waliagizwa hivi: “Unapaswa kusimama mbele ya mtu mwenye mvi, nawe umwonyeshe ufikirio mtu mzee, nawe umwogope Mungu wako. Mimi ni Yehova.” (Mambo ya Walawi 19:32) Hivyo, katika Israeli, kuwaheshimu waliozeeka kulihusianishwa sana na uhusiano wa mtu pamoja na Yehova Mungu. Mtu ambaye aliwatesa wazee hangedai kwamba anampenda Mungu.

Ni kweli kwamba Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa. Hata hivyo, wako chini ya “sheria ya Kristo,” ambayo inaongoza sana mwenendo na mtazamo wao, kutia ndani kuwapenda na kuwahangaikia wazazi na wazee. (Wagalatia 6:2; Waefeso 6:1-3; 1 Timotheo 5:1-3) Wakristo huonyesha upendo si kwa sababu wanaagizwa wafanye hivyo lakini kwa sababu wanachochewa kutoka moyoni. Mtume Petro alihimiza hivi: “Pendaneni sana kutoka moyoni.”—1 Petro 1:22.

Mwanafunzi Yakobo anaonyesha sababu inayopaswa kutuchochea hata zaidi kuwatunza waliozeeka. Aliandika hivi: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao, na kuendelea kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu.” (Yakobo 1:27) Yakobo anakazia wazo muhimu lenye kuvutia. Maneno yake yanaonyesha jinsi Yehova anavyowathamini wapendwa hao.

Hivyo, haitoshi tu kuepuka kuwatesa wazee. Badala yake, tunapaswa kuonyesha kwamba tunawahangaikia sana kwa kuwatimizia mambo muhimu. (Ona kisanduku “Upendo Huonyeshwa kwa Matendo,” kwenye ukurasa wa 6-7.) Yakobo aliandika hivi: “Imani bila matendo imekufa.”—Yakobo 2:26.

Kuwafariji “Katika Dhiki Yao”

Tunajifunza jambo lingine kutokana na maneno ya Yakobo. Ona kwamba Yakobo aliwaambia Wakristo wawatunze wajane “katika dhiki yao.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “dhiki” linamaanisha hasa taabu, matatizo, au mateso yanayotokana na mikazo ya hali zetu maishani. Hakuna shaka kwamba wengi wa waliozeeka miongoni mwetu wanapatwa na taabu kama hizo. Baadhi yao huhisi upweke. Wengine wanashuka moyo sana kwa sababu ya udhaifu unaotokana na uzee. Hata wale wanaoshiriki kikamilifu katika utumishi wa Mungu huenda wakavunjika moyo. Fikiria mfano wa John, * mhubiri mwaminifu wa Ufalme wa Mungu kwa zaidi ya miaka 40, na ambaye ametumia miaka 30 kati ya hiyo katika utumishi wa pekee wa wakati wote. Sasa akiwa na zaidi ya miaka 80, John anasema kwamba nyakati nyingine yeye huhisi kuvunjika moyo. Anasema: “Mara nyingi mimi hukumbuka makosa yangu, makosa mengi sana. Ninafikiri sikuzote kwamba ningefanya vizuri zaidi.”

Watu kama hao wanaweza kufarijiwa kwa kujua kwamba, ingawa Yehova ni mkamilifu, hatutazamii tutende kama watu wakamilifu. Ingawa Yehova anajua makosa yetu, Biblia inasema hivi kumhusu: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Naam, Yehova hakazii uangalifu makosa yetu lakini yeye huona yaliyo moyoni. Tunajuaje hilo?

Mfalme Daudi, ambaye alifanya makosa mengi, aliongozwa kwa roho ya Mungu kuandika maneno yafuatayo, kwenye Zaburi 139:1-3: “Ee Yehova, umenichunguza kabisa, nawe unanijua. Wewe mwenyewe umepata kujua kuketi kwangu na kusimama kwangu. Umeichunguza fikira yangu tokea mbali. Umepima kusafiri kwangu na kulala kwangu nikiwa nimejinyoosha, nawe umezijua njia zangu zote.” Hapa neno hili “umepima” linamaanisha “kupepeta,” kama vile mkulima anavyopepeta makapi ili kubaki na nafaka. Kwa mwongozo wa roho ya Mungu, Daudi anatuhakikishia kwamba Yehova anaweza kupepeta au kusamehe makosa yetu na kukumbuka mambo mazuri tuliyofanya.

Baba yetu wa mbinguni mwenye rehema anakumbuka na kuthamini mambo mazuri tunayofanya maadamu tunaendelea kuwa waaminifu kwake. Naam, Biblia inasema kwamba Mungu angeona jambo hilo kuwa ukosefu wa uadilifu ikiwa angesahau kazi yetu na upendo ambao tumeonyesha kwa ajili ya jina lake.—Waebrania 6:10.

“Mambo ya Zamani Yamepitilia Mbali”

Biblia inaonyesha kwamba hapo mwanzoni Mungu hakukusudia wanadamu wapatwe na matatizo ya uzee. Wanadamu walianza kupatwa na matatizo ya uzee baada tu ya wazazi wetu wa kwanza, mwanamume na mwanamke wa kwanza, kumwasi Muumba wao. (Mwanzo 3:17-19; Waroma 5:12) Hali hiyo haitaendelea milele.

Kama ilivyotajwa tayari, hali nyingi mbaya zinazotupata leo, kutia ndani kuwatesa wazee, ni uthibitisho wa kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. (2 Timotheo 3:1) Mungu anakusudia kuondoa matokeo ya dhambi, kutia ndani madhara ya uzee na kifo. Biblia inasema hivi: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, maumivu yanayotokana na uzee yatakwisha. Wazee hawatateswa tena. (Mika 4:4) Hata wale waliokufa na ambao wako katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa ili wao pia wapewe nafasi ya kuishi milele katika dunia paradiso. (Yohana 5:28, 29) Wakati huo, itakuwa wazi kuliko wakati mwingine kwamba Yehova Mungu anawajali si wazee tu, bali pia wote wanaomtii.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Bila shaka, wajane wengine si wazee. Kwa mfano, andiko la Mambo ya Walawi 22:13 linaonyesha kwamba Mungu huwajali pia wajane walio vijana.

^ fu. 11 Si jina lake halisi.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Upendo Huonyeshwa kwa Matendo

Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wazee wa kutaniko ndio walio katika mstari wa mbele kuwaonyesha heshima waliozeeka. Wanalichukua kwa uzito shauri hili la mtume Petro: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu.” (1 Petro 5:2) Kuwatunza watu wenye umri mkubwa ni sehemu ya kazi ya kulitunza kundi la Mungu. Hata hivyo, huenda hilo likahusisha nini?

Ili kujua vizuri mahitaji ya watu waliozeeka, mtu anahitaji kuwa mwenye subira na kuwatembelea ili kuongea nao. Labda wanahitaji mtu wa kuwasaidia kununua vitu dukani, kufanya usafi, kuwapeleka kwenye mikutano ya Kikristo, kuwasomea Biblia na vichapo vya Kikristo, na mambo mengine mengi. Inapowezekana, mipango mizuri inapaswa kufanywa na kutekelezwa. *

Namna gani ikiwa ndugu au dada mwenye umri mkubwa kutanikoni anahitaji pesa kwa sababu ya hali ya dharura? Kwanza, itakuwa vizuri kuona ikiwa ndugu au dada huyo ana watoto au watu wa ukoo wanaoweza kumsaidia. Hilo linapatana na yale yanayosemwa kwenye 1 Timotheo 5:4: “Ikiwa mjane yeyote ana watoto au wajukuu, acha hao wajifunze kwanza kuzoea ujitoaji-kimungu nyumbani kwao wenyewe na kuendelea kuwalipa wazazi na wazazi wa wazazi wao malipo yanayowastahili, kwa maana hilo linakubalika machoni pa Mungu.”

Huenda ikawa mzee huyo anahitaji kusaidiwa kujua iwapo anaweza kupata huduma ambazo serikali inatoa. Labda baadhi ya watu kutanikoni wangependa kusaidia. Ikiwa haiwezekani kupata msaada kwa njia hizo, wazee wa kutaniko wanaweza kuamua ikiwa mtu huyo anastahili kusaidiwa na kutaniko. Katika visa fulani, misaada kama hiyo iliruhusiwa katika kutaniko la karne ya kwanza, kwa kuwa mtume Paulo alimwandikia hivi mfanyakazi mwenzake Timotheo: “Mjane ambaye amekuwa mwenye umri usiopungua miaka 60, mke wa mume mmoja, awekwe katika orodha, mwenye kutolewa ushahidi juu ya matendo yaliyo mazuri, ikiwa alilea watoto, ikiwa alipokea wageni, ikiwa aliosha miguu ya watakatifu, ikiwa aliwasaidia wale walio katika dhiki, ikiwa alifuata kwa bidii kila tendo jema.”—1 Timotheo 5:9, 10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 25 Kwa habari zaidi, ona makala “Kutimiza Mahitaji ya Walio na Umri Mkubwa Kati Yetu—Takwa Gumu la Kikristo,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 1988.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Dorkasi aliwajali wajane waliokuwa katika uhitaji.—Matendo 9:36-39