Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pata Uradhi kwa Kutumia Kanuni za Biblia

Pata Uradhi kwa Kutumia Kanuni za Biblia

Pata Uradhi kwa Kutumia Kanuni za Biblia

BILA shaka umewahi kumwona paka akiwa amejikunja huku akiwa amelala kuonyesha kwamba ameridhika. Ingekuwa vizuri kama nini kujikunja kama paka huyo na kufurahia uradhi kama huo! Hata hivyo, kwa watu wengi, uradhi haupatikani kwa urahisi wala haudumu. Kwa nini?

Kwa sababu sisi hufanya makosa kwa kutokamilika na lazima tuvumilie makosa ya wengine. Isitoshe, tunaishi katika kipindi ambacho Biblia inakiita “siku za mwisho,” ambacho ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Hata ikiwa tulithamini uradhi tuliokuwa nao tulipokuwa watoto, wengi wetu sasa tunaathiriwa na ‘nyakati hizi za hatari.’ Je, tunaweza kupata uradhi leo?

Ona kwamba Maandiko yanasema kuwa hizi nyakati za hatari zingekuwa ngumu kushughulika nazo wala si kwamba haingewezekana kushughulika nazo. Tunaweza kushughulika nazo kwa kutumia kanuni za Biblia. Huenda tusiweze kutatua matatizo yetu kila wakati, lakini tunaweza kupata kiasi fulani cha uradhi. Hebu tuzungumzie kanuni tatu zitakazotusaidia.

Dumisha Maoni Yanayofaa

Ili tupate uradhi, ni lazima tudumishe maoni yanayofaa kuhusu kupungukiwa kwetu na kupungukiwa kwa wengine. Katika barua aliyowaandikia Waroma, mtume Paulo anasema hivi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Hatuwezi kuelewa kikamili sehemu mbalimbali za utukufu wa Yehova. Mfano mmoja unaonyeshwa na maneno ya Mwanzo 1:31: “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.” Wakati wowote Yehova anapoamua kutazama kile ambacho amefanya, sikuzote anaweza kusema ‘ni chema sana.’ Hakuna mwanadamu anayeweza kusema hivyo sikuzote kuhusu kazi zake. Ili tupate uradhi, kwanza ni lazima tukubali kwamba tumepungukiwa. Hata hivyo, mengi yanahusika. Tunapaswa kuelewa na kukubali maoni ya Yehova.

Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “dhambi” linatokana na neno linalomaanisha kukosa shabaha. (Waroma 3:9) Kwa mfano: Wazia mtu anayetazamia kupata tuzo katika mashindano ya kugonga shabaha kwa mshale. Ana mishale mitatu. Anarusha mshale wa kwanza lakini anakosa shabaha kwa meta moja. Akitumia mshale wa pili analenga vizuri lakini tena anakosa shabaha kwa sentimeta 30. Analenga mshale wa tatu kwa makini sana lakini anakosea tu kwa sentimeta mbili. Alikuwa karibu sana, lakini bado hakugonga shabaha.

Sisi sote ni kama mtu huyo aliyekosa shabaha. Wakati mwingine ‘tunakosa shabaha’ sana. Nyakati nyingine tunajitahidi lakini bado tunakosa shabaha. Sisi hukata tamaa kwa sababu tunajitahidi sana, lakini bado hatufanikiwi. Sasa, acheni tuzungumze tena kuhusu yule mpiga-mishale.

Pole kwa pole anaondoka akiwa amehuzunika kwa sababu alitaka sana ile tuzo. Kwa ghafula, yule anayesimamia mashindano hayo anamwita na kumpa tuzo, akimwambia: “Ninataka kukupa tuzo hii kwa sababu ninakupenda, nami niliona jinsi ulivyojitahidi sana.” Mpiga-mishale huyo anafurahi sana!

Naam, anafurahi sana! Kila mtu atakayepokea kutoka kwa Mungu “zawadi” ya uzima wa milele akiwa mkamilifu atahisi hivyo. (Waroma 6:23) Baadaye, kila kitu ambacho watu watafanya kitakuwa kizuri, hawatakosa shabaha tena kamwe. Watapata uradhi kamili. Kwa sasa, tukiwa na maoni hayo, tutajihisi vizuri na kuhisi vizuri kuhusu wengine.

Tambua Kwamba Kila Kitu Kinahitaji Wakati

Ni kweli kwamba kila kitu huchukua wakati. Hata hivyo, je, umeona jinsi inavyokuwa vigumu kuridhika wakati kile unachotazamia kinapoonekana kuchukua muda mrefu kuliko ulivyotazamia au wakati hali mbaya inapoonekana kuchukua muda mrefu kuliko ulivyofikiri? Hata hivyo, wengine wameweza kudumisha uradhi katika hali kama hizo. Fikiria mfano wa Yesu.

Kabla ya kuja duniani, Yesu aliweka kielelezo kizuri cha kuwa mtiifu huko mbinguni. Hata hivyo, “alijifunza kutii” akiwa hapa duniani. Jinsi gani? “Kutokana na mambo aliyoteseka.” Mwanzoni, alikuwa ameona watu wakiteseka lakini hakuwa amewahi kuteseka yeye mwenyewe. Alipokuwa duniani, hasa tangu alipobatizwa huko Yordani mpaka alipokufa huko Golgotha, alipitia majaribu mengi. Hatujui mambo yote kuhusu jinsi Yesu ‘alivyofanywa mkamilifu’ katika hali hizo, lakini tunajua kwamba hatua hiyo ilichukua wakati.—Waebrania 5:8, 9.

Yesu alifaulu kwa sababu alitafakari “shangwe iliyowekwa mbele yake,” yaani, zawadi ya uaminifu wake. (Waebrania 12:2) Hata hivyo, wakati mwingine “alitoa dua na pia maombi . . . pamoja na vilio vyenye nguvu na machozi.” (Waebrania 5:7) Huenda wakati mwingine tukasali kwa njia hiyohiyo. Yehova huonaje sala hizo? Mstari huohuo unaonyesha kwamba Yehova alimsikiliza Yesu “vizuri.” Mungu atatusikiliza pia. Kwa nini?

Kwa sababu Yehova anajua kupungukiwa kwetu, naye hutusaidia. Kuna mambo ambayo hatuwezi kuvumilia. Msemo mmoja huko Benin, barani Afrika, unasema: “Maji mengi hatimaye huwaua hata vyura.” Yehova anajua vizuri wakati tunapokaribia kushindwa kuvumilia. Kwa upendo anaandaa “rehema na . . . fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa.” (Waebrania 4:16) Hivyo ndivyo alivyomtendea Yesu, naye amewatendea hivyo wengine wengi. Fikiria jinsi Monika alivyopata msaada huo.

Monika alipokuwa akikua, hakuwa na wasiwasi wowote naye alikuwa mwenye shauku na mtazamo mzuri. Mnamo 1968, akiwa na umri wa miaka 20 hivi, alishtuka alipoambiwa kwamba ana ugonjwa wa neva, ugonjwa ambao mara nyingi hufanya sehemu moja ya mwili kupooza. Hilo lilibadili maisha yake kabisa na akahitaji kufanya marekebisho makubwa katika utumishi wake wa wakati wote. Monika alitambua kwamba ugonjwa huo ungeendelea kwa muda mrefu. Miaka 16 baadaye alisema: “Bado ugonjwa huu hauwezi kutibiwa na huenda ukaendelea mpaka wakati mfumo mpya wa Mungu utakapofanya mambo yote kuwa mapya.” Alikubali kwamba haikuwa rahisi: “Ingawa rafiki zangu husema kwamba nina shauku na eti bado nina furaha kama zamani, . . . rafiki zangu wa karibu sana wanajua kwamba wakati mwingine mimi hulia sana.”

Hata hivyo, Monika alisema hivi: “Nimejifunza kuwa na subira na kufurahia maendeleo yoyote madogo katika afya yangu. Uhusiano wangu pamoja na Yehova umeimarika kwa kuwa nimeelewa kwamba wanadamu hawana uwezo wa kukabiliana na magonjwa. Ni Yehova peke yake anayeweza kuponya kabisa.” Kwa msaada wa Yehova, Monika amedumisha uradhi na amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 40.

Ni kweli kwamba hali kama ya Monika ni ngumu. Lakini kwa hakika, utapata uradhi ukitambua kwamba mambo mengine huenda yakachukua muda mrefu kuliko unavyotazamia. Kama Monika, wewe pia unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakupa “msaada kwa wakati unaofaa.”

Usijilinganishe na Wengine —Weka Miradi Unayoweza Kufikia

Wewe ni tofauti na watu wengine. Hakuna mtu aliye sawa kabisa na wewe. Msemo fulani wa lugha ya Kiguni barani Afrika unaonyesha wazo hilo kwa njia hii rahisi: “Vidole vyote havilingani.” Ingekuwa upumbavu kulinganisha kidole kimoja na kingine. Hungependa Yehova akulinganishe na mtu mwingine, wala hatawahi kufanya hivyo. Hata hivyo, kila mahali wanadamu hupenda kujilinganisha na wengine na hilo linaweza kufanya wasiwe na uradhi. Ona mfano ambao Yesu alitoa kuhusu jambo hilo kama tunavyosoma kwenye Mathayo 20:1-16.

Yesu alizungumza kuhusu “bwana” fulani ambaye alihitaji wafanyakazi katika shamba lake la mizabibu. Aliwaona watu fulani wasio na kazi akawaajiri “asubuhi na mapema,” labda saa 12. Wakakubaliana kwamba atawalipa mshahara wa nyakati hizo, yaani, dinari moja kwa kufanya kazi muda wa saa 12. Bila shaka, watu hao walifurahi kupata kazi kwa mshahara uleule wa kawaida. Baadaye, bwana huyo aliona watu wengine wasio na kazi akawaajiri kuanzia saa 3 asubuhi, wengine saa 6, wengine saa 9, na hata wengine saa 11 jioni. Hakuna yeyote kati ya watu hao ambaye angefanya kazi siku nzima. Bwana huyo aliwaahidi kuwalipa “kilicho haki,” nao wakakubali.

Ilipofika jioni, bwana huyo alimwamuru msimamizi wake awalipe mshahara. Alimwambia awaite wafanyakazi na kuwalipa kwanza wale walioajiriwa mwisho. Hao walikuwa wamefanya kazi kwa saa moja tu, lakini inashangaza kwamba walipata mshahara wa siku nzima. Tunaweza kuwazia mazungumzo ambayo yalifuata. Inaelekea wale waliokuwa wamefanya kazi kwa saa 12 walikata kauli kwamba watapokea zaidi. Lakini wao pia walilipwa mshahara uleule.

Walitendaje? “Walipoipokea wakaanza kumnung’unikia mwenye nyumba na kusema, ‘Hawa wa mwisho walifanya kazi kwa saa moja; na bado umewafanya kuwa sawa na sisi tuliofanya kazi ngumu mchana kutwa katika lile joto lenye kuchoma!’”

Lakini, bwana huyo aliona mambo kwa njia tofauti. Alisema kwamba walipokea kile walichokubaliana, naye hakupunguza chochote. Kwa wale wengine, aliamua kuwalipa mshahara wa siku nzima, zaidi ya vile walivyotazamia. Kwa kweli, hakuna aliyepokea chini ya kiasi kile walichokubaliana; wengi walipata zaidi ya kile walichotazamia. Basi, mwishowe, bwana huyo aliuliza hivi: “Je, si halali kwangu kufanya kile ninachotaka na vitu vyangu mwenyewe?”

Wazia sasa ikiwa yule msimamizi angewalipa wale wa kwanza, kisha waondoke mara moja. Wangeridhika. Walinung’unika tu walipoona kwamba wale wengine walikuwa wamepokea mshahara uleule kwa kufanya kazi kwa muda mfupi. Hilo liliwakasirisha, hata wakaanza kumnung’unikia bwana huyo ambaye walipaswa kumshukuru kwa sababu ya kuwapa kazi.

Mfano huo unaonyesha vizuri yale yanayotukia tunapojilinganisha na wengine. Ukitafakari juu ya uhusiano wako pamoja na Yehova na kumshukuru kwa baraka ambazo amekupa, utapata uradhi. Usilinganishe hali yako na ya wengine. Ukiona ni kana kwamba Yehova ameamua kuwafanyia wengine mambo ya ziada, shangilia pamoja nao.

Hata hivyo, Yehova anatazamia ufanye jambo fulani. Jambo gani? Andiko la Wagalatia 6:4 linasema: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake.” Yaani, jiwekee miradi inayofaa. Panga mambo unayoweza kutimiza, kisha uyafuatilie. Ikiwa mradi huo unafaa na unautimiza, utakuwa na “sababu ya kufurahi.” Utapata uradhi.

Utapata Baraka

Kanuni tatu ambazo tumezungumzia zinaonyesha kwamba kutumia kanuni za Biblia kunaweza kutusaidia kupata uradhi hata katika siku hizi za mwisho na licha ya kutokamilika. Katika usomaji wako wa Biblia kila siku, unaweza kujitahidi kutafuta kanuni kama hizo, ziwe zimeelezwa waziwazi au kutajwa katika masimulizi na mifano.

Ikiwa unahisi kwamba uradhi wako unapungua, jitahidi kujua kisababishi. Kisha, tafuta kanuni unazoweza kutumia kurekebisha hali hiyo. Kwa mfano, huenda ukachunguza ukurasa wa 110-111 wa kitabu “Kila Andiko Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa.” * Kitabu cha Methali kinazungumziwa hapo, nacho kina kanuni na mashauri mengi sana chini ya vichwa 12. The Watch Tower Publications Index * (Index des publications Watch Tower) na Watchtower Library on CD-ROM * ni vyanzo vizuri sana vya habari. Kuvitumia kwa ukawaida vifaa hivyo kutakuwezesha kupata kwa urahisi kanuni unazoweza kutumia.

Karibuni Yehova atawapa wale wanaostahili uzima wa milele ulio mkamilifu katika dunia paradiso. Watapata uradhi mwingi maishani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 30 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 30 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 30 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Waroma 3:23

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Yesu “alijifunza kutii kutokana na mambo aliyoteseka.”—Waebrania 5:8, 9

[Blabu katika ukurasa wa 15]

“Atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”—Wagalatia 6:4