Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazee Wanapuuzwa na Kuteswa

Wazee Wanapuuzwa na Kuteswa

Wazee Wanapuuzwa na Kuteswa

MLINZI mmoja alipokuwa akilinda usiku, alishtuka alipoona jambo lenye kuogopesha. Nje ya nyumba moja ya kifahari aliona maiti mbili za wenzi wa ndoa waliozeeka ambao waliruka kutoka orofa ya nane ya nyumba hiyo. Ingawa kifo chao kilishtua watu, sababu ya kujiua kwao ndiyo iliyokuwa yenye kushtua hata zaidi. Barua iliyopatikana ndani ya mfuko wa mume ilisema hivi: “Tunajiua kwa sababu tunateswa na kusumbuliwa sikuzote na mwana wetu na mke wake.”

Huenda kisa hicho kisiwe cha kawaida, lakini visababishi vya visa kama hivyo ni vya kawaida. Naam, watu waliozeeka huteswa karibu kila mahali ulimwenguni. Fikiria mifano ifuatayo:

• Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 4 ya watu wenye umri mkubwa huko Kanada huteswa au kudhulumiwa, mara nyingi na mtu wa familia. Hata hivyo, watu wengi wenye umri mkubwa huaibika na kuogopa kuzungumzia shida wanazopata. Wataalamu wanasema kwamba huenda idadi kamili ikakaribia asilimia 10.

• Gazeti moja (India Today) linaripoti hivi: “Ijapokuwa familia nchini India huonekana kuwa imara, taifa hilo linasambaratika kwa sababu watu waliozeeka wanazidi kupuuzwa na watoto wao.”

• Kulingana na makadirio sahihi zaidi yaliyopo, “kati ya milioni 1 na milioni 2 ya Wamarekani wenye umri wa miaka 65 au zaidi wamewahi kuumizwa, kudhulumiwa, au kuteswa kwa njia nyingine na mtu ambaye walimtegemea awatunze au awalinde,” lasema Shirika la Kitaifa Linaloshughulikia Wazee Wanaoteswa. Mwanasheria mmoja huko San Diego, California, analiita tatizo la kuwatesa wazee kuwa “mojawapo ya matatizo mazito zaidi katika utekelezaji wa sheria leo.” Anaongeza hivi: “Ninaona kwamba tatizo hilo litaendelea kuongezeka miaka kadhaa ijayo.”

• Huko Canterbury, New Zealand, watu wengi wanaona kwamba wazee wanapuuzwa na watu wa familia, hasa wale wanaotumia dawa za kulevya, wale wanaolewa, au kucheza kamari. Hesabu ya visa vya kuwatesa wazee huko Canterbury imeongezeka sana kutoka 65 mwaka wa 2002 hadi 107 mwaka wa 2003. Msimamizi mkuu wa shirika moja linaloshughulikia kuzuia visa kama hivyo anasema kwamba idadi hiyo ni ndogo sana ikilinganishwa na idadi kubwa ya wazee wanaoteswa leo.

• Shirikisho la Japani la Mashirika ya Mawakili lilisema kwamba “wazee wanaoteswa wanahitaji kushughulikiwa zaidi hata kuliko watoto wanaotendewa vibaya au watu wanaoathiriwa na jeuri yoyote ya nyumbani,” lasema gazeti moja (The Japan Times). Kwa nini? Likionyesha mojawapo ya sababu, gazeti hilo (Times) linasema hivi: “Vikilinganishwa na visa vya kuwatendea kwa ukatili watoto au wenzi wa ndoa, visa vya kuwatesa wazee havijulikani haraka kwa sababu wazee wanapotendewa jeuri na watoto wao, wao huhisi kwamba hawakutimiza vizuri daraka lao kama wazazi, na serikali na wenye mamlaka wameshindwa kusuluhisha tatizo hilo.”

Mifano hiyo michache ya mambo yanayotukia ulimwenguni inatokeza maswali haya: Kwa nini wazee wengi wanapuuzwa na kuteswa? Je, kuna tumaini lolote kwamba mambo yatakuwa mazuri? Kuna faraja gani kwa waliozeeka?