Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Hutangaza “Tangu Mwanzo Ule Mwisho”

Yehova Hutangaza “Tangu Mwanzo Ule Mwisho”

Yehova Hutangaza “Tangu Mwanzo Ule Mwisho”

“Yeye anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.”—ISAYA 46:10.

1, 2. Ni jambo gani la ajabu kuhusu matukio yanayohusiana na kuangushwa kwa Babiloni, nalo linaonyesha nini kumhusu Yehova?

NI USIKU. Maaskari adui wananyemelea kupitia Mto Efrati huku wakielekea kwenye shabaha yao, jiji kuu la Babiloni. Wanapokaribia lango la jiji, wanaona jambo la kushangaza. Malango mawili kwenye ukuta wa Babiloni yameachwa wazi! Maaskari hao wanapanda kutoka mtoni, kisha wanaingia jijini. Kufumba na kufumbua, jiji hilo linatekwa. Bila kukawia, kiongozi wa maaskari hao anayeitwa Koreshi anaanza kusimamia eneo hilo lililotekwa, na baadaye anaagiza kwamba mateka Waisraeli waachiliwe huru. Maelfu ya watu walio uhamishoni wanarudi nyumbani kurudisha ibada ya Yehova huko Yerusalemu.—2 Mambo ya Nyakati 36:22, 23; Ezra 1:1-4.

2 Wanahistoria wanaunga mkono kabisa matukio hayo ya mwaka wa 539-537 K.W.K. Jambo la ajabu ni kwamba matukio hayo yalijulikana karibu miaka 200 mapema. Kupitia roho yake, Yehova alimwongoza nabii wake Isaya afafanue mapema hivyo kuhusu kuanguka kwa Babiloni. (Isaya 44:24–45:7) Mungu hakufunua tu mambo yaliyohusiana na kuangushwa kwa Babiloni, bali pia alitaja jina la kiongozi wa mashambulizi hayo. * Akizungumza na Waisraeli, ambao walikuwa mashahidi wake wakati huo, Yehova alisema hivi: “Kumbukeni mambo ya kwanza ya zamani za kale, kwamba mimi ni Mungu wala hakuna Mungu mwingine, wala yeyote kama mimi; Yeye anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.” (Isaya 46:9, 10a) Naam, Yehova ni Mungu anayeweza kujua kimbele mambo yatakayotukia wakati ujao.

3. Tutachunguza majibu ya maswali gani?

3 Mungu anajua mambo mangapi kuhusu wakati ujao? Je, Yehova anajua kimbele mambo ambayo kila mmoja wetu atafanya? Je, amepanga kimbele mambo yatakayotupata wakati ujao? Katika makala hii na ile inayofuata, tutachunguza jinsi Biblia inavyojibu maswali hayo na mengine yanayohusiana nayo.

Yehova Ni Mungu wa Unabii

4. Ni nani Chanzo cha unabii ulioandikwa katika Biblia?

4 Kwa kuwa Yehova anaweza kujua kimbele mambo ya wakati ujao, aliwaongoza kwa roho watumishi wake wa nyakati za Biblia waandike unabii mwingi ambao unatujulisha kimbele yale ambayo amekusudia kufanya. Yehova anatangaza hivi: “Mambo ya kwanza—tazama, yamekuja, lakini ninayatangaza mambo mapya. Kabla hayajaanza kutokea, mimi huwafanya ninyi myasikie.” (Isaya 42:9) Watu wa Mungu wamebarikiwa kwelikweli!

5. Ni wajibu gani unaotokana na kujua kimbele mambo ambayo Yehova atafanya?

5 Nabii Amosi anatuhakikishia hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hatafanya lolote isipokuwa awe amewafunulia watumishi wake manabii jambo lake la siri.” Kujua kimbele mambo yatakayotukia wakati ujao huleta wajibu fulani. Ona mfano mzuri ambao Amosi anatumia: “Kuna simba ambaye amenguruma! Ni nani hataogopa?” Kama vile wanadamu na wanyama huchukua hatua mara moja wakati simba aliye karibu anaponguruma, ndivyo Amosi na manabii wengine walivyotangaza ujumbe wa Yehova bila kukawia. “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amesema! Ni nani ambaye hatatoa unabii?”—Amosi 3:7, 8.

“Neno” la Yehova “Hakika Litafanikiwa”

6. “Shauri” la Yehova lilitimiaje kuhusiana na kuanguka kwa Babiloni?

6 Yehova alisema hivi kupitia nabii wake Isaya: “Shauri langu mwenyewe litasimama, na kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya.” (Isaya 46:10b) “Shauri” la Mungu, yaani, mapenzi yake au kusudi lake kuhusu Babiloni, lilihusisha kumwita Koreshi kutoka Uajemi ili ashinde Babiloni na kuliangusha. Yehova alitangaza kusudi hilo miaka mingi mapema. Kama tulivyotaja tayari, kusudi hilo lilitimia mwaka wa 539 K.W.K.

7. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote “neno” la Yehova hufanikiwa?

7 Karne nne hivi kabla ya Koreshi kushinda Babiloni, Mfalme Yehoshafati wa Yuda alikabili majeshi ya muungano ya Amoni na Moabu. Mfalme huyo alisali hivi akiwa na uhakika: “Ee Yehova Mungu wa mababu zetu, je, wewe si Mungu mbinguni, na je, wewe hutawali juu ya falme zote za mataifa, na je, mkononi mwako hamna nguvu na uwezo, wala hakuna anayeweza kusimama imara kupingana nawe?” (2 Mambo ya Nyakati 20:6) Isaya alikuwa na uhakika huohuo aliposema: “Yehova wa majeshi mwenyewe ametoa shauri, na ni nani anayeweza kulivunja? Na mkono wake umenyooshwa, na ni nani anayeweza kuurudisha nyuma?” (Isaya 14:27) Baadaye, wakati Mfalme Nebukadneza wa Babiloni aliporudishiwa fahamu baada ya kurukwa na akili, alikubali hivi kwa unyenyekevu: “Hakuna yeyote anayeweza kuzuia mkono [wa Mungu] au anayeweza kumuuliza, ‘Umekuwa ukifanya nini?’” (Danieli 4:35) Naam, Yehova anawahakikishia watu wake hivi: “Neno langu . . . halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” (Isaya 55:11) Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba sikuzote “neno” la Yehova hutimia. Kusudi la Mungu hakika litafanikiwa.

“Kusudi la Milele” la Mungu

8. Eleza maana ya “kusudi la milele” la Mungu.

8 Katika barua yake kwa Wakristo wa Efeso, mtume Paulo alisema kwamba Mungu ana “kusudi la milele.” (Waefeso 3:11) Huo si mpango tu, kana kwamba Mungu alihitaji kupangia jinsi ambavyo angetimiza jambo fulani. Badala yake, kusudi hilo linahusiana na azimio la Yehova la kutimiza mambo aliyokuwa amekusudia mwanzoni kwa ajili ya wanadamu na dunia. (Mwanzo 1:28) Ili tuelewe uhakika wa kusudi lake, acheni tuchunguze unabii wa kwanza katika Biblia.

9. Andiko la Mwanzo 3:15 linahusianaje na kusudi la Mungu?

9 Ahadi iliyo katika Mwanzo 3:15 inaonyesha kuwa mara tu baada ya Adamu na Hawa kutenda dhambi, Yehova aliamua kwamba mwanamke wake wa mfano angetokeza uzao, au mwana. Pia, Yehova aliona kimbele matokeo ya uadui kati ya mwanamke wake na Shetani na kati ya uzao wa mwanamke na wa Shetani. Ingawa Yehova angeruhusu Uzao wa mwanamke wake upate jeraha kwenye kisigino, kwa wakati wake unaofaa, Uzao huo ungemponda nyoka, au Shetani Ibilisi, kichwani. Kabla ya wakati huo kufika, kusudi la Yehova liliendelea bila kukoma kupitia ukoo uliochaguliwa mpaka Yesu alipotokea akiwa Masihi aliyeahidiwa.—Luka 3:15, 23-38; Wagalatia 4:4.

Mambo Ambayo Yehova Anaamua Kimbele

10. Je, Yehova aliamua kimbele tangu mwanzo kwamba Adamu na Hawa wangetenda dhambi? Eleza.

10 Akizungumza kuhusu daraka la Yesu katika kusudi la Mungu, mtume Petro aliandika hivi: “Yeye [Yesu] alijulikana kimbele kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu, lakini alifunuliwa mwishoni mwa nyakati kwa ajili yenu.” (1 Petro 1:20) Je, Yehova aliamua kimbele tangu mwanzo kwamba Adamu na Hawa wangetenda dhambi na kwamba dhabihu ya fidia iliyoandaliwa na Yesu Kristo ingehitajiwa? Hapana. Maneno “kuwekwa msingi” yametafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kutupa mbegu chini.” Je, kuna ‘mbegu zozote zilizotupwa chini,’ au kuna mimba yoyote ya mwanadamu iliyotungwa kabla ya Adamu na Hawa kutenda dhambi? Hapana. Adamu na Hawa walipata watoto baada ya kutotii. (Mwanzo 4:1) Kwa hiyo, baada ya uasi huo, kabla ya Hawa kupata mimba, Yehova aliamua kimbele kwamba “uzao” ungetokea. Mpango wa upendo wa fidia uliwezekana kupitia kifo na ufufuo wa Yesu, na ni kupitia fidia hiyo kwamba dhambi iliyorithiwa na kazi zote za Shetani zitakomeshwa.—Mathayo 20:28; Waebrania 2:14; 1 Yohana 3:8.

11. Yehova aliamua kimbele jambo gani linalohusiana na kutimizwa kwa kusudi lake?

11 Mungu aliamua kimbele jambo lingine linalohusiana na kutimizwa kwa kusudi lake. Jambo hilo linaonyeshwa na maneno ambayo Paulo aliwaandikia Waefeso, kwamba Mungu ‘atakusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.’ Kisha, akizungumza kuhusu “vitu vilivyo mbinguni,” yaani, wale ambao wanachaguliwa kuwa warithi pamoja na Kristo, Paulo alisema hivi: “Tuliagizwa kimbele kulingana na kusudi lake yeye anayetenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.” (Waefeso 1:10, 11) Naam, Yehova aliagiza kimbele au aliamua kimbele kwamba idadi ndogo ya wanadamu ingefanyiza sehemu ya pili ya uzao wa mwanamke wa Mungu na kushirikiana na Kristo kuleta faida za fidia. (Waroma 8:28-30) Mtume Petro anawataja wanadamu hao kuwa “taifa takatifu.” (1 Petro 2:9) Kupitia maono, mtume Yohana alipata pendeleo la kujua idadi ya wale ambao wangekuwa warithi pamoja na Kristo, yaani, 144,000. (Ufunuo 7:4-8; 14:1, 3) Kwa kuwa wanamuunga mkono Kristo kuwa Mfalme, wanatumikia “kwa ajili ya sifa ya utukufu [wa Mungu].”—Waefeso 1:12-14.

12. Tunajuaje kwamba maisha ya kila mmoja wa wale 144,000 hayakupangiwa kimbele?

12 Kwa kuwa Mungu aliamua kimbele kwamba kutakuwa na hao 144,000, hiyo haimaanishi kwamba watu fulani walipangiwa kimbele kumtumikia Mungu kwa uaminifu katika wadhifa huo. Mashauri yaliyo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliandikwa hasa ili kuwaongoza na kuwaimarisha watiwa-mafuta wadumishe utimilifu na kuendelea kustahili mwito wao wa mbinguni. (Wafilipi 2:12; 2 Wathesalonike 1:5, 11; 2 Petro 1:10, 11) Yehova anajua kimbele kwamba watu 144,000 watastahili kutumikia katika kutimizwa kwa kusudi lake. Lakini kustahili kwao kunategemea jinsi kila mmoja aliyepata mwito huo anavyotenda maishani mwake. Na kila mmoja wao anachagua jinsi atakavyotenda.—Mathayo 24:13.

Mambo Ambayo Yehova Anajua Kimbele

13, 14. Uwezo wa Yehova wa kujua mambo kimbele hupatana na nini, na kwa nini?

13 Kwa kuwa Yehova ni Mungu wa unabii na mwenye kusudi, yeye hutumiaje uwezo wake wa kujua kimbele mambo yatakayotukia wakati ujao? Kwanza kabisa, tunahakikishiwa kwamba njia zote za Mungu ni za kweli, za uadilifu, na za upendo. Mtume Paulo alipowaandikia Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza W.K., alithibitisha kwamba kiapo cha Mungu na ahadi yake ndiyo “mambo mawili yasiyobadilika ambayo katika hayo Mungu hawezi kamwe kusema uwongo.” (Waebrania 6:17, 18) Katika barua yake kwa mwanafunzi Tito, Paulo alitaja pia jambo hilo alipoandika kwamba Mungu ‘hawezi kusema uwongo.’—Tito 1:2.

14 Isitoshe, ingawa Yehova ana nguvu zisizo na mipaka, yeye hatendi kamwe isivyo haki. Musa alisema kwamba Yehova ni “Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Lolote ambalo Yehova anafanya linapatana na utu wake wenye kupendeza. Matendo yake yanaonyesha jinsi sifa zake kuu zinavyopatana kabisa, na sifa hizo ni upendo, hekima, haki, na nguvu.

15, 16. Ni uchaguzi gani ambao Yehova aliweka mbele ya Adamu katika shamba la Edeni?

15 Fikiria jinsi sifa hizo zote zinavyohusiana na matukio ya shamba la Edeni. Akiwa Baba mwenye upendo, Yehova aliwaandalia wanadamu kila kitu walichohitaji. Alimpa Adamu uwezo wa kufikiri, kuchanganua mambo, na kufanya uamuzi. Tofauti na wanyama ambao kwa kawaida huongozwa na silika, Adamu alikuwa na uwezo wa kuchagua. Kwa sababu hiyo, baada ya kumuumba Adamu, Mungu alitazama chini akiwa kwenye kiti chake cha enzi mbinguni na kuona kwamba “kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.”—Mwanzo 1:26-31; 2 Petro 2:12.

16 Yehova alipomwamuru Adamu asile kutokana na “mti wa ujuzi wa mema na mabaya,” alimpa maagizo ya kutosha ili Adamu aamue kile atakachofanya. Alimruhusu Adamu kula “matunda ya kila mti wa bustani” isipokuwa matunda ya mti mmoja tu, naye akaonya kwamba kifo kingetokea iwapo angekula matunda ya mti huo uliokatazwa. (Mwanzo 2:16, 17) Alimweleza Adamu matokeo ya matendo yake. Adamu angefanya nini?

17. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova huchagua mambo ambayo anataka kujua kimbele?

17 Inaonekana kwamba Yehova alichagua kutoona kimbele yale ambayo Adamu na Hawa wangefanya, hata ingawa Yeye ana uwezo wa kujua kimbele mambo yote. Basi, jambo linalozungumziwa hapa si ikiwa Yehova anaweza kuona kimbele wakati ujao, bali ikiwa yeye huchagua kufanya hivyo. Isitoshe, tunaweza kukata kauli kwamba, kwa kuwa Yehova ni Mungu mwenye upendo, hangeamua kimbele kimakusudi na kikatili kwamba wanadamu wangeasi na kupatwa na matokeo yenye kuhuzunisha. (Mathayo 7:11; 1 Yohana 4:8) Hivyo, Yehova huchagua mambo ambayo anataka kujua kimbele.

18. Kwa nini hatuwezi kusema kwamba Yehova amepungukiwa eti kwa sababu yeye huchagua mambo ambayo anataka kujua kimbele?

18 Kwa kuwa Yehova huchagua mambo ambayo anataka kujua kimbele, je, hilo linamaanisha kwamba amepungukiwa kwa kadiri fulani? Hapana. Musa alisema kwamba Yehova ni “Mwamba,” na kwamba “kazi zake ni kamilifu.” Hapaswi kulaumiwa kwa sababu ya matokeo ya dhambi ya wanadamu. Mambo yote mabaya yanayotupata leo yanatokana na lile tendo ovu la kutotii. Mtume Paulo alieleza wazi kwamba “kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Waroma 5:12; Yeremia 10:23.

19. Makala inayofuata itazungumzia maswali gani?

19 Kupitia mazungumzo haya tumeona kwamba Yehova hatendi kamwe isivyo haki. (Zaburi 33:5) Badala yake, Yehova hutumia uwezo wake, sifa zake, na viwango vyake kupatana na kusudi lake. (Waroma 8:28) Akiwa Mungu wa unabii, Yehova hutangaza “tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.” (Isaya 46:9, 10) Pia, tumeona kwamba Yehova huchagua mambo ambayo anataka kujua kimbele. Basi, mambo hayo yanatuhusuje? Tunaweza kuonyeshaje kwamba maamuzi yetu yanapatana na kusudi la Mungu lenye upendo? Na tutapata baraka gani tunapofanya hivyo? Makala inayofuata itazungumzia maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Ona ukurasa wa 28 wa broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni mifano gani ya kale inayoonyesha kwamba sikuzote “neno” la Mungu ‘hakika linafanikiwa’?

• Ni mambo gani ambayo Yehova ameamua kimbele kuhusiana na ‘kusudi lake la milele’?

• Yehova hutumiaje uwezo wake wa kujua kimbele mambo yatakayotukia wakati ujao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Yehoshafati alimtumaini Yehova

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mungu alitabiri kwamba Yesu atakufa na kufufuliwa

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, Yehova aliamua kimbele mambo ambayo Adamu na Hawa wangefanya?