Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Jinsi Ninavyoipenda Sheria Yako!”

“Jinsi Ninavyoipenda Sheria Yako!”

“Jinsi Ninavyoipenda Sheria Yako!”

“Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.”—ZABURI 119:97.

1, 2. (a) Mwandikaji wa Zaburi ya 119 aliyeongozwa kwa roho alikabili hali gani? (b) Alitendaje alipokabili hali hizo, na kwa nini?

MWANDIKAJI wa Zaburi ya 119 alikabili jaribu kali. Adui wenye kimbelembele ambao walipuuza sheria ya Mungu walimdhihaki na kusema uwongo kumhusu. Wakuu walifanya mashauriano dhidi yake na kumtesa. Waovu walimzunguka, na maisha yake yalikuwa hatarini. Mambo yote hayo yalimfanya ‘akose usingizi kwa sababu ya huzuni.’ (Zaburi 119:9, 23, 28, 51, 61, 69, 85, 87, 161) Licha ya kukabili majaribu hayo, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.”—Zaburi 119:97.

2 Huenda ukajiuliza hivi, “Sheria ya Mungu ilimfariji mtunga-zaburi kwa njia gani?” Alitegemezwa kwa kuamini kwamba Yehova anamjali. Ingawa alitaabishwa na wapinzani wake, mtunga-zaburi alipata furaha kwa kutambua faida za kutii sheria hiyo. Alitambua kwamba Yehova alikuwa amemtendea kwa fadhili. Isitoshe, kutii mwongozo ulio katika sheria ya Mungu kulimfanya awe mwenye hekima kuliko adui zake na hata kulimhifadhi hai. Kutii sheria hiyo kulimfanya awe na amani na dhamiri njema.—Zaburi 119:1, 9, 65, 93, 98, 165.

3. Kwa nini si rahisi kwa Wakristo kutii viwango vya Mungu leo?

3 Baadhi ya watumishi wa Mungu leo wanakabili pia majaribu makali ya imani. Huenda tusikabili hali yenye kuhatarisha uhai kama mtunga-zaburi, lakini tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Watu wengi tunaoshughulika nao kila siku hawapendi viwango vya Mungu, wana miradi ya ubinafsi na ya kimwili, wana kiburi, wala hawana heshima. (2 Timotheo 3:1-5) Mara nyingi vijana Wakristo hukabili mambo yanayohatarisha maadili yao mema. Katika hali kama hizo, inaweza kuwa vigumu kuendelea kumpenda Yehova na yaliyo mema. Tunaweza kujilindaje?

4. Mtunga-zaburi alionyeshaje kwamba anaithamini sheria ya Mungu, na je, Wakristo wanapaswa kufanya vivyo hivyo?

4 Mtunga-zaburi alivumilia mikazo aliyokuwa akikabili kwa sababu alitenga wakati ili asome kwa bidii na kutafakari sheria ya Mungu. Hivyo, akaipenda sana sheria hiyo. Naam, karibu kila mstari wa Zaburi ya 119 unataja jambo fulani kuhusu sheria ya Yehova. * Leo, Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale. (Wakolosai 2:14) Hata hivyo, kanuni zinazotajwa katika Sheria hiyo ni muhimu hata leo. Kanuni hizo zilimfariji mtunga-zaburi, nazo zinaweza kuwafariji watumishi wa Mungu wanaojitahidi sana kukabiliana na matatizo ya leo.

5. Tutachunguza mambo gani katika Sheria ya Musa?

5 Acheni tuone jinsi tunavyoweza kutiwa moyo kwa kuchunguza mambo matatu tu katika Sheria ya Musa. Mambo hayo ni mpango wa Sabato, maandalizi ya kuokota masalio, na amri iliyokataza kutamani. Tutakapochunguza kila moja ya mambo hayo, tutaona kwamba ili tuweze kukabiliana na matatizo ya leo ni muhimu tuelewe kanuni zinazotegemeza sheria hizo.

Kutosheleza Uhitaji Wetu wa Kiroho

6. Wanadamu wote wana mahitaji gani ya msingi?

6 Mwanadamu aliumbwa na mahitaji kadha wa kadha. Kwa mfano, ili mtu aendelee kuwa na afya nzuri anahitaji chakula, kinywaji, na makao. Hata hivyo, mwanadamu anahitaji pia kutosheleza “uhitaji [wake] wa kiroho.” Asipofanya hivyo, hawezi kuwa na furaha ya kweli. (Mathayo 5:3) Yehova aliona ni muhimu sana kutosheleza uhitaji huo wa asili hivi kwamba aliwaamuru watu wake wasimamishe shughuli zao za kawaida kwa siku moja kila juma ili wakazie fikira mambo ya kiroho.

7, 8. (a) Mungu alionyeshaje kwamba siku ya Sabato ilikuwa tofauti na siku nyingine? (b) Sabato iliwekwa kwa kusudi gani?

7 Mpango wa Sabato ulikazia umuhimu wa kutilia maanani mambo ya kiroho. Katika Biblia, neno “sabato” linatajwa kwa mara ya kwanza wakati mana ilipoandaliwa jangwani. Waisraeli waliambiwa kwamba wanapaswa kukusanya mkate huo ulioandaliwa kimuujiza kwa siku sita. Siku ya sita walipaswa kukusanya “mkate wa siku mbili,” kwa sababu mkate huo haungeandaliwa siku ya saba. Siku hiyo ya saba ilikuwa “sabato takatifu kwa Yehova,” na kila mtu alipaswa kuendelea kukaa mahali pake wakati huo. (Kutoka 16:13-30) Mojawapo ya zile Amri Kumi ilisema kwamba kazi yoyote isifanywe siku ya Sabato. Siku hiyo ilikuwa takatifu. Adhabu ya kuipuuza ilikuwa kifo.—Kutoka 20:8-11; Hesabu 15:32-36.

8 Sheria ya Sabato ilionyesha jinsi Yehova alivyojali hali ya kimwili na ya kiroho ya watu wake. Yesu alisema hivi: “Sabato ilikuja kwa ajili ya mwanadamu.” (Marko 2:27) Sheria hiyo haikuwaruhusu tu Waisraeli wapumzike bali pia iliwapa nafasi ya kumkaribia Muumba wao na kuonyesha kwamba wanampenda. (Kumbukumbu la Torati 5:12) Siku hiyo ilitengwa kwa ajili ya mambo ya kiroho peke yake. Mambo hayo yalitia ndani familia kuabudu pamoja, kusali, na kutafakari Sheria ya Mungu. Mpango huo uliwazuia Waisraeli wasitumie wakati wao wote na nguvu zao zote katika mambo ya kimwili. Sabato iliwakumbusha kwamba uhusiano wao pamoja na Yehova ndilo jambo muhimu zaidi maishani mwao. Yesu alirudia kanuni hiyo isiyobadilika aliposema hivi: “Imeandikwa, ‘Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’”—Mathayo 4:4.

9. Wakristo wanajifunza nini kutokana na mpango wa Sabato?

9 Ingawa watu wa Mungu hawako tena chini ya wajibu wa kuwa na pumziko la sabato la saa 24, wanaweza kujifunza mambo fulani kutokana na mpango wa Sabato. (Wakolosai 2:16) Mpango huo unatukumbusha kwamba tunapaswa kutanguliza mambo ya kiroho. Mambo matakatifu hayapaswi kupuuzwa kwa sababu ya kuhangaikia sana vitu vya kimwili au tafrija. (Waebrania 4:9, 10) Basi, tunaweza kujiuliza hivi: “Ninatanguliza mambo gani maishani mwangu? Je, ninatanguliza kujifunza, kusali, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kuhubiri habari njema ya Ufalme? Au, je, mambo mengine yamechukua nafasi ya mambo hayo ya kiroho?” Tukitanguliza mambo ya kiroho maishani mwetu, Yehova anatuhakikishia kwamba hatutakosa vitu vya msingi maishani.—Mathayo 6:24-33.

10. Tunaweza kufaidikaje tunapotenga wakati kwa ajili ya mambo ya kiroho?

10 Kutenga wakati kujifunza Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia, na vilevile kutafakari mambo tunayojifunza, kunaweza kutusaidia kumkaribia Yehova zaidi. (Yakobo 4:8) Miaka 40 iliyopita, Susan alianza kutenga wakati ili kujifunza Biblia kwa ukawaida. Anakubali kwamba mwanzoni hakufurahia kufanya hivyo. Aliona kujifunza kuwa mzigo. Lakini kadiri alivyoendelea kujifunza, ndivyo alivyofurahia kufanya hivyo. Sasa, yeye husikitika sana anapokosa kuwa na funzo la kibinafsi. Anasema hivi: “Kujifunza kumenisaidia kumjua Yehova na kumwona kama Baba. Ninaweza kumwamini, kumtegemea, na kumkaribia kwa uhuru katika sala. Inapendeza sana kuona jinsi Yehova anavyowapenda sana watumishi wake, jinsi anavyonijali, na jinsi ambavyo amenisaidia.” Naam, sisi pia tunaweza kupata shangwe nyingi sana tukitosheleza mahitaji yetu ya kiroho kwa ukawaida!

Sheria ya Mungu Kuhusu Kuokota Masalio

11. Fafanua mpango wa kuokota masalio.

11 Jambo la pili katika Sheria ya Musa ambalo linaonyesha jinsi Mungu alivyojali hali ya watu wake ni haki ya kuokota masalio. Yehova aliamuru kwamba wakati mkulima Mwisraeli alipovuna mazao ya shamba lake, watu wenye uhitaji walipaswa waruhusiwe kuokota masalio ambayo wavunaji waliacha. Wakulima hawakupaswa kuvuna kila kitu kwenye ukingo wa mashamba yao, wala hawakupaswa kukusanya zabibu au zeituni zilizobaki. Hawakupaswa kurudi kuchukua masuke ya nafaka yaliyosahauliwa mashambani. Huo ulikuwa mpango wa upendo wa kuwasaidia maskini, wakaaji wageni, mayatima, na wajane. Ni kweli kwamba kazi ya kuokota masalio ilikuwa ngumu, lakini kazi hiyo ingewazuia wasiombe-ombe.—Mambo ya Walawi 19:9, 10; Kumbukumbu la Torati 24:19-22; Zaburi 37:25.

12. Mpango wa kuokota masalio uliwawezesha wakulima kufanya nini?

12 Sheria ya kuokota masalio haikutaja kiasi cha mazao ambacho wakulima walipaswa kuwaachia wenye uhitaji. Wakulima walikuwa na uhuru wa kuamua ikiwa wangeacha ukingo wa mashamba yao ya nafaka zisizovunwa ukiwa mpana au mwembamba. Hivyo, mpango huo uliwafundisha kuwa wakarimu. Mpango huo uliwawezesha wakulima kuonyesha kwamba wanamthamini Yule aliyeandaa mavuno hayo, kwa maana “anayemwonyesha maskini kibali anamtukuza [Mtengenezaji wake].” (Methali 14:31) Boazi alifanya hivyo. Kwa fadhili, alihakikisha kwamba yule mjane Ruthu anakusanya nafaka nyingi alipokuwa akiokota masalio katika mashamba yake. Yehova alimbariki sana Boazi kwa ukarimu wake.—Ruthu 2:15, 16; 4:21, 22; Methali 19:17.

13. Tunajifunza nini kutokana na sheria ya kale ya kuokota masalio?

13 Kanuni inayotegemeza sheria ya kuokota masalio haikubadilika. Yehova anataka watumishi wake wawe wakarimu, hasa kuelekea wenye uhitaji. Kadiri tunavyokuwa wakarimu zaidi, ndivyo tutakavyobarikiwa zaidi. Yesu alisema hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. Watawamwagia katika mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa pamoja na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.”—Luka 6:38.

14, 15. Tunaweza kuonyeshaje ukarimu, na kufanya hivyo huleta faida gani kwetu na kwa wale tunaowasaidia?

14 Mtume Paulo alituhimiza “tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Hivyo, tunahitaji kuhakikisha kwamba Wakristo wenzetu wanapata msaada wa kiroho wakati wowote ambapo imani yao inajaribiwa. Lakini huenda pia wakahitaji msaada ili wafike kwenye Jumba la Ufalme au kununua vitu dukani. Je, katika kutaniko lenu kuna watu ambao ni wazee kwa umri, wagonjwa, au wale wasioweza kutoka nyumbani kwa sababu ya hali zao, ambao watathamini ukiwatembelea ili kuwatia moyo au kuwasaidia? Tukiwa macho kutambua mahitaji ya watu kama hao, Yehova anaweza kututumia kujibu sala ya mwenye uhitaji. Ingawa kuwasaidia wengine ni wajibu wa Kikristo, yule anayetoa msaada hufaidika pia. Tunapowaonyesha waabudu wenzetu kwamba tunawapenda kikweli, sisi hupata shangwe nyingi, uradhi mwingi, na kibali cha Yehova. —Methali 15:29.

15 Wakristo huonyesha kwamba hawana ubinafsi kwa njia nyingine muhimu, yaani, kutumia wakati na nguvu zao kuongea kuhusu makusudi ya Mungu. (Mathayo 28:19, 20) Yeyote ambaye amepata shangwe ya kumsaidia mwingine kufikia hatua ya kuweka maisha yake wakfu kwa Yehova, anajua kwamba maneno haya ya Yesu ni ya kweli: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Kujilinda Dhidi ya Tamaa

16, 17. Amri ya kumi ilikataza nini, na kwa nini?

16 Jambo la tatu ambalo tutachunguza katika Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ni amri ya kumi, ambayo ilikataza kutamani. Sheria ilisema hivi: “Usiitamani nyumba ya mwenzako. Usimtamani mke wa mwenzako, wala mtumwa wake wala kijakazi wake wala ng’ombe-dume wake wala punda wake wala chochote cha mwenzako.” (Kutoka 20:17) Hakuna mwanadamu ambaye angeweza kuhakikisha kwamba amri hiyo inafuatwa kwa sababu hakuna mwanadamu anayeweza kusoma mioyo. Hata hivyo, amri hiyo ilifanya Sheria iwe bora kuliko mfumo wowote wa sheria wa wanadamu. Ilimfanya kila Mwisraeli atambue kwamba atatoa hesabu mbele za Yehova, ambaye anaweza kujua mielekeo ya moyo. (1 Samweli 16:7) Isitoshe, amri hiyo ililenga chanzo cha matendo mengi maovu.—Yakobo 1:14.

17 Sheria iliyokataza kutamani iliwahimiza watu wa Mungu wasifuatie vitu vya kimwili, wasiwe na pupa, na wasilalamike kuhusu hali yao maishani. Pia, iliwalinda wasishawishiwe kuiba au kufanya mambo yasiyo ya adili. Sikuzote kutakuwa na watu ambao wana vitu vya kimwili ambavyo tungependa kuwa navyo, au watu ambao kwa njia moja au nyingine wanaonekana kuwa wamefanikiwa kuliko sisi. Tusipodhibiti mawazo yetu katika hali hizo, tunaweza kukosa furaha na kuwaonea wengine wivu. Biblia inasema kwamba kutamani ni “hali ya akili iliyokataliwa.” Ni afadhali kutotamani.—Waroma 1:28-30.

18. Ni roho gani iliyopo leo ulimwenguni, nayo ina madhara gani?

18 Roho ya ulimwengu leo huwachochea watu kufuatia vitu vya kimwili na kushindana. Matangazo ya biashara huwafanya watu watamani kununua bidhaa mpya na mara nyingi huonyesha kwamba tusipozinunua hatuwezi kupata furaha. Hiyo ndiyo roho iliyoshutumiwa katika Sheria ya Yehova. Roho nyingine iliyoshutumiwa ni ile ya kutamani kufanikiwa maishani na kutajirika kupitia njia yoyote ile. Mtume Paulo alionya hivi: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu. Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10.

19, 20. (a) Ni mambo gani yaliyo muhimu zaidi kwa mtu anayependa sheria ya Yehova? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

19 Wale wanaoipenda sheria ya Mungu wanatambua hatari zinazoweza kusababishwa na roho ya kufuatia vitu vya kimwili, nao wanalindwa kutokana nayo. Kwa mfano, mtunga-zaburi alisali hivi kwa Yehova: “Uelekeze moyo wangu kwa vikumbusho vyako, wala si kwa faida. Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu, kuliko maelfu ya vipande vya dhahabu na fedha.” (Zaburi 119:36, 72) Kusadiki kwamba maneno hayo ni ya kweli kutatusaidia kudumisha usawaziko ambao utatuwezesha kuepuka mitego ya kufuatia vitu vya kimwili, pupa, na kutoridhika na hali yetu maishani. Siri ya kupata faida kubwa ni “ujitoaji-kimungu,” bali si kukusanya mali.—1 Timotheo 6:6.

20 Kanuni zinazoitegemeza Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli wa kale ni muhimu katika nyakati hizi ngumu sawa na vile zilivyokuwa muhimu wakati Yehova alipompa Musa Sheria hiyo. Kadiri tunavyotumia kanuni hizo maishani mwetu, ndivyo tutakavyozielewa zaidi, kuzipenda zaidi, na kupata furaha zaidi. Sheria inatufunza mambo mengi muhimu, na maisha ya watu wanaosimuliwa katika Biblia yanatukumbusha waziwazi umuhimu wa mambo hayo. Tutazungumzia baadhi ya watu hao katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kati ya ile mistari 176 ya zaburi hiyo, ni mistari minne tu ambayo haitaji angalau mojawapo ya maneno haya: amri, maamuzi ya hukumu, sheria, maagizo, masharti, vikumbusho, maneno, njia, au neno la Yehova.

Ungejibuje?

• Kwa nini mwandikaji wa Zaburi ya 119 aliipenda sheria ya Yehova?

• Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na mpango wa Sabato?

• Sheria ya Mungu kuhusu kuokota masalio ina faida gani leo?

• Amri iliyokataza kutamani inatulindaje?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Sheria ya Sabato ilikazia nini?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Sheria ya kuokota masalio inatufunza nini?