Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwongozo Bora wa Kupata Furaha

Mwongozo Bora wa Kupata Furaha

Mwongozo Bora wa Kupata Furaha

WANADAMU wote wana haki ya “kujitahidi kupata Furaha.” Hayo yalikuwa maoni ya watungaji wa Azimio la Uhuru la Marekani. Hata hivyo, kuna tofauti kati ya kujitahidi kufikia mradi fulani na kuufikia. Ingawa vijana wengi wanafuatia kazi katika nyanja za burudani na michezo, ni wangapi unaojua ambao wamefaulu kupata kile walichotamani sana? Mwimbaji mmoja mashuhuri anayejua jinsi ilivyo vigumu kuwa mwanamuziki mwenye mafanikio alisema: “Ni vigumu kufanikiwa.”

Ikiwa unahisi kwamba wewe pia hutafanikiwa kupata furaha, jipe moyo. Ukitafuta furaha kwa njia inayofaa, utaipata. Kwa nini? Makala iliyotangulia ilimtaja Yehova kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Mungu anatoa mwongozo katika Biblia ili usikate tamaa unapotafuta furaha. Yehova anaweza kukusaidia kushinda mambo yanayosababisha huzuni. Kwa mfano, fikiria faraja ambayo Yehova anakupa mpendwa wako anapokufa.

Mpendwa Anapokufa

Je, jambo lolote zuri linaweza kusemwa kuhusu kifo? Kifo kinawatenganisha wazazi na watoto. Kinawatenganisha marafiki wa karibu, nacho huvuruga usalama wa jamii zilizo imara. Familia yenye furaha inaweza kulemewa na huzuni mpendwa anapokufa.

Ni wazi kwamba kifo kinasikitisha sana. Hata hivyo, watu wengine hukana ukweli huo nao husema kwamba kifo ni baraka. Fikiria yale yaliyotukia baada ya Kimbunga cha Katrina kuikumba Ghuba ya Mexico mnamo Agosti 2005. Kwenye mazishi ya mtu mmoja aliyekufa kutokana na kimbunga hicho, kasisi mmoja alisema hivi: “Hakufa kwa sababu ya Katrina. Mungu ndiye aliyemwita.” Katika pindi nyingine, mfanyakazi mmoja wa hospitali mwenye nia njema alimwambia binti ya mwanamke mmoja aliyekufa kwamba asihuzunike kwa kuwa Mungu alimchukua mama yake na kumpeleka mbinguni. Binti huyo alipaaza sauti: “Kwa nini alimchukua mama yangu?”

Bila shaka, maoni hayo ya uwongo kuhusu kifo mara nyingi hayawafariji wale waliofiwa. Kwa nini? Kwa sababu hayaonyeshi ukweli kuhusu kifo. Jambo baya hata zaidi ni kwamba maoni hayo yanaonyesha kwamba Mungu ndiye anayewachukua marafiki na wapendwa katika familia kwa njia yenye kuogofya na yenye kuumiza sana. Badala ya kuwa chanzo cha faraja, Mungu anaonwa kuwa muuaji mbaya sana. Hata hivyo, Neno la Mungu linasema ukweli kuhusu kifo.

Biblia inasema kifo ni adui. Inafananisha kifo na mfalme ambaye amewatawala wanadamu. (Waroma 5:17; 1 Wakorintho 15:26) Kifo ni adui mwenye nguvu sana hivi kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kukishinda, na kila mtu anayekufa ni kati ya wengi ambao wameangamizwa na kifo. Ukweli huo wa Biblia unatusaidia kuelewa kabisa kwa nini tunahuzunika na kujihisi hoi wakati mpendwa anapokufa. Ukweli huo unathibitisha kwamba hisia hizo ni za kawaida. Hata hivyo, je, Mungu hutumia adui yetu kifo ili kuwachukua wapendwa wetu mbinguni? Acheni Biblia ijibu swali hilo.

Andiko la Mhubiri 9:5, 10 linasema hivi: “Wafu, hawajui lolote kamwe . . . Hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika [Sheoli], mahali unapokwenda.” Sheoli ni nini? Ni kaburi ambamo wanadamu huenda wanapokufa. Kaburini, wafu hawafanyi lolote, hawasongi, hawahisi, wala hawafikirii jambo lolote. Ni kana kwamba wanalala usingizi mzito. * Hivyo, Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu hawachukui wapendwa wetu ili wawe pamoja naye huko mbinguni. Kwa sababu ya kifo, wako kaburini bila uhai.

Yesu alithibitisha ukweli huo baada ya kifo cha rafiki yake Lazaro. Yesu alilinganisha kifo na usingizi. Ikiwa Lazaro alienda mbinguni kuwa pamoja na Mungu Mweza-Yote, halingekuwa jambo la fadhili kwa Yesu kumrudisha duniani ili mwishowe afe tena. Simulizi lililoongozwa kwa roho ya Mungu linasema kwamba kwenye kaburi, Yesu alipaaza sauti hivi: “Lazaro, njoo huku nje!” Biblia inaendelea kusema: “Huyo mtu aliyekuwa mfu akatoka.” Hivyo, Lazaro akawa hai tena. Yesu alijua kwamba Lazaro hakuondoka duniani na kwenda mahali pengine. Alikuwa amelala kaburini akiwa amekufa.—Yohana 11:11-14, 34, 38-44.

Tukio hilo linalozungumziwa katika Biblia hutusaidia kuelewa kwamba kifo si njia ambayo Mungu hutumia ili kuwahamisha wanadamu kutoka duniani hadi mbinguni. Hivyo, tunaweza kumkaribia Mungu, tukijua kwamba si yeye ambaye ametusababishia huzuni. Pia, tunaweza kuwa na uhakika kwamba anaelewa kabisa huzuni na madhara yanayosababishwa na adui yetu, kifo. Na ukweli wa Biblia kuhusu hali ya wafu unathibitisha kwamba wafu hawateseki kamwe katika moto wa mateso wala katika purgatori, lakini wamo kaburini bila uhai. Hivyo, tunapowakumbuka wapendwa wetu waliokufa, hatupaswi kumchukia Mungu wala kuogopa kwa sababu ya kutojua mahali walipo. Isitoshe, katika Biblia Yehova anatufariji zaidi.

Tumaini Huleta Furaha

Maandiko ambayo tumezungumzia yanaonyesha kwamba kuwa na tumaini ni muhimu ili kupata furaha ya kweli. Katika Biblia neno “tumaini” linamaanisha kutarajia mema kwa uhakika. Ili kuona jinsi tumaini linavyoweza kutuletea furaha sasa, acheni tuzungumzie zaidi simulizi linaloonyesha jinsi Yesu alivyomfufua Lazaro.

Kuna angalau sababu mbili zilizomchochea Yesu kufanya muujiza huo. Sababu ya kwanza ilikuwa kuondoa huzuni ya Martha, Maria, na pia marafiki waliokuwa wakiomboleza. Kwa mara nyingine tena, wangeweza kushirikiana na mpendwa wao. Hata hivyo, Yesu alimtajia Martha sababu ya pili iliyokuwa muhimu zaidi: “Je, sikukuambia kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?” (Yohana 11:40) Kitabu kimoja (The New Testament in Modern English) kilichoandikwa na J. B. Phillips, kinatafsiri sentensi ya mwisho kuwa “maajabu ambayo Mungu anaweza kufanya.” Kwa kumfufua Lazaro, Yesu alionyesha kimbele yale ambayo Yehova Mungu anaweza kufanya na yale ambayo atafanya wakati ujao. Hebu tuchunguze zaidi “maajabu ambayo Mungu anaweza kufanya.”

Kwenye Yohana 5:28, 29, Yesu alisema hivi: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” Hilo linamaanisha kwamba wafu wote walio katika Sheoli, kutia ndani wapendwa wetu, watafufuliwa. Andiko la Matendo 24:15 linaeleza mengi zaidi kuhusu tukio hilo lenye kustaajabisha kwa kusema hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Hivyo, hata “wasio waadilifu,” yaani, watu wengi ambao hawakumjua na kumtumikia Yehova, watapewa nafasi ya kupata kibali cha Mungu wakati ujao.

Ufufuo huo utafanyika wapi? Andiko la Zaburi 37:29 linasema hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” Hebu fikiria maana ya maneno hayo! Familia na marafiki waliotenganishwa na kifo watakutana tena hapa duniani. Bila shaka, unapowazia jinsi utakavyofurahia maisha pamoja na wapendwa wako, moyo wako unajawa na furaha.

Yehova Anataka Uwe Mwenye Furaha

Tumechunguza njia mbili ambazo Yehova anaweza kutumia kuongeza furaha yako licha ya matatizo unayokabili. Kwanza, kupitia Biblia, anaandaa ujuzi na mwongozo ili kukusaidia kukabiliana na matatizo kwa mafanikio. Zaidi ya kutusaidia kukabiliana na huzuni inayotokana na kifo, mashauri ya Biblia yanaweza pia kutusaidia kukabiliana na matatizo ya afya na ya kiuchumi. Mashauri hayo yanaweza kukuimarisha kuvumilia ukosefu wa haki katika jamii na misukosuko ya kisiasa. Ukiyatumia maishani mwako, yanaweza kukusaidia kukabiliana na matatizo mengine ya kibinafsi.

Pili, kwa kujifunza Biblia, unapata tumaini ambalo haliwezi kulinganishwa na chochote ambacho wanadamu wanaweza kuandaa. Ufufuo wa marafiki na watu wa familia ni sehemu ya tumaini ambalo Biblia inafundisha. Andiko la Ufunuo 21:3, 4 linatueleza hivi zaidi: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja [na wanadamu]. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Hilo linamaanisha kwamba jambo lolote linalosababisha huzuni maishani mwako litatoweka milele hivi karibuni. Mambo ambayo Biblia inaahidi yatatimia, na unaweza kuyaona yanapotimia. Kujua kwamba nyakati bora ziko mbele yetu hutufariji. Pia, kujua kwamba hatutateseka milele baada ya kifo ni sababu nyingine ya kuwa wenye furaha.

Kwa mfano: Miaka mingi iliyopita Maria alimwona mume wake akiteseka sana hadi alipokufa kwa ugonjwa wa kansa. Muda mfupi baada ya kifo cha mume wake, ilimbidi yeye na binti zake watatu wahame nyumba yao kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi. Miaka miwili baadaye, Maria alitambua kwamba alikuwa pia na ugonjwa wa kansa. Amefanyiwa upasuaji mkubwa mara mbili naye huvumilia maumivu makali kila siku. Licha ya matatizo hayo, ana mtazamo mzuri ambao unamwezesha kuwatia wengine moyo. Anadumishaje furaha yake?

Maria anasema: “Ninapokuwa na tatizo, ninajaribu kutolifikiria sana. Ninaepuka kujiuliza maswali kama: ‘Kwa nini mambo haya yamenipata? Kwa nini ninateseka hivi? Kwa nini mimi ni mgonjwa?’ Maoni yasiyofaa huchosha akili sana. Badala yake, ninatumia nguvu zangu kumtumikia Yehova na kuwasaidia wengine. Mambo hayo hunifurahisha.”

Kuwa na tumaini kunamsaidiaje Maria? Anatarajia sana wakati Yehova atakapowaondolea wanadamu magonjwa na matatizo mengine. Anapoenda hospitali kupata matibabu, anazungumza kuhusu tumaini lake pamoja na wagonjwa wengine wa kansa ambao huenda hawana tumaini. Tumaini hilo lina umuhimu gani kwa Maria? Anasema hivi: “Mara nyingi ninafikiria yale ambayo Biblia inasema kwenye Waebrania 6:19, ambapo Paulo anataja tumaini kuwa nanga ya nafsi. Bila nanga hiyo, utapeperuka kama mashua inayoelea wakati wa dhoruba. Lakini ukifungiliwa kwenye nanga hiyo, utakuwa salama licha ya kukabiliana na matatizo yaliyo kama dhoruba.” ‘Tumaini hilo la uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi’ linamsaidia Maria kuendelea kuwa mwenye furaha. Tumaini hilo linaweza pia kukusaidia.—Tito 1:2.

Kupitia funzo la Biblia, unaweza kupata furaha ya kweli licha ya matatizo. Hata hivyo, huenda ukawa na shaka kuhusu faida za kujifunza Biblia. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukuonyesha majibu ya Biblia unayohitaji ili uwe mwenye furaha kwelikweli. Unapongojea kutimizwa kwa tumaini ambalo Yehova anatoa, unaweza kuwa kati ya wale wanaozungumziwa kwa njia ifuatayo: “Watafikia furaha na kushangilia, na huzuni na kuugua zitakimbia kabisa.”—Isaya 35:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kitabu kimoja (Encyclopædia Britannica, 2003) kinasema kwamba Sheoli ni “mahali ambapo hapana maumivu wala furaha, wala adhabu, wala thawabu.”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Ni kweli ya Biblia tu inayoweza kutuliza huzuni

[Picha katika ukurasa wa 7]

Tumaini la Biblia la ufufuo linaweza kukusaidia uwe mwenye furaha