Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naam, Unaweza Kupata Furaha

Naam, Unaweza Kupata Furaha

Naam, Unaweza Kupata Furaha

FURAHA ya kweli na ya kudumu haipatikani kwa urahisi. Hiyo ni kwa sababu watu wengi hutafuta furaha mahali pasipofaa. Wanaweza tu kuipata ikiwa wana rafiki wanayemtegemea na anayestahili kuwaongoza!

Biblia ni chanzo cha mwongozo unaohitajiwa. Fikiria kitabu chake kimoja tu, kitabu cha Zaburi. Kitabu hicho ni mkusanyo wa nyimbo takatifu 150 zilizoimbiwa Yehova Mungu, na karibu nusu yake zilitungwa na Mfalme Daudi wa Israeli la kale. Lakini jambo muhimu hata zaidi kuliko kujua waandikaji, ni kujua kwamba kitabu hicho kiliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu ya Yehova, ambaye ni Rafiki mkuu zaidi wa wanadamu. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba kina mwongozo wa Yehova unaokusudiwa kutufaidi na kutuonyesha njia ya kupata furaha.

Waandikaji wa Zaburi walikuwa na uhakika kwamba furaha hutokana na kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Mwenye furaha ni mtu anayemwogopa Yehova.” (Zaburi 112:1) Uhusiano wa kibinadamu, vitu vya kimwili, au mafanikio ya mtu haviwezi kuleta furaha inayotokana na kuwa miongoni mwa “watu ambao Mungu wao ni Yehova.” (Zaburi 144:15) Watumishi wengi wa Mungu leo wamethibitisha ukweli huo.

Mfano mmoja ni Susanne, ambaye ana umri wa miaka 40 hivi. * Alisema hivi: “Leo watu wengi hujiunga na vikundi fulani ili kufanya mambo yanayowapendeza. Hata hivyo, mara nyingi hawamwoni kila mtu katika kikundi hicho kuwa rafiki. Watu wa Yehova ni tofauti kabisa. Upendo wetu kwa Yehova hutufanya tupendane. Tukiwa kati ya watu wa Mungu tunastarehe, hata tuwe wapi. Umoja huo huboresha maisha yetu sana. Ni nani wengine wanaoweza kusema kwamba wana marafiki kutoka jamii, malezi, na mataifa mbalimbali? Ninaweza kusema kwa moyo wote kwamba furaha hutokana na kuwa miongoni mwa watu wa Yehova.”

Maree, aliyezaliwa Scotland, alijifunza pia kwamba ili mtu awe na furaha ni lazima awe na uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Alisema: “Kabla ya kujifunza kweli ya Biblia, nilifurahia kutazama filamu zenye kutisha. Lakini usiku singeweza kulala bila kushika msalaba kwa sababu nilifikiri ungeweza kufukuzia mbali mizuka na watu wanaonyonya wengine damu ambao huonyeshwa kwenye filamu nyingi. Hata hivyo, baada ya kujifunza kweli na kuacha kutazama filamu za aina hiyo, niliweza kulala bila woga kwa sababu ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, nami nilifurahia kumtumikia Mungu mwenye nguvu zaidi kuliko roho waovu au watu wanaodhaniwa kuwanyonya wengine damu.”

Kumtegemea Yehova Huleta Furaha

Hatuna sababu ya kutilia shaka uwezo mwingi na hekima isiyo na mipaka ya Muumba wetu. Akijua kwamba angekuwa na uhakika kamili katika Yehova na kwamba angepata kimbilio Kwake, Daudi aliandika hivi: “Mwenye furaha ni mwanamume ambaye amemfanya Yehova kuwa tegemeo lake.”—Zaburi 40:4.

Maria alisema: “Maisha yangu huko Hispania na kwingineko yamenifunza kwamba tunapofanya mambo kwa njia ya Yehova tunafanikiwa, hata iwe hisia na mwelekeo wetu unatuelekeza vingine. Na hilo hutokeza furaha kwa sababu sikuzote njia ya Yehova ndiyo bora.”

Andreas, mzee Mkristo ambaye ametumikia katika nchi mbalimbali za Ulaya, anaamini pia kwamba tunaweza kumtegemea Yehova. Alisema hivi: “Ndugu yangu mkubwa mwenye imani tofauti na yangu, alinichochea sana nilipokuwa kijana, akinitia moyo nitafute kazi yenye mshahara mnono. Alihuzunika sana nilipoingia katika utumishi wa wakati wote badala ya kutegemea ahadi za kupata marupurupu baada ya kustaafu. Sijakosa chochote kwa muda wote ambao nimekuwa katika utumishi wa wakati wote, nami nimepata baraka ambazo wengine wanaweza kuwazia tu.”

Mnamo 1993, Felix alialikwa kusaidia kupanua ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Selters, Ujerumani. Kazi ilipokamilika, alialikwa kutumikia Betheli. Aliitikiaje? “Nilikubali mwaliko huo bila kuwa na uhakika. Lakini sasa nimekuwa hapa kwa miaka kumi hivi, nami ninasadiki kwamba Yehova alijibu sala zangu. Anajua kile kinachonifaa zaidi. Kwa kumtegemea kabisa na kumwacha aniongoze, ninampa nafasi ya kunionyesha kile anachotaka nifanye.”

Susanne, aliyetangulia kutajwa, alitaka kuwa mtumishi wa wakati wote, au painia, lakini hakuweza kupata kazi ya muda. Aliendelea kungoja kwa mwaka mmoja huku akimtegemea Yehova. Alisema hivi: “Nilituma maombi ya kuwa painia wa kawaida. Nilikuwa nimeweka pesa akibani ambazo zingenitegemeza kwa mwezi mmoja. Nao ulikuwa mwezi wenye kupendeza sana. Huduma yangu iliniletea shangwe kubwa, lakini sikufanikiwa kupata kazi. Hata hivyo, kama Yehova anavyoahidi, hakuniacha. Katika siku ya mwisho ya mwezi, nilipata kazi. Hapo ndipo nilipotambua kwamba ninaweza kumtegemea Yehova kabisa! Kuingia katika utumishi wa wakati wote kumeniridhisha na kuniletea furaha maishani.”

Kukubali Mashauri Kutoka kwa Mungu Huleta Furaha

Mfalme Daudi alifanya makosa fulani mazito. Nyakati nyingine, alihitaji shauri la hekima. Je, tuko tayari kukubali shauri na maagizo kama Daudi?

Wakati mmoja Aida, kutoka Ufaransa, alitambua kwamba alikuwa amefanya kosa kubwa sana. Alisema hivi: “Hangaiko langu kuu lilikuwa kuwa na uhusiano pamoja na Yehova tena. Sikuhangaishwa na kitu kingine chochote.” Aliomba msaada kutoka kwa wazee Wakristo. Sasa akiwa ametumikia kwa zaidi ya miaka 14 katika utumishi wa wakati wote, anasema hivi: “Inaridhisha kama nini kujua kwamba Yehova alinisamehe!”

Kukubali shauri la kimungu kunaweza kutuzuia tusifanye makosa. Judith alieleza hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka 20, nilimpenda kimahaba mwanabiashara mmoja Mjerumani ambaye alijitahidi sana kunipendeza. Aliheshimiwa sana, alifanikiwa maishani, na tayari alikuwa ameoa! Nilitambua kwamba nilihitaji kuamua ikiwa nitatii sheria za Yehova au nitazipuuza kabisa. Nilizungumza na wazazi wangu. Baba yangu alisema mambo waziwazi akinikumbusha mambo ambayo Yehova alitazamia kutoka kwangu. Alitaja mambo bila kuficha na hicho ndicho nilichohitaji! Hata hivyo, nilijaribu kutafuta kisingizio cha kutotii kanuni za Mungu. Kwa majuma mengi, mama yangu alitumia jioni nyingi akinieleza kwamba sheria za Mungu ni muhimu na zinaokoa uhai. Ninashukuru sana kwamba hatimaye moyo wangu ulivutwa kwa Yehova. Nimepata furaha kubwa kwa kutiwa nidhamu na kufundishwa naye. Nimetumikia kwa miaka mingi katika utumishi wa wakati wote na nimepata mwenzi Mkristo anayenipenda na anayempenda Yehova kwa moyo wote.”

Bila shaka, mambo hayo yanaonyesha ukweli wa maneno haya ya Daudi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa maasi yake, ambaye dhambi yake imefunikwa. Mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hamhesabii kosa.”—Zaburi 32:1, 2.

Furaha Inayotokana na Kuwajali Wengine

“Mwenye furaha ni mtu yeyote anayetenda kwa kumfikiria mtu wa hali ya chini,” Daudi aliandika. Aliongeza hivi: “Katika siku ya msiba Yehova atamwokoa. Yehova mwenyewe atamlinda na kumhifadhi hai. Atatangazwa kuwa mwenye furaha.” (Zaburi 41:1, 2) Jinsi Daudi alivyomshughulikia kwa upendo Mefiboshethi yule mwana mwenye kulemaa wa Yonathani, rafiki mpendwa wa Daudi, ni mfano mzuri wa mtazamo unaofaa kuwaelekea watu wa hali ya chini.—2 Samweli 9:1-13.

Marlies, ambaye ametumikia akiwa mmishonari kwa miaka 47, ana pendeleo la kuwahubiria watu ambao walilazimika kutoroka maeneo hatari ya Afrika, Asia, na Ulaya Mashariki. Alisema hivi: “Wana matatizo mbalimbali na kwa kawaida wao huhisi kuwa hawatakikani na kwamba wanabaguliwa. Sikuzote inafurahisha kuwasaidia watu kama hao.”

Marina, mwenye umri wa miaka 40 hivi, aliandika hivi: “Kwa kuwa mimi ni mseja, ninajua kwamba mtu hufarijika sana anapokuwa na marafiki wanaomjali. Hilo hunichochea kuwatia watu moyo kwa kuwapigia simu au kuwaandikia barua. Wengi wamethamini. Mimi hupata shangwe ninapowasaidia wengine.”

Dimitar, ambaye ana umri wa miaka 20 na kitu aliandika hivi: “Nililelewa na mama yangu. Nilipokuwa kijana, nilifurahi kuzoezwa kwenye huduma kila juma na mwangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko. Bado ninamshukuru kwa uvumilivu wake. Ninajua kwamba sikuzote haikuwa rahisi kunichochea.” Kwa sababu Dimitar anathamini msaada aliopata, sasa anawasaidia wengine: “Mimi huandamana na kijana au mtu mwingine mwenye umri mkubwa kwenye huduma ya shambani angalau mara moja kwa mwezi.”

Kitabu cha Zaburi hutaja pia mambo mengine ambayo huchangia furaha. Jambo moja ni umuhimu wa kutegemea nguvu za Yehova badala ya kujitegemea: “Wanadamu wenye furaha ni wale ambao nguvu zao ziko kwako [Yehova].”—Zaburi 84:5.

Hali za Corinna zinathibitisha hilo. Alihamia nchi iliyokuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri. “Nilikabili lugha mpya, utamaduni mpya, na njia mpya ya kufikiri. Nilihisi kana kwamba niko katika ulimwengu mwingine. Niliingiwa na wasiwasi nilipofikiria kuhubiri katika eneo ambalo sikuzoea. Nilimwomba Yehova msaada, na kwa nguvu zake niliweza kuhubiri siku nzima katika eneo la mbali. Baada ya muda, nikazoea kufanya hivyo. Nilianzisha mafunzo mengi ya Biblia, na bado ninanufaika kutokana na utendaji huo. Nilijifunza kwamba kwa nguvu za Yehova, tunaweza kushinda hata vizuizi vinavyoonekana kuwa vikubwa sana.”

Naam, kuna mambo mbalimbali ambayo huchangia furaha. Hayo yanatia ndani kusitawisha urafiki pamoja na Mungu na watu wake, kumtegemea Yehova kabisa, kukubali shauri lake, na kuwajali wengine. Kwa kutembea katika njia za Yehova na kutii sheria zake, tunaweza kufurahia kibali chake.—Zaburi 89:15; 106:3; 112:1; 128:1, 2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Maria

[Picha katika ukurasa wa 13]

Maree

[Picha katika ukurasa wa 13]

Susanne na Andreas

[Picha katika ukurasa wa 15]

Corinna

[Picha katika ukurasa wa 15]

Dimitar