Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ninavipenda Vikumbusho Vyako”

“Ninavipenda Vikumbusho Vyako”

“Ninavipenda Vikumbusho Vyako”

“Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi.”—WAROMA 15:4.

1. Yehova anatupa vikumbusho kwa njia gani, na kwa nini tunavihitaji?

YEHOVA huwapa watu wake vikumbusho ili viwasaidie kukabiliana na matatizo ya nyakati hizi ngumu. Tunapata baadhi ya vikumbusho hivyo tunaposoma Biblia, na tunapata vingine kupitia habari au maelezo yanayotolewa kwenye mikutano ya Kikristo. Mambo mengi tunayosoma au kusikia katika pindi hizo si mapya. Huenda tulijifunza habari hizo zamani. Hata hivyo, kwa kuwa sisi husahau, tunahitaji kuendelea kujikumbusha makusudi, sheria, na maagizo ya Yehova. Tunapaswa kuthamini vikumbusho vya Mungu. Vinatutia moyo kwa kutusaidia kukumbuka sababu zilizotuchochea kuishi kupatana na mapenzi ya Mungu. Kwa sababu hiyo, mtunga-zaburi alimwimbia Yehova hivi: “Ninavipenda vikumbusho vyako.”—Zaburi 119:24.

2, 3. (a) Kwa nini Yehova amehifadhi mpaka leo masimulizi ya watu wa nyakati za Biblia? (b) Ni masimulizi gani katika Maandiko yatakayozungumziwa katika makala hii?

2 Ingawa Neno la Mungu liliandikwa karne nyingi zilizopita, lina nguvu. (Waebrania 4:12) Linasimulia maisha ya watu wa kale. Ingawa desturi na maoni ya watu yamebadilika sana tangu nyakati za Biblia, mara nyingi matatizo tunayokabili yanafanana na yale ambayo watu walikabili nyakati hizo. Masimulizi mengi yaliyohifadhiwa katika Biblia kwa faida yetu yana mifano yenye kutia moyo ya watu waliompenda Yehova na kumtumikia kwa uaminifu licha ya hali ngumu sana. Masimulizi mengine yanaonyesha mwenendo ambao Mungu anachukia. Yehova alitaka mifano yote hiyo, mizuri na mibaya, iandikwe katika Biblia ili iwe vikumbusho kwetu. Ni kama vile mtume Paulo alivyoandika: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.”—Waroma 15:4.

3 Acheni tuzungumzie masimulizi matatu yanayopatikana katika Maandiko: simulizi la Daudi na Sauli, simulizi la Anania na Safira, na simulizi linaloonyesha jinsi Yosefu alivyojiendesha alipokabiliwa na mke wa Potifa. Masimulizi yote hayo yanatufunza mambo muhimu.

Kushikamana na Mipango ya Mungu

4, 5. (a) Ni hali gani iliyokuwapo kati ya Mfalme Sauli na Daudi? (b) Daudi alitendaje kuhusu chuki ya Sauli?

4 Mfalme Sauli hakuwa mwaminifu kwa Yehova wala hakustahili kuwatawala watu Wake. Kwa hiyo, Mungu alimkataa, naye akamwagiza nabii Samweli amtie mafuta Daudi kuwa mfalme atakayefuata wa Israeli. Daudi alipoonyesha uhodari na ushujaa wake vitani na kusifiwa na watu, Sauli alianza kumwona kuwa adui. Sauli alijaribu tena na tena kumuua. Lakini katika pindi zote hizo, Daudi aliponyoka kwa sababu Yehova alikuwa pamoja naye.—1 Samweli 18:6-12, 25; 19:10, 11.

5 Kwa miaka mingi, Daudi alilazimika kuwa mkimbizi. Daudi alipopata nafasi ya kumuua Sauli, waandamani wake walimchochea afanye hivyo, huku wakimwambia Daudi kwamba Yehova alikuwa amemtia adui yake mkononi mwake. Hata hivyo, Daudi alikataa kufanya hivyo kwa sababu alikuwa mshikamanifu kwa Yehova na aliheshimu cheo cha Sauli akiwa mfalme aliyetiwa mafuta wa watu wa Mungu. Kwa kuwa Yehova ndiye aliyekuwa amemweka rasmi Sauli kuwa mfalme wa Israeli, Yeye pia ndiye angemwondoa wakati ambapo angeona inafaa kufanya hivyo. Daudi aliona kwamba hakuwa na haki ya kuingilia kati. Baada ya kujitahidi juu chini kulingana na hali ili kumfanya Sauli aache kumchukia, Daudi alikata kauli hii: “Yehova mwenyewe atampiga; au siku yake itakuja naye atakufa, au ataanguka vitani, na kufagiliwa mbali. Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba ninyooshe mkono wangu juu ya mtiwa-mafuta wa Yehova!”—1 Samweli 24:3-15; 26:7-20.

6. Kwa nini tunapendezwa na simulizi la Daudi na Sauli?

6 Simulizi hilo linatufunza jambo muhimu. Je, umewahi kujiuliza kwa nini matatizo fulani hutokea katika kutaniko la Kikristo? Huenda mtu fulani anatenda kwa njia isiyofaa. Huenda hajafanya kosa zito, lakini mwenendo wake unakuudhi. Unapaswa kufanya nini? Kwa sababu ya kumjali Mkristo huyo na kwa sababu ya ushikamanifu wako kwa Yehova, huenda ukaamua kuzungumza naye kwa fadhili ukiwa na kusudi la kusuluhisha mambo. Lakini, namna gani tatizo hilo likiendelea? Baada ya kufanya yote uwezayo, inafaa umwachie Yehova jambo hilo. Hivyo ndivyo Daudi alivyofanya.

7. Kwa kumwiga Daudi, tunapaswa kufanya nini tukitendewa isivyo haki au tukibaguliwa?

7 Au huenda unakabili matatizo kwa sababu ya ukosefu wa haki katika jamii au ubaguzi wa kidini. Huenda usiweze kubadili hali hizo sasa. Inaweza kuwa vigumu sana kuvumilia hali kama hizo, lakini tunajifunza jambo fulani kutokana na jinsi Daudi alivyofanya alipotendewa isivyo haki. Zaburi ambazo Daudi aliandika hazionyeshi tu jinsi alivyosali kwa Mungu ili amwokoe kutoka mkononi mwa Sauli, bali pia zinaonyesha jinsi alivyokuwa mshikamanifu kwa Yehova na kuhangaikia kutukuzwa kwa jina la Mungu. (Zaburi 18:1-6, 25-27, 30-32, 48-50; 57:1-11) Daudi alibaki akiwa mshikamanifu kwa Yehova hata ingawa Sauli aliendelea kumdhulumu kwa miaka mingi. Sisi pia tunapaswa kuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova na kwa tengenezo lake hata tukitendewa isivyo haki au wengine wakifanya mambo yasiyofaa. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anajua hali hiyo.—Zaburi 86:2.

8. Mashahidi wa Yehova huko Msumbiji walitendaje wakati ushikamanifu wao kwa Yehova ulipojaribiwa?

8 Wakristo huko Msumbiji wameendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova wakati wa majaribu. Katika mwaka wa 1984, vijiji vyao vilivamiwa mara nyingi na kikundi fulani cha waasi wenye silaha. Waasi hao walipora nyumba na kuziteketeza, na hata kuwaua watu. Wakristo hao wa kweli hawangeweza kujilinda. Wakaaji wa eneo hilo walilazimishwa kujiunga na kikundi fulani cha kijeshi au kukiunga mkono kwa njia nyingine. Mashahidi wa Yehova waliona kwamba jambo hilo linapingana na msimamo wao wa Kikristo wa kutojihusisha na vita. Mashahidi hao walipokataa kujiunga na kikundi hicho, washiriki wa kikundi hicho walikasirika sana. Mashahidi 30 waliuawa katika kipindi hicho cha msukosuko, lakini hata kifo hakingeweza kuvunja ushikamanifu wa watu wa Mungu. * Kama Daudi, walivumilia walipotendewa isivyo haki, lakini mwishowe wakawa washindi.

Kikumbusho Kinachotuonya

9, 10. (a) Tunaweza kufaidikaje kutokana na mifano fulani inayotajwa katika Maandiko? (b) Matendo ya Anania na Safira yalikuwa na ubaya gani?

9 Mifano ya baadhi ya watu wanaotajwa katika Maandiko ni vikumbusho vinavyotuonya kuhusu mwenendo tunaopaswa kuepuka. Naam, Biblia ina masimulizi mengi kuhusu watu, hata watumishi wa Mungu, ambao walitenda mabaya na kuvuna mabaya. (1 Wakorintho 10:11) Simulizi moja linahusu Anania na Safira, wenzi wa ndoa ambao walikuwa katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza huko Yerusalemu.

10 Baada ya Pentekoste ya 33 W.K., waamini wapya waliobaki huko Yerusalemu ili wafaidike na ushirika wa mitume walihitaji msaada wa kimwili. Baadhi ya washiriki wa kutaniko waliuza mali zao ili kuhakikisha kwamba hakuna yeyote aliyekuwa na uhitaji. (Matendo 2:41-45) Anania na Safira waliuza shamba na kuwapelekea mitume sehemu fulani tu ya pesa walizopata, huku wakidai kwamba hizo ndizo pesa zote walizopata. Ni kweli kwamba Anania na Safira walikuwa na haki ya kutoa pesa nyingi au kidogo, lakini walikuwa na nia mbaya, nao hawakuwa wanyoofu. Walitaka kuwapendeza watu na kudanganya kwamba wanafanya mengi sana. Kwa mwongozo wa roho takatifu, mtume Petro alifichua udanganyifu na unafiki wao, naye Yehova akawaua.—Matendo 5:1-10.

11, 12. (a) Ni Maandiko gani yanayotukumbusha kuhusu unyoofu? (b) Tunapata faida gani kwa kuwa wanyoofu?

11 Tukishawishiwa kudanganya ili watu watuone kuwa wazuri, acheni tukumbuke simulizi la Anania na Safira. Tunaweza kuwadanganya wanadamu wenzetu, lakini hatuwezi kumdanganya Yehova. (Waebrania 4:13) Mara nyingi Maandiko yanatuhimiza tuwe wanyoofu tunaposhughulika na wenzetu, kwa sababu waongo hawatakuwapo katika dunia yenye uadilifu. (Methali 14:2; Ufunuo 21:8; 22:15) Sababu ya kufanya hivyo ni wazi. Shetani Ibilisi ndiye anayeendeleza uwongo wote.—Yohana 8:44.

12 Tunapata faida nyingi kwa kuwa wanyoofu maishani. Tunakuwa na dhamiri safi na uradhi unaotokana na kuaminiwa na wengine. Katika visa vingi, Wakristo wamepata kazi, au wamedumisha kazi, kwa sababu ya kuwa wanyoofu. Hata hivyo, faida kubwa zaidi ni kwamba unyoofu hutufanya tuwe rafiki za Mungu Mweza-Yote.—Zaburi 15:1, 2.

Kudumisha Usafi wa Kiadili

13. Yosefu alikabili hali gani, naye alitendaje?

13 Yosefu, mwana wa yule mzee wa ukoo Yakobo, aliuzwa utumwani akiwa na umri wa miaka 17. Baada ya muda, alipelekwa katika nyumba ya Potifa, ambaye alikuwa ofisa wa makao ya mfalme wa Misri. Yosefu alipokuwa huko, mke wa bwana wake alivutiwa naye. Mwanamke huyo alitamani kufanya ngono na Yosefu, ambaye alikuwa kijana mwenye sura nzuri. Siku baada ya siku, mwanamke huyo alimsihi hivi: “Lala nami.” Yosefu alikuwa mbali na familia yao, katika nchi ambayo hakuna mtu aliyemjua. Huenda angeweza kufanya ngono na mwanamke huyo bila watu wengine kujua. Lakini mwishowe, wakati mke wa Potifa alipomshika, Yosefu alikimbia.—Mwanzo 37:2, 18-28; 39:1-12.

14, 15. (a) Kwa nini tunapendezwa na simulizi la Yosefu? (b) Kwa nini mwanamke mmoja Mkristo anafurahi kwamba alifuata vikumbusho vya Mungu?

14 Yosefu alilelewa katika familia inayomwogopa Mungu, naye alijua kwamba ni kosa kwa watu ambao si mume na mke kufanya ngono pamoja. Aliuliza hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” Huenda alikata kauli hiyo kwa sababu alijua ile kanuni ambayo Mungu aliwapa wanadamu huko Edeni, yaani, kanuni ya kuwa na mume mmoja na mke mmoja. (Mwanzo 2:24) Watu wa Mungu leo wanaweza kufaidika kwa kutafakari jinsi Yosefu alivyotenda katika hali hiyo. Katika maeneo fulani, watu huona kwamba ni sawa kufanya uasherati, na vijana ambao hukataa kufanya mambo yasiyo ya adili hudhihakiwa na vijana wenzao. Watu wazima wengi hufanya ngono nje ya ndoa. Hivyo, simulizi la Yosefu ni kikumbusho kinachofaa leo. Mungu angali anaona uasherati na uzinzi kuwa dhambi. (Waebrania 13:4) Watu wengi ambao wametumbukia katika ngono haramu wanakubali kwamba inafaa sana kuepuka kufanya hivyo. Baadhi ya matokeo mabaya ya ngono haramu ni kuaibika, kusumbuliwa na dhamiri, wivu, kupata mimba, na kuambukizwa ugonjwa wa zinaa. Maandiko yanatukumbusha kwamba mtu anayezoea kufanya uasherati “anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.”—1 Wakorintho 5:9-12; 6:18; Methali 6:23-29, 32.

15 Shahidi mmoja wa Yehova mseja anayeitwa Jenny, * ana sababu za kuthamini vikumbusho vya Mungu. Akiwa kazini, mwanamume mmoja mwenye sura nzuri alionyesha kwamba anapendezwa naye kimahaba. Jenny alipokataa kumwonyesha upendezi wowote, mtu huyo alizidisha jitihada zake. Jenny anasema hivi: “Ilibidi nipambane ili kudumisha usafi wa kiadili kwa sababu ni kawaida kuhisi vizuri wakati mtu wa jinsia tofauti anapoonyesha kwamba anapendezwa nawe.” Hata hivyo, Jenny alitambua kwamba mtu huyo alikuwa akitaka kufanya ngono naye kama alivyokuwa amefanya na wanawake wengi. Jenny alipohisi kwamba azimio lake la kutofanya jambo lisilo la adili limeanza kudhoofika, alimwomba Yehova amsaidie kubaki mwaminifu Kwake. Jenny alitambua kwamba mambo aliyojifunza alipokuwa akifanya utafiti katika Biblia na vichapo vya Kikristo yalikuwa kama vikumbusho ambavyo vilimwimarisha kukaa macho. Kikumbusho kimoja kilichomsaidia ni simulizi la Yosefu na mke wa Potifa. Jenny anamalizia kwa kusema hivi: “Maadamu ninaendelea kujikumbusha jinsi ninavyompenda Yehova sana, sihitaji kuogopa kwamba nitafanya ubaya huu mkubwa na kumtendea Yehova dhambi.”

Tilia Maanani Vikumbusho vya Mungu!

16. Tunaweza kufaidikaje kwa kujikumbusha na kutafakari kuhusu maisha ya watu wanaotajwa katika Biblia?

16 Sote tunaweza kuzidisha uthamini wetu kwa ajili ya viwango vya Yehova kwa kujitahidi kuelewa kwa nini alitaka masimulizi fulani yahifadhiwe katika Maandiko kwa ajili yetu. Masimulizi hayo yanafundisha nini? Ni sifa au mielekeo gani ya watu wanaosimuliwa katika Biblia tunayohitaji kuiga au kuepuka? Neno la Mungu lina masimulizi ya watu wengi. Wote wanaopenda kufundishwa na Mungu wanaweza kufaidika kwa kusitawisha hamu kwa ajili ya hekima inayotokeza uhai, kutia ndani mambo tunayojifunza kutokana na mifano ambayo Yehova amehifadhi vizuri. Mara nyingi gazeti hili limekuwa na masimulizi ya maisha kuhusu watu ambao tunaweza kujifunza kutoka kwao. Kwa nini usitenge wakati kujikumbusha masimulizi hayo?

17. Unahisije kuhusu vikumbusho vya Yehova, na kwa nini unahisi hivyo?

17 Tunathamini sana jinsi Yehova anavyowajali wale wanaojitahidi kufanya mapenzi yake! Sisi si wakamilifu, kama vile wanaume na wanawake wanaotajwa katika Biblia hawakuwa wakamilifu. Hata hivyo, masimulizi kuhusu matendo yao yanaweza kutufaidi sana. Tukitilia maanani vikumbusho vya Yehova, tunaweza kuepuka kufanya makosa mazito, nasi tunaweza kuiga mifano bora ya watu waliotembea katika njia za uadilifu. Tukifanya hivyo, tutakubaliana na wimbo huu wa mtunga-zaburi: “Wenye furaha ni wale wanaoshika vikumbusho [vya Yehova]; wanaendelea kumtafuta kwa moyo wote. Nafsi yangu imeshika vikumbusho vyako, nami navipenda sana.”—Zaburi 119:2, 167.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona 1996 Yearbook of Jehovah’s Witnesses (Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1996), ukurasa wa 160-162.

^ fu. 15 Jina limebadilishwa.

Ungejibuje?

• Maoni ya Daudi kumhusu Sauli yanatufunza nini?

• Simulizi la Anania na Safira linatufunza nini?

• Kwa nini simulizi la maisha ya Yosefu linatupendeza hasa leo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwa nini Daudi hakukubali Sauli auawe?

[Picha katika ukurasa wa 27]

Tunajifunza nini kutokana na simulizi la Anania na Safira?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ni nini kilichomfanya Yosefu akatae kushawishiwa kufanya uasherati?