Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ongezeko Katika Nchi ya Uganda Yenye Makabila Mengi

Ongezeko Katika Nchi ya Uganda Yenye Makabila Mengi

Ongezeko Katika Nchi ya Uganda Yenye Makabila Mengi

NCHI ya Uganda ambayo ni maridadi sana iko katikati ya Bonde Kuu la Ufa la Afrika Mashariki, na iko pande zote mbili za ikweta. Ina mandhari mbalimbali, mimea mingi, na wanyama wenye kupendeza. Kwa kuwa nchi hiyo iko kwenye uwanda wa juu wa Afrika, ina hali ya hewa ya wastani na milima yenye kupendeza inayoenea kwa kilometa nyingi.

Uganda ni mojawapo ya nchi chache zenye milima yenye theluji na maeneo yenye joto katika sehemu ndogo. Upande wa magharibi kuna Milima ya Ruwenzori yenye vilele vilivyo na theluji ambayo huitwa pia Milima ya Mwezi, na upande wa mashariki kuna maeneo makavu. Kwenye nyanda za Uganda kuna tembo, nyati, na simba. Sokwe, nyani, na zaidi ya aina 1,000 za ndege huishi milimani kwenye misitu mikubwa. Sehemu nyingi za bara la Afrika hukumbwa na ukame na njaa, lakini Uganda ina mito mingi na maziwa kama vile Ziwa Viktoria ambalo ndilo ziwa la pili kwa ukubwa ulimwenguni lenye maji yasiyo na chumvi. Maji ya upande wa kaskazini wa ziwa hilo hutiririka kwenye Mto Nile. Si ajabu kwamba Winston Churchill alitaja nchi hiyo kuwa “lulu ya Afrika”!

“Lulu” Yang’aa Leo

Hata hivyo, jambo lenye kuvutia zaidi nchini Uganda ni watu wa makabila mbalimbali ambao ni wenye urafiki na wakarimu. Nchi hiyo yenye watu wengi wanaodai kuwa “Wakristo” ina mchanganyiko wa makabila mengi na watu wenye utamaduni mbalimbali. Hata leo watu hao wanatofautiana kwa mila na mavazi.

Hivi karibuni, watu wengi huko Uganda wamekubali habari njema ya Biblia kuhusu wakati amani ya kudumu itakapoenea duniani pote. (Zaburi 37:11; Ufunuo 21:4) Si rahisi kupeleka ujumbe huo kwa watu katika nchi hiyo yenye ukubwa kama wa Uingereza.

Kuanzia mwanzo mdogo mwaka wa 1955 wakati mtu wa kwanza nchini Uganda alipobatizwa katika Ziwa Viktoria na kuwa Shahidi wa Yehova, hatimaye “mdogo” akawa elfu mwaka wa 1992. Tangu mwaka wa 1955, kumekuwa na ongezeko lenye kuendelea. Hilo linapatana na maneno haya ya Mungu yenye kutia moyo: “Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.”—Isaya 60:22.

Kushinda Vizuizi vya Lugha

Ingawa Kiingereza ndiyo lugha rasmi inayozungumzwa sana, hasa shuleni, Waganda wengi huzungumza lugha zao za asili. Hivyo, ili kuwapelekea watu habari njema, Mashahidi wa Yehova hufikiria pia lugha nyingine zinazozungumzwa sana na watu. Hilo limekuwa jambo muhimu kwa sababu zaidi ya asilimia 80 ya watu milioni 25 nchini Uganda wanaishi katika maeneo ya mashambani au katika miji midogo, ambako watu wanategemea sana lugha zao za asili katika mawasiliano ya kila siku. Jitihada kubwa zinahitajiwa ili kuwafikia watu hao wanaozungumza lugha mbalimbali na kutosheleza mahitaji yao ya kiroho.

Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wamejitahidi kutosheleza mahitaji hayo kwa kuwahubiria watu katika lugha zao za asili na kwa kutayarisha vichapo vya Biblia katika lugha mbalimbali. Kwenye ofisi ya tawi huko Kampala, jiji kuu, vikundi vya watafsiri vinatafsiri katika lugha nne: Kiacholi, Kilhukonzo, Kiganda, na Runyankore. Isitoshe, makusanyiko yanayofanywa katika lugha mbalimbali nchini kote yanahudhuriwa na watu wengi, zaidi ya mara mbili ya idadi ya Mashahidi wa Yehova nchini Uganda. Hilo linaonyesha waziwazi kwamba jitihada za kuwahubiria watu wanaozungumza lugha mbalimbali zinachochea ongezeko hilo la haraka la kiroho. Lakini si hayo tu.

Mapainia Waongoza Kazi

Makutaniko huunga mkono kwa hiari mpango wa kuhubiri maeneo ya mbali kwa muda wa miezi mitatu kila mwaka. (Matendo 16:9) Mapainia vijana au wahubiri wa wakati wote wenye bidii wanaozidi kuongezeka, wanaongoza katika kazi hiyo. Wanasafiri hadi maeneo ya mbali ambako habari njema haijawahi kuhubiriwa.

Mashahidi wawili walitumwa kutumikia kwa muda wa miezi mitatu wakiwa mapainia wa pekee huko Bushenyi, mji mdogo ulio magharibi mwa Uganda. Walijiunga na Shahidi mmoja wa Yehova wa eneo hilo ili kuhubiri na kupanga mikutano ya Kikristo. Kwa muda wa mwezi mmoja, mapainia hao wawili walikuwa wakijifunza Biblia kwa ukawaida na watu 40, na 17 kati yao walianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Mapainia hao wanasema: “Baadhi ya wale tulioachia broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? * walikuja nyumbani kwetu siku chache baadaye wakiwa na karatasi kadhaa zilizoandikwa majibu ya maswali yaliyo katika broshua hiyo. Walitaka kujua ikiwa majibu yao yalikuwa sahihi.” Leo, katika mji huo kuna kutaniko lenye Jumba la Ufalme.

Mapainia wawili walisafiri kwenda katika eneo la magharibi mwa Uganda ambako habari njema haikuwa imehubiriwa bado. Waliandika hivi: “Hakika watu wana kiu ya kweli ya Biblia. Kwa muda wa miezi mitatu ambayo tumekuwa hapa, tumeweza kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia 86.” Hivi karibuni kikundi cha Mashahidi kilianzishwa rasmi katika eneo hilo.

Wafanyakazi Wengine Wenye Bidii Shambani

Miongoni mwa mapainia wenye bidii, kuna wale ambao wametumikia kwa miaka mingi. Kabla ya kuwa Shahidi wa Yehova, Patrick alikuwa mpiga-zumari katika jeshi la angani la mtawala wa zamani wa Uganda, Idi Amin. Miezi sita baada ya Patrick kubatizwa mwaka wa 1983, alianza huduma ya wakati wote. Leo yeye ni mwangalizi anayesafiri, anayetembelea makutaniko na kuyatia moyo.

Margaret alibatizwa mwaka wa 1962. Licha ya kwamba anakaribia miaka 80 na ana matatizo ya nyonga ambayo humzuia asitembee sana, yeye hutumia saa 70 hivi kila mwezi akiwaeleza majirani wake tumaini la Biblia. Yeye hutandaza vichapo juu ya kiti nje ya nyumba yake na kuanzisha mazungumzo na mpita-njia yeyote ambaye angependa kusikiliza habari njema kuhusu ulimwengu mpya wenye amani.

Simon, mkulima kutoka mashariki mwa Uganda, alitafuta ukweli kwa miaka 16 hadi mwaka wa 1995 alipopata baadhi ya vichapo vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Mambo aliyosoma yalimchochea kutaka kujua mengi zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu na kusudi zuri la Yehova kuelekea dunia. Kwa kuwa hakukuwa na Mashahidi huko Kamuli mahali alipoishi, Simon alisafiri karibu kilometa 140 hadi Kampala ili kuwatafuta. Leo, kuna kutaniko katika kijiji hicho.

“Hatutoki Hapa”

Kama katika maeneo mengine barani Afrika, watu wengi hutazamia kikundi cha kidini kiwe na mahali panapofaa pa ibada. Hilo lilionekana kuwa tatizo kubwa katika makutaniko kadhaa ya Mashahidi wa Yehova, kwa kuwa hayakuwa na pesa za kujenga Majumba ya Ufalme yanayofaa. Ni vigumu kueleza shukrani za akina ndugu wakati mpango wa kujenga haraka Majumba ya Ufalme ulipoanzishwa ulimwenguni pote mwishoni mwa mwaka wa 1999. Kwa muda wa miaka mitano iliyofuata, Majumba ya Ufalme mapya 40 yalikamilishwa nchini Uganda. Leo, karibu kila kutaniko lina Jumba zuri la Ufalme. Ujenzi huo unawapa watu wa maeneo hayo ujumbe huu, “Hatutoki hapa.” Ujenzi wa Majumba ya Ufalme umechangia ongezeko.

Kutaniko dogo kaskazini mwa Uganda lilikuwa likifanyia mikutano chini ya miembe yenye majani mengi. Uwanja ulipopatikana, kazi ilianza mara moja. Ndugu wa ujenzi na Mashahidi wenyeji walianza ujenzi wa Jumba la Ufalme. Mwanasiasa wa zamani aliyejulikana sana katika eneo hilo alishangazwa na kazi hiyo. Aliruhusu banda lake la gari litumiwe kwa ajili ya mikutano hadi Jumba la Ufalme lilipokamilishwa. Pia, alikubali kujifunza Biblia pamoja na mmoja wa wajenzi wa kujitolea. Sasa yeye ni mhubiri mwenye bidii aliyebatizwa, na anafurahi kumwabudu Yehova katika Jumba la Ufalme maridadi!

Kwenye ujenzi wa Jumba moja la Ufalme kusini-mashariki mwa nchi, mjenzi mmoja mwenyeji alichochewa sana na roho ya urafiki, upendo, na ushirikiano alioona miongoni mwa akina ndugu hivi kwamba akajitolea kusaidia. Siku ya mwisho ya ujenzi, alifanya kazi usiku mzima ili Jumba la Ufalme liwe tayari kwa ajili ya kuwekwa wakfu asubuhi iliyofuata. Alisema hivi: “Ninyi tu ndio mnaopendana kikweli, na si kwa maneno matupu tu.”

Ongezeko Linatarajiwa Licha ya Matatizo

Kwa kuwa maeneo mapya yanahubiriwa huko Uganda, idadi ya Mashahidi wa Yehova inaongezeka hatua kwa hatua na watu wengi wanaopendezwa wanashirikiana na makutaniko. Hata hivyo, kwa sasa hangaiko ni kuhusu idadi kubwa ya wakimbizi wanaomiminika Uganda. Vita vya wenyewe kwa wenyewe katika nchi jirani vinawaathiri pia watu wa Yehova. Mashahidi walio katika kambi za wakimbizi wamethibitisha kwamba wanamtumaini Yehova kabisa. Ofisa mmoja mkuu kutoka nchi jirani ambaye aliwatesa Mashahidi wakati kulipokuwa na marufuku katika nchi hiyo, anakumbuka kwamba wakati mmoja alikuwa tajiri. Baada ya kujifunza Biblia katika mojawapo ya kambi za wakimbizi na kuwa Shahidi, alisema hivi: “Vitu vya kimwili na cheo kikuu katika ulimwengu huu havina thamani ya kweli. Ingawa sasa mimi ni maskini na mgonjwa, maisha yangu ni bora kuliko yalivyokuwa hapo mbeleni. Ninamjua Yehova, na ninathamini sana pendeleo la sala. Zaidi ya kuwa na tumaini hakika la wakati ujao, ninajua kwa nini tunapaswa kuvumilia matatizo ya leo. Hivyo, nina amani ya moyoni ambayo sikuwa nayo hapo awali.”

Imesemwa kwamba ukitia kijiti jioni kwenye udongo wenye rutuba wa Uganda, kufikia asubuhi kijiti hicho kitakuwa kimeota. Ongezeko la kiroho linaloshuhudiwa katika nchi hiyo linaonyesha kwamba udongo wa kiroho ni wenye rutuba sana pia. Tunamshukuru Yehova Mungu kwa kuruhusu wakati ili watu wengi zaidi wa makabila mbalimbali ya Uganda wajifunze kuhusu Ufalme. Yesu alilinganisha ubora wa Ufalme na “lulu moja ya thamani kubwa.” Watu wengi huko Uganda wameanza kutambua jambo hilo.—Mathayo 13:45, 46.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Ramani katika ukurasa wa 8]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

SUDAN

UGANDA

Mto Nile

Kamuli

Tororo

Kampala

Bushenyi

Ziwa Viktoria

KENYA

TANZANIA

RWANDA

[Picha katika ukurasa wa 9]

Watatu kati ya mapainia wengi wenye bidii

[Picha katika ukurasa wa 10]

Patrick

[Picha katika ukurasa wa 10]

Margaret

[Picha katika ukurasa wa 10]

Simon

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kusanyiko la wilaya huko Tororo

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

Background: © Uganda Tourist Board