Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Somo Kuhusu Kiburi na Unyenyekevu

Somo Kuhusu Kiburi na Unyenyekevu

Somo Kuhusu Kiburi na Unyenyekevu

Tukio fulani katika maisha ya Mfalme Daudi linaonyesha tofauti kati ya unyenyekevu wa kweli na kiburi. Ilikuwa baada ya Daudi kushinda Yerusalemu na kulifanya kuwa jiji lake kuu. Daudi alimwona Yehova kuwa Mfalme halisi wa Israeli, hivyo akapanga kwamba Sanduku la Agano, lililowakilisha kuwapo kwa Mungu, lipelekwe jijini humo. Tukio hilo lilikuwa muhimu sana kwa Daudi hivi kwamba alionyesha shangwe yake waziwazi akifuata makuhani waliobeba Sanduku la Agano. Wakaaji wa Yerusalemu walimwona mfalme wao “akirukaruka” na “kucheza dansi . . . kwa nguvu zake zote.”—1 Mambo ya Nyakati 15:15, 16, 29; 2 Samweli 6:11-16.

Hata hivyo, Mikali, mke wa Daudi hakujiunga na msafara huo wenye shangwe. Alitazama kutoka dirishani na badala ya kufurahia jinsi Daudi alivyomsifu Yehova, “akaanza kumdharau moyoni mwake.” (2 Samweli 6:16) Kwa nini Mikali alihisi hivyo? Inaonekana kwamba alijiona kuwa mtu wa maana sana kwa sababu ya kuwa binti ya Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli, na mke wa mfalme wa pili wa Israeli. Huenda alihisi kwamba mume wake, mfalme, hakupaswa kujiunga na watu wa kawaida kusherehekea kwa njia ya kujishushia heshima. Majivuno yake yalionekana kwa jinsi alivyomsalimu Daudi aliporudi nyumbani. Alisema hivi kwa dhihaka: “Lo! Jinsi mfalme wa Israeli alivyojitukuza leo wakati alipojifunua leo mbele ya macho ya vijakazi wa watumishi wake, kama vile mmoja wa watu wapumbavu anavyojifunua!”—2 Samweli 6:20.

Daudi alitendaje alipochambuliwa na Mikali? Daudi alimkemea Mikali kwa kumwambia kwamba Yehova alimkataa Sauli, baba yake, na badala yake akamchagua yeye. Daudi akaongeza hivi: “Nitajipuuza hata zaidi kuliko hivi, nitajishusha machoni pangu mwenyewe; nami nimeamua kujitukuza pamoja na wale vijakazi uliowataja.”—2 Samweli 6:21, 22.

Naam, Daudi aliazimia kuendelea kumtumikia Yehova kwa unyenyekevu. Mtazamo huo unatusaidia kuelewa sababu iliyomfanya Yehova amwone Daudi kuwa “mtu anayekubalika kwa moyo wangu.” (Matendo 13:22; 1 Samweli 13:14) Kwa hakika, Daudi alikuwa anafuata kielelezo bora zaidi cha unyenyekevu, yaani, unyenyekevu wa Yehova Mungu. Inapendeza kwamba usemi ambao Daudi alitumia alipomwambia Mikali “nitajishusha” unatokana na kitenzi cha Kiebrania ambacho pia hutumiwa kuonyesha maoni ya Mungu kuhusu wanadamu. Ingawa Yehova ndiye Mtu mkuu zaidi katika ulimwengu wote, andiko la Zaburi 113:6, 7 linasema kwamba “anajishusha [yaani, anajiweka chini au kujiondoa katika cheo chake au ukuu wake anaposhughulika na mtu aliye chini yake] kutazama mbingu na dunia, akimwinua mtu wa hali ya chini kutoka kwenye mavumbi; humwinua maskini kutoka kwenye shimo la majivu.”

Kwa kuwa Yehova ni mnyenyekevu, anachukia “macho ya majivuno” ya watu wenye kiburi. (Methali 6:16, 17) Kwa sababu ya kuonyesha sifa hiyo mbaya na kutomheshimu yule ambaye Mungu alimchagua kuwa mfalme, Mikali alinyimwa pendeleo la kumzalia Daudi mwana, naye akafa bila kupata mtoto. Hilo ni somo kwetu! Wote wanaotaka kupata kibali cha Mungu lazima watii maneno haya: “Jifungeni unyenyekevu wa akili kuelekeana ninyi wenyewe, kwa sababu Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”—1 Petro 5:5.