Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Utunze Mzabibu Huu’!

‘Utunze Mzabibu Huu’!

‘Utunze Mzabibu Huu’!

WALE wapelelezi 12 walitembelea sehemu mbalimbali za Nchi ya Ahadi. Musa aliwaambia waone jinsi wakaaji walivyo na walete mazao ya nchi hiyo. Walipendezwa hasa na zao gani? Karibu na Hebroni, waliona shamba la mizabibu lililokuwa na zabibu kubwa sana hivi kwamba ilihitaji wapelelezi wawili kubeba kishada kimoja tu. Mizabibu hiyo ilipendeza sana hivi kwamba wapelelezi hao wakapaita mahali hapo penye rutuba “bonde la mto la Eshkoli” au “Kishada cha Zabibu.”—Hesabu 13:21-24.

Katika karne ya 19, mgeni aliyetembelea Palestina alisema: “Eshkoli, au bonde la Zabibu, . . . bado lina mizabibu mingi na zabibu zake ndizo nzuri na kubwa zaidi nchini Palestina.” Ingawa mizabibu ya Eshkoli ilikuwa mingi sana, nchi ya Palestina ilizaa zabibu nzuri katika nyakati za Biblia. Rekodi za Misri zinaonyesha kwamba Mafarao waliagiza divai kutoka Kanaani.

Kitabu kimoja (The Natural History of the Bible) kinasema: “Vilima [vya Palestina] vyenye miamba vina udongo wenye changarawe, navyo hupata mwangaza mwingi wa jua, joto la kiangazi, na maji ya mvua yanayotiririka upesi wakati wa baridi kali. Hali hizo hufanya eneo hilo liwe na mizabibu mingi.” Isaya alionyesha kwamba maeneo fulani yalikuwa na mizabibu 1,000.—Isaya 7:23.

‘Nchi ya Mizabibu’

Musa aliwaambia Waisraeli kwamba watarithi nchi ya “mizabibu na tini na makomamanga.” (Kumbukumbu la Torati 8:8) Kulingana na kitabu fulani (Baker Encyclopedia of Bible Plants), “mizabibu ilikuwa mingi sana katika Palestina ya kale hivi kwamba mbegu za zabibu zimepatikana katika karibu kila eneo lililochimbuliwa.” Mizabibu ya Nchi ya Ahadi ilizaa sana kiasi cha kwamba katika mwaka wa 607 K.W.K., majeshi ya Nebukadneza yalipoharibu Yuda, watu waliobaki katika nchi hiyo ‘walikusanya divai na matunda ya wakati wa kiangazi kwa wingi sana.’—Yeremia 40:12; 52:16.

Ili kuzalisha divai kwa wingi, wakulima Waisraeli waliitunza sana mizabibu yao. Kitabu cha Isaya kinaeleza jinsi ambavyo mtunza-mizabibu Mwisraeli angechimba shamba lililo milimani na kuondoa mawe makubwa kabla ya kupanda “mzabibu bora mwekundu.” Kisha, huenda angejenga ukuta wa mawe, akitumia mawe aliyotoa kwenye udongo. Ukuta huo ungelinda shamba la mizabibu lisikanyagwe na ng’ombe na kuzuia mbweha, nguruwe-mwitu, na wezi. Pia, huenda angechimba shinikizo la divai na kujenga mnara mdogo. Mnara huo ungekuwa mahali penye baridi pa kukaa wakati wa mavuno ambapo mizabibu ilihitaji kulindwa hata zaidi. Baada ya kufanya kazi yote hiyo, angetazamia mavuno mazuri ya zabibu.—Isaya 5:1, 2. *

Ili kuhakikisha kwamba anapata mavuno mengi, kwa kawaida mkulima alipunguza matawi ya mizabibu ili kuboresha mazao, naye aliondoa magugu na miiba. Huenda angetilia maji shamba la mizabibu katika miezi ya kiangazi ikiwa mvua ya majira ya kuchipua haikutosha.—Isaya 5:6; 18:5; 27:2-4.

Wakati wa kuvuna zabibu, mwishoni mwa majira ya kiangazi, ulikuwa wakati wa shangwe. (Isaya 16:10) Neno “Gitithi” linapatikana katika utangulizi wa zaburi tatu. (Zaburi 8, 81, na 84) Neno hilo la pekee la muziki linatafsiriwa kuwa “mashinikizo ya divai” katika Septuajinti na huenda likaonyesha kwamba Waisraeli waliimba zaburi hizo wakati wa mavuno ya zabibu. Ingawa zabibu zilitumiwa hasa kutengeneza divai, Waisraeli walizila pia zikiwa hazijakaushwa, na nyakati nyingine walizikausha na kuzitumia kutengeneza keki.—2 Samweli 6:19; 1 Mambo ya Nyakati 16:3.

Mzabibu wa Israeli

Nyakati nyingine Biblia huwafafanua watu wa Mungu kuwa mzabibu. Huo ni mfano unaofaa tunapofikiria jinsi Waisraeli walivyothamini mzabibu. Kwenye Zaburi ya 80, Asafu alilinganisha taifa la Israeli na mzabibu ambao Yehova alikuwa amepanda Kanaani. Nchi ililimwa ili mzabibu wa Israeli usitawi na kukomaa. Lakini miaka ilipopita, kuta zilizolinda mzabibu huo zilianguka. Taifa hilo halikuendelea kumtegemea Yehova, naye akaacha kulilinda. Kama nguruwe-mwitu anayekanyaga-kanyaga shamba la mzabibu, ndivyo mataifa adui walivyoharibu mali ya Israeli. Asafu alimwomba Yehova alisaidie taifa hilo ili lipate tena utukufu lililokuwa nao. Alimsihi hivi: ‘Utunze mzabibu huu.’—Zaburi 80:8-15.

Isaya aliifananisha “nyumba ya Israeli” na shamba la mzabibu ambalo hatua kwa hatua lilizaa “zabibu-mwitu” au zabibu zilizooza. (Isaya 5:2, 7) Zabibu-mwitu ni ndogo kuliko zabibu za shambani na hazina nyama nyingi, nazo mbegu zake huchukua nafasi kubwa ya tunda. Zabibu-mwitu haziwezi kutumiwa kutengeneza divai wala kuliwa. Huo ni mfano mzuri unaowakilisha taifa lililoasi imani ambalo matunda yake yalikuwa ni uvunjaji wa sheria badala ya uadilifu. Si Mkulima wa mizabibu aliyetokeza matunda hayo yasiyofaa. Yehova alifanya yote awezayo ili kufanya taifa hilo lizae matunda. Aliuliza hivi: “Kuna kitu gani ambacho bado sijalifanyia shamba langu la mizabibu, ambacho bado sijafanya ndani yake?”—Isaya 5:4.

Kwa kuwa mzabibu wa Israeli haukuwa unazaa, Yehova alionya kwamba angevunja ukuta wa ulinzi aliokuwa amejenga kuzunguka watu wake. Kamwe hangepunguza tena matawi ya mzabibu huo wa mfano wala kuulimia. Mvua ya majira ya kuchipua ambayo mmea huo ulitegemea haingenyesha, na miiba na magugu yangejaa katika shamba hilo la mizabibu.—Isaya 5:5, 6.

Musa alitabiri kwamba uasi-imani wa Waisraeli ungefanya hata mashamba yao ya mizabibu halisi yanyauke. Alisema hivi: “Mashamba ya mizabibu utayapanda na hakika utayapalilia, lakini pia hutakunywa divai yoyote wala kukusanya chochote, kwa sababu mdudu atazila.” (Kumbukumbu la Torati 28:39) Mzabibu unaweza kunyauka baada ya siku kadhaa mdudu akiingia katika shina lake na kuula.—Isaya 24:7.

“Mzabibu wa Kweli”

Kama vile Yehova alivyowafananisha Waisraeli na mzabibu, Yesu alitumia mfano huohuo pia. Jioni ya mwisho ambayo Yesu alikuwa na wanafunzi wake, aliwaambia hivi: “Mimi ndiye mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima.” (Yohana 15:1) Yesu aliwafananisha wanafunzi wake na matawi ya mzabibu. Kama vile matawi ya mzabibu halisi yanavyopata nguvu kutoka kwenye shina, wanafunzi wa Kristo wanapaswa kubaki katika muungano na yeye. Yesu alisema: “Bila mimi hamwezi kufanya lolote kamwe.” (Yohana 15:5) Wakulima hupanda mzabibu kwa sababu ya matunda yake, na Yehova anatazamia watu wake wazae matunda ya kiroho. Hilo humletea Mungu aliye Mkulima wa mzabibu uradhi na utukufu.—Yohana 15:8.

Katika kisa cha mzabibu halisi, kuzaa matunda mengi hutegemea kupunguza matawi na kuusafisha, na Yesu anazungumzia hatua hizo mbili. Mkulima anaweza kupunguza matawi mara mbili kila mwaka ili kuhakikisha mzabibu unazaa kwa wingi. Katika miezi ya baridi kali, matawi mengi ya mzabibu huenda yakakatwa. Mkulima huondoa matawi mengi ya mwaka uliopita. Huenda akaacha matawi matatu au manne, na katika kila tawi huenda akaacha chipukizi moja au mawili. Machipukizi hayo machanga yanayofanana na machipukizi ya mwaka uliopita, ndiyo yatakayokuwa matawi yenye kuzaa matunda wakati ujao wa kiangazi. Mwishowe, baada ya kumaliza kupunguza matawi, mkulima huyateketeza.

Yesu anafafanua kupunguzwa huko hivi: “Ikiwa yeyote hakai katika muungano pamoja nami, huyo hutupwa nje kama tawi na hukauka; na watu hukusanya matawi hayo na kuyatupa ndani ya moto nayo yanateketezwa.” (Yohana 15:6) Ingawa wakati huo huenda mzabibu ukaonekana kuwa hauna matawi, matawi fulani hupunguzwa tena wakati wa majira ya kuchipua.

Yesu alisema: “Kila tawi ndani yangu lisilozaa matunda yeye huliondolea mbali.” (Yohana 15:2) Huenda hilo likamaanisha kupunguzwa kunakofanywa baadaye, baada ya mzabibu kutokeza matawi mapya ya kutosha na vishada vidogo vya zabibu kuonekana wazi. Mkulima huyachunguza kwa makini matawi mapya ili kutofautisha kati ya yale yanayozaa na yale yasiyozaa matunda. Matawi yasiyozaa matunda yakiachwa kwenye mzabibu, bado yatapata lishe na maji kutoka kwenye shina. Hivyo, mkulima huyaondoa matawi hayo ili yale tu yanayozaa yapate lishe.

Mwishowe, Yesu anazungumzia hatua ya kusafisha. Anaeleza hivi: “Kila tawi linalozaa matunda yeye hulisafisha, lipate kuzaa matunda zaidi.” (Yohana 15:2) Mara tu matawi yasiyozaa yanapoondolewa, mkulima huchunguza kwa makini kila tawi linalozaa matunda. Mara nyingi yeye hupata machipukizi madogo upande wa chini wa tawi linalozaa matunda. Machipukizi hayo pia huhitaji kuondolewa. Yakiachwa yakue, yatafyonza utomvu wa mzabibu ambao ungetokeza maji muhimu kwa ajili ya zabibu. Pia, majani makubwa yanaweza kutolewa ili kuwezesha zabibu changa kupata mwangaza wa jua. Hizo ni hatua muhimu ili kuwezesha matawi yanayozaa kutokeza matunda kwa wingi.

‘Endeleeni Kuzaa Matunda Mengi’

Matawi ya mfano ya “mzabibu wa kweli” yanawakilisha Wakristo watiwa-mafuta. Lakini, ni lazima “kondoo wengine” pia wathibitishe kwamba wao ni wafuasi wa Kristo wanaozaa matunda. (Yohana 10:16) Wao pia wanaweza kuzaa “matunda mengi” na kumpa utukufu Baba yao wa mbinguni. (Yohana 15:5, 8) Mfano wa Yesu wa mzabibu wa kweli hutukumbusha kwamba wokovu unategemea kubaki katika muungano pamoja na Kristo na kuzaa matunda mazuri ya kiroho. Yesu alisema: “Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile mimi nilivyoshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.”—Yohana 15:10.

Katika siku za Zekaria, Mungu aliahidi mabaki waaminifu wa Israeli kwamba nchi itakuwa tena na ‘mbegu ya amani; mzabibu utazaa matunda yake, na dunia itatoa mazao yake.’ (Zekaria 8:12) Mzabibu unatumiwa pia kuonyesha amani ambayo watu wa Mungu watafurahia wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu. Mika alitabiri hivi: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha; kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hivyo.”—Mika 4:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kulingana na kitabu kimoja (Encyclopaedia Judaica), wakulima Waisraeli walipendelea mizabibu iliyozaa zabibu za zambarau zinazojulikana kama sorek. Yaelekea aina hiyo ya mizabibu ndiyo inayozungumziwa katika Isaya 5:2. Zabibu hizo zilitokeza divai tamu nyekundu.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mzabibu ulionyauka karibuni

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kupunguza matawi katika majira ya baridi kali

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuteketeza matawi yasiyofaa