Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitihada za Kutafuta Ujuzi

Jitihada za Kutafuta Ujuzi

Jitihada za Kutafuta Ujuzi

“KUWA na ujuzi ni bora kuliko kutokuwa nao,” akasema Laura Fermi, mke wa mwanafizikia mashuhuri, Enrico Fermi. Huenda wengine wakapinga maoni hayo kwa kusema kwamba mambo usiyoyajua hayawezi kukudhuru. Hata hivyo, watu wengi wanaamini kwamba maneno hayo ni ya kweli katika utafiti wa kisayansi na katika hali nyingine za maisha. Kwa karne nyingi kutojua ukweli kumewafanya watu wengi wawe katika giza kiakili, kiadili, na kiroho.—Waefeso 4:18.

Hiyo ndiyo sababu watu wenye akili hutafuta ujuzi. Wanataka kujua kusudi la maisha na hali ya wakati ujao. Wamejaribu njia mbalimbali katika jitihada zao za kutafuta ujuzi. Acheni tuone kwa ufupi baadhi ya njia hizo.

Kutafuta Ujuzi Katika Dini

Kulingana na mapokeo ya dini ya Budha, mwanzilishi wa dini hiyo, Siddhārtha Gautama, alisikitishwa sana kwamba wanadamu wanateseka na kufa. Aliwaomba walimu wa dini ya Kihindu wamsaidie kupata “njia ya kweli.” Baadhi yao walipendekeza zoea la yoga na kujinyima kupita kiasi. Hatimaye, Gautama aliona kuwa njia ya kupata ujuzi wa kweli ni kutafakari kwa undani.

Wengine wametumia dawa za kulevya katika jitihada zao za kutafuta ujuzi. Kwa mfano, leo washiriki wa kanisa la Wahindi wa Marekani wanasema kwamba mmea mmoja unaopumbaza akili “hufunua ujuzi uliofichwa.”

Mwanafalsafa Mfaransa wa karne ya 18, Jean-Jacques Rousseau aliamini kwamba mtu yeyote anayeomba kwa unyoofu anaweza kupata ufunuo wa kiroho kutoka kwa Mungu. Kwa njia gani? Kwa kusikiliza “yale ambayo Mungu anauambia moyo.” Kisha, kulingana na Rousseau, jinsi unavyohisi kuhusu mambo, yaani, hisia zako na dhamiri yako, zitakuwa “mwongozo hakika unapokabiliana na maoni mengi ya wanadamu yenye kutatanisha.”—History of Western Philosophy.

Kutafuta Ujuzi kwa Kufikiri

Watu wengi walioishi wakati wa Rousseau walipinga vikali njia hiyo ya kidini. Kwa mfano, Mfaransa mwenzake, Voltaire, aliona kwamba dini haikuwaelimisha watu bali ilikuwa kisababishi kikuu kilichofanya Ulaya iwe katika hali ya kutojua, ushirikina, na ubaguzi kwa karne nyingi wakati wa kile kipindi ambacho wanahistoria wanakiita Enzi za Giza.

Voltaire aliungana na harakati za Ulaya za kutafuta ujuzi kwa kutumia akili. Wanaharakati hao waliunga mkono maoni ya Wagiriki wa kale ya kwamba ujuzi wa kweli unatokana na kufikiri na uchunguzi wa kisayansi. Mshiriki mwingine wa harakati hiyo, Bernard de Fontenelle, alihisi kwamba kufikiri kwa wanadamu peke yake kutawaongoza katika “karne yenye ujuzi mwingi hivi kwamba karne zote zilizopita zitaonwa kuwa hazikuwa na ujuzi.”—Encyclopædia Britannica.

Hayo ni baadhi tu ya maoni yenye kupingana kuhusu jinsi ya kupata ujuzi. Je, kweli kuna “mwongozo hakika” unaoweza kutusaidia kupata kweli? Hebu ona yale ambayo makala inayofuata inasema kuhusu chanzo chenye kutegemeka cha ujuzi.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Gautama (Budha), Rousseau, na Voltaire walitafuta ujuzi kwa njia mbalimbali