Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana, Chagueni Kumtumikia Yehova

Vijana, Chagueni Kumtumikia Yehova

Vijana, Chagueni Kumtumikia Yehova

“Jichagulieni leo yule mtakayemtumikia.”—YOSHUA 24:15.

1, 2. Ni ubatizo gani usiofaa ambao umefanywa na dini zinazodai kuwa za Kikristo?

“ACHENI [watoto] wawe Wakristo wanapokuwa na uwezo wa kumjua Kristo.” Maneno hayo yaliandikwa karibu na mwisho wa karne ya pili W.K. na mwandikaji anayeitwa Tertullian. Alikuwa akipinga zoea la kuwabatiza watoto ambalo lilikuwa linaanza kutia mizizi katika Ukristo wa uwongo wa siku zake. Baba wa Kanisa, Augustine, ambaye hakukubaliana na Tertullian na Biblia, alidai kwamba ubatizo unaondoa dhambi ya asili na kwamba watoto wanaokufa bila kubatizwa wanahukumiwa moto wa mateso. Imani hiyo iliendeleza zoea la kuwabatiza watoto wachanga haraka iwezekanavyo baada ya kuzaliwa.

2 Dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo ambazo hufuatwa na watu wengi bado huwabatiza watoto wachanga. Isitoshe, historia inaonyesha kwamba watawala na viongozi wa kidini wa mataifa yanayodai kuwa ya Kikristo waliwalazimisha “wapagani” kubatizwa baada ya kuwashinda vitani. Hata hivyo, ubatizo wa watoto na ubatizo wa kuwalazimisha watu wazima haupatani na Biblia.

Leo, Tunajiweka Wakfu kwa Hiari

3, 4. Ni nini kinachoweza kuwasaidia watoto ambao wazazi wao wamejiweka wakfu, wajiweke wakfu kwa hiari?

3 Biblia inaonyesha kwamba Mungu huwaona watoto wadogo kuwa watakatifu hata ikiwa mzazi mmoja tu ndiye Mkristo mwaminifu. (1 Wakorintho 7:14) Je, hilo hufanya watoto hao wawe watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu? Hapana. Hata hivyo, watoto wanaolelewa na wazazi ambao wamejiweka wakfu kwa Yehova hupewa mazoezi ambayo yanaweza kuwasaidia wajiweke wakfu kwa Yehova kwa hiari. Mfalme mwenye hekima Sulemani aliandika hivi: “Ee mwanangu, shika amri ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako. . . . Unapotembea huku na huku, itakuongoza; unapolala, itakulinda; na unapokuwa umeamka, hiyo yenyewe itakuhangaikia. Kwa maana amri hiyo ni taa, na sheria ni nuru, nayo makaripio ya nidhamu ndiyo njia ya uzima.”—Methali 6:20-23.

4 Mwongozo wa wazazi Wakristo unaweza kuwa ulinzi kwa watoto, maadamu wanakubali kuufuata. Sulemani alisema hivi pia: “Mwana mwenye hekima ndiye anayemfanya baba ashangilie, naye mwana mjinga ni huzuni ya mama yake.” “Ewe mwanangu, sikia uwe na hekima, na kuuongoza moyo wako katika njia hiyo.” (Methali 10:1; 23:19) Naam, enyi vijana, ili mfaidike na mazoezi yanayotolewa na wazazi wenu, mnapaswa kuwa tayari kukubali mashauri na nidhamu. Hamzaliwi mkiwa na hekima, lakini mnaweza ‘kuwa na hekima’ na hivyo kufuata kwa hiari “njia ya uzima.”

Mwongozo wa Akilini Unamaanisha Nini?

5. Ni shauri gani ambalo Paulo aliwapa watoto na akina baba?

5 Mtume Paulo aliandika hivi: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hilo ni jambo la uadilifu: ‘Mheshimu baba yako na mama yako’; ambayo ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi: ‘Ili mambo yakuendee vema nawe ukae muda mrefu duniani.’ Nanyi, akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:1-4.

6, 7. Kuwalea watoto katika “mwongozo wa akilini wa Yehova” kunatia ndani nini, na kwa nini kufanya hivyo hakumaanishi kwamba wazazi wanawapotosha watoto wao?

6 Je, wazazi Wakristo wanawapotosha watoto wao wanapowalea katika “nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova”? Hapana. Ni nani anayeweza kuwashutumu wazazi wanaowafundisha watoto wao mambo ambayo wanaona kuwa sawa na yenye manufaa kiadili? Watu wasioamini kwamba kuna Mungu hawashutumiwi wanapowafundisha watoto wao kwamba hakuna Mungu. Wakatoliki wanahisi kwamba wana wajibu wa kuwalea watoto wao kulingana na Ukatoliki, na hawashutumiwi wanapojitahidi kufanya hivyo. Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova hawapaswi kulaumiwa kwamba wanaongoza vibaya akili za watoto wao wanapowalea kulingana na maoni ya Yehova yanayotegemea kweli za msingi na kanuni za adili.

7 Kulingana na kitabu kimoja (Theological Dictionary of the New Testament), neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “mwongozo wa akilini” kwenye Waefeso 6:4 linarejelea jitihada za “kurekebisha akili, kusahihisha kosa, na kuboresha mtazamo wa kiroho.” Namna gani ikiwa kijana anakataa kufundishwa na wazazi kwa sababu ya uvutano wa marika, yaani, kutamani kuwa kama vijana wenzake? Ni nani anayeweza kulaumiwa kwamba anamwathiri kijana huyo, je, ni wazazi wake au vijana wenzake? Ikiwa vijana wenzake ndio wanaomshawishi kutumia dawa za kulevya, kunywa kileo kupindukia, au kujihusisha katika ukosefu wa adili, je, wazazi wanapaswa kulaumiwa wanapojitahidi kurekebisha maoni ya mtoto wao na kumsaidia kutambua matokeo mabaya ya mwenendo huo hatari?

8. ‘Kumshawishi Timotheo kuamini’ kulihusisha nini?

8 Mtume Paulo alimwandikia hivi kijana Timotheo: “Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini, ukijua ni kutoka kwa watu gani ulijifunza hayo na kwamba tangu utoto mchanga umeyajua maandishi matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (2 Timotheo 3:14, 15) Tangu Timotheo alipokuwa mtoto mchanga, mama yake na nyanya yake walimwekea msingi imara wa kumwamini Mungu kupitia ujuzi wa Maandiko Matakatifu. (Matendo 16:1; 2 Timotheo 1:5) Baadaye, walipokuwa Wakristo, hawakumlazimisha Timotheo kuwa mwamini, bali ‘walimshawishi’ kwa kumsaidia kufikiri kwa kutumia ujuzi wa Maandiko.

Yehova Anakualika Uchague

9. (a) Yehova aliwaonyeshaje heshima viumbe wake, na kwa sababu gani? (b) Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alitumiaje uhuru wake wa kuchagua?

9 Yehova angeweza kutuumba kama mashini, tukiwa tumepangiwa kimbele kufanya mapenzi yake, na bila uwezo wa kufanya maamuzi tofauti. Lakini, alituonyesha heshima kwa kutupa uhuru wa kuchagua. Mungu wetu anataka tujitiishe kwake kwa hiari. Anafurahi anapoona viumbe wake, wazee kwa vijana, wakimtumikia kwa sababu wanampenda. Yehova alisema hivi kuhusu Mwana wake mzaliwa-pekee ambaye ndiye kielelezo bora zaidi cha kujitiisha kwa hiari kufanya mapenzi ya Mungu: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Mwana huyo mzaliwa wa kwanza alimwambia Baba yake hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.”—Zaburi 40:8; Waebrania 10:9, 10.

10. Ili tumtumikie Yehova kwa njia inayokubalika, tunahitaji kufanya nini?

10 Yehova anatarajia wale wanaomtumikia chini ya uongozi wa Mwana wake wawe tayari kujitiisha kufanya mapenzi Yake kama Yesu alivyofanya. Akiwa anatoa unabii, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Watu wako watajitoa kwa hiari katika siku ya jeshi lako. Katika fahari za utakatifu, kutoka tumbo la uzazi la mapambazuko, una kundi lako la vijana kama matone ya umande.” (Zaburi 110:3) Tengenezo zima la Yehova, iwe ni sehemu ya mbinguni au ya duniani, linafanya kazi kwa kujitiisha kwa upendo kufanya mapenzi ya Mungu.

11. Ni uchaguzi gani ambao umewekwa mbele ya vijana wanaolelewa na wazazi waliojiweka wakfu?

11 Hivyo, enyi vijana, ni vizuri muelewe kwamba hakuna atakayewalazimisha kubatizwa iwe ni wazazi wenu au wazee Wakristo katika kutaniko lenu. Ninyi wenyewe ndio mnaopaswa kujiamulia kumtumikia Yehova. Yoshua aliwaambia Waisraeli hivi: ‘Mtumikieni Yehova kwa njia isiyo na kosa na katika kweli. Jichagulieni leo yule mtakayemtumikia.’ (Yoshua 24:14-22) Vivyo hivyo, mnapaswa kuchagua kwa hiari kujiweka wakfu kwa Yehova na kujitoa ili kufanya mapenzi yake.

Kukubali Daraka Lako

12. (a) Ingawa wazazi wanaweza kuwazoeza watoto wao, ni jambo gani ambalo hawawezi kuwafanyia? (b) Ni wakati gani ambapo kijana anakuwa na daraka mbele za Yehova kuhusiana na maamuzi anayofanya?

12 Kuna wakati ambapo vijana hawalindwi tena na uaminifu wa wazazi wao. (1 Wakorintho 7:14) Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa mtu anajua jinsi ya kufanya yaliyo sawa na bado hayafanyi, hiyo ni dhambi kwake.” (Yakobo 4:17) Wazazi hawawezi kumtumikia Mungu kwa ajili ya watoto wao wala watoto hawawezi kumtumikia Mungu kwa ajili ya wazazi wao. (Ezekieli 18:20) Je, umejifunza kumhusu Yehova na makusudi yake? Je, una umri wa kutosha kuelewa mambo ambayo umejifunza na kuwa na uhusiano pamoja naye? Ikiwa ndivyo, je, si jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba Mungu anaona kuwa unaweza kuamua kumtumikia?

13. Ni maswali gani ambayo vijana ambao hawajabatizwa wanapaswa kujiuliza?

13 Je, wewe ni kijana ambaye hajabatizwa mwenye wazazi wanaomwabudu Mungu, na unahudhuria mikutano ya Kikristo, na hata kushiriki kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme? Ikiwa ndivyo, jiulize hivi kwa unyoofu: ‘Kwa nini ninafanya mambo yote hayo? Je, ninahudhuria mikutano na kushiriki katika kazi ya kuhubiri kwa sababu wazazi wangu wanatarajia nifanye hivyo au kwa sababu ninataka kumpendeza Yehova?’ Je, umejihakikishia mwenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu”?—Waroma 12:2.

Kwa Nini Unaahirisha Kubatizwa?

14. Ni mifano gani katika Biblia inayoonyesha kwamba hatupaswi kuahirisha kubatizwa bila sababu?

14 “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Mwethiopia aliyemuuliza mhubiri Filipo swali hilo alikuwa ametoka kufundishwa kwamba Yesu ndiye Masihi. Lakini, Mwethiopia huyo alikuwa na ujuzi wa kutosha wa Maandiko hivi kwamba alitambua kuwa hakupaswa kukawia kutangaza kwamba kuanzia wakati huo na kuendelea angemtumikia Yehova akiwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo, na hilo lilimfanya ashangilie sana. (Matendo 8:26-39) Vivyo hivyo, mwanamke mmoja aliyeitwa Lidia ambaye Mungu alifungua wazi moyo wake ili “asikilize kwa makini mambo yaliyokuwa yakisemwa na Paulo,” ‘alibatizwa’ mara moja yeye na watu wa nyumba yake. (Matendo 16:14, 15) Pia, mlinzi wa jela huko Filipi aliwasikiliza Paulo na Sila ‘walipomwambia neno la Yehova,’ na “yeye na walio wake wakabatizwa bila kukawia.” (Matendo 16:25-34) Hivyo, ikiwa una ujuzi wa msingi kumhusu Yehova na makusudi yake, unatamani kwa unyoofu kufanya mapenzi yake, una sifa nzuri kutanikoni, unahudhuria mikutano kwa ukawaida, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme, kwa nini unaahirisha kubatizwa?—Mathayo 28:19, 20.

15, 16. (a) Ni maoni gani yasiyofaa ambayo huenda yakawazuia vijana fulani wasibatizwe? (b) Kujiweka wakfu na kubatizwa kunawezaje kuwa ulinzi kwa vijana?

15 Je, inawezekana kwamba unasitasita kuchukua hatua hiyo muhimu kwa sababu unaogopa kuadhibiwa ikiwa utatenda jambo lisilofaa? Ikiwa ndivyo, fikiria jambo hili: Je, ungekataa kujifunza kuendesha gari eti kwa sababu tu unaogopa kwamba siku moja utasababisha msiba barabarani? Hapana! Vivyo hivyo, hupaswi kusita kubatizwa ikiwa unastahili. Kwa kweli, ukijiweka wakfu kwa Yehova na kukubali kufanya mapenzi yake, utachochewa sana kufanya yote uwezayo kukataa kutenda mambo maovu. (Wafilipi 4:13) Enyi vijana, tafadhali sikilizeni, msifikiri kwamba mkiahirisha kubatizwa mtaepuka kutozwa hesabu. Mnapokuwa na umri wa kutosha, mtatozwa hesabu na Yehova kuhusu jinsi mnavyotenda iwe mmebatizwa au la.—Waroma 14:11, 12.

16 Mashahidi wengi ulimwenguni pote wanahisi kwamba uamuzi wao wa kubatizwa walipokuwa vijana uliwasaidia sana. Fikiria mfano wa Shahidi mmoja mwenye umri wa miaka 23 huko Ulaya Magharibi. Anakumbuka kwamba kubatizwa akiwa na umri wa miaka 13 kulimchochea awe macho ili asishindwe na “tamaa zinazotukia ujanani.” (2 Timotheo 2:22) Akiwa bado kijana, alifanya uamuzi wa kuwa mhudumu wa wakati wote. Leo, anafurahi kutumikia kwenye ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Vijana wote ambao wameamua kumtumikia Yehova, kutia ndani wewe, wanatarajia kupokea baraka nyingi.

17. Ni muhimu tuendelee kufahamu “mapenzi ya Yehova” katika mambo gani?

17 Tunapojiweka wakfu na kubatizwa tunaanza kuishi tukitilia maanani mapenzi ya Yehova katika mambo yote tunayofanya. Kutimiza wakfu wetu kunatia ndani ‘kujinunulia wakati.’ Tunafanyaje hivyo? Tunafanya hivyo kwa kununua wakati ambao huenda tungeutumia kufuatia mambo yasiyo na maana na badala yake tunautumia kujifunza Biblia kwa makini, kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, na kushiriki kadiri iwezekanavyo katika kazi ya kuhubiri “habari njema ya ufalme.” (Waefeso 5:15, 16; Mathayo 24:14) Wakfu wetu kwa Yehova na tamaa yetu ya kufanya mapenzi yake itatuongoza katika sehemu zote za maisha yetu, kutia ndani jinsi tunavyojiburudisha, jinsi tunavyokula na kunywa, na aina ya muziki tunaosikiliza. Kwa nini usichague aina ya burudani ambayo utaweza kufurahia milele? Maelfu ya vijana Mashahidi wenye furaha watakueleza kwamba kuna njia nyingi nzuri za kujiburudisha bila kupita mipaka ya “mapenzi ya Yehova.” —Waefeso 5:17-19.

“Tutakwenda Pamoja Nanyi”

18. Ni swali gani ambalo vijana wanapaswa kujiuliza?

18 Tangu mwaka wa 1513 K.W.K. hadi Pentekoste 33 W.K., Yehova alikuwa na watu duniani waliopangwa kitengenezo ambao alichagua wamwabudu na kuwa mashahidi wake. (Isaya 43:12) Watoto Waisraeli walizaliwa katika taifa hilo. Tangu Pentekoste, Yehova amekuwa na “taifa” jipya duniani, Israeli wa kiroho, “watu kwa ajili ya jina lake.” (1 Petro 2:9, 10; Matendo 15:14; Wagalatia 6:16) Mtume Paulo anasema kwamba Kristo amejisafishia mwenyewe “watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.” (Tito 2:14) Ninyi vijana mna uhuru wa kutafuta mahali ambapo watu hao wanapatikana. Leo, ni nani ambao wanafanyiza “taifa la uadilifu linaloshika mwenendo wa uaminifu,” wanaoishi kulingana na kanuni za Biblia, wanaotenda wakiwa Mashahidi waaminifu wa Yehova, na kutangaza Ufalme wake kuwa tumaini pekee la wanadamu? (Isaya 26:2-4) Chunguza dini zinazodai kuwa za Kikristo na dini nyingine, na ulinganishe mwenendo wa washiriki wa dini hizo na yale ambayo Biblia hutaka watumishi wa kweli wa Mungu wafanye.

19. Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wamesadiki jambo gani?

19 Mamilioni ya watu ulimwenguni pote, kutia ndani vijana wengi, wamesadiki kwamba mabaki ya Mashahidi wa Yehova watiwa-mafuta wanafanyiza ‘taifa hilo la uadilifu.’ Watu hao wanawaambia hivi Waisraeli hao wa kiroho: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.” (Zekaria 8:23) Tunatumaini na kusali kwamba ninyi vijana mtaamua kuwa miongoni mwa watu wa Mungu na hivyo ‘kuchagua uzima,’ yaani, uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Yehova.—Kumbukumbu la Torati 30:15-20; 2 Petro 3:11-13.

Kwa Kupitia

• Mwongozo wa akilini unatia ndani nini?

• Ni utumishi wa aina gani unaokubaliwa na Yehova?

• Vijana wote wanaolelewa na wazazi waliojiweka wakfu wanapaswa kufanya uchaguzi gani?

• Kwa nini hatupaswi kuahirisha ubatizo bila sababu nzuri?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Utamsikiliza nani?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kujiweka wakfu na kubatizwa kunaweza kukulindaje?

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ni nini kinachokuzuia usibatizwe?