Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walizaliwa Katika Taifa Teule la Mungu

Walizaliwa Katika Taifa Teule la Mungu

Walizaliwa Katika Taifa Teule la Mungu

“Ni ninyi ambao Yehova Mungu amewachagua ninyi muwe watu wake.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 7:6.

1, 2. Yehova aliwafanyia watu wake mambo gani makuu, na Waisraeli waliingia katika uhusiano gani pamoja na Mungu?

KATIKA mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova alianzisha uhusiano mpya pamoja na watumishi wake duniani. Mwaka huo, aliinyenyekeza serikali kuu ya ulimwengu na kuwakomboa Waisraeli kutoka utumwani. Kwa kufanya hivyo, akawa Mwokozi na Mmiliki wao. Kabla ya kuchukua hatua, Mungu alimwambia Musa hivi: “Waambie wana wa Israeli, ‘Mimi ni Yehova, nami hakika nitawatoa chini ya mizigo ya Wamisri na kuwakomboa kutoka katika utumwa wao, nami kwa kweli nitawaokoa ninyi kwa mkono ulionyooshwa na kwa hukumu kubwa. Nami hakika nitawachukua kwangu muwe watu wangu, nami kwa kweli nitakuwa Mungu kwenu.’”—Kutoka 6:6, 7; 15:1-7, 11.

2 Muda mfupi baada ya kuondoka Misri, Waisraeli waliingia katika uhusiano wa agano pamoja na Mungu wao, Yehova. Badala ya kushughulika na mtu mmoja-mmoja, familia, au vikundi vya makabila, kuanzia wakati huo na kuendelea Yehova angekuwa na watu au taifa lililopangwa kitengenezo duniani. (Kutoka 19:5, 6; 24:7) Aliwapa watu wake sheria ambazo ziliongoza maisha yao ya kila siku, na hasa ibada yao. Musa aliwaambia hivi: “Ni taifa gani kubwa ambalo lina miungu iliyo karibu nalo kama Yehova Mungu wetu alivyo tunapomwitia nyakati zote? Na kuna taifa gani kubwa lenye masharti na maamuzi ya hukumu ya uadilifu kama sheria yote hii ninayoweka mbele yenu leo?”—Kumbukumbu la Torati 4:7, 8.

Kuzaliwa Katika Taifa la Mashahidi

3, 4. Ni nini iliyokuwa sababu muhimu ya kuwapo kwa taifa la Israeli?

3 Karne nyingi baadaye, Yehova aliwakumbusha Waisraeli, kupitia nabii wake Isaya kuhusu sababu muhimu ya kuwapo kwa taifa lao. Isaya alisema hivi: “Yehova, Muumba wako, Ee Yakobo, na Mfanyizaji wako, Ee Israeli, amesema hivi: ‘Usiogope, kwa maana nimekukomboa. Nimekuita kwa jina lako. Wewe ni wangu. Kwa maana mimi ni Yehova Mungu wako, Mtakatifu wa Israeli Mwokozi wako. . . . Walete wanangu kutoka mbali, na binti zangu kutoka mwisho wa dunia, kila mtu ambaye anaitwa kwa jina langu na ambaye nimemuumba kwa ajili ya utukufu wangu, ambaye nimemfanya, ndiyo, ambaye nimemfanyiza. Ninyi ni mashahidi wangu,’ asema Yehova, ‘mtumishi wangu ambaye nimemchagua, . . . watu ambao nimejifanyia, ili wasimulie sifa zangu.’”—Isaya 43:1, 3, 6, 7, 10, 21.

4 Wakiwa watu walioitwa kwa jina la Yehova, Waisraeli wangetumikia wakiwa mashahidi wa enzi yake kuu kwa mataifa mengine. Walipaswa kuwa watu ‘walioumbwa kwa ajili ya utukufu wa Yehova.’ Walipaswa ‘kusimulia sifa za Yehova,’ kueleza matendo yake ya ajabu ya ukombozi na hivyo kulitukuza jina lake takatifu. Kwa ufupi, walipaswa kuwa taifa la mashahidi wa Yehova.

5. Ni katika njia gani Waisraeli walikuwa taifa lililojiweka wakfu?

5 Katika karne ya 11 K.W.K., Mfalme Sulemani alionyesha kwamba Yehova alifanya Israeli kuwa taifa lililotengwa. Alisema hivi katika sala kwa Yehova: “Wewe mwenyewe uliwatenga wawe urithi wako kutoka katika vikundi vyote vya watu wa dunia.” (1 Wafalme 8:53) Pia, Waisraeli wakiwa mtu mmoja-mmoja walikuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Yehova. Mapema, Musa aliwaambia hivi: “Ninyi ni wana wa Yehova Mungu wenu. . . . Kwa maana ninyi ni watu watakatifu kwa Yehova Mungu wenu.” (Kumbukumbu la Torati 14:1, 2) Hivyo, vijana Waisraeli hawakuhitaji kujiweka wakfu kwa Yehova. Walizaliwa wakiwa washiriki wa taifa la Mungu lililojiweka wakfu. (Zaburi 79:13; 95:7) Kila kizazi kipya kilifundishwa sheria za Yehova, nacho kilikuwa na wajibu wa kuzishika kwa sababu ya agano lililowapatanisha Waisraeli na Yehova.—Kumbukumbu la Torati 11:18, 19.

Walikuwa na Uhuru wa Kuchagua

6. Ni uchaguzi gani ambao kila Mwisraeli alipaswa kufanya?

6 Ingawa Waisraeli walizaliwa katika taifa lililojiweka wakfu, kila Mwisraeli alipaswa kufanya uamuzi wa kibinafsi wa kumtumikia Mungu. Kabla ya kuingia Nchi ya Ahadi, Musa aliwaambia hivi: “Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye; kwa maana yeye ni uhai wako na urefu wa siku zako, ili ukae katika nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zako Abrahamu, Isaka na Yakobo kwamba atawapa wao.” (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Hivyo, Waisraeli wakiwa mtu mmoja-mmoja walipaswa kuchagua kumpenda Yehova, kuisikiliza sauti yake, na kushikamana naye. Kwa kuwa Waisraeli walikuwa na uhuru wa kuchagua, walipaswa kukubali matokeo ya uchaguzi wao.—Kumbukumbu la Torati 30:16-18.

7. Ni nini kilichotukia baada ya watu wa kizazi cha Yoshua kufa?

7 Kipindi cha Waamuzi kilionyesha wazi matokeo ya kuwa mwaminifu na ya kutokuwa mwaminifu. Kabla tu ya kipindi hicho kuanza, Waisraeli walifuata kielelezo kizuri cha Yoshua, nao wakabarikiwa. “Watu wakaendelea kumtumikia Yehova siku zote za Yoshua na siku zote za wale wanaume wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua na ambao walikuwa wameona kazi yote kubwa ya Yehova ambayo aliwafanyia Israeli.” Hata hivyo, muda mfupi baada ya kifo cha Yoshua, “kizazi kingine kikaanza kutokea baada yao ambacho hakikumjua Yehova wala ile kazi ambayo alikuwa amewafanyia Israeli. Na wana wa Israeli wakaanza kufanya yaliyo mabaya machoni pa Yehova.” (Waamuzi 2:7, 10, 11) Yaelekea Waisraeli wasio na uzoefu wa kizazi hicho kipya hawakuthamini urithi wao wakiwa washiriki wa taifa lililojiweka wakfu kwa Mungu wao, Yehova, ambaye aliwafanyia matendo yenye nguvu zamani.—Zaburi 78:3-7, 10, 11.

Kuishi Kulingana na Wakfu Wao

8, 9. (a) Ni mpango gani uliowawezesha Waisraeli kuonyesha kwamba walikuwa wamejiweka wakfu kwa Yehova? (b) Wale waliotoa matoleo ya hiari walipata faida gani?

8 Yehova aliwapa watu wake nafasi ya kuishi kulingana na wakfu wao wakiwa taifa. Kwa mfano, Sheria yake ilikuwa na mfumo wa kutoa dhabihu, au matoleo, na baadhi ya matoleo hayo yalikuwa ya lazima, na mengine yalikuwa ya hiari. (Waebrania 8:3) Dhabihu hizo zilitia ndani matoleo ya kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na matoleo ya ushirika ambayo yalitolewa kwa hiari. Hizo zilikuwa zawadi zilizotolewa kwa Yehova ili kumshukuru na kupata kibali chake.—Mambo ya Walawi 7:11-13.

9 Dhabihu hizo za hiari zilimfurahisha Yehova. Matoleo ya kuteketezwa na matoleo ya nafaka yalionwa kuwa “harufu ya kumtuliza Yehova.” (Mambo ya Walawi 1:9; 2:2) Katika dhabihu ya ushirika, damu na mafuta ya mnyama vilitolewa kwa Yehova, lakini sehemu fulani za nyama zililiwa na makuhani na yule aliyetoa dhabihu hiyo. Hivyo, huo ulikuwa mlo wa mfano ulioonyesha uhusiano wenye amani pamoja na Yehova. Sheria ilisema hivi: “Sasa ikiwa mtamtolea Yehova dhabihu ya ushirika, mtaitoa ili mjipatie kibali.” (Mambo ya Walawi 19:5) Ingawa Waisraeli wote walikuwa wakfu kwa Yehova kupitia kuzaliwa, wale waliotamani kumchagua Yehova kuwa Mungu wao kwa kutoa matoleo ya hiari ‘walijipatia kibali’ nao walibarikiwa sana.—Malaki 3:10.

10. Katika siku za Isaya na za Malaki Yehova alionyeshaje kwamba alichukizwa?

10 Hata hivyo, mara kwa mara, taifa la Israeli lililojiweka wakfu lilikosa uaminifu kwa Yehova. Kupitia nabii wake Isaya, Yehova aliwaambia hivi: “Hukuniletea kondoo wa matoleo yako mazima ya kuteketezwa, wala hukunitukuza kwa dhabihu zako. Mimi sikukulazimisha unitumikie na zawadi.” (Isaya 43:23) Isitoshe, matoleo ambayo hayakutolewa kwa hiari na kwa upendo hayakuwa na thamani machoni pa Yehova. Kwa mfano, miaka 300 hivi baada ya siku za Isaya, katika siku za nabii Malaki, Waisraeli walikuwa wakitoa wanyama wenye kasoro. Hivyo, Malaki aliwaambia hivi: “‘Sipendezwi nanyi hata kidogo,’ Yehova wa majeshi amesema, ‘nami sifurahii toleo la zawadi kutoka mkononi mwenu.’ . . . ‘Nanyi mmeleta kitu ambacho kimenyakuliwa, na chenye kilema, na kilicho kigonjwa; ndiyo, mmekileta kama zawadi. Je, naweza kukifurahia mkononi mwenu?’ Yehova amesema.”—Malaki 1:10, 13; Amosi 5:22.

Taifa Lililojiweka Wakfu Lakataliwa

11. Waisraeli walipewa nafasi gani?

11 Yehova aliwaahidi Waisraeli hivi walipokuwa taifa lililojiweka wakfu kwake: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mtakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, kwa sababu dunia nzima ni yangu. Na ninyi wenyewe mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.” (Kutoka 19:5, 6) Masihi aliyeahidiwa angetokea miongoni mwao, naye angewapa nafasi ya kwanza ya kuwa washiriki wa Ufalme wa Mungu. (Mwanzo 22:17, 18; 49:10; 2 Samweli 7:12, 16; Luka 1:31-33; Waroma 9:4, 5) Lakini Waisraeli wengi hawakuishi kulingana na wakfu wao. (Mathayo 22:14) Walimkataa Masihi na hatimaye wakamuua.—Matendo 7:51-53.

12. Yesu alisema maneno gani yanayoonyesha kwamba Waisraeli walikataliwa na Yehova wakiwa taifa lililojiweka wakfu?

12 Siku chache kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia hivi viongozi wa dini ya Kiyahudi: “Je, hamkusoma kamwe katika Maandiko, ‘Jiwe ambalo wajenzi walilikataa ndilo limekuwa jiwe kuu la pembeni. Limetokana na Yehova, nalo ni la kustaajabisha machoni petu’? Ndiyo sababu ninawaambia ninyi, Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mathayo 21:42, 43) Ili kuonyesha kwamba Yehova alikuwa amewakataa wakiwa taifa lililojiweka wakfu Kwake, Yesu alisema hivi: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na ambaye huwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara ngapi nilitaka kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga vyake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka. Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”— Mathayo 23:37, 38.

Taifa Jipya Lililojiweka Wakfu

13. Ni maneno gani ya kinabii ambayo Yehova alisema katika siku za Yeremia?

13 Wakati wa nabii Yeremia, Yehova alitabiri jambo fulani jipya kuhusiana na watu wake. Tunasoma hivi: “‘Tazama! Siku zinakuja,’ asema Yehova, ‘nami nitafanya agano jipya pamoja na nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda; si kama lile agano ambalo nilifanya pamoja na mababu zao katika ile siku nilipowashika mkono na kuwatoa katika nchi ya Misri, “agano langu ambalo wao walilivunja, ingawa mimi mwenyewe nilikuwa mume kwao,” asema Yehova.’ ‘Kwa maana hili ndilo agano nitakalofanya pamoja na nyumba ya Israeli baada ya siku hizo,’ asema Yehova. ‘Nitaitia sheria yangu ndani yao, nami nitaiandika katika moyo wao. Nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.’”—Yeremia 31:31-33.

14. Ni wakati gani na kwa msingi gani taifa jipya la Yehova lililojiweka wakfu lilitokezwa? Eleza ni nani wanaofanyiza taifa hilo jipya.

14 Msingi wa agano hilo jipya uliwekwa wakati Yesu alipokufa na baadaye kumtolea Baba yake thamani ya damu yake iliyomwagwa, mwaka wa 33 W.K. (Luka 22:20; Waebrania 9:15, 24-26) Hata hivyo, agano jipya lilianzishwa wakati roho takatifu ilipomwagwa siku ya Pentekoste 33 W.K., na taifa jipya la “Israeli wa Mungu” likazaliwa. (Wagalatia 6:16; Waroma 2:28, 29; 9:6; 11:25, 26) Akiwaandikia Wakristo watiwa-mafuta, mtume Petro alisema hivi: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mtangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu. Kwa kuwa wakati mmoja ninyi mlikuwa si watu, lakini sasa ninyi ni watu wa Mungu.” (1 Petro 2:9, 10) Uhusiano wa pekee kati ya Yehova na taifa la Israeli la asili ulikuwa umekoma. Katika mwaka wa 33 W.K., baraka za Yehova zilikuwa zimeondolewa kwa Israeli wa kidunia na kupewa Israeli wa kiroho, kutaniko la Kikristo, “taifa lenye kuzaa matunda” ya Ufalme wa Kimasihi.—Mathayo 21:43.

Kujiweka Wakfu Kibinafsi

15. Siku ya Pentekoste 33 W.K., Petro aliwahimiza wasikilizaji wake wakubali ubatizo gani?

15 Baada ya Pentekoste 33 W.K., kila mtu, Myahudi au asiye Myahudi, alipaswa kujiweka wakfu kwa Mungu kibinafsi na kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” * (Mathayo 28:19) Siku ya Pentekoste, mtume Petro aliwaambia hivi Wayahudi na wageuzwa-imani: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.” (Matendo 2:38) Zaidi ya kuonyesha kwamba walikuwa wamejiweka wakfu kwa Yehova, Wayahudi na wageuzwa-imani hao walipaswa kuonyesha kwa ubatizo wao kwamba walikuwa wamemkubali Yesu kuwa njia ambayo Yehova anatumia kusamehe dhambi zao. Walipaswa kumtambua kuwa Kuhani Mkuu wa Yehova na Kiongozi wao, Kichwa cha kutaniko la Kikristo.—Wakolosai 1:13, 14, 18.

16. Katika siku za Paulo, watu wenye mwelekeo unaofaa, Wayahudi na wasio Wayahudi, walifanyaje ili wawe washiriki wa Israeli wa kiroho?

16 Miaka mingi baadaye, mtume Paulo alisema hivi: “Kwa wale walio katika Damasko kwanza na pia kwa wale walio katika Yerusalemu, na juu ya nchi yote ya Yudea, na kwa mataifa nilienda nikiuleta ujumbe kwamba wao wanapaswa kutubu na kumgeukia Mungu kwa kufanya matendo yanayostahili toba.” (Matendo 26:20) Baada ya kuwasadikisha Wayahudi na wasio Wayahudi kwamba Yesu alikuwa Kristo, Masihi, Paulo aliwasaidia wajiweke wakfu na kubatizwa. (Matendo 16:14, 15, 31-33; 17:3, 4; 18:8) Kwa kumgeukia Mungu, wanafunzi hao wapya wakawa washiriki wa Israeli wa kiroho.

17. Ni kazi gani ya kutiwa muhuri ambayo imekaribia mwisho wake, na ni kazi gani nyingine inayofanyika haraka?

17 Leo, kutiwa muhuri kwa mwisho kwa mabaki ya Israeli wa kiroho kunakaribia. Kutakapokamilishwa, wale “malaika wanne” wanaozishika zile pepo za uharibifu za “dhiki kuu” wataruhusiwa kuziachilia. Kwa sasa, kazi ya kukusanywa kwa washiriki wa “umati mkubwa,” wanaotarajia kuishi milele duniani, inafanyika haraka. “Kondoo wengine” wanachagua kwa hiari kuweka imani yao katika “damu ya Mwana-Kondoo” nao wanabatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova. (Ufunuo 7:1-4, 9-15; 22:17; Yohana 10:16; Mathayo 28:19, 20) Miongoni mwa watu hao kuna vijana wengi ambao wamelelewa na wazazi Wakristo. Ikiwa wewe ni mmoja wa vijana hao, utafurahi kusoma makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2003, ukurasa wa 30-31.

Kwa Kupitia

• Kwa nini watoto Waisraeli hawakuhitaji kujiweka wakfu kwa Yehova kibinafsi?

• Waisraeli wangeweza kuonyeshaje kwamba waliishi kulingana na wakfu wao?

• Kwa nini Yehova aliwakataa Waisraeli kuwa taifa lake lililojiweka wakfu, na nafasi yao ilichukuliwa na nani?

• Tangu Pentekoste 33 W.K. na kuendelea, Wayahudi na wasio Wayahudi walipaswa kufanya nini ili kuwa washiriki wa Israeli wa kiroho?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Watoto Waisraeli walizaliwa wakiwa washiriki wa taifa teule la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kila Mwisraeli alipaswa kufanya uamuzi wa kibinafsi wa kumtumikia Mungu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Matoleo ya hiari yaliwapa Waisraeli nafasi ya kuonyesha wanampenda Yehova

[Picha katika ukurasa wa 25]

Baada ya Pentekoste 33 W.K., wafuasi wa Kristo walipaswa kujiweka wakfu kwa Mungu kibinafsi na kuonyesha wakfu huo kwa njia ya ubatizo