Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanafurahia Kufanya Mapenzi ya Mungu

Wanafurahia Kufanya Mapenzi ya Mungu

Wanafurahia Kufanya Mapenzi ya Mungu

YESU aliwawekea Wakristo wote kielelezo bora aliposali hivi kwa Baba yake: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Watumishi wengi wa Mungu leo hujitiisha kwa Yehova kama Yesu alivyojitiisha katika sala hiyo. Miongoni mwao ni wanafunzi 52 wa darasa la 120 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Mnamo Machi 11, 2006, wahitimu hao walifurahi kujua kwamba watafanya mapenzi ya Mungu katika nchi mbalimbali, hata chini ya hali ngumu.

Ni nini ambacho kimewachochea wahitimu hao kuruhusu mapenzi ya Yehova yawaongoze maishani? Chris na Leslie, wenzi wa ndoa waliopewa mgawo wa kuwa wamishonari nchini Bolivia, walisema hivi: “Kwa kuwa tumejikana wenyewe, tunataka kufanya yote tuwezayo tukishirikiana na tengenezo la Yehova.” (Marko 8:34) Jason na Chere waliopewa mgawo wa kuwa wamishonari nchini Albania, walisema hivi: “Tumekabili matatizo mbalimbali katika kila mgawo ambao tumepokea katika tengenezo la Yehova. Hata hivyo, tumejifunza kwamba tunapaswa kumtegemea Yehova kabisa.”

Watiwa Moyo Wajitiishe kwa Mapenzi ya Yehova

George Smith, Mwanabetheli anayetumika katika Idara ya Sanaa, alifungua programu ya kuhitimu kwa sala. Mwenyekiti wa programu ya kuhitimu Stephen Lett, ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, aliwakaribisha wahudhuriaji wote. Wageni kutoka nchi 23 waliwasili katika Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, ili kuhudhuria tukio hilo lenye kufurahisha. Ndugu Lett aliwaambia wahitimu kwamba wanaenda kutimiza “jambo fulani muhimu.” Alikazia kwamba wamishonari hao wapya wataweza kupindua kwa nguvu za Maandiko mafundisho ya uwongo yaliyo kama “ngome zenye nguvu.” (2 Wakorintho 10:4, 5) Alimalizia hivi: “Mtapata shangwe nyingi kutumiwa na Yehova kupindua ngome zenye nguvu zilizo ndani ya watu wenye mioyo minyoofu mtakaokutana nao katika migawo yenu!”

Harold Jackson, mmoja wa wafanyakazi kwenye makao makuu alitoa hotuba yenye kichwa “Mambo Machache ya Kukumbuka.” Alitaja kwamba wamishonari hao wapya hawapaswi kusahau kamwe ‘kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu.’ (Mathayo 6:33) Wanapaswa kukumbuka kwamba “upendo hujenga” na ndio siri ya kufanikiwa. (1 Wakorintho 8:1) Alisema: “Acheni upendo uwaongoze mnaposhughulika na wengine.”

Kisha, Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza ambaye alitumikia akiwa mmishonari kuanzia mwaka wa 1979 hadi 2003, aliwauliza hivi wahitimu, “Je, Mnajua Daraka Lenu?” Alikazia umuhimu wa kuwa na usawaziko maishani mwao na katika huduma. Wakristo wana daraka la kuwa na bidii katika kupanda na kutilia maji mbegu za kweli. Hata hivyo, daraka la ukuzi wa kiroho ni la Yehova, kwa kuwa ‘Mungu ndiye anayezikuza.’ (1 Wakorintho 3:6-9) Ndugu Jackson aliongeza hivi: “Yehova anatarajia mwendelee kujiimarisha kiroho. Lakini mna daraka gani kubwa zaidi? Kumpenda Yehova na kuwapenda watu mnaoenda kuwatumikia.”

Lawrence Bowen, mwalimu wa Gileadi, alizungumzia kichwa “Jueni Namna Mnavyopaswa Kujiendesha.” Aliwakumbusha wanafunzi kwamba Yehova aliwaongoza na kuwalinda Waisraeli kimuujiza wakiwa nyikani. (Kutoka 13:21, 22) Yeye hutuongoza na kutulinda leo. Njia moja ambayo anatumia kufanya hivyo ni kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta, ambalo ni “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Timotheo 3:14, 15) Wamishonari hao wapya wanahitaji kutegemeza ile kweli, inayowaongoza na kuwalinda wanyenyekevu.

Mwalimu mwingine wa Gileadi, Wallace Liverance, aliwahimiza wahitimu wasisahau neno la Mungu lililo “nyuma” yao. Neno la Mungu liko nyuma katika maana ya kwamba liliandikwa karne nyingi zilizopita. Kama mchungaji anayeita kundi la kondoo kutoka nyuma, Yehova yuko nyuma ya watu wake, akiwaelekeza kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Isaya 30:21; Mathayo 24:45-47) Shule ya Gileadi iliwasaidia wahitimu kuithamini zaidi jamii hiyo ya mtumwa. “Mtumwa” huyo ameandaa Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Msemaji aliwatia moyo wahitimu hivi: “Bebeni hazina hii yenye habari zilizohifadhiwa, na muitumie kuwafundisha wengine.”—Mathayo 13:52.

Kufanya Mapenzi ya Mungu Katika Huduma ya Shambani

Katika sehemu yenye kichwa “Hamu ya Kuitangaza Habari Njema,” mwalimu wa Gileadi, Mark Noumair, alizungumzia baadhi ya mambo ambayo wahitimu walifurahia katika huduma ya hadharani walipohudhuria Shule ya Gileadi. (Waroma 1:15) Wahitimu waliohojiwa walionyesha kwamba kwa kweli walikuwa na hamu kubwa ya kuhubiri katika kila pindi.

Wahitimu walitiwa moyo zaidi wakati waangalizi watatu wanaosafiri wa huko Marekani walipohojiwa na Kenneth Flodin. Richard Keller na Alejandro Lacayo, ambao zamani walitumikia huko Amerika Kusini na Kati, walieleza jinsi walivyokabiliana na majaribu mbalimbali na baraka walizopata walipokuwa wamishonari. Moacir Felisbino alieleza kuhusu mazoezi aliyopata alipotumikia pamoja na wamishonari huko Brazili, ambako alilelewa.

Wamishonari watatu wenye uzoefu, Robert Jones, Woodworth Mills, na Christopher Slay, walihojiwa na David Schafer. Ndugu hao watatu walieleza jinsi walivyojifunza kumtegemea Yehova walipokabili matatizo. Waliwahakikishia wahitimu kwamba mazoezi waliyopata katika tengenezo la Yehova yaliwatayarisha vizuri kwa ajili ya migawo yao ya umishonari. Ndugu Mills alimalizia hivi: “Kilichonisaidia zaidi si elimu ya Gileadi, bali ni mambo ambayo shule hiyo ilinifunza kuhusu unyenyekevu na upendo.”

Mshiriki wa Baraza Linaloongoza Guy Pierce, alitoa hotuba ya msingi yenye kichwa “Yehova Hatashindwa Kamwe.” Adamu alishindwa, lakini je, hilo lilimaanisha kwamba Mungu alishindwa? Je, Mungu alishindwa kumuumba Adamu akiwa mkamilifu, kama wengine wanavyosema? Sivyo hata kidogo, kwa kuwa “Mungu wa kweli aliwafanya wanadamu wakiwa wanyoofu.” (Mhubiri 7:29) Utimilifu wa Yesu chini ya jaribu kubwa sana duniani ulithibitisha kwamba “Adamu hakuwa na sababu ya kushindwa,” akasema msemaji. Jaribu la utii ambalo Adamu alikabili katika bustani ya Edeni halikuwa gumu sana kama lile ambalo Yesu alikabili na kushinda. Lakini, Adamu alishindwa. Hata hivyo, Yehova hatashindwa kamwe. Kusudi lake litatimia. (Isaya 55:11) Ndugu Pierce aliwaambia wamishonari hao wapya hivi: “Mna pendeleo la kumheshimu Yehova kupitia roho yenu ya kujidhabihu. Yehova na awe na kila mmoja wenu popote mtakapomtumikia mkiwa wamishonari.”

Baada ya mwenyekiti, Ndugu Lett, kusoma salamu kutoka ofisi za tawi mbalimbali za Mashahidi wa Yehova, aliwapa wahitimu diploma na migawo yao. Vernon Wisegarver, mshiriki wa muda mrefu wa Betheli, alitoa sala ya kumalizia.

Wahudhuriaji 6,872 walihisi kwamba programu hiyo iliwachochea kufanya mapenzi ya Mungu kwa bidii zaidi. (Zaburi 40:8) Andrew na Anna walisema: “Tulijiweka wakfu kwa Yehova. Tulimwahidi Yehova kwamba tutafanya chochote anachotaka. Sasa Yehova anataka twende Kamerun, barani Afrika.” Wao pamoja na wahitimu wengine wana hamu kubwa ya kuanza mgawo ambao utawaletea uradhi na kusudi maishani. Naam, wanafurahia kufanya mapenzi ya Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 17]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi: 6

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 20

Idadi ya wanafunzi: 52

Wastani wa umri: 35.7

Wastani wa miaka katika kweli: 18.3

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 14.5

[Picha katika ukurasa wa 18]

Darasa la 120 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Wright, S.; Suárez, B.; Croisant, B.; Davenport, L. (2) Johnson, A.; Ali, C.; Cady, K.; Guerrero, P.; Ases, A. (3) Ortiz, L.; Lyall, K.; Uzeta, M.; Perez, R.; Backus, K.; Caterina, C. (4) Palmer, B.; Loving, D.; Macdonough, J.; Bostock, D.; Benetatos, L. (5) Jasicki, M.; Sarafianos, E.; Stelter, C.; Vaira, R.; Woon, J.; Prentice, K. (6) Davenport, H.; Croisant, H.; Perez, M.; Vaira, E.; Suárez, A.; Caterina, I.; Wright, C. (7) Cady, K.; Macdonough, J.; Ortiz, M.; Woon, J.; Ali, J.; Ases, M. (8) Sarafianos, G.; Lyall, D.; Uzeta, C.; Stelter, P.; Prentice, G.; Johnson, A.; Benetatos, C. (9) Palmer, J.; Jasicki, W; Backus, J.; Bostock, S.; Guerrero, J. M.; Loving, S.