Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kazia Fikira Mema ya Tengenezo la Yehova

Kazia Fikira Mema ya Tengenezo la Yehova

Kazia Fikira Mema ya Tengenezo la Yehova

“Hakika tutashiba mema ya nyumba yako.”—ZABURI 65:4.

1, 2. (a) Mipango iliyohusiana na hekalu ingewafaidi watu wa Mungu jinsi gani? (b) Daudi aliungaje mkono ujenzi wa hekalu?

DAUDI wa Israeli la kale ni mmoja wa watu wa pekee sana ambao wanazungumziwa katika Maandiko ya Kiebrania. Mchungaji huyo, ambaye pia alikuwa mwanamuziki, nabii, na mfalme alimtegemea kabisa Yehova Mungu. Uhusiano wake wa karibu sana pamoja na Yehova ulimchochea kutamani kumjengea Mungu nyumba. Nyumba hiyo, au hekalu, ingekuwa kituo cha ibada ya kweli huko Israeli. Daudi alijua kwamba mipango iliyohusiana na hekalu ingewaletea watu wa Mungu shangwe na baraka. Hivyo, Daudi aliimba hivi: “Mwenye furaha ni yule unayemchagua [Yehova] na kumfanya akaribie, ili apate kukaa katika nyua zako. Hakika tutashiba mema ya nyumba yako, mahali patakatifu pa hekalu lako.”—Zaburi 65:4.

2 Daudi hakuruhusiwa asimamie ujenzi wa nyumba ya Yehova. Badala yake, Sulemani mwana wake ndiye aliyepewa pendeleo hilo. Daudi hakunung’unika eti kwa sababu mtu mwingine amepewa pendeleo ambalo yeye mwenyewe alilitamani sana. Jambo la maana kwake lilikuwa ujenzi wa hekalu. Aliunga mkono mradi huo kwa moyo wote kwa kumpa Sulemani ramani za ujenzi ambazo alikuwa amepokea kutoka kwa Yehova. Zaidi ya hayo, Daudi alipanga maelfu ya Walawi katika migawanyo ya utumishi, naye akachanga kiasi kikubwa cha dhahabu na fedha kwa ajili ya ujenzi wa hekalu.—1 Mambo ya Nyakati 17:1, 4, 11, 12; 23:3-6; 28:11, 12; 29:1-5.

3. Watumishi wa Mungu wana mtazamo gani kuelekea mipango ya ibada ya kweli?

3 Waisraeli waaminifu waliunga mkono mipango iliyofanywa kwa ajili ya ibada ya kweli kwenye nyumba ya Mungu. Tukiwa watumishi wa Yehova leo, sisi pia huunga mkono mipango ya ibada katika sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Hivyo, tunaonyesha kwamba tuna mtazamo kama wa Daudi. Hatulalamiki. Badala yake, tunakazia fikira mema ya tengenezo la Mungu. Je, umewahi kufikiria mambo mengi mema ambayo tunaweza kuyathamini? Hebu tuzungumzie baadhi ya mambo hayo.

Kuwathamini Wale Wanaoongoza

4, 5. (a) “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hutimizaje utume wake? (b) Mashahidi wengine wamehisije kuhusu chakula cha kiroho wanachopokea?

4 Tuna sababu nzuri za kumthamini “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliyewekwa rasmi na Yesu Kristo kusimamia mali zake duniani. Jamii ya mtumwa inayofanyizwa na Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho huongoza kazi ya kuhubiri habari njema, hupanga mikutano ya ibada, na kuchapisha vitabu vinavyozungumzia Biblia katika lugha zaidi ya 400. Mamilioni ya watu ulimwenguni pote huthamini na kutumia ‘chakula hicho cha kiroho kwa wakati unaofaa.’ (Mathayo 24:45-47) Naam, hakuna sababu ya kunung’unika kuhusu chakula hicho.

5 Kwa miaka mingi, Elfi, Shahidi mmoja wa Yehova ambaye ni mzee kwa umri, amefarijiwa na kupata msaada kwa kutumia mashauri ya Kimaandiko yaliyo katika vichapo vya jamii ya mtumwa. Elfi alishukuru sana na kuandika hivi: “Siwezi kufanikiwa bila tengenezo la Yehova.” Peter na Irmgard pia wamekuwa watumishi wa Mungu kwa miaka mingi. Irmgard anathamini habari zote zinazochapishwa na “tengenezo la Yehova lenye upendo na linalojali.” Habari hizo zinatia ndani zile zinazotayarishwa kwa ajili ya watu wenye mahitaji ya pekee, kama wale wasioweza kuona au kusikia vizuri.

6, 7. (a) Utendaji wa makutaniko ulimwenguni pote unasimamiwaje? (b) Wengine wamesema nini kuhusu sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova?

6 “Mtumwa mwaminifu” huwakilishwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, ambalo ni kikundi kidogo cha wanaume waliotiwa mafuta kwa roho wanaotumikia kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi watumishi wa Yehova wenye uzoefu watumikie kwenye ofisi za tawi ambazo zinasimamia utendaji wa makutaniko zaidi ya 98,000 ulimwenguni pote. Wanaume wanaofikia matakwa ya Biblia huwekwa rasmi kuwa wazee na watumishi wa huduma katika makutaniko hayo. (1 Timotheo 3:1-9, 12, 13) Wazee huliongoza na kulichunga kwa upendo kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao. Kuna faida kubwa kama nini kuwa sehemu ya kundi hilo na kufurahia upendo na umoja unaopatikana miongoni mwa “ushirika mzima wa akina ndugu”!—1 Petro 2:17; 5:2, 3.

7 Badala ya kunung’unika, mara nyingi akina ndugu na dada hueleza jinsi wanavyothamini mwongozo wa kiroho wenye upendo kutoka kwa wazee. Mfano mmoja ni wa Birgit, ambaye ni mke Mkristo mwenye miaka zaidi ya 30. Kabla ya kufikia umri wa miaka 20, alikuwa na mashirika mabaya na alikuwa karibu kutumbukia katika dhambi. Lakini mashauri ya Biblia yaliyo wazi kutoka kwa wazee na msaada wa waamini wenzake ulimsaidia kuepuka hatari. Birgit anahisije sasa? Anasema hivi: “Ninashukuru sana kwamba bado niko katika tengenezo la Yehova ambalo linapendeza sana.” Mvulana mmoja mwenye umri wa miaka 17 anayeitwa Andreas anasema hivi: “Kwa kweli hili ni tengenezo la Yehova, tengenezo bora zaidi ulimwenguni.” Je, hatupaswi kuthamini mambo mema katika sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova?

Wale Wanaoongoza Si Wakamilifu

8, 9. Baadhi ya watu walioishi wakati mmoja na Daudi walitendaje, na Daudi alitendaje?

8 Bila shaka, wale waliowekwa rasmi kuongoza ibada ya kweli si wakamilifu. Wote hukosea, na wengine wana udhaifu ambao wanajitahidi sana kurekebisha. Je, jambo hilo linapaswa kutuhuzunisha? Hapana. Hata watu waliopewa madaraka mengi katika Israeli la kale walifanya makosa mazito. Kwa mfano, Daudi alipokuwa kijana, aliombwa aende kumpigia muziki Mfalme Sauli ili kumtuliza. Baadaye, Sauli alijaribu kumuua Daudi, na ilimbidi Daudi akimbie ili kuokoa uhai wake.—1 Samweli 16:14-23; 18:10-12; 19:18; 20:32, 33; 22:1-5.

9 Waisraeli wengine walitenda kwa hila. Kwa mfano, Yoabu, mkuu wa jeshi la Daudi, alimuua Abneri ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa Sauli. Absalomu alipanga njama dhidi ya baba yake, Daudi, ili anyakue ufalme. Na Daudi alisalitiwa na Ahithofeli, mshauri wake mwenye kutegemeka. (2 Samweli 3:22-30; 15:1-17, 31; 16:15, 21) Lakini Daudi hakulalamika kwa uchungu; wala hakuacha ibada ya kweli. Badala yake, Daudi alitenda kwa njia tofauti kabisa. Taabu zilimchochea Daudi kushikamana na Yehova na kudumisha mtazamo wake mzuri ambao alikuwa ameonyesha wakati alipokimbia kwa sababu ya Sauli. Wakati huo, Daudi aliimba hivi: “Unionyeshe kibali, Ee Mungu, unionyeshe kibali, kwa maana nafsi yangu imekukimbilia wewe; na katika kivuli cha mabawa yako nimekimbilia mpaka shida zipitilie mbali.”—Zaburi 57:1.

10, 11. Mkristo mmoja anayeitwa Gertrud alikabili hali gani alipokuwa kijana, naye alisema nini kuhusu kutokamilika kwa waamini wenzake?

10 Hatuna sababu ya kulalamika kwamba kuna hila katika tengenezo la Mungu leo. Yehova wala malaika wake wala wachungaji wa kiroho hawawezi kukubali watu waovu wenye hila waendelee kuwepo katika kutaniko la Kikristo. Hata hivyo, sisi sote hukabili hali ya kutokamilika kwa wanadamu, iwe ni kutokamilika kwetu au kutokamilika kwa watumishi wengine wa Mungu.

11 Alipokuwa kijana, mwabudu mmoja wa Yehova wa muda mrefu anayeitwa Gertrud alishutumiwa kwa uwongo kwamba yeye si mhubiri wa wakati wote wa Ufalme bali yeye ni mdanganyifu. Alitendaje? Je, Gertrud alinung’unika kwa kutendewa hivyo? Hapana. Muda mfupi kabla ya kifo chake katika mwaka wa 2003 akiwa na umri wa miaka 91, alikumbuka yaliyopita na kusema hivi: “Mambo hayo na mengine yamenifundisha kwamba licha ya makosa ya watu, Yehova huongoza kazi yake muhimu, ambayo ametupa sisi wanadamu wasio wakamilifu.” Gertrud alipokabili kutokamilika kwa watumishi wenzake wa Mungu, alisali kwa Yehova kutoka moyoni.

12. (a) Wakristo fulani wa karne ya kwanza waliweka mfano gani mbaya? (b) Tunapaswa kukazia fikira nini?

12 Kwa kuwa hata Wakristo washikamanifu na wenye bidii zaidi si wakamilifu, wakati mtumishi aliyewekwa rasmi anapokosea, acheni tuendelee “kufanya mambo yote bila kunung’unika.” (Wafilipi 2:14) Litakuwa jambo lenye kuhuzunisha kama nini ikiwa tutafuata mfano mbaya wa watu fulani katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza! Kulingana na mwanafunzi Yuda, walimu wa uwongo wa wakati huo walikuwa ‘wakipuuza mamlaka na kuwatukana watukufu.’ Isitoshe, watenda-dhambi hao walikuwa “wanung’unikaji, walalamikaji juu ya fungu lao maishani.” (Yuda 8, 16) Tusiwaige kamwe walalamikaji hao wenye kunung’unika. Badala yake acheni tukazie fikira mambo mazuri ambayo tunapata kutoka kwa “mtumwa mwaminifu.” Acheni tuthamini mema ya tengenezo la Yehova na ‘kuendelea kufanya mambo yote bila kunung’unika.’

“Maneno Hayo Yanashtua”

13. Wengine walitendaje waliposikia mafundisho fulani ya Yesu Kristo?

13 Ingawa wengine katika karne ya kwanza walinung’unika dhidi ya watumishi waliowekwa rasmi, wengine walinung’unika kwa sababu ya mafundisho ya Yesu. Kama ilivyoandikwa katika Yohana 6:48-69, Yesu alisema hivi: “Yule ambaye hula mwili wangu na kunywa damu yangu ana uzima wa milele.” Waliposikia maneno hayo, “wengi kati ya wanafunzi wake . . . wakasema: ‘Maneno hayo yanashtua; ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?’” Yesu alijua kwamba ‘wanafunzi wake walikuwa wakinung’unika juu ya hilo.’ Isitoshe, ‘kwa sababu ya hilo wengi kati yao wakaenda zao kwenye mambo yaliyo nyuma wakawa hawatembei tena pamoja naye.’ Lakini si wanafunzi wote walionung’unika. Ona kilichotukia wakati Yesu alipowauliza wale mitume 12 hivi: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Mtume Petro alimjibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele; na sisi tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.”

14, 15. (a) Kwa nini watu wachache huchukizwa na mafundisho fulani ya Kikristo? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Emanuel?

14 Katika nyakati zetu, watu wachache sana miongoni mwa watu wa Mungu wamechukizwa na mafundisho fulani ya Kikristo na kunung’unika dhidi ya sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Kwa nini hilo hutukia? Mara nyingi kunung’unika huko husababishwa kwa kutoelewa njia ya Mungu ya kufanya mambo. Muumba huwafunulia watu wake ukweli hatua kwa hatua. Hivyo, uelewaji wetu wa Maandiko unahitaji kuboreshwa mara kwa mara. Wengi kati ya watu wa Yehova hufurahia marekebisho hayo. Wachache ‘huwa waadilifu kupita kiasi’ na kuchukizwa na mabadiliko hayo. (Mhubiri 7:16) Huenda wakafanya hivyo kwa sababu ya kiburi, na wengine huangukia mtego wa kutegemea akili zao. Hata sababu iwe nini, kunung’unika kwa aina hiyo ni hatari, kwa sababu kunaweza kuturudisha katika ulimwengu na njia zake.

15 Kwa mfano, Shahidi mmoja anayeitwa Emanuel alichambua mambo fulani aliyosoma katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Aliacha kusoma vichapo vyetu vya Kikristo na mwishowe akawaambia wazee wa kutaniko lao kwamba ameacha kuwa Shahidi wa Yehova. Lakini baada ya muda mfupi, Emanuel alitambua kwamba mafundisho ya tengenezo la Yehova ni ya kweli. Aliwafikia Mashahidi, akakubali kosa lake, naye akarudishwa kuwa Shahidi wa Yehova. Hivyo, Emanuel akapata furaha tena.

16. Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuondoa mashaka kuhusu mafundisho fulani ya Kikristo?

16 Namna gani tukihisi kwamba tunataka kunung’unika kwa sababu tuna mashaka kuhusu mafundisho fulani ambayo watu wa Yehova wanaamini? Acheni tuwe na subira. Mwishowe huenda “mtumwa mwaminifu” akachapisha habari fulani ambazo zitajibu maswali yetu na kuondoa mashaka yetu. Ni jambo la hekima kuomba msaada wa wazee Wakristo. (Yuda 22, 23) Sala, funzo la kibinafsi, na kushirikiana pamoja na waamini wenzetu wanaohangaikia mambo ya kiroho kunaweza kutusaidia pia kuondoa mashaka na kuthamini zaidi kweli za Biblia zenye kuimarisha imani ambazo tumejifunza kupitia njia ya Yehova ya mawasiliano.

Dumisha Mtazamo Unaofaa

17, 18. Badala ya kunung’unika, tunapaswa kuwa na mtazamo gani, na kwa nini?

17 Ni kweli kwamba wanadamu wasio wakamilifu wamerithi dhambi, na huenda wengine wakawa na mwelekeo wenye nguvu wa kunung’unika bila sababu. (Mwanzo 8:21; Waroma 5:12) Lakini tukiwa na tabia ya kunung’unika, tunaweza kuhatarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. Hivyo, tunahitaji kudhibiti mwelekeo wa kunung’unika.

18 Badala ya kunung’unika kuhusu mambo katika kutaniko, inafaa tudumishe mtazamo unaofaa na kufuata ratiba inayotuwezesha kuwa na shughuli nyingi, shangwe, hofu ya Mungu, usawaziko, na imani yenye nguvu. (1 Wakorintho 15:58; Tito 2:1-5) Yehova anaongoza mambo yote katika tengenezo lake, na Yesu anajua mambo yanayotendeka katika kila kutaniko, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza. (Ufunuo 1:10, 11) Kwa subira, mngojee Mungu na Kristo, Kichwa cha kutaniko. Wachungaji wenye kutegemeka wanaweza kutumiwa kurekebisha mambo yanayohitaji kunyooshwa.—Zaburi 43:5; Wakolosai 1:18; Tito 1:5.

19. Hadi wakati ambapo Ufalme utaongoza shughuli zote za wanadamu, tunapaswa kukazia fikira nini?

19 Hivi karibuni, mfumo huu mbovu wa mambo utakomeshwa, na Ufalme wa Kimasihi utaongoza shughuli zote za wanadamu. Kabla ya wakati huo, ni muhimu sana kila mmoja wetu adumishe mtazamo unaofaa! Hilo litatusaidia kutambua sifa nzuri za waamini wenzetu, badala ya kukazia fikira udhaifu wao. Tutapata furaha tunapofikiria sifa zao nzuri. Badala ya kuumia kihisia kwa sababu ya kunung’unika, tutatiwa moyo na kujengwa kiroho.

20. Tutapata baraka gani tukiwa na mtazamo unaofaa?

20 Mtazamo unaofaa utatusaidia pia kukumbuka baraka nyingi tunazopata kwa kushirikiana na sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Ulimwenguni pote, hilo tu ndilo tengenezo linaloonyesha ushikamanifu kwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Unahisije kuhusu jambo hilo la kweli na kuhusu pendeleo la kumwabudu Mungu wa pekee wa kweli, Yehova? Acha mtazamo wako uwe kama wa Daudi, aliyeimba hivi: “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja. Mwenye furaha ni yule unayemchagua na kumfanya akaribie, ili apate kukaa katika nyua zako. Hakika tutashiba mema ya nyumba yako.”—Zaburi 65:2, 4.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunapaswa kuwathamini wale wanaoongoza kutanikoni?

• Tunapaswa kutendaje wakati akina ndugu wenye madaraka wanapokosea?

• Tunapaswa kuonaje marekebisho katika uelewaji wa Maandiko?

• Ni mambo gani yanayoweza kumsaidia Mkristo kuondoa mashaka?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Daudi alimpa Sulemani ramani za ujenzi na kuunga mkono ibada ya kweli kwa moyo wote

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wazee Wakristo hutoa msaada wa kiroho kwa hiari