Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, mtu anaweza kutengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo kwa sababu ya kuhusika katika uchafu kama vile anavyoweza kutengwa na ushirika kwa sababu ya uasherati au mwenendo mpotovu?

Ndiyo, mtu anaweza kutengwa na ushirika wa kutaniko ikiwa anaendelea kufanya uasherati, kuhusika katika aina fulani za uchafu, au mwenendo mpotovu, bila kutubu. Mtume Paulo anataja dhambi zote hizo tatu pamoja na dhambi nyingine ambazo zinaweza kumfanya mtu atengwe na ushirika, anapoandika hivi: “Matendo ya mwili ni wazi, nayo ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu . . . Ninawaonya ninyi kimbele . . . kwamba wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-21.

Uasherati (Kigiriki, por·neiʹa) unahusisha kufanya ngono haramu nje ya ndoa ya Kimaandiko. Uasherati unatia ndani uzinzi, umalaya, ngono kati ya watu ambao hawajaoana, ngono ya mdomo na ya mkundu na pia kushika-shika viungo vya uzazi vya mtu mwingine ambaye si mwenzi wako wa ndoa. Mtu anayefanya uasherati bila kutubu hastahili kuwa katika kutaniko la Kikristo.

Mwenendo mpotovu (Kigiriki, a·selʹgei·a) unahusisha “ufisadi; ufasiki; mwenendo wa kukosa aibu; mwenendo wa ukware.” Kamusi moja (The New Thayer’s Greek-English Lexicon) inafafanua neno hilo la Kigiriki kuwa “uchu usiozuilika, . . . kupita kiasi, kutokuwa na aibu, ufidhuli.” Kulingana na kamusi nyingine, mwenendo mpotovu ni tabia “inayokiuka mipaka yote ya mambo yanayokubalika katika jamii.”

Kama vile maelezo hayo yanavyoonyesha, “mwenendo mpotovu” unatia ndani mambo mawili: (1) Mwenendo wenyewe unakiuka kabisa sheria za Mungu, na (2) mtazamo wa mkosaji ni wa kukosa heshima na wa ufidhuli.

Hivyo, “mwenendo mpotovu” haurejelei mwenendo mbaya katika mambo madogo. Unahusiana na matendo ambayo yanavunja kabisa sheria za Mungu na ambayo yanaonyesha mtazamo wa kikaidi au wa dharau, yaani, mtazamo ambao unaonyesha ukosefu wa heshima au hata dharau kuelekea mamlaka, sheria, na kanuni za maadili. Paulo anahusianisha mwenendo mpotovu na ngono haramu. (Waroma 13:13, 14) Kwa kuwa andiko la Wagalatia 5:19-21 linaorodhesha mwenendo mpotovu kati ya mazoea yenye dhambi ambayo yanaweza kumfanya mtu asistahili kuurithi Ufalme wa Mungu, ni wazi kwamba mtu anaweza kukaripiwa au hata kutengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo kwa sababu ya kuhusika katika mwenendo mpotovu.

Uchafu (Kigiriki, a·ka·thar·siʹa) ni neno lenye maana pana zaidi kuliko maneno matatu yanayotafsiriwa “uasherati,” “uchafu,” na “mwenendo mpotovu.” Neno hilo linatia ndani uchafu wa kila namna, yaani, uchafu katika mambo ya ngono, katika usemi, katika matendo, na katika mazoea ya kidini. “Uchafu” unatia ndani dhambi nyingi nzito.

Kama inavyoonyeshwa kwenye 2 Wakorintho 12:21, Paulo anazungumza kuhusu wale ambao “hapo zamani walitenda dhambi lakini hawajatubu kutokana na unajisi wao na uasherati na mwenendo mpotovu ambao wamezoea kutenda.” Kwa kuwa “unajisi” au uchafu unatajwa pamoja na “uasherati na mwenendo mpotovu,” aina fulani za uchafu zinahitaji kuchukuliwa hatua ya kihukumu. Hata hivyo, uchafu ni neno linalohusisha mambo mengi sana kutia ndani mambo ambayo hayahitaji kuchukuliwa hatua ya kihukumu. Kama vile nyumba inavyoweza kuwa chafu kwa kiasi fulani au chafu sana, uchafu wa kiadili una viwango tofauti.

Kulingana na andiko la Waefeso 4:19, Paulo alisema kwamba watu wengine ‘waliishiwa na ufahamu wote wa maadili’ na kwamba “walijitoa wenyewe ili kuwa na mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.” Kwa hiyo, Paulo anaorodhesha “ukosefu wa usafi . . . kwa pupa” pamoja na mwenendo mpotovu. Ikiwa mtu aliyebatizwa anazoea kutenda “ukosefu wa usafi . . . kwa pupa” bila kutubu, anaweza kutengwa na ushirika wa kutaniko kwa msingi wa kuhusika katika mwenendo mchafu sana.

Tuseme watu wawili wanaochumbiana wanapapasana-papasana na kubusiana-busiana mara nyingi na kuamsha hamu ya ngono. Wazee wanaweza kuamua kwamba hata ingawa watu hao hawakuonyesha mtazamo wa kikaidi unaothibitisha mwenendo mpotovu, mwenendo wao ulionyesha pupa kwa kiasi fulani. Kwa hiyo, wazee wanaweza kuchukua hatua ya kihukumu kwa sababu watu hao walihusika katika mwenendo mchafu sana. Mwenendo mchafu sana unaweza pia kuwa msingi unaofaa wa kushughulikia kisa cha mtu mwenye zoea la kumpigia simu mtu mwingine ili kuzungumza waziwazi kuhusu ngono hasa ikiwa yule anayefanya hivyo amewahi kushauriwa kuhusu jambo hilo.

Wazee wanahitaji utambuzi wanapofanya maamuzi kama hayo. Ili kuamua iwapo kuna msingi wa kuchukua hatua ya kihukumu, wazee wanapaswa kuchunguza kwa uangalifu jambo lililofanywa na kuona ni kwa kadiri gani lilifanywa. Mtu hahukumiwi kwamba amehusika katika mwenendo mpotovu eti kwa sababu tu amekataa kukubali mashauri ya Kimaandiko wala hahukumiwi kwa kuhesabu mara ambazo anaweza kufanya dhambi fulani kabla hatua ya kihukumu kuchukuliwa. Wazee wanapaswa kufikiria kwa makini na kusali kuhusu kila hali na kuchunguza jambo lililotukia, lilitukia mara ngapi, aina ya mwenendo huo usiofaa, kadiri ulivyofanywa, na kusudi na nia ya mkosaji.

Mwenendo mchafu sana hauhusu tu dhambi za kingono. Kwa mfano, huenda mvulana aliyebatizwa akavuta sigara kadhaa kwa kipindi cha muda mfupi na kuungama mbele ya wazazi wake. Anaazimia kutovuta sigara tena. Huo ni uchafu, lakini haukufikia kiwango cha kuwa mwenendo mchafu sana au ‘ukosefu wa usafi unaofanywa kwa pupa.’ Shauri la Kimaandiko kutoka kwa mzee mmoja au wazee wawili pamoja na msaada wa wazazi linatosha. Lakini, ikiwa mvulana huyo huvuta sigara kwa ukawaida, tendo hilo litakuwa kuunajisi mwili kimakusudi, na halmashauri ya hukumu inapaswa kuundwa ili kushughulikia kesi hiyo ya mwenendo mchafu sana. (2 Wakorintho 7:1) Mvulana huyo asipoonyesha toba, anapaswa kutengwa na ushirika.

Wakristo wengine wametazama ponografia (picha za ngono). Kufanya hivyo ni kumchukiza Mungu, na wazee wanaweza kushtuka wanapogundua kwamba mwamini mwenzao amefanya hivyo. Lakini hilo halimaanishi kwamba kila mara mtu anapotazama ponografia kuna msingi wa kuunda halmashauri ya hukumu. Tuseme ndugu fulani alitazama mara kadhaa picha za ngono zisizo wazi sana (soft-core). Anaaibika kwa sababu ya jambo hilo, anaungama kwa mzee, naye anaazimia kutorudia dhambi hiyo tena. Mzee huyo anaweza kuamua kwamba mwenendo wa ndugu huyo haukufikia kiwango cha kuwa ‘ukosefu wa usafi unaofanywa kwa pupa,’ wala hakuwa na mtazamo wa ukaidi, unaoonyesha mwenendo mpotovu. Ingawa hakuna msingi wa kuchukua hatua ya kihukumu, uchafu wa aina hiyo unahitaji shauri thabiti la Kimaandiko, na labda, kuendelea kusaidiwa na wazee.

Hata hivyo, tuseme Mkristo amekuwa akitazama picha za ngono zenye kuchukiza sana zinazoonyesha ngono potovu, na amefanya juu chini kuficha dhambi hiyo. Huenda picha hizo za ngono zikaonyesha wanawake wakilalwa kinguvu na kikundi cha watu wengi, kumfunga mtu na kufanya naye ngono, kuwatesa watu kikatili, kuwatendea wanawake kikatili, au hata ngono kati ya watoto. Wengine wanapojua mwenendo wake, anaaibika sana. Huenda bado hajawa mkaidi, lakini wazee wanaweza kuamua kwamba ‘amejitoa mwenyewe’ kufanya zoea hilo chafu, naye amezoea ‘ukosefu wa usafi kwa pupa,’ yaani, mwenendo mchafu sana. Halmashauri ya hukumu inaweza kuundwa kwa sababu mtu huyo amehusika katika mwenendo mchafu sana. Mkosaji huyo asipoonyesha toba ya kimungu, pamoja na azimio la kuacha kabisa kutazama ponografia, anapaswa kutengwa na ushirika. Ikiwa mkosaji huyo aliwaalika wengine nyumbani kwake kutazama ponografia, na hivyo kuipendekeza kwao, hilo lingeonyesha kwamba ana mtazamo wa ukaidi unaoonyesha kwamba ana mwenendo mpotovu.

Sikuzote, maneno ya Kimaandiko “mwenendo mpotovu” yanahusisha dhambi nzito, kwa kawaida dhambi ya kingono. Wazee wanapojaribu kutambua mwenendo mpotovu, wanapaswa kuangalia waone ikiwa dhambi hiyo inahusisha ukaidi, ufasiki, uchafu, kutokuwa na aibu, na ikiwa ni jambo linalowashangaza watu kwa jumla. Kwa upande mwingine, huenda makosa mazito dhidi ya sheria ya Yehova yanayofanywa na mtu ambaye hana mtazamo wa kikaidi yakahusu “pupa.” Visa kama hivyo vinapaswa kushughulikiwa kwa msingi wa kuhusika katika mwenendo mchafu sana.

Kuamua iwapo mtu amehusika katika mwenendo mchafu sana au mwenendo mpotovu ni daraka zito, kwa kuwa uhai unahusika. Wale wanaoamua visa kama hivyo wanapaswa kusali na kumwomba Mungu roho yake takatifu, utambuzi, na uelewaji. Wazee wanahitaji kudumisha usafi wa kutaniko, na maamuzi yao yanapaswa kutegemea Neno la Mungu na pia mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 18:18; 24:45) Leo hasa, katika siku hizi zenye uovu, wazee wanapaswa kukumbuka maneno haya: “Oneni mnalofanya, kwa sababu hamhukumu kwa ajili ya mwanadamu bali kwa ajili ya Yehova.”—2 Mambo ya Nyakati 19:6.