Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uthibitisho Usio wa Kimaandiko Kuhusu Waisraeli

Uthibitisho Usio wa Kimaandiko Kuhusu Waisraeli

Uthibitisho Usio wa Kimaandiko Kuhusu Waisraeli

KATIKA Jumba la Makumbusho la Cairo huko Misri kuna jiwe lenye maandishi kuhusu ushindi wa Farao Merneptah. Kulingana na makadirio ya wasomi, mwana huyo wa 13 wa Ramses wa Pili alitawala kati ya mwaka wa 1212 na 1202 K.W.K., yaani, mwishoni mwa kipindi cha Waamuzi katika Israeli la kale. Mistari miwili ya mwisho kwenye jiwe hilo inasema hivi: “Kanaani imeporwa kabisa. Ashkeloni limetwaliwa, Gezeri limetekwa, [na] Yanoamu limeharibiwa kabisa. Israeli limeachwa ukiwa, na uzao wake umeangamia.”

Neno “Israeli” linamaanisha nini katika muktadha huu? Katika maandishi ya kuchorwa, ishara fulani zisizotamkwa ziliongezwa kwenye maneno ili kuonyesha kikundi cha maneno yenyewe. Kitabu kimoja (The Rise of Ancient Israel) kinasema hivi: “Ishara zilizoongezwa kwenye maneno matatu kati ya hayo manne, yaani, Ashkeloni, Gezeri na Yanoamu, zinaonyesha kwamba maneno hayo yanawakilisha majiji. . . . Hata hivyo, ishara iliyoongezwa kwenye neno Israeli, inaonyesha kwamba neno hilo linahusiana na watu.”—Italiki ni zetu.

Maandishi hayo yanamaanisha nini? Mhariri na mwandishi Hershel Shanks anajibu hivi: “Jiwe la Merneptah linaonyesha kwamba kulikuwa na watu walioitwa Israeli mwaka wa 1212 K.W.K. na kwamba farao wa Misri aliwajua, naye alihisi kuwa lilikuwa jambo linalofaa kujisifia jinsi alivyowashinda vitani.” Profesa William G. Dever wa elimu ya kuchunguza vitu vya kale huko Mashariki ya Kati, anasema hivi: “Maandishi ya jiwe la Merneptah yanaonyesha hivi kwa uhakika: Huko Kanaani kuna watu wanaojiita ‘Israeli’ nao Wamisri waliwaita ‘Israeli,’ na kwa kuwa Wamisri hawapendelei Biblia, haiwezekani kwamba walijitungia watu hususa na wa pekee wanaoitwa Israeli ili kupata umashuhuri.”

Katika Biblia, neno Israeli linatajwa kwa mara ya kwanza kuhusiana na jina alilopewa mzee wa ukoo Yakobo. Wazao wa wana 12 wa Yakobo walijulikana baadaye kuwa “wana wa Israeli.” (Mwanzo 32:22-28, 32; 35:9, 10) Miaka mingi baadaye, nabii Musa na pia Farao wa Misri walitumia neno “Israeli” walipozungumza kuhusu wazao wa Yakobo. (Kutoka 5:1, 2) Jiwe hilo la Merneptah ndio uthibitisho wa mapema zaidi usio wa Kimaandiko ambao unataja watu wanaoitwa Israeli.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Jiwe la Merneptah

Ishara tatu za mwisho (kutoka kulia hadi kushoto)—kijiti na mwanamume na mwanamke walioketi huwatambulisha Israeli kuwa taifa la kigeni

[Hisani]

Egyptian National Museum, Cairo, Egypt/Giraudon/The Bridgeman Art Library