Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Humkomboa Anayeteseka

Yehova Humkomboa Anayeteseka

Yehova Humkomboa Anayeteseka

“Mwadilifu ana misiba mingi, lakini Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo.”—ZABURI 34:19.

1, 2. Ni tatizo gani ambalo Mkristo mmoja mwaminifu alikabili, na kwa nini huenda tukahisi hivyo?

MWANAMKE mmoja kijana anayeitwa Keiko * amekuwa Shahidi wa Yehova kwa zaidi ya miaka 20. Kwa muda fulani, alitumikia akiwa painia wa kawaida, au mhubiri wa wakati wote wa Ufalme. Alithamini sana pendeleo hilo. Hata hivyo, muda mfupi uliopita, Keiko alikata tamaa na kujihisi mpweke. Anasema hivi: “Nilikuwa nikilia sana.” Ili kushinda mawazo yake yasiyofaa, Keiko alitumia wakati mwingi kujifunza. “Hata hivyo, singeweza kubadili hali yangu,” anasema Keiko. “Nilishuka moyo sana hivi kwamba nilitamani tu kufa.”

2 Je, umewahi kuhisi hivyo? Ukiwa Shahidi wa Yehova, una sababu nyingi za kushangilia kwa kuwa ujitoaji-kimungu “una ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.” (1 Timotheo 4:8) Kwa sasa, unaishi katika paradiso ya kiroho! Hata hivyo, je, hilo linamaanisha kwamba huwezi kuteseka? La! Biblia inasema hivi: “Mwadilifu ana misiba mingi.” (Zaburi 34:19) Hilo halishangazi kwa kuwa “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Kwa njia fulani, sote tunapatwa na matokeo mabaya ya uvutano huo wa Ibilisi.—Waefeso 6:12.

Matokeo ya Kuteseka

3. Toa mifano katika Biblia inayohusu watumishi wa Mungu waliotaabika sana.

3 Kuteseka kwa muda mrefu kunaweza kuathiri kabisa mtazamo wetu. (Methali 15:15) Fikiria mfano wa yule mwanamume mnyoofu Ayubu. Akiwa katika majaribu makali, Ayubu alisema hivi: “Mwanadamu, aliyezaliwa na mwanamke, ana maisha mafupi na yenye kujaa msukosuko.” (Ayubu 14:1) Shangwe ya Ayubu ilitoweka. Kwa muda fulani, alifikiri kwamba Yehova alikuwa amemwacha. (Ayubu 29:1-5) Mbali na Ayubu, kuna watumishi wengine wa Mungu waliotaabika sana. Biblia inatueleza kwamba Hana alikuwa na “uchungu katika nafsi” kwa sababu hakuwa na mwana. (1 Samweli 1:9-11) Rebeka alipokuwa akitaabishwa na hali fulani katika familia yake, alisema hivi: “Nimekuja kuyachukia sana haya maisha yangu.” (Mwanzo 27:46) Daudi alipokuwa akitafakari kuhusu makosa yake, alisema hivi: “Nimetembea huku na huku kwa huzuni mchana kutwa.” (Zaburi 38:6) Mifano hiyo michache inaonyesha wazi kwamba wanaume na wanawake waliomwogopa Mungu ambao waliishi kabla ya Ukristo walishuka moyo nyakati nyingine.

4. Kwa nini haishangazi kwamba kuna “nafsi zilizohuzunika” miongoni mwa Wakristo leo?

4 Namna gani Wakristo? Mtume Paulo aliona kwamba ni muhimu kuwaambia Wathesalonike ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:14) Kitabu kimoja kinasema kwamba neno la Kigiriki linalotafsiriwa “nafsi zilizohuzunika” linaweza kurejelea wale “wanaolemewa kwa muda na matatizo ya maisha.” Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba baadhi ya watiwa-mafuta katika kutaniko la Thesalonike walikuwa wameshuka moyo. Leo, miongoni mwa Wakristo kuna wale walioshuka moyo pia. Lakini kwa nini wameshuka moyo? Acheni tuchunguze sababu tatu.

Hali Yetu ya Dhambi Inaweza Kututaabisha

5, 6. Tunaweza kupata faraja gani kutokana na andiko la Waroma 7:22-25?

5 Tofauti na waovu ambao ‘wameishiwa na ufahamu wote wa maadili,’ Wakristo wa kweli wanataabishwa na hali yao ya dhambi. (Waefeso 4:19) Huenda wakahisi kama alivyohisi Paulo, ambaye aliandika hivi: “Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya viungo vyangu.” Kisha Paulo akasema hivi: “Maskini mimi!”—Waroma 7:22-24.

6 Je, umewahi kuhisi kama Paulo? Si vibaya kujua kwamba una udhaifu kwa sababu hilo linaweza kukuonyesha uzito wa dhambi na kuimarisha azimio lako la kuepuka mabaya. Lakini huhitaji kuendelea kutaabika kwa sababu ya makosa yako. Baada ya kusema maneno yaliyonukuliwa hapo juu, Paulo aliongeza hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Waroma 7:25) Naam, Paulo aliamini kwamba damu ya Yesu iliyomwagwa ingeweza kumkomboa kutokana na dhambi iliyorithiwa.—Waroma 5:18.

7. Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu asihuzunike kwa sababu ya mielekeo ya kutenda dhambi?

7 Ukihisi unalemewa na mielekeo yako ya kutenda dhambi, pata faraja katika maneno haya ya mtume Yohana, aliyeandika hivi: “Yeyote akitenda dhambi, tuna msaidizi kwa Baba, Yesu Kristo, mtu mwadilifu. Na yeye ni dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:1, 2) Ukihuzunika kwa sababu ya mielekeo yako ya kutenda dhambi, kumbuka sikuzote kwamba Yesu alikufa kwa ajili ya watenda-dhambi, wala si kwa ajili ya watu wakamilifu. Kwa kweli, “wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Waroma 3:23.

8, 9. Kwa nini tunapaswa kuepuka kujilaumu?

8 Hata hivyo, tuseme kwamba ulitenda dhambi nzito wakati uliopita. Bila shaka, huenda mara nyingi umemtajia Yehova jambo hilo katika sala. Umepokea msaada wa kiroho kutoka kwa wazee Wakristo. (Yakobo 5:14, 15) Ulitubu kikweli, na hivyo ukabaki kutanikoni. Au huenda uliliacha tengenezo la Mungu kwa muda fulani, lakini baadaye ukatubu na kuwa tena na msimamo safi. Katika hali zote hizo, huenda ukakumbuka dhambi yako ya zamani na kuhuzunika. Hali hiyo ikitokea, kumbuka kwamba Yehova huwasamehe “kwa njia kubwa” wale wanaotubu kikweli. (Isaya 55:7) Isitoshe, Yehova hataki ujilaumu na kuhisi kwamba huna tumaini. Shetani ndiye anayetaka uhisi hivyo. (2 Wakorintho 2:7, 10, 11) Ibilisi ataharibiwa kwa sababu anastahili kuharibiwa, lakini angependa wewe pia uhisi kwamba unastahili hukumu hiyohiyo. (Ufunuo 20:10) Usimwache Shetani atumie mbinu hiyo ili kuharibu imani yako. (Waefeso 6:11) Badala yake, anapotumia mbinu hiyo, ‘chukua msimamo umpinge,’ kama vile unavyompinga katika mambo mengine.—1 Petro 5:9.

9 Kwenye Ufunuo 12:10, Shetani anaitwa “mshtaki wa ndugu zetu,” yaani, Wakristo watiwa-mafuta. ‘Yeye huwashtaki mchana na usiku’ mbele za Mungu. Kutafakari mstari huo huenda kukakusaidia kuona kwamba Shetani, yule mshtaki wa uwongo, angefurahi kukuona ukijishtaki na kujilaumu, ingawa Yehova hafurahi. (1 Yohana 3:19-22) Kwa nini uendelee kuumia kwa sababu ya makosa yako kiasi cha kutaka kukata tamaa? Usimwache Shetani aharibu uhusiano wako pamoja na Mungu. Usimwache Ibilisi akupofushe ili usione kwamba Yehova ni “mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo.”—Kutoka 34:6.

Udhaifu Wetu Unaweza Kutuvunja Moyo

10. Ni katika njia gani udhaifu wetu unaweza kutuvunja moyo?

10 Wakristo wengine wanavunjika moyo kwa sababu ya jinsi udhaifu wao unavyoathiri utumishi wao kwa Mungu. Je, hivyo ndivyo unavyohisi? Huenda ugonjwa mbaya, uzee, au hali nyinginezo zikakuzuia usitumie wakati mwingi katika huduma kama ulivyofanya zamani. Ni kweli kwamba Wakristo wanatiwa moyo kununua wakati kwa ajili ya utumishi wa Mungu. (Waefeso 5:15, 16) Lakini namna gani ikiwa udhaifu unakuzuia usitimize mengi zaidi katika huduma na hivyo kukufanya uvunjike moyo?

11. Tunaweza kufaidikaje na shauri la Paulo kwenye Wagalatia 6:4?

11 Biblia inatuhimiza tusiwe goigoi bali tuwe “waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” (Waebrania 6:12) Tunaweza kufanya hivyo tukichunguza kielelezo chao kizuri na kujitahidi kuiga imani yao. Hata hivyo, hakuna faida tutakayopata tukijilinganisha na wengine isivyofaa na kukata kauli kwamba hakuna jambo zuri tunalofanya. Kwa hiyo, ni vizuri tufuate shauri hili la Paulo: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”—Wagalatia 6:4.

12. Kwa nini tunaweza kushangilia kwa sababu ya utumishi tunaomtolea Yehova?

12 Wakristo wana sababu nzuri za kushangilia, hata ikiwa hawawezi kutimiza mengi kwa sababu ya matatizo makubwa ya afya. Biblia inatuhakikishia hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Waebrania 6:10) Huenda hali zisizoweza kuepukika zikafanya iwe vigumu kwako kutimiza mengi zaidi kama ulivyofanya zamani. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova, huenda ukatimiza mengi zaidi katika sehemu nyingine za huduma ya Kikristo, kama vile kuhubiri kupitia simu na kuandika barua. Unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova Mungu atakubariki ukimtumikia kwa nafsi yako yote na kwa sababu ya upendo wako kwake na kwa wanadamu wenzako.—Mathayo 22:36-40.

“Nyakati za Hatari” Zinaweza Kutuvunja Moyo

13, 14. (a) Huenda tukapata taabu gani kwa sababu ya kuishi katika ‘nyakati hizi za hatari’? (b) Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba kuna ukosefu wa upendo wa asili leo?

13 Ingawa tunatarajia uzima katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, kwa sasa tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Tunafarijika kujua kwamba matukio yenye kuhuzunisha yanaonyesha kuwa ukombozi wetu unakaribia. Hata hivyo, sisi pia tunaathiriwa na hali zinazotuzunguka. Kwa mfano, namna gani ikiwa huna kazi? Huenda kazi haipatikani kwa urahisi, na kadiri miezi inavyopita, unajiuliza ikiwa Yehova anaona shida zako au anasikiliza sala zako. Au huenda unabaguliwa katika jamii au kutendewa isivyo haki. Hata unaposoma vichwa vikuu vya magazeti unaweza kuhisi kama Loti mwadilifu, “aliyetaabishwa sana” na mwenendo mpotovu wa majirani wake.—2 Petro 2:7.

14 Kuna jambo moja hususa kuhusu siku hizi za mwisho ambalo hatuwezi kupuuza. Biblia ilitabiri kwamba watu wengi watakuwa “wasio na upendo wa asili.” (2 Timotheo 3:3) Katika nyumba nyingi watu wa familia hawapendani. Kitabu kimoja (Family Violence) kinasema hivi: “Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kuuawa, kushambuliwa, kuumizwa kihisia, au kutendewa vibaya kingono na watu wa familia kuliko na mtu mwingine yeyote. Mahali ambapo watu wanapaswa kuonyeshwa upendo na kujihisi salama ndipo penye hatari zaidi kwa baadhi ya watu wazima na watoto.” Wale ambao wamepitia hali mbaya kama hizo katika familia zao, wanaweza kuwa na mahangaiko na kukata tamaa katika miaka ya baadaye. Namna gani ikiwa umepatwa na mambo hayo?

15. Ni kwa njia gani upendo wa Yehova ni mkuu kuliko wa mwanadamu yeyote?

15 Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” (Zaburi 27:10) Inafariji kujua kwamba Yehova anatupenda kuliko hata mzazi yeyote wa kibinadamu! Ingawa kukataliwa, kutendewa vibaya, au kuachwa na wazazi kunaweza kusababisha huzuni nyingi, mambo hayo hayaathiri jinsi Yehova anavyokujali. (Waroma 8:38, 39) Kumbuka kwamba Mungu huwavuta wale anaowapenda. (Yohana 3:16; 6:44) Hata wanadamu wawe wamekutendea mambo gani, Baba yako wa mbinguni anakupenda!

Hatua za Kukabiliana na Kuvunjika Moyo

16, 17. Mtu anaweza kulindaje nguvu zake za kiroho anapovunjika moyo?

16 Unaweza kuchukua hatua mbalimbali ili kukabiliana na kuvunjika moyo. Kwa mfano, fuata ratiba nzuri ya utendaji wa Kikristo. Tafakari Neno la Mungu, hasa unapovunjika moyo sana. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Niliposema: ‘Hakika mguu wangu utatembea ukitikisika,’ fadhili zako zenye upendo, Ee Yehova, ziliendelea kunitegemeza. Fikira zangu zinazofadhaisha zilipokuwa nyingi ndani yangu, faraja zako mwenyewe zilianza kuikumbatia nafsi yangu.” (Zaburi 94:18, 19) Kusoma Biblia kwa ukawaida kutakusaidia kujaza akili yako maneno na mawazo yenye kufariji na yenye kutia moyo.

17 Sala ni muhimu pia. Hata usipoweza kusema kabisa yale unayohisi moyoni mwako, Yehova anajua yale unayojaribu kusema. (Waroma 8:26, 27) Mtunga-zaburi alitoa uhakikisho huu: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”—Zaburi 55:22.

18. Ni hatua gani ambazo mtu aliyeshuka moyo anaweza kuchukua?

18 Watu wengine hukata tamaa kwa sababu ya kushuka moyo sana. * Ikiwa unahisi hivyo, basi jaribu kukazia fikira ulimwengu mpya wa Mungu na wakati ambapo “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Ikiwa wewe hushuka moyo mara nyingi, huenda ikafaa umwone daktari. (Mathayo 9:12) Pia, ni muhimu kujali afya yako ya kimwili. Ni muhimu kula chakula chenye afya na kufanya mazoezi. Hakikisha kwamba unapumzika vya kutosha. Usiangalie televisheni hadi usiku wa manane, na uepuke tafrija ambazo zinakuchosha. Zaidi ya hayo, endelea kushiriki katika utumishi mbalimbali unaompendeza Mungu. Ingawa wakati wa Yehova wa ‘kufuta kila chozi’ haujafika, atakusaidia kuvumilia.—Ufunuo 21:4; 1 Wakorintho 10:13.

Kuishi “Chini ya Mkono Wenye Nguvu wa Mungu”

19. Yehova anawaahidi nini wale wanaoteseka?

19 Biblia inatuhakikishia kwamba ingawa mwadilifu hupatwa na misiba mingi, “Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo.” (Zaburi 34:19) Mungu hufanyaje hivyo? Mtume Paulo aliposali tena na tena ili akombolewe kutokana na “mwiba katika mwili” wake, Yehova alimwambia hivi: “Nguvu zangu zinakamilishwa katika udhaifu.” (2 Wakorintho 12:7-9) Yehova alimwahidi Paulo nini, naye anakuahidi nini? Mungu hakuahidi kukuponya kimuujiza, bali anakuahidi kukupa nguvu za kuvumilia.

20. Licha ya majaribu tunayokabili, andiko la 1 Petro 5:6, 7 linatuhakikishia nini?

20 Mtume Petro aliandika hivi: “Jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue ninyi katika wakati unaofaa; huku mkitupa mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.” (1 Petro 5:6, 7) Kwa kuwa Yehova anakujali, hatakuacha kamwe. Atakutegemeza licha ya majaribu yanayokupata. Kumbuka kwamba Wakristo waaminifu wako “chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu.” Tunapoendelea kumtumikia Yehova, yeye hutupa nguvu ili tuvumilie. Tukiendelea kuwa waaminifu kwake, hakuna jambo linaloweza kutudhuru kiroho daima. Hivyo basi, acheni tuwe watimilifu kwa Yehova ili tuweze kufurahia uzima wa milele katika ulimwengu mpya alioahidi na kuona siku atakapomkomboa kabisa mtu anayeteseka!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Jina limebadilishwa.

^ fu. 18 Hali ya kushuka moyo sana haimaanishi tu kuvunjika moyo bali ni hali ya kuhuzunika sana kwa muda mrefu. Kwa habari zaidi, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1988, ukurasa wa 25-29; Novemba 15, 1988, ukurasa wa 21-24; na Septemba 1, 1996, ukurasa wa 30-31.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini hata watumishi wa Yehova huteseka?

• Ni mambo gani yanayoweza kuwafanya baadhi ya watu wa Mungu wavunjike moyo?

• Yehova anatusaidiaje kukabiliana na mahangaiko yetu?

• Ni katika njia gani tuko “chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Licha ya majaribu, watu wa Yehova wana sababu ya kushangilia

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kuhubiri kupitia simu ni njia moja ya kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote