Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hatimaye Familia Yetu Yaungana!

Hatimaye Familia Yetu Yaungana!

Simulizi la Maisha

Hatimaye Familia Yetu Yaungana!

LIMESIMULIWA NA SUMIKO HIRANO

Nilikuwa nimepata njia bora ya maisha, nami nilitaka mume wangu aifurahie pia. Hilo lingetukia baada ya miaka 42.

MIMI na mume wangu tulifunga ndoa mwaka wa 1951, nilipokuwa na umri wa miaka 21. Katika kipindi cha miaka minne, tulizaa watoto wawili wavulana, nami nilikuwa nimeridhika kabisa maishani.

Siku moja mwaka wa 1957, dada yangu mkubwa aliniambia kwamba alikuwa akitembelewa na mmishonari mmoja Shahidi wa Yehova. Ingawa alikuwa mfuasi wa dini ya Buddha, dada yangu alianza kujifunza Biblia na mmishonari huyo naye akanitia moyo nijifunze Biblia pia. Nilikubali kujifunza. Nilikuwa mshiriki wa kanisa moja la Kiprotestanti, nami nilifikiri kwamba ningeweza kuwaonyesha Mashahidi wa Yehova mafundisho yao ya uwongo.

Baada ya muda mfupi, nilitambua kwamba sikuijua Biblia. Nilimuuliza mmishonari huyo, “Yehova ni nani?” Sikuwahi kusikia jina hilo likitumiwa kanisani. Mmishonari huyo, Daphne Cooke (ambaye baadaye aliitwa Pettitt), alinionyesha andiko la Isaya 42:8, ambalo linasema waziwazi kwamba Yehova ndilo jina la Mungu Mweza-Yote. Daphne alijibu maswali yangu yote kwa kutumia Biblia.

Nilimuuliza kasisi wa kanisa letu maswali hayohayo. Aliniambia hivi: “Ni dhambi kuuliza maswali. Amini tu mambo unayoambiwa.” Ingawa sikuona kwamba ni makosa kuuliza maswali, kwa muda wa miezi sita nilienda kanisani kila Jumapili asubuhi kisha alasiri nikahudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova.

Jinsi Ndoa Yangu Ilivyoathiriwa

Mambo niliyojifunza katika Biblia yalinisisimua, nami nilimweleza mume wangu Kazuhiko mambo hayo pia. Kila wakati baada ya kujifunza na kuhudhuria mikutano, nilimweleza mambo niliyojifunza. Kwa sababu hiyo, uhusiano wetu ulianza kuharibika. Hakutaka niwe Shahidi wa Yehova. Lakini nilifurahia sana kujifunza Biblia hivi kwamba niliendelea kujifunza na kushirikiana na Mashahidi.

Kabla ya kuondoka nyumbani ili kuhudhuria mikutano ya usiku, nilikuwa nikimtayarishia Kazuhiko chakula alichopenda sana, lakini alianza kwenda kula katika mikahawa. Niliporudi nyumbani baada ya mikutano, mara nyingi nilimkuta amekasirika na hakutaka kuzungumza. Baada ya siku mbili au tatu, hasira yake ilipungua, lakini huo ulikuwa wakati kwa ajili ya mkutano mwingine tena.

Wakati huo, niliugua ugonjwa wa kifua kikuu, ugonjwa ambao ulikuwa umesababisha vifo vya watu wengi katika familia ya mume wangu. Kazuhiko akawa na wasiwasi sana, naye akaniambia kwamba nikipona nitaweza kufanya chochote nipendacho. Nilimwomba tu jambo moja, kwamba aniruhusu niwe nikihudhuria mikutano ya kila juma. Akakubali.

Nilipata nafuu baada ya miezi sita, na muda wote huo nilijifunza Biblia kwa bidii sana. Nilitafuta makosa katika mafundisho ya Mashahidi huku nikidhani kwamba nitaacha kujifunza nikipata angalau kosa moja tu. Sikupata kosa lolote. Badala yake, makosa ya Kanisa la Kiprotestanti yalionekana wazi. Nilijifunza kuhusu upendo na haki ya Yehova nami nikaelewa faida ya kuishi kulingana na sheria zake.

Nilipopata nafuu, mume wangu alitimiza ahadi yake naye hakunizuia nisihudhurie mikutano. Niliendelea kukomaa kiroho, na mnamo Mei 1958, nikabatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Nilitamani sana familia yangu ijiunge nami katika kumwabudu Mungu wa kweli.

Kuwasaidia Watoto Wangu Kiroho

Sikuzote watoto wangu waliandamana nami kwenye mikutano na katika mahubiri, lakini mambo fulani yaliyotukia yalinisaidia kuelewa kwamba walikuwa wakiendelea kuijua Biblia. Siku moja, mwana wangu Masahiko, aliyekuwa na umri wa miaka sita, alikuwa akicheza nje ya nyumba. Nilisikia sauti kubwa na mtu fulani akipiga mayowe. Jirani yangu aliingia nyumbani kwangu akikimbia na kupiga mayowe huku akisema kwamba mwana wangu amegongwa na gari. Je, alikuwa amekufa? Nilijitahidi kutulia na kutoka nje haraka. Nilitetemeka sana nilipoona baiskeli yake iliyopondwa, lakini nikamwona akija akiwa ameumia kidogo tu. Aliponikumbatia alisema hivi: “Mama, Yehova amenisaidia, sivyo?” Kumwona akiwa hai na kusikia maneno hayo mazuri, kulinifanya nilie.

Siku nyingine, katika huduma, tulikutana na mwanamume mzee ambaye alisema hivi kwa sauti kubwa: “Kwa nini mnamlazimisha mtoto mdogo azunguke nanyi huku na huku? Ninamhurumia.” Kabla sijasema neno lolote, Tomoyoshi, mwenye umri wa miaka minane alisema hivi: “Babu, mama yangu hanilazimishi kuhubiri. Ninahubiri kwa sababu ninataka kumtumikia Yehova.” Mzee huyo alimkodolea macho kwa mshangao bila kusema lolote.

Kwa upande wa kiroho, watoto wangu hawakuwa na baba. Lilikuwa daraka langu kuwafundisha kweli za Biblia, ingawa mimi mwenyewe nilikuwa na mengi ya kujifunza. Nilisitawisha upendo, imani, na bidii, na kujitahidi kuweka kielelezo kizuri. Kila siku nilimshukuru Yehova mbele ya watoto wangu. Niliwaeleza mambo niliyofurahia katika mahubiri. Hilo liliwatia moyo. Walipoulizwa baadaye kwa nini walikuwa mapainia, au wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, walijibu hivi: “Tuliona kwamba mama yetu alifurahia kutumikia akiwa painia, nasi tulitaka tuwe wenye furaha pia.”

Nilikuwa mwangalifu sana nisiseme vibaya kuhusu baba yao au mtu yeyote kutanikoni. Nilitambua kwamba kuzungumza vibaya kuhusu wengine kungeweza kuwaathiri watoto wangu. Hawangeweza kumheshimu yule anayesemwa vibaya na pia yule anayesema vibaya juu ya wengine.

Kushinda Vizuizi vya Kufanya Maendeleo

Mwaka wa 1963 kazi ya mume wangu ilifanya familia yetu ihamie Taiwan. Aliniambia kwamba ikiwa ningewahubiria Wajapani walioishi huko, ningesababisha matatizo makubwa. Tungerudishwa Japani, na kampuni yao ingekabili matatizo. Alitaka kututenganisha na Mashahidi.

Huko Taiwan, mikutano yote ilifanywa katika Kichina, na Mashahidi wa huko walitukaribisha kwa shauku. Niliamua kujifunza Kichina ili kuwahubiria wenyeji badala ya kuwahubiria Wajapani. Kwa njia hiyo, ningeepuka matatizo ambayo mume wangu aliyataja.

Urafiki wetu pamoja na Mashahidi wa Taiwan ulituimarisha. Harvey na Kathy Logan, ambao walikuwa wamishonari, walitusaidia sana. Ndugu Logan alikuwa baba wa kiroho wa wavulana wangu. Aliwaonyesha kwamba kumtumikia Yehova hutokeza shangwe, bali si maisha magumu. Nina hakika kwamba wavulana wangu waliamua kumtumikia Yehova tulipokuwa huko Taiwan.

Tukiwa huko Taiwan, Tomoyoshi na Masahiko walisoma katika shule moja ya Wamarekani, ambako walijifunza Kiingereza na Kichina. Elimu hiyo iliwatayarisha kwa ajili ya utumishi wa wakati ujao wakiwa wahudumu wa Mungu wa kweli, Yehova. Ninamshukuru sana Yehova kwa kutupa baraka nyingi za kudumu katika kipindi kilichoonekana kuwa kigumu kwetu. Baada ya miaka mitatu na nusu yenye kufurahisha sana huko Taiwan, familia yetu ilirudi tena Japani.

Sasa wavulana wetu walikuwa wamebalehe na walitaka uhuru. Nilitumia wakati mwingi kuzungumza nao juu ya kanuni za Kimaandiko, na Yehova aliwasaidia katika kipindi hicho kigumu. Baada ya kumaliza shule ya sekondari, Tomoyoshi alianza upainia. Aliwasaidia watu wanne kujiweka wakfu na kubatizwa katika miaka ya kwanza ambayo alifanya upainia. Masahiko alifuata kielelezo cha ndugu yake naye akaanza kazi ya upainia baada tu ya kumaliza shule ya sekondari. Alisaidia vijana wanne kuwa Mashahidi katika miaka minne ya kwanza ya upainia.

Kisha Yehova aliwabariki watoto hao hata zaidi. Tomoyoshi alijifunza pamoja na mume wa mwanamke mmoja ambaye nilimsaidia kujua kweli za Biblia. Mabinti wao wawili wakawa pia Mashahidi. Baadaye, Tomoyoshi akamwoa binti mkubwa, Nobuko, na Masahiko akamwoa yule mdogo, Masako. Tomoyoshi na Nobuko wanatumikia sasa kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Naye Masahiko na Masako ni wamishonari huko Paraguai.

Mume Wangu Abadilika Hatua kwa Hatua

Mume wangu hakujali imani yetu kwa muda wote huo, lakini tuliona dalili za mabadiliko. Wengine waliponipinga, alitetea imani yangu na hata aliunga mkono kweli za Biblia bila yeye kutambua. Aliwasaidia Mashahidi waliokuwa katika uhitaji. Alisema hivi katika hotuba yake fupi wakati wa arusi ya mmoja wa watoto wetu: “Kufundisha watu njia inayofaa ya maisha ndiyo kazi nzuri zaidi, na ngumu zaidi. Wana wangu na wake zao wamechagua kufanya kazi hiyo ngumu. Tafadhali, wasaidieni.” Mambo yote hayo yalinifanya niamini kwamba hakika mume wangu angejiunga nasi kumtumikia Yehova.

Nilipanga mambo ili ashirikiane na Mashahidi nyumbani kwetu. Nilimwalika Kazuhiko kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo na pia kwenye Ukumbusho wa Kifo cha Kristo. Kazi yake ilipomruhusu, alihudhuria mikutano hiyo, ingawa alifanya hivyo shingo upande. Mara nyingi nilifikiri kwamba angekubali funzo la Biblia, hivyo nikaalika wazee Wakristo nyumbani. Lakini alikataa kujifunza, nami sikuelewa sababu yake ya kukataa.

Nilikumbuka maneno haya ya mtume Petro: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.” (1 Petro 3:1, 2) Nilitambua kwamba sikufuata shauri hilo sikuzote. Ili kulifuata kikamili, nilihitaji kuboresha hali yangu ya kiroho.

Mwaka wa 1970, nilianza upainia nikiwa na mradi wa kuwa mtu wa kiroho zaidi. Miaka 10 ilipita, halafu 20. Hata hivyo, mume wangu hakubadilika. Siku moja mwanafunzi mmoja wa Biblia aliniambia hivi: “Haikosi kwamba unaumia unapoona kwamba unawasaidia watu wengine huku ukishindwa kumsaidia mume wako.” Maneno hayo yalinivunja moyo, lakini sikukata tamaa.

Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1980, wazazi wetu walikuwa wamezeeka sana. Kuwatunza na kutimiza madaraka yangu mengine kulinichosha na kunifadhaisha. Kwa miaka mingi, wote walipinga imani yangu katika Yehova, lakini nilijitahidi sana kuwaonyesha kwamba ninawapenda. Punde tu kabla ya kifo chake, mama yangu aliyekuwa na umri wa miaka 96 aliniambia hivi: “Sumiko, nikifufuliwa, nitajiunga na dini yako.” Nilitambua kwamba jitihada zangu hazikuwa za bure.

Mume wangu aliona yote ambayo niliwafanyia wazazi wetu. Ili kuonyesha shukrani, alianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Alihudhuria mikutano kwa miaka mingi lakini hakufanya maendeleo yoyote. Niliendelea kujitahidi kumpendeza. Nilialika marafiki wake na hata wanabiashara wenzake wa nchi za kigeni nyumbani kwetu kwa ajili ya chakula. Nilijiunga naye katika tafrija. Saa za mapainia zilipopunguzwa hadi 70 kila mwezi, nilitumia wakati mwingi zaidi pamoja naye.

Kustaafu Kwaleta Mabadiliko

Mume wangu alistaafu mwaka wa 1993. Nilianza kufikiri kwamba hatimaye atakuwa na wakati wa kujifunza Biblia. Lakini alisema kwamba kumwabudu Mungu eti kwa sababu sasa ana wakati ni kukufuru. Hivyo, akasema kwamba angemwabudu Mungu wakati moyo wake ungemsukuma kufanya hivyo na kwamba sipaswi kumlazimisha.

Siku moja Kazuhiko aliniuliza ikiwa ningetumia miaka inayobaki ya maisha yangu kuishi kwa ajili yake. Maneno hayo yaliniumiza kwa sababu nilikuwa nimejitahidi juu chini kumpendeza tangu tulipofunga ndoa. Nilikuwa nimejitahidi sana kumfurahisha, lakini alihisi kwamba nilijitoa zaidi kwa Yehova kuliko kujitoa kwake. Baada ya kufikiria jambo hilo kwa muda, nilimjibu kwamba singeweza kumfanyia zaidi ya yale niliyokuwa nimemfanyia. Lakini ikiwa angejiunga nami katika yale niliyokuwa nikifanya, tungeanza kufurahia maisha mapya ambayo yangedumu, si kwa miaka michache tu, bali milele. Muda wa siku kadhaa, mume wangu hakunijibu. Mwishowe akaniuliza hivi: “Je, sasa utanifundisha Biblia?” Kila ninapokumbuka maneno hayo, mimi hufurahi.

Mwanzoni nilifanya mipango ili mzee mmoja Mkristo ajifunze na mume wangu, lakini akaniambia hivi: “Sitajifunza na mtu yeyote, ila wewe.” Hivyo, tukaanza kujifunza Biblia kila siku. Kwa kuwa ninashirikiana na kutaniko la Kichina na mume wangu huzungumza vizuri lugha hiyo, tulijifunza katika Kichina. Pia, tulisoma Biblia nzima pamoja kabla ya mwaka mmoja kwisha.

Wakati huo, mzee mmoja wa kutaniko la Kichina, pamoja na mke wake, walipendezwa nasi. Ingawa wana umri mdogo kuliko watoto wetu, walikuwa marafiki wetu wa kweli. Pia, Mashahidi wengine wengi walipendezwa sana na mume wangu. Walitutendea kwa ukarimu na walizungumza na Kazuhiko kana kwamba alikuwa baba yao. Jambo hilo lilimfurahisha sana.

Siku moja tulipokea mwaliko wa arusi moja kutanikoni ambao ulitumwa kwa jina la mume wangu. Aliguswa moyo sana kwa sababu alitambuliwa kuwa kichwa cha familia, naye akaamua kuhudhuria arusi hiyo. Muda si muda, akaanza kuzungumza kwa urafiki pamoja na Mashahidi, naye akaanza kujifunza Biblia pamoja na mzee mmoja Mkristo. Funzo la Biblia, kuhudhuria mikutano, na upendo ambao alionyeshwa kutanikoni ulimsaidia kufanya maendeleo mazuri ya kiroho.

Hatimaye Familia Yaungana

Mnamo Desemba 2000, mume wangu alibatizwa ili kuonyesha kwamba alikuwa amejiweka wakfu kwa Yehova. Wanangu na wake zao walitoka mbali kuja kuona “muujiza” huo wa kisasa. Ilichukua miaka 42, lakini hatimaye familia yetu imeungana.

Sasa kila asubuhi, sisi wawili huzungumzia andiko la siku na kusoma Biblia pamoja. Kila siku, tunafurahia mazungumzo ya kiroho na kushiriki pamoja mambo ya kiroho. Mume wangu sasa ni mtumishi wa huduma kutanikoni na hivi karibuni alitoa hotuba ya watu wote katika Kichina. Ninamshukuru Yehova kwa kutuunganisha. Ninatazamia kulitetea jina lake na enzi kuu yake milele pamoja na wapendwa wangu wote.

[Ramani katika ukurasa wa 13]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

CHINA

JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA KOREA

JAMHURI YA KOREA

Bahari ya Japani

JAPANI

Tokyo

Bahari ya Mashariki ya China

TAIWAN

Taipei

[Picha katika ukurasa wa 12]

Pamoja na familia yangu mwaka wa 1958, mwaka niliobatizwa

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tuliimarishwa kiroho na marafiki kama vile Harvey na Kathy Logan tulipohama kutoka Tokyo hadi Taipei

[Picha katika ukurasa wa 15]

Leo familia yetu imeungana katika ibada ya kweli