Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumwogopa Mungu Ni “Nidhamu ya Hekima”

Kumwogopa Mungu Ni “Nidhamu ya Hekima”

Kumwogopa Mungu Ni “Nidhamu ya Hekima”

HEKIMA ya kweli imetayarisha karamu kubwa. “Imetuma watumishi wake wa kike, ili ipate kupaaza sauti juu ya vilele vya mji: ‘Yeyote ambaye hana uzoefu, na ageuke aje hapa.’ Amemwambia yeyote ambaye amepungukiwa moyoni: ‘Njooni, mle mkate wangu na mshiriki kunywa divai ambayo nimechanganya. Waacheni wasio na uzoefu mpate kuendelea kuishi, na mtembee moja kwa moja katika njia ya uelewaji.’”—Methali 9:1-6.

Kula kwenye meza ya hekima hakusababishi jambo lolote baya au lenye kuumiza. Kusikiliza hekima ya kimungu iliyo katika methali zilizoongozwa kwa roho ya Mungu na kukubali nidhamu yake huwa na matokeo bora. Acheni tuchunguze maneno yenye hekima yanayopatikana kwenye Methali 15:16-33. * Kutii mashauri ya methali hizo fupi kunaweza kutusaidia kutosheka na vitu vichache, kufanya maendeleo, na kuwa na shangwe maishani. Kufanya hivyo kunaweza pia kutusaidia kufanya maamuzi mazuri na kutuwezesha kubaki katika njia inayoongoza kwenye uzima.

Wakati Ambapo Vitu Vichache Ni Bora

Mfalme Sulemani wa Israeli la kale anasema hivi: “Afadhali kuwa na vitu vichache pamoja na kumwogopa Yehova kuliko kuwa na vitu vingi pamoja na mvurugo.” (Methali 15:16) Ni upumbavu kumpuuza Muumba na kutanguliza vitu vya kimwili maishani mwetu. Maisha kama hayo ni ya ubatili sana nayo husababisha mahangaiko mengi. Inasikitisha sana wakati mtu anapozeeka na kutambua kwamba maisha yake yote hayakuwa na kusudi wala maana! Si jambo la hekima kujikusanyia vitu vingi pamoja na “mvurugo.” Ni afadhali kujifunza siri ya kutosheka na kuishi kulingana na siri hiyo! Tunapata uradhi wa kweli kwa kumwogopa Yehova na kwa kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye, bali si kwa kuwa na vitu vya kimwili.—1 Timotheo 6:6-8.

Sulemani anakazia kwamba kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine ni muhimu zaidi kuliko kuwa na vitu vingi vya kimwili, anaposema hivi: “Afadhali chakula cha mboga za majani mahali penye upendo kuliko ng’ombe-dume aliyenoneshwa pamoja na chuki.” (Methali 15:17) Naam, upendo katika familia ni bora zaidi kuliko kuwa na vyakula vingi vitamu. Huenda familia ya mzazi mmoja isiwe na mali nyingi. Katika nchi fulani, huenda mtu akawa tu na uwezo wa kupata chakula kisichogharimu pesa nyingi. Hata hivyo, familia hufanikiwa mahali palipo na upendo na shauku.

Huenda hali ngumu zikatokea hata katika familia ambazo kwa kawaida zina upendo. Huenda mshiriki mmoja wa familia akasema au kufanya jambo litakalomuumiza mwingine. Aliyekosewa anapaswa kutendaje? Methali 15:18 inasema hivi: “Mtu mwenye ghadhabu huchochea ugomvi, lakini yule ambaye hakasiriki upesi hutuliza mabishano.” Jibu la upole, bali si la hasira, hufanya kuwe na amani na utulivu. Shauri la methali hiyo linatumika kwa njia ileile katika sehemu nyingine za maisha, kutia ndani mambo yanayohusu kutaniko na huduma ya hadharani.

‘Njia Inapofanywa Kuwa Laini’

Methali inayofuata inakazia tofauti iliyopo kati ya mtu asiyeisikiliza hekima na wale wanaoisikiliza. Mfalme huyo mwenye hekima anasema hivi: “Njia ya mvivu ni kama boma la miiba, lakini mapito ya wanyoofu ni njia iliyofanywa kuwa laini.”Methali 15:19.

Boma la miiba ni kizuizi hatari. Mtu mvivu hufikiria kila namna ya vizuizi, naye huvitumia kuwa kisingizio ili asianze kazi fulani. Kwa upande mwingine, wanyoofu hawaogopi vizuizi wanavyoweza kukabili. Wana bidii katika kazi yao na wanakazia fikira kile wanachofanya. Hivyo, wanaepuka matatizo mengi ambayo wangekabili ikiwa wangepuuza daraka lao. Njia yao ‘inafanywa kuwa laini,’ yaani, wanafanya maendeleo. Wao huendelea kufanya kazi yao na hufurahi kuiona ikifanikiwa.

Kwa mfano, kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na kufikia ukomavu wa kiroho kunahitaji jitihada. Huenda mtu akatumia kisingizio cha kutokuwa na elimu ya kutosha, kutoweza kusoma vizuri, au kutoweza kukumbuka mambo ili asijifunze Biblia kwa bidii. Ni afadhali kuepuka kuona mambo hayo kuwa vizuizi vya kupata ujuzi! Hata ikiwa hatuna elimu ya kutosha, tunaweza kujitahidi kuboresha ustadi wetu wa kusoma na kuelewa mambo tunayosoma, labda kwa kutumia kamusi inapohitajiwa. Mtazamo mzuri hutusaidia kupata ujuzi na kufanya maendeleo ya kiroho.

‘Baba Anaposhangilia’

Mfalme wa Israeli anasema hivi: “Mwana mwenye hekima ndiye humfanya baba yake ashangilie, lakini mtu mjinga anamdharau mama yake.” (Methali 15:20) Je, wazazi hawashangilii watoto wao wanapotenda kwa hekima? Ni kweli kwamba ili kupata matokeo hayo mazuri wazazi wanapaswa kuwazoeza na kuwatia nidhamu watoto wao. (Methali 22:6) Lakini mwana mwenye hekima huwafanya wazazi wake washangilie. Kwa upande mwingine, mwana mpumbavu huwaletea huzuni kubwa.

Akitumia neno ‘kushangilia’ katika maana nyingine, mfalme mwenye hekima anasema hivi: “Mtu ambaye amepungukiwa moyoni huonea shangwe upumbavu, lakini mtu mwenye utambuzi huenda mbele moja kwa moja.” (Methali 15:21) Wale waliopungukiwa moyoni hufurahia kicheko cha upumbavu na raha ambazo hazitokezi uradhi wala furaha ya kweli. Hata hivyo, mtu mwenye utambuzi huona upumbavu wa kuwa ‘mpenda raha badala ya kumpenda Mungu.’ (2 Timotheo 3:1, 4) Kushikamana na kanuni za Mungu humsaidia kuendelea kuwa mnyoofu na kunyoosha njia yake.

Wakati ‘Mambo Yanapotimizwa’

Kutii kanuni za Mungu huleta faida nyingi katika sehemu nyingine za maisha yetu. Andiko la Methali 15:22 linasema hivi: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.”

Mazungumzo ya siri yanamaanisha kuzungumza faraghani lakini waziwazi. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “mazungumzo ya siri” linatafsiriwa kuwa “kikundi cha rafiki za karibu” kwenye Zaburi 89:7. Hilo linaonyesha hali ya kuwasiliana kama marafiki wa karibu. Badala ya kuwa mazungumzo ya juujuu tu, mazungumzo ya siri ni kuelezana waziwazi mawazo na hisia za moyoni. Waume na wake zao na pia wazazi na watoto wao wanapowasiliana kwa uhuru kwa njia hiyo, wanakuwa na amani na umoja. Lakini kutokuwa na mazungumzo ya siri husababisha mfadhaiko na matatizo katika familia.

Tunapofanya maamuzi mazito, ni jambo la hekima kutii shauri hili: “Katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” Kwa mfano, tunapochagua matibabu fulani, je, si jambo la hekima kupata maoni ya daktari zaidi ya mmoja, hasa ikiwa masuala mazito yanahusika?

Kuna faida kubwa ya kuwa na washauri wengi wakati wa kushughulikia mambo ya kiroho. Wazee wa kutaniko wanaposhauriana na kutumia pamoja hekima yao, “mambo hutimizwa.” Isitoshe, waangalizi wapya hawapaswi kusita kuomba mashauri kutoka kwa wazee wenye umri mkubwa na wenye uzoefu zaidi, hasa ikiwa kisa kinachoshughulikiwa ni kigumu.

Wakati Ambapo Mtu “Hushangilia Jibu”

Maneno yanayosemwa kwa ufahamu yanaweza kuwa na matokeo gani mazuri? Mfalme wa Israeli anasema hivi: “Mtu hushangilia jibu la kinywa chake, nalo neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!” (Methali 15:23) Je, sisi hatushangilii wakati jibu au shauri letu linapofuatwa na matokeo yanakuwa mazuri? Hata hivyo, ili shauri letu liwe na matokeo mazuri, ni lazima litimize matakwa mawili.

Kwanza, shauri hilo linapaswa kutegemea kabisa Neno la Mungu, Biblia. (Zaburi 119:105; 2 Timotheo 3:16, 17) Kisha, linapaswa kutolewa kwa wakati unaofaa. Hata maneno ambayo ni ya kweli yanaweza kuwa na madhara yanaposemwa kwa wakati usiofaa. Kwa mfano, kumshauri mtu kabla ya kumsikiliza kabisa si jambo la hekima wala halisaidii sana. Kwa hivyo, ni muhimu tuwe ‘wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema.’—Yakobo 1:19.

“Njia ya Uzima Inaelekea Juu”

Andiko la Methali 15:24 linasema hivi: “Kwa yule anayetenda kwa ufahamu njia ya uzima inaelekea juu, ili kuliepuka Kaburi lililo chini.” Mtu anayetenda kwa ufahamu anaepuka njia ya Kaburi. Yeye huepuka mazoea yenye kudhuru kama vile ngono haramu, matumizi ya dawa za kulevya, na ulevi, na hivyo anaepuka kifo cha mapema. Njia yake inaelekea kwenye uzima.

Tofauti na hilo, ona njia ya wale wasiotenda kwa ufahamu: “Yehova ataibomoa nyumba ya watu waliojiinua, lakini atauweka imara mpaka wa mjane. Hila za mtu mbaya ni chukizo kwa Yehova, lakini maneno yenye kupendeza ni safi. Mtu anayepata faida isiyo ya haki anailetea nyumba yake mwenyewe taabu, lakini anayechukia zawadi [rushwa] ndiye atakayeendelea kuishi.”Methali 15:25-27.

Akituonyesha jinsi ya kuepuka kosa moja ambalo watu wengi hufanya, mfalme wa Israeli anasema hivi: “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu, lakini kinywa cha waovu hububujika mambo mabaya.” (Methali 15:28) Methali hiyo ina shauri zuri kama nini! Mara nyingi majibu ya kijinga na ya kipumbavu ambayo hububujika kutoka kinywani hayatokezi jambo lolote zuri. Tunapofikiria mambo fulani muhimu yanayohusika katika kisa fulani, kutia ndani hali na hisia za wengine, yaelekea hatutasema jambo lolote ambalo huenda tutajutia baadaye.

Hivyo basi, kuna faida gani ya kumwogopa Mungu na kukubali nidhamu yake? Mwenye hekima anajibu hivi: “Yehova yuko mbali sana na waovu, lakini huisikia sala ya waadilifu.” (Methali 15:29) Mungu wa kweli yuko mbali na waovu. Biblia inasema hivi: “Anayegeuzia mbali sikio lake asiisikie sheria—hata sala yake ni chukizo.” (Methali 28:9) Wale wanaomwogopa Mungu na kujitahidi kufanya yaliyo sawa machoni pake wanaweza kumkaribia kwa uhuru, wakiwa na uhakika wa kwamba atawasikiliza.

Kile Ambacho “Hufanya Moyo Ushangilie”

Akilinganisha mambo kwa njia ya kusisimua, Sulemani anasema hivi: “Kung’aa kwa macho hufanya moyo ushangilie; habari ambayo ni njema huifanya mifupa inone.” (Methali 15:30) Mifupa ‘hunona’ inapojaa urojorojo. Urojorojo huo huimarisha mwili wote na kufanya moyo ushangilie. Na shangwe ya moyo huonekana kwa kung’aa kwa macho. Hayo ndiyo matokeo ya habari njema!

Je, si kweli kwamba tunatiwa moyo kwelikweli na ripoti za ongezeko la ulimwenguni pote la ibada ya Yehova? Ripoti kuhusu yote yanayotimizwa katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi hutuchochea kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Habari zinazowahusu wale ambao wamemchagua Yehova kuwa Mungu wao na kujiunga na ibada ya kweli hujaza mioyo yetu kwa shangwe. Kwa kuwa “habari njema kutoka nchi ya mbali” ni yenye kuchochea sana, ni muhimu kutoa ripoti kwa usahihi na kwa unyoofu kuhusu yale tuliyotimiza katika huduma!—Methali 25:25.

“Kabla ya Utukufu Hutangulia Unyenyekevu”

Akikazia umuhimu wa kukubali nidhamu katika hali mbalimbali, mfalme mwenye hekima anasema: “Sikio linalosikiliza karipio la uzima hukaa kati ya watu wenye hekima. Yeyote anayeepuka nidhamu anaikataa nafsi yake mwenyewe, lakini anayesikiliza karipio anajipatia utambuzi wa moyo.” (Methali 15:31, 32) Karipio, au nidhamu, hugusa moyo wa mtu na kuurekebisha, na hivyo kumfanya awe mwenye busara. Haishangazi kwamba “fimbo ya nidhamu” ndiyo huondolea mbali ‘ujinga ambao umefungwa pamoja na moyo wa mvulana’! (Methali 22:15) Yule anayeisikiliza nidhamu hujipatia pia utambuzi wa moyo, yaani, nia nzuri. Kwa upande mwingine, kukataa nidhamu ni kukataa uzima.

Naam, kuna faida kutumia na kukubali nidhamu ya hekima kwa unyenyekevu. Kufanya hivyo hakuleti tu uradhi, maendeleo, shangwe, na mafanikio, bali pia hutokeza utukufu na uzima. Andiko la Methali 15:33 linamalizia hivi: “Kumwogopa Yehova ni nidhamu ya hekima, na kabla ya utukufu hutangulia unyenyekevu.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kwa maelezo zaidi kuhusu Methali 15:1-15, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2006, ukurasa wa 13-16.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Upendo katika familia ni bora kuliko kuwa na vyakula vingi vitamu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Hata ikiwa tuna udhaifu, kuwa na mtazamo mzuri hutusaidia kupata ujuzi

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mazungumzo ya siri ni kuelezana waziwazi mawazo na hisia za moyoni

[Picha katika ukurasa wa 20]

Je, unajua jinsi “habari ambayo ni njema huifanya mifupa inone”?