Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Tunajuaje kwamba ufafanuzi kuhusu hekima kwenye Methali 8:22-31 unamhusu Yesu Kristo kabla ya kuwa mwanadamu?

Ufafanuzi kuhusu hekima unaopatikana katika kitabu cha Methali na ambao uliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu, unasema: “Yehova mwenyewe alinitokeza nikiwa mwanzo wa njia yake, nikiwa wa mapema zaidi kati ya kazi zake za zamani za kale. . . . Kabla milima yenyewe haijawekwa, kabla ya vilima, nilitokezwa kana kwamba kwa uchungu wa kuzaa . . . Alipozitayarisha mbingu nilikuwako; . . . ndipo nilipokuwa kando yake nikiwa stadi wa kazi, nami nikawa yule ambaye yeye alimpenda sana kwa njia ya pekee siku baada ya siku, nami nikawa nikifurahi mbele zake wakati wote, . . . na vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.”

Andiko hilo haliwezi kuwa linazungumzia hekima inayotoka kwa Mungu au sifa ya hekima tu. Kwa nini? Kwa sababu hekima inayozungumziwa hapo ‘ilitokezwa,’ au kuumbwa, ikiwa ndiyo mwanzo wa njia ya Yehova. Yehova Mungu amekuwapo na amekuwa mwenye hekima sikuzote. (Zaburi 90:1, 2) Hekima yake haina mwanzo; haikuumbwa wala kutokezwa. ‘Haikutokezwa kana kwamba kwa uchungu wa kuzaa.’ Isitoshe, hekima hiyo inasemwa kuwa inazungumza na kutenda, ikiwakilisha mtu fulani.—Methali 8:1.

Kitabu cha Methali kinasema kwamba tangu zamani za kale hekima ilikuwa kando ya Yehova, Muumba, ikiwa “stadi wa kazi.” Bila shaka, maneno hayo yanamhusu Yesu. Muda mrefu kabla ya Yesu kuja duniani, alifanya kazi kwa ukaribu sana pamoja na Yehova hivi kwamba Neno la Mungu linasema: “Yeye ni wa kabla ya vitu vingine vyote na kwa njia yake vitu vingine vyote vilifanywa kuwapo.”—Wakolosai 1:17; Ufunuo 3:14.

Ni jambo linalofaa kumfananisha Mwana wa Mungu na hekima, kwa kuwa ni Yeye aliyefunua makusudi na maagizo yenye hekima ya Yehova. Kabla ya kuja duniani, Yesu alikuwa Neno la Mungu, au Msemaji wa Mungu. (Yohana 1:1) Anafafanuliwa kuwa “nguvu za Mungu na hekima ya Mungu.” (1 Wakorintho 1:24, 30) Huo ni ufafanuzi wenye kuvutia kama nini kuhusu Mwana wa Mungu, ambaye aliwapenda sana wanadamu hivi kwamba akatoa uhai wake kuwa fidia kwa ajili yao!—Yohana 3:16.

[Picha katika ukurasa wa 31]

“Kabla milima yenyewe haijawekwa, . . . nilitokezwa”