Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwogope Yehova, Uwe Mwenye Furaha!

Mwogope Yehova, Uwe Mwenye Furaha!

Mwogope Yehova, Uwe Mwenye Furaha!

“Mwenye furaha ni mtu anayemwogopa Yehova.”—ZABURI 112:1.

1, 2. Tunaweza kupata nini kwa kumwogopa Yehova?

FURAHA haipatikani kwa urahisi. Furaha ya kweli inategemea kufanya maamuzi yanayofaa, kutenda mema, na kuepuka mabaya. Muumba wetu, Yehova, ametupa Neno lake, Biblia, ili kutufundisha jinsi tunavyoweza kufurahia maisha. Tukitafuta na kufuata mwongozo wa Yehova, na hivyo kuonyesha kwamba tunamwogopa Mungu, tunaweza kupata uradhi na furaha ya kweli.—Zaburi 23:1; Methali 14:26.

2 Katika makala hii, tutachunguza mifano ya nyakati za Biblia na ya kisasa ambayo inaonyesha jinsi ambavyo kumwogopa Mungu kikweli humwezesha mtu kukataa kishawishi cha kutenda mabaya na kupata ujasiri wa kutenda mema. Tutaona kwamba kumwogopa Mungu kunaweza kutupa furaha kwa kutuchochea kujirekebisha, kama Mfalme Daudi alivyofanya. Pia tutaona kwamba kumwogopa Yehova ni urithi wenye thamani sana ambao wazazi wanaweza kuwapa watoto wao. Naam, Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Mwenye furaha ni mtu anayemwogopa Yehova.”—Zaburi 112:1.

Kupata Furaha Tena

3. Ni jambo gani lililomsaidia Daudi kurudia hali nzuri baada ya kutenda dhambi?

3 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, katika visa vitatu muhimu, Daudi alikosa kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa, naye akatenda dhambi. Hata hivyo, jinsi alivyotenda alipoadhibiwa na Yehova kulionyesha kwamba licha ya dhambi alizofanya, alikuwa mtu anayemwogopa Mungu. Kwa sababu alimstahi na kumheshimu Mungu alichochewa kukubali kwamba ana hatia, akajirekebisha, na kuwa tena na uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Ingawa Daudi na watu wengine waliumia kwa sababu ya makosa yake, Yehova aliendelea kumtegemeza na kumbariki kwa sababu alitubu kikweli. Bila shaka, mfano wa Daudi unaweza kuwaimarisha Wakristo ambao wanatumbukia katika dhambi nzito leo.

4. Kumwogopa Mungu kunaweza kumsaidiaje mtu kupata furaha tena?

4 Fikiria mfano wa Sonja. * Ingawa alikuwa mhubiri wa wakati wote, Sonja alianza kuwa na mashirika mabaya, akawa na mwenendo mbaya, na ikabidi atengwe na ushirika wa kutaniko la Kikristo. Sonja aliporudia fahamu zake, alifanya juu chini kurekebisha uhusiano wake pamoja na Yehova. Baada ya muda, alirudishwa katika kutaniko. Licha ya yote hayo, Sonja hakukata tamaa kumtumikia Yehova. Muda si muda, alianza tena utumishi wa wakati wote akiwa painia. Kisha, akaolewa na mzee Mkristo mwenye sifa nzuri, na sasa Sonja anafurahi kutumikia pamoja naye kutanikoni. Ingawa Sonja anajuta kwamba aliiacha njia ya Kikristo kwa muda, anafurahi kwamba kumwogopa Mungu kulimsaidia kurudi.

Ni Afadhali Kuteseka Kuliko Kutenda Dhambi

5, 6. Eleza jinsi Daudi alivyoepuka mara mbili kumuua Sauli na kwa nini alifanya hivyo.

5 Bila shaka, ni afadhali kuepuka kutenda dhambi kwa sababu ya kumwogopa Mungu. Daudi alifanya hivyo pia. Pindi moja, Sauli na wanajeshi elfu tatu walikuwa wakimfuata Daudi. Sauli aliingia ndani ya pango ambamo Daudi na watu wake walikuwa wamejificha. Watu wa Daudi walimhimiza amuue Sauli. Kwa maoni yao, Yehova alikuwa amemtia Sauli, adui yake mkubwa, mikononi mwake! Daudi alimnyemelea Sauli kimyakimya na kukata upindo wa vazi lake. Kwa kuwa Daudi alimwogopa Mungu, hata tendo hilo lililoonekana kuwa lisilodhuru lilichoma dhamiri yake. Daudi aliwatawanya watu wake wenye hasira, akisema hivi: “Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba nimfanyie bwana wangu jambo hili, mtiwa-mafuta wa Yehova.” *1 Samweli 24:1-7.

6 Katika pindi nyingine baadaye, Sauli alipiga kambi usiku. Yeye na watu wake ‘wakashikwa na usingizi mzito kutoka kwa Yehova.’ Daudi pamoja na mpwa wake mwenye ujasiri aliyeitwa Abishai walinyemelea mpaka katikati kabisa ya kambi na kusimama mahali ambapo Sauli alikuwa amelala. Abishai alitaka kumkatilia mbali Sauli. Lakini Daudi akamzuia Abishai, kwa kuuliza hivi: “Ni nani amepata kunyoosha mkono wake juu ya mtiwa-mafuta wa Yehova, naye akabaki bila hatia?”—1 Samweli 26:9, 12.

7. Ni jambo gani lililomzuia Daudi asitende dhambi?

7 Kwa nini Daudi hakutumia nafasi hizo mbili kumuua Sauli? Kwa sababu alimwogopa Yehova kuliko Sauli. Kwa sababu ya kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa, Daudi alikuwa tayari kuteseka badala ya kutenda dhambi. (Waebrania 11:25) Aliamini kabisa kwamba Yehova huwatunza watu Wake na kwamba atamtunza. Daudi alijua kwamba angepata furaha na baraka nyingi kwa kumtii na kumtegemea Mungu, na kwamba ikiwa angempuuza Mungu basi angekosa kibali chake. (Zaburi 65:4) Pia, Daudi alijua kwamba Mungu angetimiza ahadi Yake ya kumfanya awe mfalme na kwamba angemwondoa Sauli asiwe mfalme kwa wakati wake na kwa njia yake.—1 Samweli 26:10.

Kumwogopa Mungu Hutokeza Furaha

8. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Daudi alivyotenda alipokabili mkazo?

8 Tukiwa Wakristo, tunaweza kutarajia kudhihakiwa, kuteswa, na kupatwa na majaribu mengine. (Mathayo 24:9; 2 Petro 3:3) Nyakati nyingine, tunaweza hata kupatwa na matatizo kwa sababu ya waabudu wenzetu. Hata hivyo, tunajua kwamba Yehova huona mambo yote, husikiliza sala zetu na, kwa wakati unaofaa, atanyoosha mambo kulingana na mapenzi yake. (Waroma 12:17-21; Waebrania 4:16) Hivyo, badala ya kuwaogopa wapinzani wetu, sisi humwogopa Mungu na kutarajia atukomboe. Kama Daudi, sisi hatulipizi kisasi wala hatuvunji kanuni za uadilifu ili kuepuka kuteseka. Mwishowe, kufanya hivyo hutokeza furaha. Jinsi gani?

9. Toa mfano kuonyesha jinsi kumwogopa Mungu kunavyoweza kutokeza furaha licha ya mateso.

9 Mmishonari mmoja ambaye ametumikia kwa muda mrefu barani Afrika anasema hivi: “Ninakumbuka mama mmoja na binti yake ambao walikataa kununua kadi za chama cha kisiasa kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Walishambuliwa kwa ukatili na umati wa wanaume, kisha wakaambiwa waende nyumbani. Walipokuwa wakitembea, mama huyo alijaribu kumfariji binti yake aliyekuwa akilia kwa kuwa hakuelewa sababu ya kushambuliwa. Ingawa wakati huo hawakuwa na shangwe, walikuwa na dhamiri safi. Baadaye, walifurahi sana kwamba walimtii Mungu. Ikiwa wangenunua kadi za chama hicho, basi umati ungeshangilia sana. Wanaume hao wangewapa soda na kucheza dansi wakiwa wamewazunguka mpaka nyumbani kwao. Lakini msichana huyo na mama yake wangehuzunika sana kwa sababu ya kutoshikamana na msimamo wao.” Naam, waliepuka huzuni hiyo kwa sababu walimwogopa Mungu.

10, 11. Mwanamke mmoja alipata matokeo gani mazuri kwa sababu ya kumwogopa Mungu?

10 Kumwogopa Mungu hutokeza furaha pia wakati tunapokabili majaribu yanayohusiana na kuheshimu utakatifu wa uhai. Mary alipokuwa akitarajia kujifungua mtoto wake wa tatu, daktari alimsihi atoe mimba. Daktari huyo alisema hivi: “Maisha yako yamo hatarini. Afya yako inaweza kudhoofika wakati wowote na unaweza kufa katika kipindi cha saa 24. Halafu mtoto huyo anaweza kufa pia. Vyovyote vile, siwezi kuhakikisha kwamba mtoto huyo atakuwa timamu.” Mary alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova lakini hakuwa amebatizwa. Mary anasema hivi: “Hata hivyo, nilikuwa nimeamua kumtumikia Yehova na kuendelea kumtii vyovyote iwavyo.”—Kutoka 21:22, 23.

11 Alipokuwa mjamzito, Mary aliendelea kujifunza Biblia kwa bidii na kutunza familia yake. Mwishowe, akapata mtoto. Mary anasema hivi: “Tofauti na ilivyokuwa wakati nilipojifungua mtoto wa kwanza na wa pili, wakati huu ilikuwa vigumu zaidi kujifungua, lakini sikukabili matatizo makubwa.” Kumwogopa Mungu kulimsaidia Mary kuwa na dhamiri safi, na baada ya muda akabatizwa. Mtoto huyo alipoendelea kukua, yeye pia alijifunza kumwogopa Yehova, na sasa anatumikia kwenye ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova.

‘Jitie Nguvu kwa Yehova’

12. Daudi aliimarishwaje kwa kumwogopa Mungu?

12 Kumwogopa Yehova hakukumzuia tu Daudi asitende dhambi. Kulimwimarisha achukue hatua na kutenda kwa hekima katika hali ngumu. Kwa muda wa mwaka mmoja na miezi minne, Daudi na watu wake walikimbilia Siklagi, katika maeneo ya mashambani ya Ufilisti, ili kumwepuka Sauli. (1 Samweli 27:5-7) Wakati mmoja ambapo wanaume hao walikuwa wameondoka, Waamaleki walishambulia na kuliteketeza jiji na kuchukua wake wote wa wanaume hao, watoto, na mifugo yao yote. Daudi na watu wake waliporudi na kuona kile kilichotukia, walilia sana. Kwa ghafula, huzuni yao ikageuka kuwa hasira, na watu wa Daudi wakataka kumpiga Daudi kwa mawe. Ingawa Daudi alitaabishwa na jambo hilo, hakuvunjika moyo. (Methali 24:10) Alimtegemea Yehova kwa sababu alimwogopa, naye “akajitia nguvu kwa Yehova.” Kwa msaada wa Mungu, Daudi na watu wake waliwafuata Waamaleki na kukomboa vitu vyote vilivyoporwa.—1 Samweli 30:1-20.

13, 14. Kumwogopa Mungu kulimsaidiaje Mkristo mmoja kufanya maamuzi yanayofaa?

13 Leo pia, watumishi wa Mungu hukabili hali zinazohitaji wamtegemee Yehova na kuwa na ujasiri wa kuchukua hatua. Fikiria mfano wa Kristina. Alipokuwa kijana, Kristina alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Lakini alitaka kuwa mchezaji wa piano kwenye maonyesho ya muziki, naye alifanya maendeleo makubwa kuufikia mradi wake. Isitoshe, aliogopa kuhubiri na alihofia madaraka ambayo angepata kwa kubatizwa. Kristina alipoendelea kujifunza Neno la Mungu, alianza kutambua kwamba lina nguvu. Alikuwa akijifunza kumwogopa Yehova, naye alitambua kwamba Yehova anatarajia watumishi wake wampende kwa moyo wao wote, akili yao yote, nafsi yao yote, na nguvu zao zote. (Marko 12:30) Hilo lilimchochea ajiweke wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

14 Kristina alimwomba Yehova msaada ili afanye maendeleo ya kiroho. Kristina anasema hivi: “Nilijua kwamba kwa kawaida mtu anayecheza piano kwenye maonyesho ya muziki husafiri sana, naye hucheza piano kwenye maonyesho 400 hivi kila mwaka. Hivyo, niliamua kuwa mwalimu ili kupata riziki na kuwa mhubiri wa wakati wote.” Wakati huo, tayari Kristina alikuwa amepangiwa kushiriki kwa mara ya kwanza kwenye maonyesho ya muziki yaliyofanywa katika jumba maarufu zaidi la maonyesho nchini kwao. Anasema hivi: “Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza na ya mwisho kushiriki maonyesho ya muziki.” Sasa Kristina ameolewa na mzee Mkristo. Kwa sasa, wanatumikia kwenye ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Kristina anafurahi kwamba Yehova alimpa nguvu za kufanya maamuzi yanayofaa na kwamba sasa anaweza kutumia wakati na nguvu zake kumtumikia.

Urithi Wenye Thamani

15. Daudi alitaka kuwapa watoto wake nini, naye alifanyaje hivyo?

15 Daudi aliandika hivi: “Njooni, enyi wana, nisikilizeni; nitawafundisha kumwogopa Yehova.” (Zaburi 34:11) Akiwa baba, Daudi alikusudia kuwapa watoto wake urithi wenye thamani, yaani, kumwogopa Yehova kikweli kwa njia inayofaa. Kwa maneno na kwa matendo, Daudi alionyesha kwamba Yehova si Mungu anayedai mengi mno, anayeogopesha, na aliye tayari kuwaadhibu wale wanaovunja sheria Zake, bali ni Baba mwenye upendo, anayejali, na anayewasamehe watoto Wake walio duniani. Daudi aliuliza hivi: “Makosa—ni nani anayeweza kuyatambua?” Kisha, akionyesha uhakika wake kwamba Yehova hachunguzi makosa yetu kila wakati, aliongeza hivi: “Unitangaze kuwa sina hatia ya dhambi zilizofichwa.” Daudi alikuwa na uhakika kwamba ikiwa angejitahidi awezavyo, basi maneno na mawazo yake yangempendeza Yehova.—Zaburi 19:12, 14.

16, 17. Wazazi wanaweza kuwafundishaje watoto kumwogopa Yehova?

16 Daudi ni mfano kwa wazazi leo. Ralph, ambaye anatumikia pamoja na ndugu yake kwenye ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, anasema hivi: “Wazazi wetu walifanya tuifurahie kweli. Tulipokuwa wadogo, walitushirikisha katika mazungumzo yao kuhusu utendaji wa kutaniko, nasi tukaichangamkia kweli kama wao. Walitusadikisha kwamba tunaweza kufanya mambo yenye faida katika utumishi wa Yehova. Kwa miaka kadhaa, familia yetu iliishi katika nchi yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme na kusaidia kuanzisha makutaniko mapya.

17 “Tulisaidiwa kubaki katika njia inayofaa, si kwa sababu ya sheria nyingi ngumu, bali kwa sababu wazazi wetu walimwona Yehova kuwa halisi, mwenye fadhili nyingi sana, na mwema. Wazazi wetu walijitahidi kumjua Yehova vizuri zaidi na kumpendeza, nasi tukaiga jinsi walivyomwogopa Mungu kikweli na kumpenda. Hata tulipokosea, wazazi wetu hawakutufanya tuhisi kwamba Yehova hatupendi, wala hawakutuwekea vizuizi vingi mno. Mara nyingi, walizungumza nasi kwa upole wakijaribu kufikia mioyo yetu, na katika nyakati nyingine kama hizo Mama alitokwa na machozi. Jitihada zao zilifanikiwa. Kupitia kwa maneno na matendo ya wazazi wetu, tulijifunza kwamba inapendeza kumwogopa Yehova na kwamba kuwa mmoja wa Mashahidi wake si mzigo mzito, bali ni jambo linalofurahisha.”—1 Yohana 5:3.

18. Tutapata nini tukimwogopa Mungu wa kweli?

18 Tunasoma hivi katika “maneno ya mwisho ya Daudi”: “Wakati yeye anayetawala juu ya wanadamu ni mwadilifu, akitawala kwa kumwogopa Mungu, basi ni kama nuru ya asubuhi, jua linapoangaza.” (2 Samweli 23:1, 3, 4) Inaonekana Sulemani, ambaye alikuwa mwana wa Daudi na mtawala aliyemfuata, alielewa maana ya maneno hayo kwa kuwa alimwomba Yehova ampe “moyo mtiifu” na uwezo wa ‘kutambua kati ya mema na mabaya.’ (1 Wafalme 3:9) Sulemani alitambua kwamba kumwogopa Yehova ni jambo la hekima na la kufurahisha. Baadaye, Sulemani alitoa muhtasari wa kitabu cha Mhubiri kwa maneno haya: “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu. Kwa maana Mungu wa kweli ataleta kila kazi katika hukumu, kuhusiana na kila jambo lililofichwa, liwe jema au baya.” (Mhubiri 12:13, 14) Tukitii shauri hilo, tutajionea kwamba “matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova” si hekima na furaha tu, bali pia ni “utajiri na utukufu na uzima.”—Methali 22:4.

19. Ni jambo gani litakalotusaidia kuelewa “kumwogopa Yehova”?

19 Kupitia mifano iliyo katika Biblia na mifano ya kisasa, tunatambua kwamba watumishi wa kweli wa Yehova hufaidika wanapomwogopa Mungu kwa njia inayofaa. Kumwogopa Yehova hakutuzuii tu tusifanye mambo yanayomchukiza Baba yetu wa mbinguni, bali pia kunatupa ujasiri wa kukabili adui zetu na nguvu za kuvumilia majaribu na matatizo. Hivyo, acheni sisi, vijana kwa wazee, tujifunze Neno la Mungu kwa bidii, tutafakari mambo tunayojifunza, na kumkaribia Yehova kwa ukawaida katika sala zinazotoka moyoni. Tukifanya hivyo, zaidi ya “kumjua Mungu,” tutaelewa pia “kumwogopa Yehova.”—Methali 2:1-5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 5 Huenda hilo ni jambo moja ambalo lilimchochea Daudi kutunga Zaburi ya 57 na ya 142.

Je, Unaweza Kueleza?

Ni kwa njia gani kumwogopa Mungu kunaweza

• kumsaidia mtu kurudia hali nzuri baada ya kutenda dhambi nzito?

• kutokeza furaha tunapokabili majaribu na mateso?

• kutuimarisha kufanya mapenzi ya Mungu?

• kuwa urithi wenye thamani kwa watoto wetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kumwogopa Yehova kulimzuia Daudi asimshambulie Mfalme Sauli

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kumwogopa Mungu ni urithi wenye thamani ambao wazazi wanaweza kuwapa watoto wao