Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Wakati Vizuri kwa Kuwa Huwezi Kuuhifadhi

Tumia Wakati Vizuri kwa Kuwa Huwezi Kuuhifadhi

Tumia Wakati Vizuri kwa Kuwa Huwezi Kuuhifadhi

WAKATI ni pesa. Huo ni msemo unaotumiwa sana. Kwa kweli, wakati ni tofauti sana na pesa au mali nyingine. Tofauti na pesa, chakula, mafuta, au vitu vingine, huwezi kuhifadhi wakati ili uutumie baadaye. Ni kazi bure kujaribu kuhifadhi wakati bila kuutumia. Itakuwaje ukilala muda wa saa nane na kujaribu kuhifadhi saa zilizobaki kwa kutofanya chochote? Mwishowe, saa ambazo hukutumia zinatoweka milele.

Wakati unaweza kulinganishwa na mto mkubwa unaotiririka kwa kasi. Mto huo unasonga mbele daima. Huwezi kuusimamisha wala kutumia kila tone la maji yake. Karne nyingi zilizopita, watu walianza kutengeneza magurudumu yanayozungushwa na maji kwenye kingo za mito. Waliyatumia kupata nishati kutokana na maji yaliyotiririka ili kuendesha mashini za kusagia, mashini za kupasua mbao, mabomba, na nyundo. Vivyo hivyo, unaweza kupata wakati ili uutumie kutimiza kazi nzuri bali si kuuhifadhi. Hata hivyo, ili ufanye hivyo ni lazima upambane na wezi wawili wakubwa wa wakati, yaani, kuahirisha mambo na kuwa na mambo mengi ya kufanya. Acheni tuzungumze kwanza kuhusu kuahirisha mambo.

Epuka Kuahirisha Mambo

Kuna watu wanaosema kwamba, Hupaswi kuahirisha hadi kesho jambo unaloweza kufanya leo. Lakini watu wengine hawafuati shauri hilo. Wanapokabili kazi ngumu, wao hujaribu kuiepuka kwa kuahirisha mambo. Kulingana na kamusi moja, neno “ahirisha” linamaanisha ‘kuchelewesha jambo kwa makusudi ili lifanyike baadaye.’ Mtu anayeahirisha mambo amezoea kufanya hivyo. Mkazo unapoongezeka, yeye hujituliza kwa kuahirisha kazi hiyo na kufurahi kwamba amepata “wakati wa ziada.” Lakini furaha hiyo hudumu mpaka wakati mkazo unapozidi tena.

Nyakati nyingine, huenda hali yetu ya kimwili na ya kihisia ikahitaji tuahirishe baadhi ya kazi zetu au hata kazi zote. Isitoshe, kila mtu anahitaji pia kupumzika mara kwa mara. Hata Mwana wa Mungu alipumzika. Yesu alikuwa na shughuli nyingi katika huduma yake, lakini alikuwa pia na pindi za kupumzika pamoja na wanafunzi wake. (Marko 6:31, 32) Kuna faida kupumzika. Hata hivyo, kuahirisha mambo ni tofauti na mara nyingi hutokeza madhara. Fikiria mfano huu.

Tuseme mwanafunzi fulani atafanya mtihani wa hesabu baada ya majuma matatu. Msichana huyo anahitaji kusoma vitabu vingi kabla ya mtihani. Hivyo, anahisi amekazwa. Anashawishiwa kuahirisha mambo, naye ananaswa na mtego huo. Badala ya kusoma, anatazama televisheni. Siku baada ya siku, anaahirisha mambo anayopaswa kufanya ili kufaulu mtihani. Hatimaye, usiku kabla ya mtihani, anakabiliwa na kazi ngumu ya kusoma mambo yote mara moja. Akiwa ameketi mezani, anaanza kupitia-pitia vitabu vyake.

Anatumia muda mrefu akisoma. Wakati ambapo watu wengine wa familia wanalala, msichana huyo anajilazimisha kukariri njia mbalimbali za kushughulikia hesabu. Akiwa shuleni siku inayofuata, anapambana na maswali magumu huku akili yake ikiwa imechoka. Anapata alama za chini na hivyo anaanguka mtihani huo. Analazimika kurudia somo hilo na huenda asiruhusiwe kwenda darasa la juu.

Mwanafunzi huyo amepata hasara kubwa kwa sababu ya kuahirisha mambo. Lakini kuna kanuni ya Biblia inayoweza kuwasaidia watu kuepuka hali kama ya msichana huyo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa.” (Waefeso 5:15, 16) Paulo alikuwa akiwahimiza Wakristo kutumia wakati wao kwa hekima katika utendaji wa Kikristo, lakini kanuni hiyo inaweza kutusaidia katika shughuli nyingi maishani. Kwa kuwa mara nyingi tunaweza kuamua wakati tutakapofanya kazi fulani, tutapata matokeo mazuri zaidi na tutafanya kazi hiyo haraka zaidi kwa kuianza kwa “wakati unaofaa.” Kama andiko hilo linavyoonyesha, “watu wenye hekima” hufanya hivyo.

Ni ‘wakati gani ambapo ingefaa’ mwanafunzi huyo aanze kujitayarishia mtihani huo wa hesabu? Labda angejifunza hatua kwa hatua somo hilo kila jioni kwa muda wa dakika 15 hivi. Hivyo, hangehitaji kujifunza mambo mengi usiku kabla ya mtihani, wakati ambapo angekuwa amelala. Siku ya mtihani, angekuwa amepumzika vya kutosha na tayari kabisa kwa ajili ya mtihani, na huenda angefaulu.

Hivyo, ukipewa kazi ya kufanya, ona ni ‘wakati gani unaofaa’ kuifanya na uifanye. Hivyo, utaepuka mtego wa kuahirisha mambo na matokeo yake. Pia, utapata uradhi kwa sababu umefanya kazi hiyo vizuri. Hilo ni muhimu hasa ikiwa kazi yako itawaathiri watu wengine, kama vile migawo katika kutaniko la Kikristo.

Punguza Mambo ya Kufanya

Kama ilivyotajwa awali, jambo la pili la kufanya ili kutumia vizuri wakati wetu ni kuepuka kuwa na mambo mengi ya kufanya. Tunajua kwamba inachukua wakati kushughulikia vitu, kuvipanga, kuvitumia, kuvisafisha, kuvihifadhi, na kuvitafuta. Tukiwa na vitu vingi tunahitaji pia wakati mwingi zaidi. Kufanya kazi katika chumba au nyumba iliyojaa vitu kunachukua wakati mwingi zaidi na kunafadhaisha kuliko kufanya kazi mahali pasipokuwa na vitu vingi. Isitoshe, kadiri vitu vinavyorundamana ndivyo inavyochukua wakati mwingi zaidi kupata kitu kinachohitajiwa.

Watu wenye ujuzi wa kusafisha nyumba husema kwamba karibu nusu ya wakati unaotumiwa katika usafishaji hupotea bure wakati wanapojaribu “kuondoa na kuepuka kugonga vitu na takataka zilizo njiani.” Huenda hilo ni kweli kuhusu hali nyingine maishani. Kwa hiyo, ukitaka kutumia wakati wako vizuri, chunguza mazingira yako. Je, una vitu vingi sana ambavyo vinachukua nafasi, vinakuzuia usitembee kwa uhuru na, hata kupoteza wakati wako? Ikiwa ndivyo, punguza vitu hivyo.

Huenda isiwe rahisi kuondoa vitu fulani. Inaweza kuwa vigumu kutupa vitu visivyohitajiwa ambavyo tunapenda sana. Ni kama kufiwa na rafiki tunayempenda sana. Hivyo, unaweza kuamuaje ikiwa utahifadhi kitu fulani au utakiondoa? Wengine wanatumia kanuni hii. Ikiwa hujakitumia kitu fulani kwa muda wa mwaka mmoja, basi kiondolee mbali. Namna gani ikiwa bado unasitasita kukiondoa baada ya mwaka mmoja? Kiondoe na kukiweka pamoja na vitu vingine mahali fulani kwa muda wa miezi sita. Utakapokitazama kwa mara nyingine na kutambua kwamba mwaka mmoja na nusu umepita bila wewe kukitumia, huenda ikawa rahisi zaidi kwako kukiondolea mbali. Vyovyote vile, mradi ni kupunguza vitu, yaani, kutumia wakati wako vizuri zaidi.

Bila shaka, si nyumbani au kazini tu ambako kunaweza kuwa na msongamano wa vitu. Yesu alisema kuhusu “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri” ambazo zinaweza ‘kulisonga neno’ la Mungu na kumzuia mtu ‘asizae matunda’ kuhusiana na habari njema. (Mathayo 13:22) Mtu anaweza kuwa na shughuli nyingi sana maishani hivi kwamba inakuwa vigumu kwake kuwa na usawaziko na kupata wakati unaohitajiwa kutimiza mambo muhimu zaidi ya kiroho. Matokeo ni kwamba huenda akadhoofika kiroho na mwishowe kukosa kabisa kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa, ambako kutakuwa na wakati daima wa kutimiza mambo yanayoleta uradhi na furaha ya kweli.—Isaya 65:17-24; 2 Petro 3:13.

Je, unajikuta mara nyingi ukijaribu kuingiza katika ratiba yako mambo yote ambayo unahisi unapaswa kuyatimiza, iwe yanahusu kazi yako, nyumba, gari, tafrija, safari, mazoezi ya mwili, matukio katika jamii, au mambo mengine mengi? Ikiwa ndivyo, huenda huu ndio wakati wa kufikiria jinsi ya kupunguza mambo ya kufanya ili utumie wakati mwingi zaidi kutimiza mambo ya kiroho.

Msemo mwingine ni, Wakati haumngoji mtu. Kwa kweli, wakati unasonga mbele kama mto. Hauwezi kurudi nyuma wala kuhifadhiwa; ukitoweka, unatoweka milele. Hata hivyo, kwa kufuata kanuni fulani rahisi za Biblia na kuchukua hatua chache muhimu, tunaweza kupata wakati tunaohitaji ili kutimiza “mambo yaliyo ya maana zaidi” ambayo yatatuletea faida za milele na “utukufu na sifa kwa Mungu.”—Wafilipi 1:10, 11.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kama mto unaotiririka kwa kasi, wakati unaweza kutumiwa ili kutimiza kazi nzuri

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ni ‘wakati gani ambapo ingefaa’ mwanafunzi huyu ajitayarishie mtihani?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Inachukua wakati mwingi na inachosha kufanya kazi mahali palipojaa vitu