Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Mwenye Hekima—mwogope Mungu!

Uwe Mwenye Hekima—mwogope Mungu!

Uwe Mwenye Hekima—mwogope Mungu!

“Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima.”—METHALI 9:10.

1. Kwa nini watu wengi huona ni vigumu kuelewa wazo la kumwogopa Mungu?

KUNA wakati ambapo watu walifurahia kusifiwa kwamba wanamwogopa Mungu. Leo, watu wengi huona kwamba wazo la kumwogopa Mungu limepitwa na wakati na kwamba halieleweki kwa urahisi. Huenda wakauliza hivi, ‘Ikiwa Mungu ni upendo, kwa nini nimwogope?’ Kwa maoni yao, woga ni hisia isiyofaa, inayomfanya mtu awe hoi. Hata hivyo, kama tutakavyoona, kumwogopa Mungu kikweli kunahusisha mambo mengi, bali si hisia tu.

2, 3. Kumwogopa Mungu kikweli kunahusisha nini?

2 Katika Biblia, wazo la kumwogopa Mungu linavutia. (Isaya 11:3) Kumwogopa Mungu ni kumstahi na kumheshimu sana Mungu, ni tamaa kubwa ya kuepuka kumchukiza. (Zaburi 115:11) Kunatia ndani kukubali na kushikamana na kanuni za Mungu za maadili na kutamani kuishi kulingana na maoni ya Mungu kuhusu mema au mabaya. Kitabu kimoja kinasema kwamba woga huo unaofaa unaonyesha “mtazamo muhimu sana kumhusu Mungu ambao unamwongoza mtu kutenda kwa hekima na kuepuka aina zote za uovu.” Hiyo ndiyo sababu Neno la Mungu hutuambia hivi: “Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima.”—Methali 9:10.

3 Naam, kumwogopa Mungu kunahusiana na sehemu nyingi za maisha ya wanadamu. Zaidi ya kuhusiana na hekima, kumwogopa Mungu kunahusiana pia na shangwe, amani, mafanikio, maisha marefu, tumaini, na uhakika. (Zaburi 2:11; Methali 1:7; 10:27; 14:26; 22:4; 23:17, 18; Matendo 9:31) Kunahusiana sana na imani na upendo. Naam, kumwogopa Mungu kunahusiana na mambo yote yanayohusika katika uhusiano wetu pamoja na Mungu na wanadamu wenzetu. (Kumbukumbu la Torati 10:12; Ayubu 6:14; Waebrania 11:7) Kumwogopa Mungu kunahusisha kusadiki kabisa kwamba Baba yetu wa mbinguni anamjali kila mmoja wetu na yuko tayari kutusamehe makosa yetu. (Zaburi 130:4) Ni waovu wasiotubu tu ambao wana sababu ya kutetemeka mbele za Mungu. *Waebrania 10:26-31.

Kujifunza Kumwogopa Yehova

4. Ni nini kinachoweza kutusaidia ‘kujifunza kumwogopa Yehova’?

4 Kwa kuwa ni muhimu sana tumwogope Mungu ili tufanye maamuzi kwa hekima na kupata baraka zake, tunaweza ‘kujifunzaje kumwogopa Yehova’ kwa njia inayofaa? (Kumbukumbu la Torati 17:19) Mifano mingi ya wanaume na wanawake waliomwogopa Mungu imeandikwa katika Maandiko “ili kutufundisha sisi.” (Waroma 15:4) Ili kutusaidia kuelewa maana kamili ya kumwogopa Mungu, acheni tuzungumzie maisha ya mtu mmoja kati ya hao, yaani, Mfalme Daudi wa Israeli la kale.

5. Kazi ya uchungaji ilimsaidiaje Daudi kujifunza kumwogopa Yehova?

5 Yehova alimkataa Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli, kwa sababu ya kuwaogopa watu na kwa sababu ya kutomwogopa Mungu. (1 Samweli 15:24-26) Kwa upande mwingine, maisha ya Daudi na uhusiano wake wa karibu pamoja na Yehova yalionyesha kwamba alimwogopa Mungu kikweli. Tangu alipokuwa mdogo, mara nyingi Daudi alienda nje kulisha kondoo za baba yake. (1 Samweli 16:11) Haikosi kwamba pindi ambazo Daudi alitumia kuchunga kondoo usiku huku kukiwa na nyota zilimsaidia kuelewa maana ya kumwogopa Yehova. Ingawa Daudi angeweza kuona sehemu ndogo tu ya mfumo wa nyota, alikata kauli inayofaa kwamba Mungu anastahili kuheshimiwa na kuabudiwa. Baadaye, aliandika hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini, na mwana wa mtu wa udongo hivi kwamba umtunze?”—Zaburi 8:3, 4.

6. Daudi alihisije alipotambua ukuu wa Yehova?

6 Daudi alistaajabu alipolinganisha udogo wake na ukuu wa mbingu zinazoonekana. Badala ya kumwogopesha, ujuzi huo ulimchochea kumsifu Yehova na kusema: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.” (Zaburi 19:1) Kumstahi Mungu kwa njia hiyo kulimfanya Daudi amkaribie Yehova zaidi na kulimchochea atake kujifunza na kufuata njia Zake kamilifu. Hebu wazia jinsi Daudi alivyohisi alipomwimbia Yehova hivi: “Wewe ni mkuu na unafanya mambo ya ajabu; wewe ni Mungu, wewe peke yako. Unifundishe, Ee Yehova, juu ya njia yako. Nitatembea katika kweli yako. Unganisha moyo wangu ili kuliogopa jina lako.”—Zaburi 86:10, 11.

7. Kumwogopa Mungu kulimsaidiaje Daudi kupigana na Goliathi?

7 Wafilisti waliposhambulia nchi ya Israeli, shujaa wao Goliathi mwenye urefu wa futi tisa na nusu, aliwadhihaki Waisraeli. Ni kana kwamba alisema hivi: ‘Nipeni mwanamume wa kupigana naye! Akishinda, tutawatumikia.’ (1 Samweli 17:4-10) Sauli na jeshi lake lote waliogopa, lakini Daudi hakuogopa. Daudi alijua kwamba Yehova ndiye anayepaswa kuogopwa, bali si mwanadamu, hata awe na nguvu nyingi kadiri gani. Daudi alimwambia Goliathi hivi: “Mimi naja kwako nikiwa na jina la Yehova wa majeshi . . . . Na kutaniko hili lote watajua kwamba Yehova haokoi kwa upanga wala kwa mkuki, kwa sababu vita ni vya Yehova.” Kwa msaada wa Yehova, Daudi aliliua jitu hilo akitumia kombeo na jiwe moja tu.—1 Samweli 17:45-47.

8. Tunajifunza nini kutokana na mifano inayotajwa katika Biblia kuhusu watu waliomwogopa Mungu?

8 Kama Daudi, labda tunakabili vizuizi au maadui wenye kuogopesha. Tunaweza kufanya nini? Tunaweza kushughulikia hali hizo kama Daudi na waaminifu wengine wa kale, yaani, kwa kumwogopa Mungu. Kumwogopa Mungu kunaweza kutusaidia tusiwaogope wanadamu. Nehemia, mtumishi mwaminifu wa Mungu, aliwahimiza hivi Waisraeli wenzake ambao walikuwa wakikabili upinzani: “Msiogope kwa sababu yao. Mkumbukeni Yehova, Yeye ambaye ni mkuu na Mwenye kuogopesha.” (Nehemia 4:14) Daudi, Nehemia, na watumishi wengine waaminifu wa Mungu walifanikiwa kutimiza kazi walizopewa na Mungu kwa sababu Mungu aliwasaidia. Tukimwogopa Mungu, hata sisi tutafanikiwa.

Kukabili Matatizo kwa Kumwogopa Mungu

9. Daudi alionyesha kwamba anamwogopa Mungu akiwa chini ya hali gani?

9 Baada ya Daudi kumuua Goliathi, Yehova alimpa ushindi mwingine mbalimbali. Hata hivyo, Sauli mwenye wivu alijaribu kumuua Daudi. Kwanza, alifanya hivyo bila kupangia, kisha, akatumia ujanja, na hatimaye, akatumia jeshi. Ingawa Yehova alikuwa amemhakikishia Daudi kwamba angekuwa mfalme, kwa miaka mingi Daudi alilazimika kukimbia, kupigana, na kungojea wakati wa Yehova wa kumtawaza kuwa mfalme. Licha ya majaribu yote hayo, Daudi alionyesha kwamba anamwogopa Mungu wa kweli.—1 Samweli 18:9, 11, 17; 24:2.

10. Daudi alipokabili hatari, alionyeshaje kwamba anamwogopa Mungu?

10 Wakati fulani, Daudi alikimbilia kwa Akishi, mfalme wa jiji la Gathi la Wafilisti, ambako Goliathi aliishi. (1 Samweli 21:10-15) Watumishi wa mfalme huyo walimshutumu Daudi kuwa adui wa taifa lao. Daudi alitendaje alipokabili hali hiyo hatari? Alisali kwa Yehova na kumweleza mambo waziwazi. (Zaburi 56:1-4, 11-13) Ingawa ilimbidi Daudi ajifanye kuwa mwenda-wazimu ili aponyoke, alitambua kwamba Yehova ndiye aliyemkomboa kwa kubariki jitihada zake. Kwa kumtegemea Yehova kwa moyo wote na kumwamini, Daudi alionyesha kwamba anamwogopa Mungu.—Zaburi 34:4-6, 9-11.

11. Kama Daudi, tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamwogopa Mungu wakati tunapokabili jaribu?

11 Kama Daudi, tunaweza kuonyesha kwamba tunamwogopa Mungu kwa kuamini ahadi yake ya kutusaidia kukabiliana na matatizo. Daudi alisema hivi: “Mkabidhi Yehova njia yako, na kumtegemea, naye mwenyewe atatenda.” (Zaburi 37:5) Hilo halimaanishi kwamba tumwachie Yehova matatizo yetu bila kujitahidi kuyatatua, huku tukitarajia kwamba atatusaidia. Daudi hakukaa kitako baada ya kumwomba Mungu msaada. Alitumia uwezo wa kimwili na wa kiakili ambao alipewa na Yehova ili kushughulikia tatizo lake. Hata hivyo, Daudi alijua kwamba wanadamu hawawezi kufanikiwa wanapotegemea jitihada zao tu. Sisi pia tunapaswa kufanya hivyo. Baada ya kujitahidi tuwezavyo, tunapaswa kumwachia Yehova matatizo yetu. Naam, mara nyingi hatuwezi kufanya lolote ila kumtegemea Yehova. Huo ndio wakati wa kuonyesha kwamba tunamwogopa Mungu. Tunaweza kufarijiwa na maneno haya ya Daudi aliyoyasema kutoka moyoni: “Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomwogopa.”—Zaburi 25:14.

12. Kwa nini tunapaswa kuchukua kwa uzito sala zetu, nasi hatupaswi kamwe kuwa na mtazamo gani?

12 Basi, tunapaswa kuchukua kwa uzito sala zetu na uhusiano wetu pamoja na Mungu. Tunaposali kwa Yehova, lazima ‘tuamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.’ (Waebrania 11:6; Yakobo 1:5-8) Na anapotusaidia, tunapaswa ‘kujionyesha kuwa wenye shukrani,’ kama mtume Paulo alivyotushauri. (Wakolosai 3:15, 17) Hatupaswi kamwe kuwa kama watu ambao walitajwa na Mkristo mmoja mtiwa-mafuta mwenye uzoefu mwingi: “Watu fulani wanadhani kwamba Mungu ni kama mhudumu wa hoteli. Wanapohitaji kitu, wanatoa ishara fulani ya kumwita. Na wakiisha kupata kile wanachohitaji, wanataka aondoke.” Huo si mtazamo wa kumwogopa Mungu.

Wakati Ambapo Daudi Hakumwogopa Mungu

13. Ni wakati gani ambapo Daudi hakuiheshimu Sheria ya Mungu?

13 Daudi alipoona Yehova akimsaidia wakati wa taabu, hilo lilimfanya amwogope Yehova zaidi na kumwamini zaidi. (Zaburi 31:22-24) Hata hivyo, katika visa vitatu vya pekee, Daudi hakumwogopa Mungu, na hilo lilisababisha msiba. Kisa cha kwanza ni wakati ambapo alipanga sanduku la agano la Yehova lisafirishwe kwa gari la kukokotwa hadi Yerusalemu badala ya kuwatumia Walawi kulibeba juu ya mabega yao, kama Sheria ya Mungu ilivyoagiza. Uza ndiye aliyeliendesha gari hilo. Wakati alipolishika Sanduku ili kuzuia lisianguke, alikufa papo hapo kwa sababu ya “tendo [hilo] lisilo la heshima kwa Mungu.” Naam, Uza alitenda dhambi nzito, lakini msiba huo ulitukia hasa kwa sababu Daudi hakuiheshimu Sheria ya Mungu. Kumwogopa Mungu kunamaanisha kufanya mambo kwa njia yake.—2 Samweli 6:2-9; Hesabu 4:15; 7:9.

14. Matokeo yalikuwa nini baada ya Daudi kuhesabu Israeli?

14 Baadaye, Daudi alichochewa na Shetani kuhesabu idadi ya wanaume wa vita wa Israeli. (1 Mambo ya Nyakati 21:1) Kwa kufanya hivyo, Daudi alionyesha kwamba hakumwogopa Mungu wakati huo, na hilo likasababisha kifo cha Waisraeli 70,000. Ingawa Daudi alitubu mbele za Yehova, yeye na watu wake waliteseka sana.—2 Samweli 24:1-16.

15. Ni jambo gani lililomfanya Daudi atumbukie katika dhambi ya uzinzi?

15 Tena, kwa sababu ya kutomwogopa Mungu kwa muda fulani, Daudi alifanya uzinzi pamoja na Bath-sheba, mke wa Uria. Daudi alijua kwamba ni kosa kufanya uzinzi au hata kumtamani mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine. (Kutoka 20:14, 17) Tatizo lilianza wakati Daudi alipomwona Bath-sheba akioga. Kumwogopa Mungu kikweli kungemchochea Daudi aache papo hapo kumtazama Bath-sheba na badala yake afikirie mambo mengine. Lakini, inaonekana Daudi ‘aliendelea kumtazama’ Bath-sheba mpaka tamaa yake ikamfanya asimwogope Mungu. (Mathayo 5:28; 2 Samweli 11:1-4) Daudi alisahau kwamba Yehova ndiye aliyekuwa akiongoza maisha yake yote.—Zaburi 139:1-7.

16. Daudi alipatwa na nini kwa sababu ya dhambi yake?

16 Daudi na Bath-sheba walipata mwana kupitia uhusiano wao haramu. Muda mfupi baadaye, Yehova alimtuma nabii wake Nathani ili afunue dhambi ya Daudi. Aliporudia fahamu zake, Daudi alianza tena kumwogopa Mungu, naye akatubu. Alimsihi Yehova asimtupilie mbali wala asimnyang’anye roho Yake takatifu. (Zaburi 51:7, 11) Yehova alimsamehe Daudi na kupunguza adhabu ambayo angepata, lakini Hakumkinga kutokana na matokeo yote mabaya ya matendo yake. Mwana wa Daudi alikufa, na kuanzia wakati huo familia yake ikapatwa na huzuni na misiba. Hayo ni matokeo mabaya kama nini ya kutomwogopa Mungu kwa muda fulani!—2 Samweli 12:10-14; 13:10-14; 15:14.

17. Toa mfano kuonyesha huzuni inayosababishwa na kutenda dhambi.

17 Leo, tunaweza pia kupata matokeo mabaya sana na ya kudumu tusipomwogopa Mungu katika mambo ya maadili. Hebu wazia jinsi mke mmoja kijana alivyoumia hisia alipogundua kwamba mume wake Mkristo hakuwa mwaminifu kwake alipoenda kufanya kazi katika nchi nyingine. Huku akiwa amejiinamisha chini kwa sababu ya huzuni na kushtuka, mke huyo alifunika uso wake kwa mikono yake na kulia sana. Hebu wazia muda ambao ungepita kabla ya mke huyo kuanza tena kumwamini na kumheshimu mume wake! Matokeo hayo mabaya yanaweza kuepukwa kwa kumwogopa Mungu kikweli.—1 Wakorintho 6:18.

Kumwogopa Mungu Hutuzuia Tusitende Dhambi

18. Shetani ana lengo gani, naye anatumia mbinu gani?

18 Shetani anapotosha maadili ya ulimwengu haraka sana, naye hasa anataka kuwapotosha Wakristo wa kweli. Ili kufanya hivyo, yeye hutumia njia ambayo inafika moja kwa moja katika mioyo na akili zetu, yaani, anatumia hisi zetu, hasa hisi ya kuona na ya kusikia. (Waefeso 4:17-19) Utafanya nini ikiwa bila kutarajia unaona picha za ngono, unasikia maneno machafu, au unajipata katikati ya watu wenye maadili yaliyopotoka?

19. Kumwogopa Mungu kulimsaidiaje Mkristo mmoja kushinda kishawishi?

19 Fikiria kisa cha André *, ambaye ni mzee Mkristo, baba, na daktari huko Ulaya. Wakati André alipokuwa akifanya kazi usiku wote hospitalini, mara nyingi wafanyakazi wenzake wanawake walibandika kadi zilizochorwa maumbo ya moyo kwenye kitanda chake, ili kumshawishi afanye ngono pamoja nao. André alikataa katakata kushawishiwa. Isitoshe, alitafuta kazi mahali pengine ili aondoke katika mazingira hayo mabaya. Kwa kuwa André alimwogopa Mungu, alifanya jambo la hekima lililomletea baraka. Leo, yeye ni mfanyakazi wa muda kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi ya kwao.

20, 21. (a) Kumwogopa Mungu kunaweza kutusaidiaje kuepuka kutenda dhambi? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

20 Kuendelea kufikiria mambo yasiyofaa kunaweza kumfanya mtu awe tayari kutupilia mbali uhusiano wake wenye thamani pamoja na Yehova ili kufanya tendo haramu. (Yakobo 1:14, 15) Lakini ikiwa tunamwogopa Yehova, tutaepuka watu, mahali, shughuli, na burudani ambazo zinaweza kuharibu maadili yetu, na hata kuondoka tunapokuwa katika hali kama hizo. (Methali 22:3) Huenda tukaaibika au kujinyima mambo fulani, lakini ni afadhali kufanya hivyo kuliko kupoteza kibali cha Mungu. (Mathayo 5:29, 30) Naam, kumwogopa Mungu kunahusisha kuepuka kuona kimakusudi kitu chochote kilichopotoka, kutia ndani ponografia (picha au habari za ngono), na badala yake kuyafanya macho yetu “yapite ili yasione jambo lisilofaa.” Tukifanya hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ‘atatuhifadhi hai’ na kutupa kila kitu tunachohitaji.—Zaburi 84:11; 119:37.

21 Naam, kumwogopa Mungu ni jambo la hekima sikuzote. Pia, ni chanzo cha furaha ya kweli. (Zaburi 34:9) Hilo litaonyeshwa wazi katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona makala “Maoni ya Biblia: Unaweza Kumhofuje Mungu wa Upendo?” katika gazeti la Amkeni! la Januari 8, 1998, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 19 Jina limebadilishwa.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni sifa gani za Kikristo zinazohusika katika kumwogopa Mungu?

• Kumwogopa Mungu kunamsaidiaje mtu asiwaogope wanadamu?

• Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna maoni yanayofaa kuhusu sala?

• Kumwogopa Mungu kunaweza kutuzuiaje tusitende dhambi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Daudi alijifunza kumwogopa Mungu kwa kutazama uumbaji wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 24]

Utafanya nini ukikabili kishawishi bila kutarajia?