Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanadamu Wote Wanaweza Kuheshimiwa

Wanadamu Wote Wanaweza Kuheshimiwa

Wanadamu Wote Wanaweza Kuheshimiwa

“Ni lazima tufanyize ulimwengu mpya, ulio bora, ambamo haki ya binadamu ya kuheshimiwa daima itatimizwa.”—RAIS WA MAREKANI HARRY TRUMAN, SAN FRANCISCO, CALIFORNIA, MAREKANI, APRILI 25, 1945.

KAMA watu wengi wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Rais Truman aliamini kwamba mwanadamu anaweza kujifunza kutokana na mambo ambayo yamempata na kufanyiza “ulimwengu mpya” ambamo watu wote wataheshimiwa. Inasikitisha kwamba mambo hayako hivyo leo. “Haki ya binadamu ya kuheshimiwa daima” inaendelea kukandamizwa kwa sababu tatizo hilo linasababishwa hasa na adui mkubwa wa binadamu.

Yule Anayesababisha Tatizo Hilo

Biblia inamtambulisha adui huyo kuwa Shetani Ibilisi, kiumbe mwovu wa roho, ambaye tangu mwanzo wa historia ya mwanadamu, ametilia shaka haki ya Mungu ya kutawala. Tangu Shetani alipozungumza na Hawa katika bustani ya Edeni, lengo lake limekuwa kuwafanya wanadamu waache kumtumikia Muumba wao. (Mwanzo 3:1-5) Fikiria jinsi Adamu na Hawa walivyoathiriwa waliposikiliza shauri la Ibilisi! Kwa sababu ya kutotii amri ya Mungu kuhusu matunda yaliyokatazwa, wote wawili ‘walijificha kutoka mbele za uso wa Yehova Mungu.’ Kwa nini? Adamu alisema: “Niliogopa kwa sababu nilikuwa uchi, na basi nikajificha.” (Mwanzo 3:8-10) Uhusiano wa Adamu pamoja na Baba yake wa mbinguni ulibadilika na maoni yake kujihusu yakabadilika pia. Aliona aibu, naye hakuwa tena na uhuru wa kuwa mbele za Yehova.

Kwa nini Ibilisi alitaka Adamu aache kujiheshimu? Kwa sababu mwanadamu ameumbwa kwa mfano wa Mungu, na Shetani anafurahia kuona mwanadamu akitenda kwa njia isiyoonyesha utukufu wa Mungu. (Mwanzo 1:27; Waroma 3:23) Hilo linatusaidia kuelewa ni kwa nini historia ya mwanadamu imejaa matendo yenye kushusha heshima. Akiwa “mungu wa mfumo huu wa mambo,” Shetani ameendeleza roho hiyo katika kipindi ambacho “mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (2 Wakorintho 4:4; Mhubiri 8:9; 1 Yohana 5:19) Je, hiyo inamaanisha kwamba heshima ya kweli ambayo mwanadamu anastahili kupata haitakuwapo kamwe?

Yehova Huheshimu Viumbe Wake

Fikiria tena jinsi hali ilivyokuwa katika bustani ya Edeni kabla ya Adamu na Hawa kutenda dhambi. Walikuwa na chakula kingi, kazi yenye kuridhisha, na tumaini la kuishi milele wakiwa na afya nzuri pamoja na watoto wao. (Mwanzo 1:28) Kila sehemu ya maisha yao ilionyesha kusudi la Mungu lenye upendo ambalo linawawezesha wanadamu kuheshimiwa.

Je, Yehova aliacha kuwaheshimu wanadamu baada ya Adamu na Hawa kutenda dhambi? Hapana. Aliwajali kwa sababu sasa waliona aibu kuwa uchi. Kwa upendo, Mungu aliandaa “mavazi marefu ya ngozi” badala ya majani ya mtini ambayo walikuwa wamejishonea ili kufunika viuno vyao. (Mwanzo 3:7, 21) Badala ya kuwaacha katika hali hiyo yenye kuaibisha, Mungu aliwatendea kwa heshima.

Baadaye, alipokuwa akishughulika na taifa la Israeli, Yehova aliwahurumia mayatima, wajane, na wakaaji wageni, ambao mara nyingi hudharauliwa katika jamii. (Zaburi 72:13) Kwa mfano, walipovuna nafaka, mizeituni, na zabibu, Waisraeli waliambiwa wasirudi kuchukua masalio. Badala yake, Mungu aliamuru kwamba masalio hayo ‘yakae kwa ajili ya mkaaji mgeni, kwa ajili ya mvulana asiye na baba na kwa ajili ya mjane.’ (Kumbukumbu la Torati 24:19-21) Amri hiyo ilipofuatwa, walio maskini sana hawakuhitaji kuomba-omba, nao walifanya kazi iliyoheshimiwa.

Yesu Aliwaheshimu Wengine

Alipokuwa duniani, Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliwaheshimu wengine. Kwa mfano, alipokuwa Galilaya, mtu mmoja aliyejaa ukoma alimkaribia. Kulingana na Sheria ya Musa, ili kuepuka kuambukiza wengine, mtu mwenye ukoma alipaswa kupaaza sauti hivi: “Si safi, si safi!” (Mambo ya Walawi 13:45) Hata hivyo, mtu huyo hakupaaza sauti alipomkaribia Yesu. Badala yake, alijiangusha kifudifudi na kumwomba Yesu hivi: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” (Luka 5:12) Yesu alitendaje? Yesu hakumkemea mtu huyo kwa kuvunja Sheria, wala Hakumpuuza wala kumwepuka. Badala yake, alimheshimu mtu huyo mwenye ukoma kwa kumgusa na kumwambia: “Nataka. Takasika.”—Luka 5:13.

Katika pindi nyinginezo, Yesu alionyesha uwezo wake wa kumponya mtu bila kumgusa. Nyakati nyingine aliwaponya watu akiwa mbali. Hata hivyo, katika kisa hiki aliamua kumgusa mtu huyo. (Mathayo 15:21-28; Marko 10:51, 52; Luka 7:1-10) Kwa kuwa mtu huyo “alijaa ukoma,” bila shaka hakuwa ameguswa na mtu yeyote kwa miaka mingi. Lazima alifarijika sana kuguswa tena na mtu mwingine baada ya muda mrefu! Hakutazamia kuguswa bali alitaka kuponywa tu. Lakini njia ambayo Yesu alitumia kumponya ilimsaidia mtu huyo kuhisi kwamba anaheshimiwa. Je, tunaweza kuamini kwamba inawezekana kuwaheshimu wengine hivyo leo? Ikiwa inawezekana, heshima hiyo itaonyeshwaje?

Kanuni Inayowachochea Watu Kuheshimiana

Yesu alisema maneno ambayo wengi wanayaona kuwa mafundisho maarufu zaidi yaliyowahi kutolewa kuhusu mahusiano ya wanadamu. Alisema hivi: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Kanuni hiyo humchochea mtu kumheshimu mwingine, akitarajia kuheshimiwa pia.

Uthibitisho unaonyesha kwamba si rahisi kufuata kanuni hiyo kwa kuwa mara nyingi watu hutenda kinyume. Mtu mmoja tutakayemwita Harold anasema: “Nilifurahia kuwadharau wengine. Nilitumia maneno machache tu kuwakera, kuwaaibisha, na hata nyakati nyingine kuwafanya walie.” Lakini jambo fulani lilimchochea Harold aache kuwatendea wengine vibaya. “Mashahidi wa Yehova kadhaa walianza kunitembelea. Mimi huaibika ninapokumbuka mambo niliyowaambia na jinsi nilivyowatendea nyakati nyingine. Lakini hawakuvunjika moyo, na kweli ya Biblia iligusa moyo wangu hatua kwa hatua, nayo ikanichochea kubadilika.” Leo, Harold ni mzee katika kutaniko la Kikristo.

Kisa cha Harold kinathibitisha kwamba “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Neno la Mungu lina nguvu inayogusa moyo wa mtu na kubadili kufikiri kwake na mwenendo wake. Hiyo ndiyo siri ya kuwaheshimu wengine, yaani, tamaa ya kutoka moyoni ya kutaka kuwasaidia wengine badala ya kuwaumiza, na kuwaheshimu badala ya kuwadharau.—Matendo 20:35; Waroma 12:10.

Heshima Inayofaa Yarudishwa

Tamaa hiyo ndiyo huwachochea Mashahidi wa Yehova kuwaambia wengine kuhusu tumaini zuri la Biblia. (Matendo 5:42) Hakuna njia bora zaidi ya kumheshimu mtu kuliko kumwambia “habari njema za jambo bora.” (Isaya 52:7) “Jambo bora” linatia ndani kuvaa “utu mpya” ambao utaiua “tamaa yenye madhara” ya kuwadharau wengine. (Wakolosai 3:5-10) Pia, linatia ndani kusudi la Yehova la kuondoa hali na mielekeo inayowazuia watu wasiheshimiwe, na vilevile kumwondoa Shetani Ibilisi ambaye ndiye chanzo cha mambo hayo. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 20:1, 2, 10) Wakati huo, ambapo dunia “itajawa na kumjua Yehova,” ndipo tu wanadamu wote watakapoheshimiwa.—Isaya 11:9.

Tunakualika ujifunze kuhusu tumaini hilo zuri. Kwa kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, utaelewa kwamba kutumia kanuni za Biblia humsaidia mtu kuwaheshimu wengine. Utajifunza pia jinsi Ufalme wa Mungu utakavyofanyiza ‘ulimwengu mpya na ulio bora,’ ambamo “haki ya binadamu ya kuheshimiwa daima” itatimizwa bila kukandamizwa tena.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Walidumisha Heshima Yao kwa Kuwa Watimilifu

Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 2,000 walipelekwa katika kambi za mateso za utawala wa Nazi kwa sababu ya imani yao. Baada ya kuona jinsi walivyoonyesha utimilifu wao kwa njia ya pekee sana, Gemma La Guardia Gluck, aliyekuwa mfungwa katika jela ya Ravensbrück, aliandika hivi katika kitabu chake (My Story): “Wakati mmoja polisi wa siri wa Nazi walitangaza kwamba Mwanafunzi yeyote wa Biblia ambaye angetia sahihi hati iliyoonyesha kwamba ameikana imani yake angeachiliwa huru na hangeendelea kuteswa.” Kuhusu wale waliokataa kutia sahihi hati hiyo, aliandika hivi: “Waliona afadhali waendelee kuteseka huku wakingoja ulimwengu mpya kwa subira.” Kwa nini waliamua kufanya hivyo? Sasa, Magdalena aliyetajwa katika utangulizi wa makala ya kwanza ana miaka zaidi ya 80, naye anasema hivi: “Kuwa mwaminifu kwa Yehova kulikuwa muhimu sana kuliko kufanya chochote ili kuendelea kuishi. Kujiheshimu kulimaanisha kudumisha utimilifu wetu.” *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 23 Kwa habari zaidi kuhusu familia ya Kusserow, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1985 (Kiingereza), ukurasa wa 10-15.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yesu aliwaheshimu wale aliowaponya

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mashahidi wa Yehova huwaheshimu wengine kwa kuwahubiria “habari njema za jambo bora”