Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ayubu—Mtu Mvumilivu na Mtimilifu

Ayubu—Mtu Mvumilivu na Mtimilifu

Ayubu—Mtu Mvumilivu na Mtimilifu

“Je, umeuweka moyo wako juu ya mtumishi wangu Ayubu, kwamba hakuna yeyote aliye kama yeye duniani, mtu asiye na lawama na mnyoofu, mwenye kumwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya?”—AYUBU 1:8.

1, 2. (a) Ayubu alipatwa na misiba gani? (b) Eleza jinsi maisha ya Ayubu yalivyokuwa kabla ya misiba hiyo.

MTU fulani alikuwa na vitu vingi vizuri, yaani, mali, umashuhuri, afya nzuri, na familia yenye furaha. Kisha, akapatwa na misiba mara tatu mfululizo. Alipoteza mali zake zote kwa ghafula. Baadaye, dhoruba isiyo ya kawaida ilisababisha kifo cha watoto wake wote. Muda mfupi baada ya hapo, akaugua ugonjwa wenye kudhoofisha uliotokeza majipu yenye maumivu makali kwenye mwili wake wote. Huenda unajua kwamba mtu huyo alikuwa Ayubu, anayezungumziwa hasa katika kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina lake.—Ayubu, sura ya 1 na ya 2.

2 Ayubu aliomboleza hivi: “Laiti ningekuwa kama nilivyokuwa katika miezi ya zamani.” (Ayubu 3:3; 29:2) Msiba unapotokea, kila mtu hutamani siku zilizopita. Ayubu aliishi maisha mazuri kana kwamba alikuwa amelindwa kutokana na mabaya. Watu mashuhuri walimheshimu na kutafuta mashauri kutoka kwake. (Ayubu 29:5-11) Ingawa alikuwa tajiri, alikuwa na maoni yanayofaa kuhusu pesa. (Ayubu 31:24, 25, 28) Aliwasaidia wajane na mayatima waliokuwa na uhitaji. (Ayubu 29:12-16) Naye alikuwa mwaminifu kwa mke wake.—Ayubu 31:1, 9, 11.

3. Yehova alimwonaje Ayubu?

3 Ayubu hakuwa na lawama kwa sababu alimwabudu Mungu. “Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani,” Yehova akasema, “mtu asiye na lawama na mnyoofu, mwenye kumwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.” (Ayubu 1:1, 8) Lakini, ingawa Ayubu alifuata maadili, misiba ilisambaratisha maisha yake. Kila kitu alichokuwa nacho kilitoweka, na sifa zake zilijaribiwa na uchungu mwingi aliohisi, maumivu yake ya kihisia, na kuvunjika moyo.

4. Kwa nini tutafaidika kwa kuchunguza majaribu ambayo Ayubu alikabili?

4 Bila shaka, kuna wengi miongoni mwa watumishi wa Mungu ambao wameteseka kama Ayubu. Leo, Wakristo wengi wanateseka, na hivyo wanaweza kuelewa hali iliyompata Ayubu. Hivyo, tunapaswa kufikiria maswali haya mawili: Kuchunguza majaribu ambayo Ayubu alikabili kunaweza kutusaidiaje tunapokabili msiba? Na majaribu hayo yanaweza kutusaidiaje kuwahurumia wengine wanapoteseka?

Suala la Ushikamanifu na Jaribu la Utimilifu

5. Shetani alidai kwamba Ayubu alimtumikia Mungu kwa sababu gani?

5 Kisa cha Ayubu kilikuwa cha pekee. Bila Ayubu kujua, Ibilisi alikuwa ametilia shaka kusudi la Ayubu la kumtumikia Mungu. Katika mkutano uliofanyiwa mbinguni, Yehova alitaja sifa nzuri za Ayubu, naye Shetani akajibu hivi: “Je, wewe hukuweka ukuta kumzunguka yeye na kuzunguka nyumba yake na kuzunguka kila kitu alicho nacho pande zote?” Hivyo, Shetani alidai kwamba Ayubu alichochewa na ubinafsi, na hivyo dai hilo likatia ndani watumishi wengine wote wa Mungu. Shetani alimwambia Yehova hivi: “Tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kila kitu alicho nacho, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.”—Ayubu 1:8-11.

6. Shetani alizusha suala gani muhimu?

6 Hilo lilikuwa suala muhimu. Shetani alitilia shaka njia ya Yehova ya kutawala. Je, kweli inawezekana Mungu autawale ulimwengu kwa upendo? Au kama vile Shetani alivyodokeza, je, sikuzote ubinafsi utafanikiwa? Yehova alimruhusu Ibilisi amjaribu Ayubu huku akiwa na uhakika kwamba mtumishi Wake angedumisha utimilifu na ushikamanifu, na jaribu hilo likawa mfano. Hivyo, Shetani ndiye aliyesababisha matatizo yaliyompata Ayubu kwa mfululizo. Shetani aliposhindwa katika mashambulizi yake ya kwanza, alimpiga Ayubu kwa ugonjwa wenye maumivu makali. Ibilisi alidai hivi: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.”—Ayubu 2:4.

7. Ni kwa njia gani watumishi wa Mungu leo hukabili majaribu kama ya Ayubu?

7 Ingawa Wakristo wengi leo hawateseki kama Ayubu, wanakabili dhiki za aina mbalimbali. Wengi wao hukabili mateso au matatizo ya familia. Pia, matatizo ya kiuchumi au magonjwa yanaweza kulemea. Baadhi yao wamekufa kwa sababu ya imani yao. Bila shaka, hatupaswi kufikiri kwamba kila tatizo tunalokabili husababishwa na Shetani. Huenda matatizo mengine yakasababishwa na makosa yetu au hali tuliyorithi. (Wagalatia 6:7) Sisi sote huathiriwa na uzee na misiba ya asili. Biblia inaeleza waziwazi kwamba leo Yehova hawalindi kimuujiza watumishi wake wasipatwe na matatizo hayo.—Mhubiri 9:11.

8. Shetani anaweza kutumiaje matatizo tunayokabili?

8 Hata hivyo, huenda Shetani akatumia matatizo tunayokabili ili kudhoofisha imani yetu. Mtume Paulo alitaja kwamba alisumbuliwa na “mwiba katika mwili, malaika wa Shetani,” aliyeendelea kumpiga “kofi.” (2 Wakorintho 12:7) Iwe alikuwa na matatizo ya afya, kama vile matatizo ya macho au tatizo lingine, Paulo alijua kwamba Shetani angetumia matatizo hayo na matokeo yake ili kumnyang’anya shangwe na utimilifu wake. (Methali 24:10) Leo, huenda Shetani akawachochea watu wa familia, wanashule, au hata serikali za kimabavu kuwatesa watumishi wa Mungu kwa njia fulani.

9. Kwa nini hatupaswi kushangaa sana tunapokabili shida au mateso?

9 Tunaweza kukabilianaje na matatizo hayo kwa mafanikio? Tunaweza kufanikiwa tukiyaona kuwa njia ya kuthibitisha kwamba tunampenda Yehova na tunajitiisha chini ya utawala wake. (Yakobo 1:2-4) Hata matatizo yetu yawe yanasababishwa na nini, kuelewa maana ya kuwa mshikamanifu kwa Mungu kutatusaidia tuendelee kuwa thabiti kiroho. Mtume Petro aliwaandikia Wakristo hivi: “Wapendwa, msishangazwe juu ya moto unaowaka katikati yenu, unaowapata ninyi ili kuwa jaribu, kana kwamba jambo geni linawapata.” (1 Petro 4:12) Naye Paulo akaeleza hivi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Bado Shetani anatilia shaka utimilifu wa Mashahidi wa Yehova, kama alivyofanya katika kisa cha Ayubu. Biblia inaonyesha kwamba Shetani amezidisha mashambulizi yake juu ya watu wa Mungu hasa katika hizi siku za mwisho.—Ufunuo 12:9, 17.

Kutoelewa Mambo na Mashauri Mabaya

10. Ayubu alikabili tatizo gani?

10 Ayubu alikabili tatizo ambalo hatuhitaji kukabili. Hakujua kwa nini alipatwa na misiba. Ayubu alikata kauli kimakosa kwamba “Yehova [alitoa], na Yehova [alichukua].” (Ayubu 1:21) Huenda Shetani alijaribu kimakusudi kumfanya Ayubu aamini kwamba Mungu ndiye aliyesababisha mateso yake.

11. Eleza jinsi Ayubu alivyotenda alipoteseka.

11 Ayubu alivunjika moyo sana, lakini alikataa kumlaani Mungu kama mke wake alivyomsihi afanye. (Ayubu 2:9, 10) Alisema hivi: ‘Waovu wanafanikiwa sana kuliko mimi.’ (Ayubu 21:7-9) Haikosi aliwaza hivi: ‘Kwa nini Mungu ananiadhibu?’ Wakati mwingine alitamani kufa. Alisema hivi: “Laiti ungenificha katika Kaburi, kwamba ungenificha mpaka hasira yako igeuke!”—Ayubu 14:13.

12, 13. Maneno ya wale marafiki watatu wa Ayubu yalimwathirije?

12 Marafiki watatu walimtembelea Ayubu ili ‘wamsikitikie na kumfariji.’ (Ayubu 2:11) Lakini, walithibitika kuwa “wafariji wasumbufu.” (Ayubu 16:2) Huenda Ayubu angefaidika ikiwa angepata marafiki ambao angewaeleza matatizo yake, lakini wafariji hao watatu walimfanya Ayubu achanganyikiwe hata zaidi na kukata tamaa zaidi.—Ayubu 19:2; 26:2.

13 Huenda Ayubu alijiuliza hivi: ‘Kwa nini mimi niteseke? Nimefanya nini ili niteseke hivi?’ Marafiki wake walimpa majibu yenye kupotosha kabisa. Waliwazia kwamba Ayubu alikuwa ametenda dhambi fulani nzito na ndiyo sababu alikuwa anateseka. “Je, ni nani aliyepata kuangamia bila hatia?” Elifazi akauliza. “Kulingana na yale ambayo nimeona, wale wanaotunga madhara na wale wanaopanda taabu wataivuna wenyewe.”—Ayubu 4:7, 8.

14. Kwa nini hatupaswi kuhusianisha kuteseka na mwenendo usiofaa?

14 Ni kweli kwamba matatizo yanaweza kutokea ikiwa tunapanda kwa mwili badala ya kupanda kwa roho. (Wagalatia 6:7, 8) Hata hivyo, katika mfumo huu wa sasa, tunaweza kupatwa na matatizo hata mwenendo wetu uweje. Isitoshe, hatuwezi kusema kwamba wasio na hatia hawawezi kupatwa na msiba. Ingawa Yesu Kristo hakuwa na ‘unajisi na alitengwa kutoka kwa watenda-dhambi,’ bado alikufa kwa maumivu juu ya mti wa mateso, na mtume Yakobo alifia imani. (Waebrania 7:26; Matendo 12:1, 2) Elifazi na marafiki wake wawili walifikiri kimakosa na hivyo kumfanya Ayubu ajitetee na kusisitiza kwamba hakuwa na hatia. Lakini, huenda madai yao ya ukaidi kwamba Ayubu alistahili kuteseka yaliathiri maoni yake kuhusu haki ya Mungu.—Ayubu 34:5; 35:2.

Kutafuta Msaada Tunapokabili Dhiki

15. Tunapoteseka, inafaa tuwe na maoni gani?

15 Tunajifunza nini kutokana na yaliyompata Ayubu? Huenda tukahisi kwamba hatustahili kupatwa na misiba, magonjwa, au mateso. Ni kana kwamba watu wengine hawateseki. (Zaburi 73:3-12) Wakati mwingine, huenda tukahitaji kujiuliza maswali haya muhimu: ‘Je, upendo wangu kwa Mungu unanichochea nimtumikie hata hali ziweje? Je, ninatamani kumpa Yehova “jibu kwa yule anayemdhihaki?”’ (Methali 27:11; Mathayo 22:37) Tusiruhusu kamwe mambo ambayo watu wanasema bila kufikiri yatufanye tumtilie shaka Baba yetu wa mbinguni. Dada mmoja mwaminifu aliyeugua ugonjwa wa kudumu kwa miaka mingi alisema hivi wakati fulani: “Najua kwamba ninaweza kuvumilia chochote ambacho Yehova anaruhusu. Najua atanipa nguvu ninazohitaji. Sikuzote amenipa nguvu.”

16. Neno la Mungu huwasaidiaje wale walio na matatizo?

16 Tofauti na Ayubu, sisi tunaelewa vizuri zaidi ujanja wa Shetani. “Hatukosi kuzijua mbinu zake,” au hila zake mbovu. (2 Wakorintho 2:11) Isitoshe, tuna chanzo cha hekima nyingi. Katika Biblia, tunapata masimulizi ya wanaume na wanawake waaminifu waliovumilia matatizo ya aina yote. Mtume Paulo, aliyeteseka zaidi kuliko wengine wengi, aliandika hivi: “Kwa maana mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) Shahidi mmoja huko Ulaya ambaye alifungwa kwa sababu ya imani yake wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, alitoa chakula chake cha siku tatu ili apate Biblia. Anasema: “Nilifaidika sana kwa kufanya hivyo! Licha ya njaa ya kimwili, nilipokea chakula cha kiroho kilichoniimarisha mimi pamoja na wengine katika majaribu yetu wakati huo wa taabu. Nimeitunza Biblia hiyo mpaka leo.”

17. Ni maandalizi gani kutoka kwa Mungu yanayoweza kutusaidia kuvumilia?

17 Mbali na faraja kutoka katika Maandiko, tuna vifaa vingi vinavyotusaidia kuielewa Biblia na vinavyotoa mwongozo unaofaa ili kukabiliana na shida. Ukitumia Watch Tower Publications Index, yaelekea utapata masimulizi ya Mkristo ambaye amepatwa na jaribu kama lako. (1 Petro 5:9) Pia, unaweza kufaidika ukiwaeleza wazee wenye huruma au Wakristo wengine wakomavu kuhusu hali yako. Zaidi ya yote, unaposali, unaweza kupata msaada kutoka kwa Yehova na roho yake takatifu. Paulo aliyakabilije ‘makofi’ ya Shetani? Kwa kujifunza kutegemea nguvu za Mungu. (2 Wakorintho 12:9, 10) Aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:13.

18. Wakristo wenzetu wanaweza kututiaje moyo sana?

18 Kwa hiyo, kuna msaada, nawe usisite kuutafuta. Methali moja inasema: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Kama vile mchwa wanavyoweza kuiangusha nyumba ya mbao, ndivyo kuvunjika moyo kunavyoweza kudhoofisha utimilifu wa Mkristo. Ili kushinda hatari hiyo, Yehova anatuandalia msaada kupitia watumishi wenzetu. Usiku ambao Yesu alikamatwa, malaika alimtokea na kumtia nguvu. (Luka 22:43) Akisafiri kuelekea Roma akiwa mfungwa, Paulo ‘alimshukuru Mungu na kujipa moyo’ alipokutana na akina ndugu katika Soko la Apio na Mikahawa Mitatu. (Matendo 28:15) Shahidi mmoja Mjerumani bado anakumbuka msaada aliopata alipofika katika kambi ya mateso ya Ravensbrück akiwa kijana mwoga mwenye umri wa chini ya miaka 20. Anasema hivi: “Mkristo mwenzangu aliniona mara moja na kunikaribisha kwa uchangamfu. Dada mwingine mwaminifu alinitunza, naye akawa kama mama yangu wa kiroho.”

“Uwe Mwaminifu”

19. Ni nini kilichomsaidia Ayubu kupinga jitihada za Shetani?

19 Yehova alimtaja Ayubu kuwa mtu ‘aliyeshikilia sana utimilifu wake.’ (Ayubu 2:3) Licha ya kuvunjika moyo na kutoelewa chanzo cha matatizo yake, Ayubu aliendelea kuwa imara kuhusiana na suala muhimu la ushikamanifu. Ayubu alikataa kuacha utimilifu wake. Alisisitiza hivi: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!”—Ayubu 27:5.

20. Kwa nini sifa ya uvumilivu ni muhimu?

20 Azimio kama hilo litatusaidia kudumisha utimilifu wetu chini ya hali zozote, tuwe tunakabili vishawishi, upinzani, au taabu. Yesu aliliambia kutaniko la Smirna hivi: “Usiogope mateso ambayo yanakaribia kukupata. Tazama! Ibilisi ataendelea kuwatupa gerezani baadhi yenu ili mjaribiwe kwa ukamili, na ili muwe na dhiki [shida, taabu, au uonevu] siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufikia kifo, nami nitakupa taji la uzima.”—Ufunuo 2:10.

21, 22. Tunapovumilia dhiki, tunaweza kupata faraja kwa kujua jambo gani?

21 Uvumilivu na utimilifu wetu utajaribiwa katika mfumo huu unaotawaliwa na Shetani. Hata hivyo, Yesu anatuhakikishia kwamba hatuna sababu ya kuogopa tunapoendelea kutarajia wakati ujao. Jambo muhimu ni kuwa waaminifu. “Dhiki ni ya dakika,” akasema Paulo, lakini “utukufu” au zawadi ambayo Yehova anatuahidi ‘ni yenye uzito mkubwa zaidi na zaidi na ni ya milele.’ (2 Wakorintho 4:17, 18) Hata dhiki ya Ayubu ilikuwa ya dakika ikilinganishwa na furaha aliyokuwa nayo kwa miaka mingi kabla na baada ya jaribu hilo.—Ayubu 42:16.

22 Lakini, huenda wakati fulani maishani tukahisi kwamba majaribu yetu hayaishi na kwamba hatuwezi kuvumilia mateso tunayokabili. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi kisa cha Ayubu kinavyoweza kutufundisha mengi zaidi kuhusu uvumilivu. Pia, tutajifunza jinsi ya kuwaimarisha wale wanaokabili matatizo.

Ungejibuje?

• Shetani alizusha suala gani muhimu kuhusiana na utimilifu wa Ayubu?

• Kwa nini hatupaswi kushangaa sana tunapokabili shida?

• Yehova hutusaidiaje kuvumilia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kufanya utafiti, kuzungumza na Wakristo wakomavu, na kusali kutoka moyoni kunaweza kutusaidia kuvumilia