Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Baruku Mwandishi Mwaminifu wa Yeremia

Baruku Mwandishi Mwaminifu wa Yeremia

Baruku Mwandishi Mwaminifu wa Yeremia

JE, UNAMJUA “Baruku mwana wa Neria”? (Yeremia 36:4) Ingawa anatajwa katika sura nne tu za Biblia, wasomaji wa Biblia wanajua kwamba alikuwa mwandishi na rafiki wa karibu wa nabii Yeremia. Baruku na Yeremia waliona miaka 18 ya mwisho ya ufalme wa Yuda ambayo ilikuwa na misukosuko mingi, jinsi Wababiloni walivyoharibu Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., na kuhamishwa hadi Misri.

Katika miaka ya karibuni, mihuri miwili ya udongo wa mfinyanzi * ya karne ya saba K.W.K. imegunduliwa. Mihuri hiyo ina maandishi “Ya Berekhyahu” [jina la Kiebrania la Baruku], mwana wa Neriyahu [jina la Kiebrania la Neria], Mwandishi.” Ugunduzi wa mihuri hiyo umewafanya wasomi wapendezwe tena na mtu huyo anayetajwa katika Biblia. Baruku alikuwa nani? Tunajua nini kuhusu familia yake, elimu aliyopata, na cheo chake? Tunajifunza nini kutokana na jinsi alivyosimama imara pamoja na Yeremia? Tunaweza kujifunza nini kutokana naye? Acheni tutafute majibu ya maswali hayo kwa kuchunguza habari za Biblia na za kihistoria zinazopatikana.

Malezi na Cheo Chake

Wasomi wengi leo wanasema kwamba Baruku alitoka katika familia mashuhuri ya waandishi huko Yuda. Wanatoa sababu kadhaa kuunga mkono wazo hilo. Kwa mfano, katika tafsiri fulani za Biblia Baruku anapewa cheo cha pekee, kama vile “katibu,” au “mwandishi.” Pia, Maandiko yanasema kwamba Seraya, ndugu yake, alikuwa ofisa wa cheo cha juu katika makao ya Mfalme Sedekia.—Yeremia 36:32; 51:59.

Mchunguzi wa vitu vya kale Philip J. King anaandika hivi kuhusu waandishi katika siku za Yeremia: “Waandishi, ambao walikuwa washiriki wa kikundi cha wataalamu, walikuwa mashuhuri huko Yuda mwishoni mwa karne ya saba na mapema katika karne ya sita K.W.K. . . . Maofisa wakuu wa mfalme ndio waliopewa jina hilo la cheo.”

Isitoshe, simulizi la Yeremia sura ya 36, ambalo tutachunguza kwa undani, linadokeza kwamba Baruku angeweza kuwasiliana na washauri wa mfalme na kuruhusiwa kutumia chumba cha kulia chakula, au chumba cha kukutania, cha Gemaria, ambaye alikuwa mkuu au ofisa. Msomi wa Biblia James Muilenberg anatoa hoja hii: “Baruku angeweza kuingia katika chumba hicho cha kukutania cha mwandishi huyo kwa sababu alistahili kuwa hapo na alikuwa mmoja wa maofisa wa mfalme ambao walikutana wakati wa lile tukio muhimu ambapo kitabu cha kukunjwa kilisomwa hadharani. Akiwa hapo, alikuwa kati ya wafanyakazi wenzake.”

Kitabu kimoja (Corpus of West Semitic Stamp Seals) kinatoa hoja nyingine inayoonyesha cheo cha Baruku: “Kwa kuwa muhuri wa udongo wa Berekhyahu ulipatikana pamoja na mihuri mingi ya maofisa wengine wakuu, ni sawa kukata kauli kwamba Baruku/Berekhyahu alikuwa na cheo sawa na hao maofisa wengine.” Habari zilizopo zinaonyesha kwamba huenda ikawa Baruku na ndugu yake Seraya walikuwa maofisa wakuu ambao walimuunga mkono nabii mwaminifu Yeremia katika ile miaka yenye matukio mengi kabla ya uharibifu wa Yerusalemu.

Amuunga Mkono Yeremia Hadharani

Tunapofuatanisha matukio kulingana na tarehe, Baruku anatajwa kwa mara ya kwanza katika Yeremia sura ya 36, katika “mwaka wa nne wa Yehoyakimu,” yapata mwaka wa 625 K.W.K. Kufikia wakati huo, Yeremia alikuwa ametumikia akiwa nabii kwa miaka 23.—Yeremia 25:1-3; 36:1, 4.

Wakati huo, Yehova alimwambia Yeremia hivi: “Chukua kitabu cha kukunjwa, uandike ndani yake maneno yote ambayo nimekuambia juu ya Israeli na juu ya Yuda na juu ya mataifa yote, . . . tangu siku za Yosia, mpaka leo hii.” Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “Na Yeremia akamwita Baruku mwana wa Neria ili Baruku aandike kwa kinywa cha Yeremia maneno yote ya Yehova.”—Yeremia 36:2-4.

Kwa nini Baruku aliitwa? Yeremia alimwambia hivi: “Nimefungiwa. Siwezi kuingia katika nyumba ya Yehova.” (Yeremia 36:5) Inaonekana kwamba Yeremia alipigwa marufuku asiingie katika eneo la hekalu ambako ujumbe wa Yehova ulipaswa kusomwa. Labda alizuiwa kwa sababu ujumbe wake wa mapema uliwakasirisha wenye mamlaka. (Yeremia 26:1-9) Bila shaka, Baruku alikuwa mwabudu mnyoofu wa Yehova, naye ‘alifanya kulingana na yote ambayo Yeremia nabii alikuwa amemwamuru.’—Yeremia 36:8.

Wakati mwingi ulihitajiwa ili kuandika maonyo yaliyokuwa yametolewa katika kipindi cha miaka 23 iliyopita, na huenda ikawa Yeremia alikuwa akingojea wakati unaofaa ufike. Lakini mnamo Novemba au Desemba mwaka wa 624 K.W.K., kwa ujasiri Baruku “akaanza kusoma kwa sauti katika kile kitabu maneno ya Yeremia kwenye nyumba ya Yehova, ndani ya chumba cha kulia chakula cha Gemaria . . . , masikioni mwa watu wote.”—Yeremia 36:8-10.

Mikaya mwana wa Gemaria alimjulisha baba yake na wakuu wengine mambo yaliyokuwa yametukia, nao wakamwomba Baruku asome kwa sauti kitabu hicho cha kukunjwa kwa mara ya pili. Simulizi hilo linasema hivi: “Sasa ikawa kwamba mara tu walipoyasikia yale maneno yote, wakaangaliana kwa hofu; nao wakamwambia Baruku: ‘Bila shaka tutamwambia mfalme maneno haya yote. . . . Nenda, jifiche, wewe pamoja na Yeremia, ili kwamba mtu yeyote asijue mahali mlipo.’”—Yeremia 36:11-19.

Mfalme Yehoyakimu aliposikia mambo yote ambayo Yeremia alikuwa amemwambia Baruku aandike, alikirarua kwa hasira kitabu hicho cha kukunjwa, akakitupa motoni, na kuamuru watu wake wamkamate Yeremia na Baruku. Kwa kutii amri ya Yehova, watu hao wawili waliandika nakala ya kitabu hicho walipokuwa mafichoni.—Yeremia 36:21-32.

Hapana shaka kwamba Baruku alijua hatari zinazohusika katika mgawo huo. Haikosi kwamba alijua vitisho ambavyo Yeremia alipata miaka kadhaa mapema. Huenda ikawa pia alijua kilichompata Uriya, ambaye alikuwa ametabiri “sawasawa na maneno yote ya Yeremia,” lakini akauawa kwa agizo la Mfalme Yehoyakimu. Hata hivyo, Baruku alikuwa tayari kutumia ustadi wake na uhusiano wake pamoja na maofisa wa serikali ili kumuunga mkono Yeremia katika mgawo wake.—Yeremia 26:1-9, 20-24.

Usijitafutie “Makuu”

Baruku alitaabika alipokuwa akiandika kitabu cha kwanza. Alisema hivi: “Ole wangu, sasa, kwa maana Yehova ameongeza huzuni juu ya maumivu yangu! Nimechoka kwa sababu ya kuugua kwangu, nami sikupata mahali pa kupumzika.” Kwa nini alitaabika?—Yeremia 45:1-3.

Hakuna jibu la moja kwa moja linalotolewa. Lakini hebu jaribu kuwazia hali ya Baruku. Haikosi kwamba kuandika kuhusu maonyo yaliyotolewa kwa kipindi cha miaka 23 juu ya taifa la Israeli na Yuda kulimfanya aone waziwazi uasi-imani wao na jinsi Yehova alivyowakataa. Hapana shaka Baruku alishtuka kusikia uamuzi wa Yehova wa kuharibu Yerusalemu na Yuda na kupeleka taifa hilo uhamishoni Babiloni kwa miaka 70. Yehova alifunua habari hizo mwaka huohuo na huenda ikawa ziliandikwa katika kitabu hicho cha kukunjwa. (Yeremia 25:1-11) Isitoshe, angeweza kupoteza cheo chake na kazi yake kwa sababu ya kumuunga mkono Yeremia katika kipindi hicho muhimu.

Hata ingawa sababu ya kutaabika kwake haijulikani waziwazi, Yehova mwenyewe aliingilia kati ili kumsaidia Baruku atilie maanani hukumu iliyokaribia. Yehova alisema hivi: “Kile ambacho nimekijenga ninakibomoa, na kile ambacho nimekipanda ninaking’oa, ndiyo, nchi yote.” Kisha akamshauri Baruku hivi: “Na wewe unaendelea kujitafutia makuu. Usiendelee kuyatafuta.”—Yeremia 45:4, 5.

Yehova hakutaja kihususa mambo hayo “makuu.” Lakini haikosi kwamba Baruku alijua mambo hayo, ambayo labda yalitia ndani tamaa ya kibinafsi ya kupata makuu, umashuhuri, au mali. Yehova alimshauri aone mambo kihalisi na kukumbuka mambo ambayo yangetokea: “Ninaleta msiba juu ya wote wenye mwili, . . . nami nitakupa wewe nafsi yako kuwa nyara katika mahali pote utakapoenda.” Uhai wa Baruku ungehifadhiwa popote ambapo angeenda, na hicho ndicho kitu cha thamani zaidi ambacho alikuwa nacho.—Yeremia 45:5.

Baada ya matukio hayo ya mwaka wa 625 hadi 624 K.W.K. ambayo yanasimuliwa katika Yeremia sura ya 36 na ya 45, Biblia haimtaji Baruku tena hadi miezi michache tu kabla ya Wababiloni kuharibu Yerusalemu na Yuda mwaka wa 607 K.W.K. Ni nini kilichotukia wakati huo?

Baruku Amuunga Mkono Yeremia Tena

Baruku anatajwa tena katika simulizi la Biblia wakati Yerusalemu lilipozingirwa na Wababiloni. Yeremia alikuwa “chini ya kizuizi katika Ua wa Walinzi” wakati Yehova alipomwambia anunue shamba la binamu yake huko Anathothi ili kuonyesha kwamba Waisraeli wangerudishwa. Baruku aliombwa asaidie katika shughuli za kisheria.—Yeremia 32:1, 2, 6, 7.

Yeremia alisema hivi: “Nikaandika katika hati na kutia muhuri na kuchukua mashahidi nilipokuwa nikipima pesa katika mizani. Baada ya hayo nikachukua ile hati ya ununuzi, ile iliyotiwa muhuri . . . na ile iliyoachwa wazi; kisha nikampa hati ya ununuzi Baruku.” Kisha, Yeremia akamwamuru Baruku aweke hati hizo za ununuzi katika chombo cha udongo ili ziwe salama. Wasomi fulani wanasema kwamba wakati Yeremia aliposema kwamba ‘aliandika’ hati, huenda ikawa alimwambia Baruku, mwandishi stadi, mambo ya kuandika.—Yeremia 32:10-14; 36:4, 17, 18; 45:1.

Baruku na Yeremia walifuata utaratibu wa kisheria uliotumiwa wakati huo. Utaratibu huo ulihusisha kutumia hati mbili. Kitabu kimoja (Corpus of West Semitic Stamp Seals) kinaeleza hivi: “Hati ya kwanza iliitwa ‘hati iliyotiwa muhuri’ kwa sababu ilikunjwa na kutiwa muhuri wa udongo wa mfinyanzi; hiyo ndiyo iliyokuwa nakala ya kwanza ya mapatano. . . . Hati ya pili iliyoitwa ‘hati iliyoachwa wazi’ ilikuwa nakala ya ile hati iliyotiwa muhuri, au yenye masharti, na ilikusudiwa kusomwa tu. Hivyo, kulikuwa na hati mbili, hati ya kwanza na nakala yake, ambazo ziliandikwa juu ya kurasa mbili tofauti za mafunjo.” Wachimbuzi wa vitu vya kale wamethibitisha kwamba desturi ya kuhifadhi hati hizo katika chombo cha udongo ni ya kweli.

Mwishowe, Wababiloni waliteka jiji la Yerusalemu, wakaliteketeza, na kuwapeleka watu wote uhamishoni isipokuwa watu wachache maskini. Nebukadneza alimweka Gedalia kuwa gavana. Gedalia aliuawa miezi miwili baadaye. Wayahudi waliobaki walipanga kuhamia Misri, ingawa Yeremia aliongozwa kwa roho awashauri wasifanye hivyo. Wakati huo, ndipo Baruku anatajwa tena.—Yeremia 39:2, 8; 40:5; 41:1, 2; 42:13-17.

Viongozi Wayahudi walimwambia Yeremia hivi: “Ni uwongo ambao wewe unasema. Yehova Mungu wetu hakukutuma, kusema, ‘Msiingie Misri kukaa humo mkiwa wageni.’ Bali Baruku mwana wa Neria anakuchochea juu yetu ili kututia mkononi mwa Wakaldayo, ili watuue au watupeleke uhamishoni Babiloni.” (Yeremia 43:2, 3) Huenda mashtaka hayo yakaonyesha kuwa viongozi fulani Wayahudi waliamini kwamba Baruku alikuwa akimchochea Yeremia kwa kiasi fulani. Kwa sababu ya cheo cha Baruku na urafiki wake wa muda mrefu pamoja na Yeremia huenda viongozi hao waliona kwamba Baruku hakuwa tu mwandishi wa nabii huyo. Hata iwe viongozi hao Wayahudi walikuwa na maoni gani, ujumbe huo ulitoka kwa Yehova.

Licha ya maonyo yaliyotoka kwa Mungu, Wayahudi waliobaki waliondoka huku wakimchukua “Yeremia nabii na Baruku mwana wa Neria.” Yeremia aliandika hivi: “Mwishowe wakaingia katika nchi ya Misri, kwa maana hawakuitii sauti ya Yehova; nao mwishowe wakafika mpaka Tahpanhesi,” jiji linalopakana na Sinai kwenye mlango wa mashariki wa Mto Nile. Baada ya tukio hilo, hatusomi tena kumhusu Baruku.—Yeremia 43:5-7.

Tunaweza Kujifunza Nini Kutokana na Baruku?

Tunaweza kujifunza mambo mengi muhimu kutokana na Baruku. Jambo moja muhimu tunalojifunza ni utayari wake wa kutumia ustadi wake na uhusiano wake pamoja na wakuu katika utumishi wa Yehova, bila kujali hatari. Leo Mashahidi wengi wa Yehova, wanaume kwa wanawake, wanaonyesha roho kama hiyo kwa kutumia ustadi wao kutumikia Betheli, katika kazi ya ujenzi, na katika njia nyinginezo. Unaweza kuonyeshaje roho kama ya Baruku?

Baruku alipokumbushwa kwamba hakuna wakati wa kujitafutia “makuu” katika siku za mwisho za ufalme wa Yuda, inaonekana alitii shauri hilo kwa sababu alipokea nafsi yake kuwa nyara. Inafaa tutii shauri hilo, kwa kuwa sisi pia tunaishi katika siku za mwisho za mfumo wa mambo. Kama Baruku, Yehova anaahidi kutuhifadhi hai. Je, tunaweza kutii vikumbusho hivyo kama Baruku?

Kuna jambo lingine muhimu tunaloweza kujifunza kutokana na simulizi hilo. Baruku alimsaidia Yeremia na binamu yake kufuata utaratibu wa kisheria katika shughuli yao ya kibiashara, hata ingawa walikuwa watu wa ukoo. Huo ni mfano wa Kimaandiko kwa Wakristo wanaofanya biashara pamoja na ndugu na dada zao wa kiroho. Kufuata mfano huo wa kuandika mapatano ya kibiashara ni jambo linalopatana na Maandiko, la hekima, na la upendo.

Ingawa Baruku anatajwa kifupi tu katika Biblia, yeye ni mfano bora kwa Wakristo wote leo. Je, utaiga mfano bora wa mwandishi huyo mwaminifu wa Yeremia?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Mihuri hiyo ya udongo wa mfinyanzi ilitumiwa kufunga uzi uliofunga hati muhimu. Udongo huo ulitiwa muhuri ambao ulimtambulisha mwenye hati au yule aliyeituma.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Muhuri wa udongo wa Baruku

[Hisani]

Bulla: Courtesy of Israel Museum, Jerusalem