Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Duniani Kama Ilivyo Mbinguni”

“Duniani Kama Ilivyo Mbinguni”

“Duniani Kama Ilivyo Mbinguni”

“Imani ya Wakatoliki inataja kihususa Mambo Manne ya Mwisho: Kifo, Hukumu, Moto wa Mateso, Mbinguni.”—Catholicism, kilichohaririwa na George Brantl.

ONA kwamba kwenye orodha hiyo ya mambo manne ya mwisho kuhusu wanadamu, dunia haitajwi. Hilo halishangazi sana kwa sababu Kanisa Katoliki, kama vile dini nyingine, linaamini siku moja dunia itaharibiwa. Kitabu kimoja (Dictionnaire de Théologie Catholique) kinaonyesha wazi wazo hilo chini ya kichwa kidogo “Mwisho wa Dunia”: “Kanisa Katoliki linaamini na kufundisha kwamba dunia ya leo, kama Mungu alivyoiumba na jinsi ilivyo, haitadumu milele.” Pia, katekisimu ya Kikatoliki ya hivi karibuni inasema hivi kuhusu wazo hilo: “Ulimwengu wetu . . . unakusudiwa kutoweka.” Lakini ikiwa dunia itatoweka, namna gani zile ahadi za Biblia zinazosema kwamba dunia itakuwa paradiso?

Biblia inasema waziwazi kwamba dunia itakuwa paradiso wakati ujao. Kwa mfano, nabii Isaya alisema hivi kuhusu dunia na wakaaji wake: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale. Kwa maana siku za watu wangu zitakuwa kama siku za mti; na watu wangu waliochaguliwa wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.” (Isaya 65:21, 22) Wayahudi waliopewa ahadi hizo na Mungu, waliamini kabisa kwamba siku moja nchi yao, yaani, dunia yote, ingekuwa paradiso ambayo wanadamu wangefurahia milele.

Zaburi ya 37 inathibitisha tumaini hilo. “Wapole wataimiliki dunia.” (Zaburi 37:11) Mstari huo hauzungumzii kuhusu kurudishwa kwa muda tu kwa taifa la Israeli katika Nchi ya Ahadi. Zaburi hiyohiyo inasema hivi kihususa: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) * Ona kwamba zaburi hiyo inaonyesha kuwa uzima wa milele duniani ndio zawadi ambayo “wapole” watapewa. Katika tafsiri moja ya Biblia ya Kifaransa, maelezo fulani kuhusu mstari huo yanaonyesha kwamba neno “wapole” “lina maana pana zaidi kuliko linavyoonekana katika tafsiri nyingi; linatia ndani wale walio katika uhitaji, wale wanaoteseka au wanaoteswa kwa ajili ya Yahweh, wanyenyekevu wanaojitiisha kwa Mungu.”

Duniani au Mbinguni?

Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitoa ahadi inayotukumbusha maandiko yaliyonukuliwa hapo juu: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Kwa mara nyingine tena, dunia itakuwa zawadi ya kudumu kwa ajili ya waaminifu. Hata hivyo, Yesu aliwaonyesha wazi mitume wake kwamba angeenda kuwatayarishia makao “katika nyumba ya Baba [yake]” na kwamba wangekuwa pamoja naye mbinguni. (Yohana 14:1, 2; Luka 12:32; 1 Petro 1:3, 4) Hivyo basi, tunapaswa kuelewaje ahadi kuhusiana na baraka za kidunia? Je, ahadi hizo ni muhimu leo, nazo zinawahusu nani?

Wasomi mbalimbali wa Biblia wanasema kwamba “dunia” inayotajwa katika Mahubiri ya Mlimani ya Yesu na hata katika Zaburi ya 37 si dunia halisi. Katika maelezo yake katika tafsiri moja (Bible de Glaire), F. Vigouroux aliona kwamba mistari hiyo inazungumzia “mfano wa mbingu na Kanisa.” Kulingana na Mfaransa M. Lagrange ambaye ni mtafiti wa Biblia, ahadi hiyo “si ahadi ya kwamba wapole watairithi dunia wanayokalia, wala mfumo huu wa mambo wala ule unaokuja, lakini mahali ambapo dunia hiyo itakuwa, yaani, ufalme wa mbinguni.” Kulingana na mtafiti mwingine wa Biblia, dunia hiyo ni “mfano unaotumiwa kuwakilisha mbingu.” Lakini, kulingana na watafiti wengine, “nchi ya ahadi, Kanaani, inaonwa kwa njia ya kiroho nayo inawakilisha nchi ya juu ambayo wapole wamehakikishiwa, yaani, ufalme wa Mungu. Hiyo ndiyo maana ya mfano huo katika Zaburi ya 37 na kwingineko.” Lakini je, tunapaswa kutupilia mbali ahadi za Mungu kuhusu dunia halisi?

Kusudi la Milele kwa Ajili ya Dunia

Mwanzoni, dunia ilihusianishwa moja kwa moja na kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.” (Zaburi 115:16) Hivyo, kusudi la Mungu la awali kwa ajili ya wanadamu lilihusu dunia, wala si mbingu. Yehova aliwapa wenzi wa ndoa wa kwanza kazi ya kupanua bustani ya Edeni ili ienee duniani pote. (Mwanzo 1:28) Kusudi hilo halikuwa la muda tu. Yehova anasisitiza katika Neno lake kwamba dunia itadumu milele: “Kizazi kinaenda, kizazi kinakuja; lakini dunia inasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Mhubiri 1:4; 1 Mambo ya Nyakati 16:30; Isaya 45:18.

Kwa kuwa yeye ndiye Aliye Juu Zaidi, sikuzote Mungu huhakikisha kwamba ahadi zake zinatimia. Biblia inatumia mfano wa mzunguko wa asili wa maji kueleza kwamba ahadi za Mungu haziwezi kukosa kutimia. Inasema hivi: “Kwa maana kama vile mvua inayonyesha hushuka, na theluji, kutoka mbinguni nayo hairudi mahali pale, mpaka kwa kweli iwe imeinywesha dunia na kuifanya izae na kuchipuka, . . . ndivyo litakavyokuwa neno langu [neno la Mungu] linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” (Isaya 55:10, 11) Mungu huwapa wanadamu ahadi. Wakati mwingi unaweza kupita kabla ya ahadi hizo kutimia, lakini haziwezi kukosa kutimia. Ahadi hizo ‘hurudi’ kwake baada ya kutimiza yote ambayo yalitabiriwa.

Bila shaka, Yehova ‘alipendezwa’ sana kuumba dunia kwa ajili ya wanadamu. Mwishoni mwa siku ya sita ya uumbaji, alisema kwamba kila kitu kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:31) Kuigeuza dunia kuwa paradiso ya kudumu ni sehemu ya kusudi la Mungu ambalo halijatimia. Isitoshe, ahadi za Mungu ‘hazitarudi kwake bila matokeo.’ Ahadi zote kuhusu uzima mkamilifu duniani, ambapo wanadamu wataishi milele katika amani na usalama, zitatimia.—Zaburi 135:6; Isaya 46:10.

Kusudi la Mungu Litatimia Hakika

Dhambi ya wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, ilivuruga kwa muda kusudi la awali la Mungu la kuifanya dunia kuwa paradiso. Baada ya kutotii kwao, walifukuzwa kutoka katika bustani. Hivyo, wakapoteza pendeleo la kushiriki katika kutimiza kusudi la Mungu la kuwa na wanadamu wakamilifu ambao wangeishi katika paradiso duniani. Hata hivyo, Mungu alifanya mipango ili kutimiza kusudi lake. Jinsi gani?—Mwanzo 3:17-19, 23.

Hali katika Edeni ilifanana na ya mtu anayeanza kujenga nyumba kwenye uwanja mzuri. Baada tu ya kuweka msingi, mtu fulani anakuja na kuharibu msingi huo. Badala ya kuacha mradi wake, mtu huyo anachukua hatua ili kuhakikisha kwamba anakamilisha ujenzi wa nyumba hiyo. Hata ikiwa kazi ya ziada inahitaji gharama zaidi, hiyo haimaanishi kwamba mradi wa awali haufai.

Vivyo hivyo, Mungu alifanya mipango ili kuhakikisha kutimizwa kwa kusudi lake. Muda mfupi baada ya dhambi ya wazazi wetu wa kwanza, Mungu alitangaza tumaini kwa wazao wao—“uzao” ambao ungeondoa madhara yaliyofanywa. Katika kutimiza unabii huo, sehemu ya kwanza ya uzao ilithibitika kuwa Mwana wa Mungu, Yesu, aliyekuja duniani na kutoa uhai wake kuwa fidia ili kuwakomboa wanadamu. (Wagalatia 3:16; Mathayo 20:28) Baada ya kufufuliwa na kwenda mbinguni, Yesu angekuwa Mfalme wa Ufalme huo. Yesu hasa ndiye yule mpole anayerithi dunia pamoja na waaminifu waliochaguliwa ambao wanafufuliwa kwenda mbinguni ili kutawala pamoja na Yesu katika Ufalme huo. (Zaburi 2:6-9) Hatimaye, serikali hiyo itashughulikia mambo ya dunia ili kutimiza kusudi la Mungu la awali na kuigeuza dunia kuwa paradiso. Wapole wengi “watairithi dunia” katika maana ya kwamba watafaidika na utawala wa Ufalme huo wa Yesu Kristo pamoja na wale watakaotawala naye.—Mwanzo 3:15; Danieli 2:44; Matendo 2:32, 33; Ufunuo 20:5, 6.

“Duniani Kama Ilivyo Mbinguni”

Wokovu huo ambao una matumaini mawili, yaani, tumaini la kuishi mbinguni au duniani, linatajwa katika maono ambayo mtume Yohana alipokea. Aliona wafalme kwenye viti vya ufalme mbinguni ambao walichaguliwa kutoka miongoni mwa wanafunzi waaminifu wa Kristo. Biblia inasema kihususa kuhusu wale watakaotawala pamoja na Kristo kwamba “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10) Ona mambo mawili yanayohusika katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu, yaani, dunia iliyofanywa upya kupitia uongozi wa Ufalme wa mbinguni uliofanyizwa na Yesu Kristo na warithi wenzake. Mipango yote hiyo ya Mungu itawezesha dunia kuwa Paradiso tena kulingana na kusudi la awali la Mungu.

Katika sala yake ya mfano, Yesu aliwaambia wanafunzi wake wasali kwamba mapenzi ya Mungu yatendeke “duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Je, maneno hayo yangekuwa na maana yoyote ikiwa dunia ingeharibiwa au ikiwa tu ingekuwa mfano wa mbingu? Vivyo hivyo, je, maneno hayo yangekuwa na maana yoyote ikiwa waadilifu wote wangeenda mbinguni? Mapenzi ya Mungu kuelekea dunia yanaonyeshwa wazi katika Maandiko, tangu masimulizi ya uumbaji hadi maono ya kitabu cha Ufunuo. Dunia itakuwa vile ambavyo Mungu aliikusudia iwe, yaani, paradiso. Hayo ndiyo mapenzi ambayo Mungu ameahidi kutimiza. Watu waaminifu duniani huomba mapenzi hayo yatimizwe.

Tangu mwanzo, Muumba, ambaye ni Mungu ‘asiyebadilika’ alikusudia watu waishi milele duniani. (Malaki 3:6; Yohana 17:3; Yakobo 1:17) Kwa zaidi ya miaka 100 sasa, gazeti hili, Mnara wa Mlinzi, limeeleza mambo hayo mawili yanayohusiana na kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Hilo linatuwezesha kuelewa maana ya ahadi zilizo katika Maandiko zinazoonyesha kwamba dunia itakuwa paradiso tena. Tunakualika uchunguze kwa undani zaidi mambo hayo, iwe kwa kuzungumza na Mashahidi wa Yehova au kwa kuwaandikia wachapishaji wa gazeti hili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ingawa tafsiri nyingi za Biblia zinatafsiri neno la Kiebrania ’eʹrets kuwa “nchi” badala ya “dunia,” si lazima neno ’eʹrets kwenye Zaburi 37:11, 29 litafsiriwe tu nchi ambayo taifa la Israeli lilipewa. Kitabu kimoja (Old Testament Word Studies) cha William Wilson kinafafanua neno ’eʹrets kuwa “dunia yote kwa jumla, kutia ndani sehemu zinazokaliwa na zile zisizokaliwa; neno hilo linapotumiwa katika maana isiyo pana linamaanisha sehemu fulani ya dunia, yaani, nchi fulani.” Hivyo, maana ya kwanza ya neno la Kiebrania ni sayari yetu, yaani, dunia.—Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza au la Kifaransa la Januari 1, 1986, ukurasa wa 31.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Biblia inaeleza waziwazi kwamba dunia itafanywa kuwa Paradiso wakati ujao

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, sala ya Yesu ya mfano ingekuwa na maana yoyote ikiwa dunia ingetoweka?