Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, inawezekana wanadamu watende dhambi na kufa baada ya lile jaribu la mwisho, mwishoni mwa ile Miaka Elfu?

Mistari miwili ya kitabu cha Ufunuo inatupa habari zinazotusaidia kujibu swali hilo: “Kifo na Kaburi [“Hadesi,” maelezo ya chini] vikatupwa ndani ya lile ziwa la moto. Hili linamaanisha kifo cha pili, lile ziwa la moto.” (Ufunuo 20:14) “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

Ona wakati unaohusika hapa. “Kifo na Hadesi” vinatupwa ndani ya ziwa la moto baada ya waokokaji wa Har–Magedoni, wale watakaofufuliwa, na wowote watakaozaliwa baada ya Har–Magedoni kuhukumiwa kutokana na ‘mambo yaliyoandikwa katika vile vitabu,’ au yale yote ambayo Yehova anataka wanadamu wafanye katika kipindi hicho cha miaka elfu. (Ufunuo 20:12, 13) Mtume Yohana anaandika maono mengine katika Ufunuo sura ya 21 ambayo yatatimizwa wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo Yesu. Hata hivyo, utimizo kamili wa maono hayo utakuwa mwishoni mwa ile Siku ya Hukumu ya miaka elfu. Baada ya Yesu kumrudishia Baba yake Ufalme, Yehova atakaa pamoja na watu kikamili bila kuwa na wapatanishi wowote kati yake na wanadamu. Yehova atakaa pamoja na “watu wake” milele kwa njia ya kiroho na atashughulika nao moja kwa moja. “Kifo hakitakuwapo tena” kabisa wakati ambapo wanadamu watakuwa wamefikia ukamilifu kwa kuwa manufaa ya dhabihu ya fidia ya Kristo yatakuwa yametumiwa kikamili.—Ufunuo 21:3, 4.

Hivyo, kifo kinachotajwa katika maandiko yaliyonukuliwa hapo juu ni kifo kilichotokana na Adamu ambacho kitakuwa kimeondolewa kabisa kupitia dhabihu ya fidia ya Kristo. (Waroma 5:12-21) Baada ya kifo kilichotokana na yule mtu wa kwanza kuondolewa, wanadamu watakuwa kama vile Adamu alivyokuwa alipoumbwa. Adamu alikuwa mkamilifu, lakini hilo halikumaanisha kwamba hangeweza kufa. Yehova alimwambia Adamu asile kutokana na “mti wa ujuzi wa mema na mabaya” na akasema: “Siku utakapokula, utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Kifo hicho kingetokana na kutenda dhambi kimakusudi. Baada ya jaribu la mwisho, mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu, bado wanadamu watakuwa na uhuru wa kujiamulia mambo. (Ufunuo 20:7-10) Bado watakuwa na uhuru wa kuchagua ikiwa watamtumikia Yehova au la. Hatuwezi kusema kwa uhakika kwamba hakuna mwanadamu atakayemwasi Mungu kama alivyofanya Adamu.

Itakuwaje kwa mtu atakayeamua kuasi baada ya lile jaribu la mwisho wakati kifo na Hadesi havitakuwapo? Wakati huo, kifo kilichotokana na Adamu hakitakuwapo tena. Na Hadesi, yaani, kaburi la watu walio na tumaini la ufufuo, haitakuwapo tena. Hata hivyo, Yehova anaweza kumwangamiza mwasi yeyote katika ziwa la moto, na hivyo mtu huyo hawezi kufufuliwa. Mwasi huyo atakufa kama Adamu na Hawa, lakini si kifo kilichotokana na Adamu.

Lakini hatutazamii hilo litendeke. Wale watakaopita jaribu la mwisho watakuwa tofauti na Adamu katika njia moja muhimu. Watakuwa wamejaribiwa kikamili. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba jaribu la mwisho litakuwa kamili kwa sababu Yehova anajua kuwachunguza watu kabisa. Tuna hakika kwamba jaribu la mwisho litamwondoa yeyote ambaye atatumia vibaya uhuru wa kuchagua. Hivyo, ingawa inawezekana wale watakaopita jaribu la mwisho wamwasi Mungu na kuharibiwa, kuna uwezekano mkubwa kwamba jambo hilo halitatukia.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Ni katika maana gani wanadamu watakuwa kama Adamu, baada ya lile jaribu la mwisho?