Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mmesikia Juu ya Uvumilivu wa Ayubu”

“Mmesikia Juu ya Uvumilivu wa Ayubu”

“Mmesikia Juu ya Uvumilivu wa Ayubu”

“Mmesikia juu ya uvumilivu wa Ayubu nanyi mmeona matokeo ambayo Yehova alileta, kwamba Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.”—YAKOBO 5:11.

1, 2. Wenzi fulani wa ndoa huko Poland walikabili jaribu gani?

HARALD ABT alikuwa Shahidi wa Yehova kwa muda usiozidi mwaka mmoja wakati majeshi ya Hitler yalipoteka jiji la Danzig (ambalo sasa ni Gdańsk) kaskazini mwa Poland. Kisha, hali ikawa mbaya na hatari kwa Wakristo wa kweli waliokuwa huko. Polisi wa siri wa Nazi walijaribu kumlazimisha Harald atie sahihi hati ya kukana imani yake, lakini alikataa. Baada ya majuma kadhaa gerezani, Harald alipelekwa katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen, ambapo alitishwa na kupigwa mara nyingi. Ofisa mmoja alimwonyesha Harald bomba la kutolea moshi la mahali pa kuteketeza maiti na akamwambia hivi: “Ukiendelea kushikilia imani yako, baada ya siku 14 utateketezwa na kupanda kwa Yehova wako kupitia lile bomba.”

2 Wakati Harald alipokamatwa, mke wake, Elsa, alikuwa bado anamnyonyesha binti yao mwenye umri wa miezi kumi. Lakini, polisi wa siri wa Nazi hawakumwacha Elsa. Muda mfupi baadaye, mtoto wake alichukuliwa, naye Elsa akapelekwa katika kambi ya maangamizi ya Auschwitz. Hata hivyo, yeye pia aliendelea kuvumilia kwa miaka mingi kama Harald. Unaweza kusoma habari zaidi kuhusu jinsi walivyovumilia katika gazeti la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1980. Harald aliandika hivi: “Kwa jumla, nilitumia miaka 14 ya maisha yangu katika kambi za mateso na gerezani kwa sababu ya kumwamini Mungu. Nimewahi kuulizwa hivi: ‘Je, mke wako alikusaidia kuvumilia mateso hayo?’ Bila shaka! Nilijua tangu mwanzo kwamba hataacha imani yake kamwe, na kujua hivyo kuliniimarisha sana. Nilijua angependa nife nikiwa mwaminifu kuliko kuachiliwa kwa sababu ya kukana imani. . . . Kwa miaka yote aliyokuwa katika kambi za mateso huko Ujerumani, Elsa alivumilia mateso mengi.”

3, 4. (a) Ni vielelezo vya akina nani vinavyoweza kuwatia moyo Wakristo kuvumilia? (b) Kwa nini Biblia inatusihi tuchunguze kisa cha Ayubu?

3 Mashahidi wengi wanaweza kuthibitisha kwamba si rahisi mtu kuvumilia anapoteseka. Kwa hiyo, Biblia inawashauri Wakristo wote hivi: “Wachukueni manabii kuwa kielelezo cha kupatwa na uovu na kuonyesha subira, wale waliosema katika jina la Yehova.” (Yakobo 5:10) Kwa karne nyingi, watumishi wengi wa Mungu wameteswa bila sababu. Vielelezo vya hilo ‘wingu kubwa la mashahidi’ vinaweza kututia moyo tuendelee kukimbia kwa uvumilivu shindano letu la Kikristo.—Waebrania 11:32-38; 12:1.

4 Katika Biblia, Ayubu anatajwa kuwa kielelezo cha uvumilivu. Yakobo aliandika hivi: “Tazama! Tunawatangaza kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia. Mmesikia juu ya uvumilivu wa Ayubu nanyi mmeona matokeo ambayo Yehova alileta, kwamba Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) Kisa cha Ayubu kinatuonyesha thawabu ambayo waaminifu wanatarajia kutoka kwa Yehova ambaye huwabariki. Zaidi ya hilo, kinafunua kweli zitakazotunufaisha wakati wa shida. Kitabu cha Ayubu kinatusaidia kujibu maswali haya: Tunapojaribiwa, kwa nini ni muhimu kuelewa masuala muhimu yanayohusika? Ni sifa na mitazamo gani ambayo hutusaidia kuvumilia? Tunaweza kuwaimarishaje Wakristo wenzetu wanaoteseka?

Kuelewa Mambo Yote Yanayohusika

5. Ni suala gani kuu tunalopaswa kukumbuka tunapokabili majaribu au vishawishi?

5 Ili kuendelea kuwa thabiti kiroho tunapokabili matatizo, tunahitaji kuelewa masuala yanayohusika. Tusipofanya hivyo, matatizo tunayokabili yanaweza kutukengeusha kiroho. Suala la ushikamanifu kwa Mungu ni muhimu sana. Baba yetu wa mbinguni anatusihi tufanye jambo ambalo kila mmoja wetu anapaswa kufikiria kwa uzito: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” (Methali 27:11) Hilo ni pendeleo la pekee! Ingawa sisi ni dhaifu na hatujakamilika, tunaweza kumfanya Muumba wetu ashangilie. Tunafanya hivyo wakati upendo wetu kwa Yehova unapotuwezesha kustahimili majaribu na vishawishi. Upendo wa kweli wa Kikristo huvumilia mambo yote. Haushindwi kamwe.—1 Wakorintho 13:7, 8.

6. Shetani humdhihaki Yehova jinsi gani, naye hufanya hivyo kwa kadiri gani?

6 Kitabu cha Ayubu kinamtambulisha waziwazi Shetani kuwa ndiye anayemdhihaki Yehova. Pia, kinafunua mwelekeo mbovu wa adui huyo asiyeonekana na tamaa yake ya kuharibu uhusiano wetu pamoja na Mungu. Kama inavyoonyeshwa katika kisa cha Ayubu, Shetani anamshtaki kila mtumishi wa Yehova kuwa anachochewa na ubinafsi na anajaribu kuonyesha kwamba upendo wao kwa Mungu unaweza kupoa. Amemdhihaki Mungu kwa maelfu ya miaka. Shetani alipotupwa chini kutoka mbinguni, sauti kutoka mbinguni ilimtaja kuwa “mshtaki wa ndugu zetu” na ikasema kwamba yeye huwashtaki “mchana na usiku mbele za Mungu wetu.” (Ufunuo 12:10) Kwa kuvumilia kwa uaminifu, tunaweza kuthibitisha kwamba mashtaka yake hayana msingi.

7. Ni njia gani bora ya kushinda udhaifu wa kimwili?

7 Tunapaswa kukumbuka kwamba Ibilisi atatumia dhiki yoyote tunayokabili ili kujaribu kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. Shetani alimjaribu Yesu wakati gani? Ni wakati Yesu alipoona njaa baada ya kufunga kwa siku nyingi. (Luka 4:1-3) Hata hivyo, nguvu za kiroho zilimwezesha Yesu kukataa katakata vishawishi vya Ibilisi. Ni muhimu sana tushinde udhaifu wowote wa kimwili, uwe umesababishwa na ugonjwa au uzee, kwa kutumia nguvu za kiroho! Ingawa “mtu tuliye kwa nje anachakaa,” hatukati tamaa kwa sababu “mtu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku baada ya siku.”—2 Wakorintho 4:16.

8. (a) Hisia zisizofaa zinaweza kutudhoofishaje? (b) Yesu alikuwa na mtazamo gani?

8 Isitoshe, hisia zisizofaa zinaweza kuharibu hali yetu ya kiroho. Huenda mtu akajiuliza, ‘Kwa nini Yehova anaruhusu hali hii?’ Baada ya kutendewa isivyofaa, huenda mwingine akauliza, ‘Ndugu anawezaje kunitendea hivi?’ Hisia hizo zinaweza kutufanya tupuuze masuala muhimu na kukazia fikira hali zetu tu. Mfadhaiko ambao Ayubu alipata kwa sababu ya marafiki wake watatu ambao walisema mambo yaliyopotoka ulimuumiza sana kihisia kama vile ugonjwa wake ulivyomdhoofisha kimwili. (Ayubu 16:20; 19:2) Vilevile, mtume Paulo alionyesha kwamba hasira ya muda mrefu inaweza ‘kumpa Ibilisi nafasi.’ (Waefeso 4:26, 27) Badala ya kuzungumza na wengine kwa hasira au kufikiria sana hali fulani isiyofaa, Wakristo watafaidika wakimwiga Yesu kwa ‘kuendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu,’ Yehova Mungu. (1 Petro 2:21-23) Kuwa na ‘mwelekeo wa akili’ wa Yesu kunaweza kutulinda sana dhidi ya mashambulizi ya Shetani.—1 Petro 4:1.

9. Mungu anatupa uhakikisho gani kuhusu mizigo tunayobeba na vishawishi tunavyokabili?

9 Zaidi ya yote, tusione kamwe matatizo kuwa uthibitisho wa kwamba Mungu hapendezwi nasi. Hali hiyo ya kutoelewa mambo ilimuumiza Ayubu wakati aliposhambuliwa kwa maneno makali ya watu waliodai kumfariji. (Ayubu 19:21, 22) Biblia inatupa uhakikisho huu: “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Mbali na hilo, Yehova anaahidi kutusaidia kubeba mzigo wowote unaotulemea na kutuandalia njia ya kushinda kishawishi chochote tunachokabili. (Zaburi 55:22; 1 Wakorintho 10:13) Kwa kumkaribia Mungu wakati wa shida, tunaweza kuona mambo kwa njia inayofaa na kufanikiwa kumpinga Ibilisi.—Yakobo 4:7, 8.

Mambo ya Kutusaidia Kuvumilia

10, 11. (a) Ni nini kilichomsaidia Ayubu kuvumilia? (b) Kuwa na dhamiri nzuri kulimsaidiaje Ayubu?

10 Ayubu alishikilia utimilifu wake licha ya hali yake mbaya, kutukanwa na watu waliodai kuwa wafariji wake, na kutojua chanzo cha misiba yake. Tunaweza kujifunza nini kutokana na uvumilivu wake? Bila shaka, uaminifu wake kwa Yehova ndio uliomwezesha kuvumilia. ‘Alimwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.’ (Ayubu 1:1) Hiyo ilikuwa njia yake ya maisha. Hata wakati ambapo hakuelewa kilichofanya mambo yaharibike kwa ghafula, Ayubu alikataa kumkana Yehova. Ayubu aliamini kwamba anapaswa kumtumikia Mungu wakati hali ni nzuri au mbaya.—Ayubu 1:21; 2:10.

11 Pia, kuwa na dhamiri nzuri kulimfariji Ayubu. Ilipoonekana wazi kwamba atakufa, alipata faraja kwa kujua alikuwa amefanya yote awezayo kuwasaidia wengine, alikuwa ameshika viwango vya uadilifu vya Yehova, na kujiepusha na kila namna ya ibada ya uwongo.—Ayubu 31:4-11, 26-28.

12. Ayubu alitendaje baada ya kusaidiwa na Elihu?

12 Ni kweli kwamba Ayubu alihitaji msaada ili kurekebisha maoni yake kuhusu mambo fulani. Ayubu alikubali msaada huo kwa unyenyekevu, na hivyo akavumilia. Elihu alitoa shauri la hekima, naye Ayubu alilisikiliza kwa heshima na kukubali kurekebishwa na Yehova. “Nilisema, lakini sikuwa ninaelewa,” akasema. “Ninayatangua niliyosema, nami ninatubu katika mavumbi na majivu.” (Ayubu 42:3, 6) Licha ya ugonjwa uliokuwa unamsumbua, Ayubu alifurahi kujua kwamba kurekebisha maoni yake kwa njia hiyo kulimsaidia amkaribie Mungu. Ayubu alisema: “Nimepata kujua kwamba [Yehova] unaweza kufanya mambo yote.” (Ayubu 42:2) Kwa sababu Yehova alimfafanulia Ayubu ukuu Wake, Ayubu alielewa wazi zaidi kuwa yeye ni duni sana akilinganishwa na Muumba wake.

13. Ayubu alifaidikaje kwa kuwa mwenye rehema?

13 Hatimaye, Ayubu ni mfano mzuri wa rehema. Wafariji wake wa uwongo walimuumiza sana kihisia, lakini wakati Yehova alipomwomba asali kwa ajili yao, alifanya hivyo. Baadaye, Yehova akamponya Ayubu. (Ayubu 42:8, 10) Ni wazi kwamba kinyongo hakitatusaidia kuvumilia, lakini upendo na rehema zitatusaidia. Tusipoweka kinyongo tunaburudika kiroho, na Yehova hutubariki.—Marko 11:25.

Washauri Wenye Hekima Wanaotusaidia Kuvumilia

14, 15. (a) Mshauri anahitaji kuwa na sifa gani ili aweze kuwafariji wengine? (b) Eleza mambo yaliyomwezesha Elihu afaulu kumsaidia Ayubu.

14 Jambo lingine tunaloweza kujifunza kutokana na kisa cha Ayubu ni umuhimu wa washauri wenye hekima. Hao ni ndugu ‘waliozaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.’ (Methali 17:17) Hata hivyo, kama tunavyoona katika kisa cha Ayubu, washauri wengine wanaweza kuumiza badala ya kufariji. Mshauri mzuri anapaswa kuonyesha hisia-mwenzi, heshima, na fadhili, kama Elihu. Wazee na Wakristo wengine wakomavu wanaweza kuwasaidia akina ndugu waliolemewa na matatizo warekebishe maoni yao, na kwa kufanya hivyo wanaweza kujifunza mengi kutokana na kitabu cha Ayubu.—Wagalatia 6:1; Waebrania 12:12, 13.

15 Kuna mambo mengi mazuri tunayojifunza kutokana na jinsi Elihu alivyoshughulikia hali hiyo. Alisikiliza kwa makini kabla ya kujibu maoni yenye kasoro ya marafiki watatu wa Ayubu. (Ayubu 32:11; Methali 18:13) Elihu alimwita Ayubu kwa jina na kumsihi kama rafiki. (Ayubu 33:1) Tofauti na wale wafariji watatu wa uwongo, Elihu hakujiona kuwa bora kuliko Ayubu. Alisema hivi: “Mimi pia niliumbwa kutoka kwenye udongo.” Hakutaka kumuumiza Ayubu zaidi kwa kuzungumza bila kufikiri. (Ayubu 33:6, 7; Methali 12:18) Badala ya kumchambua Ayubu kwa sababu ya matendo yake ya awali, Elihu alimpongeza kwa uadilifu wake. (Ayubu 33:32) La muhimu hata zaidi ni kwamba Elihu alikuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu mambo, naye alimsaidia Ayubu kujua kwamba kamwe Yehova hawezi kutenda isivyo haki. (Ayubu 34:10-12) Alimtia moyo Ayubu amngojee Yehova badala ya kujaribu kujionyesha kuwa mwadilifu. (Ayubu 35:2; 37:14, 23) Bila shaka, wazee Wakristo na wengine wanaweza kufaidika kutokana na mambo hayo.

16. Wafariji watatu wa Ayubu walitumiwaje na Shetani?

16 Shauri la hekima la Elihu lilikuwa tofauti kabisa na maneno yenye kuumiza ya Elifazi, Bildadi, na Sofari. Yehova aliwaambia hivi: “Ninyi hamkusema mambo ya kweli kunihusu.” (Ayubu 42:7) Hata kama walidai kuwa na makusudi mazuri, walitumiwa na Shetani badala ya kuwa marafiki waaminifu. Tangu mwanzo, wote watatu walidai kwamba Ayubu ndiye aliyepaswa kulaumiwa kwa matatizo yaliyompata. (Ayubu 4:7, 8; 8:6; 20:22, 29) Kulingana na Elifazi, Mungu hana imani na watumishi wake, wala hajali ikiwa sisi ni waadilifu au la. (Ayubu 15:15; 22:2, 3) Elifazi hata alimshtaki Ayubu kwa makosa ambayo hakutenda. (Ayubu 22:5, 9) Kwa upande mwingine, Elihu alimsaidia Ayubu kwa njia ya kiroho, na hilo ndilo lengo la kila mshauri mwenye upendo.

17. Tunapaswa kukumbuka nini tunapojaribiwa?

17 Tunaweza kujifunza jambo lingine kuhusu uvumilivu katika kitabu cha Ayubu. Mungu wetu mwenye upendo huona hali yetu na anataka na anaweza kutusaidia kwa njia mbalimbali. Mwanzoni tulisoma kuhusu kisa cha Elsa Abt. Ona mkataa aliofikia: “Kabla ya kukamatwa, nilisoma barua ya dada mmoja aliyeandika kwamba wakati wa majaribu makali, roho ya Yehova hututuliza sana. Nilifikiri kwamba alitia chumvi kidogo. Lakini nilipokabili majaribu, nilitambua kwamba yale aliyosema ni kweli. Kwa hakika, hivyo ndivyo mambo yanavyokuwa. Si rahisi kuwazia hivyo ikiwa hujapata majaribu. Lakini ilikuwa hivyo kwangu. Yehova husaidia.” Elsa hakuwa anazungumzia mambo ambayo Yehova anaweza kufanya au aliwahi kufanya zamani katika siku za Ayubu. Alikuwa anazungumzia wakati wetu. Naam, “Yehova husaidia!”

Mwenye Furaha Ni Mtu Anayevumilia

18. Ayubu alipata faida gani kwa kuvumilia?

18 Wengi wetu hatutakabili matatizo makali kama yale ambayo Ayubu alikabili. Hata tupate majaribu gani katika mfumo huu, tuna sababu nzuri za kudumisha utimilifu wetu kama Ayubu. Kwa kweli, uvumilivu uliboresha maisha ya Ayubu. Ulimfanya awe kamili. (Yakobo 1:2-4) Uliimarisha uhusiano wake na Mungu. Ayubu alisema hivi: “Nimesikia habari zako kwa fununu, lakini sasa jicho langu mwenyewe linakuona wewe.” (Ayubu 42:5) Ayubu alishikilia utimilifu wake na hivyo kumthibitisha Shetani kuwa mwongo. Miaka mingi baadaye, Yehova bado alimtaja Ayubu, mtumishi wake, kuwa kielelezo cha uadilifu. (Ezekieli 14:14) Utimilifu na uvumilivu wake huwachochea watu wa Mungu hata leo.

19. Kwa nini unahisi kwamba uvumilivu ni muhimu?

19 Yakobo alipowaandikia Wakristo wa karne ya kwanza kuhusu uvumilivu, alitaja uradhi unaotokana na kuvumilia. Naye alitumia mfano wa Ayubu kuwakumbusha kwamba Yehova huwapa thawabu watumishi wake waaminifu. (Yakobo 5:11) Tunasoma hivi kwenye Ayubu 42:12: “Naye Yehova akaubariki mwisho wa Ayubu baadaye kuliko mwanzo wake.” Mungu alimpa Ayubu mara mbili ya vitu alivyopoteza, naye akaishi miaka mingi na yenye furaha. (Ayubu 42:16, 17) Vivyo hivyo, maumivu, mateso, au huzuni yoyote ambayo huenda tukavumilia wakati wa mwisho wa mfumo huu wa mambo, itaondolewa na kusahauliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Isaya 65:17; Ufunuo 21:4) Tumesikia kuhusu uvumilivu wa Ayubu, na kwa msaada wa Yehova, tumeazimia kumwiga Ayubu. Biblia inaahidi hivi: “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima, ambalo Yehova aliwaahidi wale wanaoendelea kumpenda.”—Yakobo 1:12.

Ungejibuje?

• Tunaweza kufanyaje moyo wa Yehova ushangilie?

• Kwa nini hatupaswi kukata kauli kwamba tunateseka kwa sababu Mungu hapendezwi nasi?

• Ni mambo gani yaliyomsaidia Ayubu kuvumilia?

• Tunaweza kumwigaje Elihu tunapowaimarisha waamini wenzetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mshauri mzuri huonyesha hisia-mwenzi, heshima, na fadhili

[Picha katika ukurasa wa 29]

Elsa na Harald Abt