Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ongezeko Lenye Kutia Moyo Kwenye Kisiwa Maridadi

Ongezeko Lenye Kutia Moyo Kwenye Kisiwa Maridadi

Ongezeko Lenye Kutia Moyo Kwenye Kisiwa Maridadi

WAGENI huko Taiwan hufurahia kuona mimea mingi kwenye kisiwa hicho. Mimea midogo ya mpunga yenye rangi ya kijani kibichi hukomaa na kuwa na rangi ya manjano wakati wa mavuno. Kuna misitu yenye miti mingi milimani. Tofauti na ilivyo katika majiji yenye watu wengi, mimea mingi ya kijani kwenye mashamba na milima huburudisha sana. Hayo ndiyo mambo yaliyomchochea Mzungu wa kwanza aliyeona kisiwa hicho kukiita Ilha Formosa, au “Kisiwa Maridadi.”

Naam, Taiwan ni kisiwa kidogo maridadi, chenye urefu wa kilometa 390 na upana wa kilometa 160. Sehemu kubwa ya kisiwa hicho ina milima mirefu. Mlima Yü Shan (Mlima Morrison) ni mrefu kuliko Mlima Fuji wa Japani au Mlima Cook wa New Zealand. Kando ya milima hiyo na bahari, kuna nyanda nyembamba za pwani zenye watu wengi wa Taiwan. Sasa nchi hiyo ina watu zaidi ya milioni 22.

Ukuzi Tofauti

Hata hivyo, kuna ukuzi wa namna nyingine ambao unazidi kuonekana wazi huko Taiwan, yaani, ukuzi wa kiroho. Ukuzi huo unaonekana katika bidii ambayo watu hao, vijana kwa wazee, huonyesha wanapomjua Mungu wa kweli, Yehova. Kwa kweli, inatia moyo kuona ongezeko la idadi ya wale wanaofanya kazi kwa bidii ili kuwasaidia wengine kujifunza kumhusu Yehova na kusudi lake.

Majengo zaidi huhitajiwa kunapokuwa na ongezeko. Mnamo Desemba 1990, uwanja ulinunuliwa ili kupanua ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Ofisi ya tawi ya kwanza huko Taipei ilikuwa ndogo sana, hivyo haingeweza kushughulikia utendaji wa wahubiri wa Ufalme 1,777 waliokuwa huko Taiwan wakati huo. Baada ya miaka mingi ya kazi ngumu iliyofanywa na wafanyakazi wa kujitolea wa kimataifa na wenyeji wa umri mbalimbali, majengo mapya ya Hsinwu yalikuwa tayari kutumiwa mnamo Agosti 1994. Wakati huo kulikuwa na wahubiri 2,515 walioeneza habari njema za Neno la Mungu, Biblia. Sasa, zaidi ya miaka kumi baadaye, idadi hiyo imeongezeka mara mbili kufikia wahubiri zaidi ya 5,500, na kila mwezi karibu robo moja ya idadi hiyo hushiriki katika utumishi wa wakati wote. Kinachopendeza zaidi ni vijana ambao ni kama “matone ya umande” ya asubuhi yenye kuburudisha.—Zaburi 110:3.

Vijana Wanafanya Maendeleo ya Kiroho

Wahubiri wengi wenye bidii wa habari njema ni vijana. Baadhi yao ni wanafunzi wa shule za msingi. Kwa mfano, katika mji mmoja kaskazini mwa Taiwan, mwanamume mmoja na mke wake walialikwa kuhudhuria kwa mara ya kwanza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambapo Mashahidi wa Yehova hujifunza jinsi ya kufundisha kweli za Biblia. Mwanamume huyo na mke wake walishangaa kuona mvulana mdogo, Weijun, akisoma Biblia jukwaani kwa ustadi mwingi kuliko hata watu wazima wengi. Halafu kwenye mikutano mingine ambayo walihudhuria, walishangaa sana kuona hata watoto ambao hawajaenda shule wakitoa maelezo mazuri. Wenzi hao wa ndoa walieleza jinsi watoto hao wanavyojiendesha vizuri kwenye Jumba la Ufalme.

Kwa nini vijana hao wanazingatia sana elimu ya Biblia katika nchi hiyo ambako watu wengi ni wafuasi wa Buddha na Tao? Ni kwa sababu wazazi wao Wakristo wametumia kanuni za Biblia na wamejenga familia zenye furaha ambazo hutanguliza uhusiano wao pamoja na Yehova. Kwa kuwa wazazi wa Weijun wanajitahidi kufanya watoto wao wafurahie mahubiri na funzo la familia la Biblia, ndugu na dada mkubwa wa mvulana huyo mdogo tayari ni Mashahidi waliobatizwa. Hivi karibuni wakati Weijun alipoomba akubaliwe kuwa mhubiri, mama yake alieleza kwamba tayari mvulana huyo alikuwa amewaachia watu magazeti mengi mwezi huo kuliko jumla ya yale ambayo wengine katika familia yao waliwaachia watu. Bila shaka, anapenda kuzungumza na watu kuhusu kweli, kutoa maelezo mikutanoni, na kuwaambia wengine mambo ambayo amejifunza.

Vijana Wanapoendelea Kukua

Vijana hao hufanya nini wanapokuwa watu wazima? Wengi wao huendelea kumpenda Yehova kikweli na pia kupenda huduma. Kwa mfano, Huiping ni mwanafunzi. Siku moja mwalimu wake alisema kwamba washiriki wa dini fulani hawakubali damu lakini hajui hao ni akina nani. Baada ya wanafunzi kuondoka darasani, kijana huyo Mkristo alimweleza mwalimu wake kwamba watu hao ni Mashahidi wa Yehova, naye akamweleza pia sababu zao za kukataa damu.

Mwalimu mwingine alionyesha video kuhusu magonjwa ya zinaa. Video hiyo ilitaja andiko la 1 Wakorintho 6:9, lakini mwalimu huyo alidai kwamba Biblia haishutumu ngono za watu wa jinsia moja. Huiping alimweleza mwalimu huyo maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo.

Wakati mwanafunzi mwenzake Shuxia alipokuwa akitayarisha ripoti kuhusu jeuri katika familia, Huiping alimpa gazeti la Amkeni! la Novemba 8, 2001, lenye kichwa “Msaada kwa Wanawake Wanaopigwa” naye akamweleza Shuxia kwamba gazeti hilo lina habari nyingi za Biblia kuhusu jambo hilo. Hatimaye, Shuxia akawa mhubiri ambaye hajabatizwa. Sasa Shuxia na Huiping wanawahubiria wengine habari njema.

Wakristo wengi shuleni huona si rahisi kujitambulisha kuwa watu wanaoishi kulingana na kanuni za Biblia. Hali ni hivyo hasa katika miji midogo ya mashambani. Kwa sababu ya imani yake na kazi yake ya kuhubiri, Zhihao alivumilia mikazo ya marika. Anasema hivi: “Niliogopa sana kukutana na wanafunzi wenzangu nilipokuwa nikihubiri. Nyakati nyingine, ningekutana hata na wanafunzi kumi, nao wangenidhihaki!” Siku moja, mwalimu alimchagua Zhihao azungumze mbele ya wanafunzi wenzake kuhusu dini yake. “Niliamua kuanza habari yangu na sura ya 1 ya kitabu cha Mwanzo na baadaye kuzungumzia maswali kama: Ni nani aliyeiumba dunia na vitu vyote vilivyomo? Mwanadamu alitoka wapi? Niliposoma Biblia, wengine walianza kunicheka, wakisema kwamba nilikuwa mshirikina. Hata hivyo, niliendelea na kumaliza habari yangu. Baadaye, nilipata nafasi ya kuzungumza uso kwa uso na baadhi ya wanafunzi wenzangu kuhusu kazi na imani yetu. Sasa, wanaponiona nikihubiri, hawanicheki tena!”

Zhihao anaendelea: “Kwa kuwa wazazi wangu ni Mashahidi, tunazungumzia andiko la siku kila asubuhi. Pia, tunajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Hivyo, ninaweza kumkabili yeyote anayenidhihaki ninapofundisha wengine kweli za Biblia zenye kuburudisha.”

Tingmei ni mwanafunzi katika shule ya ufundi ya wasichana. Wakati mmoja alialikwa kwenda matembezi pamoja na baadhi ya wanafunzi wenzake na wavulana kutoka shule nyingine. Alitambua hatari ya kiadili ya kushirikiana na wanafunzi hao, naye akaamua kutoenda pamoja nao. Walimwalika mara kadhaa, hata ingawa alizungumza na wanafunzi wenzake habari nzuri kutoka katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. * Wasichana hao walimdhihaki, wakisema kwamba ni mshamba. Hata hivyo, muda si muda hekima ya kufuata kanuni za Biblia ilionekana wazi wakati mmoja wa wasichana hao alipopata mimba na kuitoa. Tingmei anasema hivi: “Kufanya yale ambayo Yehova anaamuru kumenifanya niwe na dhamiri safi. Kwa sababu hiyo, nina shangwe moyoni na ninahisi nimeridhika sana.”

Kukabiliana na Mambo Yanayozuia Ongezeko

Ruiwen ni mmoja wa marafiki wa karibu sana wa Tingmei. Alipokuwa kijana, Ruiwen alihisi kwamba kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kwenda kuhubiri kulichosha sana. Lakini, baada ya kuona tofauti kati ya upendo wa kweli wa washiriki wa kutaniko na urafiki wa kijuujuu tu wa wanafunzi wenzake, Ruiwen alikuwa na hakika kwamba alihitaji kufanya mabadiliko fulani maishani mwake. Alianza kuwahubiria wanafunzi wenzake na haraka akatambua wazi zaidi yale ambayo alihitaji kufanya. Alianza upainia msaidizi, akihubiri zaidi ya saa 50 kila mwezi. Kisha akaanza upainia wa kawaida, akihubiri zaidi ya saa 70 kila mwezi. Ruiwen anasema hivi: “Ninamshukuru Yehova sana. Hakuchoka nami. Ingawa nilifanya mambo yaliyomhuzunisha, bado ananipenda. Pia, mama yangu na wengine kutanikoni walinionyesha upendo. Kwa kuwa sasa ninaongoza mafunzo matano ya Biblia, ninahisi kwamba ninafanya kazi yenye kuridhisha zaidi.”

Katika shule moja ya sekondari ya mashambani, watoto wawili Mashahidi walichaguliwa wawakilishe shule hiyo katika mashindano ya dansi za kienyeji. Walipojua mambo yaliyohusishwa katika mashindano hayo, vijana hao Mashahidi walihisi kwamba kuyashiriki kungechafua dhamiri yao ya Kikristo. Walipojaribu kueleza maoni yao kuhusu mashindano hayo na kuomba wasihusishwe, ombi lao lilikataliwa. Walimu waliwaambia kwamba kwa kuwa majina yao yalitajwa, lazima waende kushiriki. Kwa kuwa hawakukubali jambo hilo, vijana hao Mashahidi walituma barua kwenye kituo cha Intaneti cha wizara ya elimu na kueleza tatizo lao. Ingawa vijana hao hawakujibiwa moja kwa moja, shule hiyo ilipokea mwongozo wa kutomlazimisha mtu yeyote kushiriki katika mashindano kama hayo. Vijana hao walifurahi sana kuona kwamba mazoezi ya Biblia waliyopewa yalifinyanga si tu dhamiri yao bali pia yaliwaimarisha kutetea yaliyo sawa!

Hata wale walio na udhaifu wa kimwili hufurahia sana kuwaeleza wengine tumaini la Biblia. Minyu alizaliwa akiwa amepooza. Kwa kuwa hawezi kutumia mikono yake, yeye hufungua kurasa za Biblia kwa ulimi wake ili kupata andiko analotaka kusoma. Wakati anapotoa hotuba kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika Jumba la Ufalme, yeye hulala juu ya kitanda na msaidizi wake hukalia kiti kifupi huku akimshikia maikrofoni. Inatia moyo kama nini kuona jinsi Minyu anavyojitahidi kutayarisha sehemu zake!

Minyu alipotaka kuwa mhubiri wa Ufalme, dada kadhaa kutanikoni walijifunza jinsi ya kuhubiri kupitia simu ili waweze kumsaidia. Minyu hubonyeza namba za simu kwa ulimi wake huku dada wengine wakimsaidia kuandika rekodi ya simu hizo. Anafurahia sana kazi hiyo hivi kwamba amekuwa painia msaidizi. Anazungumza na watu kuhusu Ufalme wa Mungu saa 50 hadi 60 kila mwezi kwa kutumia simu. Amepata watu ambao wanakubali vichapo vya Biblia, nao wanamruhusu kufanya ziara za kurudia. Kwa sasa anaongoza mafunzo matatu ya Biblia pamoja na watu ambao alipata kupitia simu.

Naam, kama matone ya umande yenye kuburudisha, wavulana na wasichana hao katika makutaniko 78 ya Mashahidi wa Yehova huko Taiwan ni wenye furaha na wana bidii ya kuwapelekea mamilioni ya watu habari njema ya Ufalme yenye kuokoa uhai katika kisiwa hicho chenye watu wengi. Hiyo ni sehemu ndogo tu ya yale yanayotimizwa ulimwenguni pote kuhusiana na unabii huu wa Biblia: “Watu wako watajitoa kwa hiari katika siku ya jeshi lako. Katika fahari za utakatifu, kutoka tumbo la uzazi la mapambazuko, una kundi lako la vijana kama matone ya umande.” (Zaburi 110:3) Vijana hao wanawatia moyo wahubiri waliozeeka ambao ni wafanyakazi wenzao, na zaidi ya yote, wanamfurahisha sana Baba yao wa mbinguni, Yehova Mungu.—Methali 27:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

MAJUMBA MENGINE YA UFALME YANAHITAJIWA

Kwa sababu ya kuongezeka kwa idadi ya wahubiri huko Taiwan, ni vigumu sana kuwa na Majumba ya Ufalme ya kutosha. Kwa nini? Kwa sababu tofauti na maeneo fulani ya mashambani, ni vigumu sana kupata viwanja vinavyofaa ili kujenga Majumba ya Ufalme. Isitoshe, ardhi inauzwa kwa bei ghali, na kuna sheria kali za ardhi. Katika majiji na miji mikubwa, uwezekano uliopo ni kukodi tu majengo ya ofisi na kuyageuza kuwa Majumba ya Ufalme. Hata hivyo, ofisi nyingi zina paa fupi, kodi ya juu, ulinzi mkali, na mambo hayo na mengineyo yanafanya zisitumiwe kuwa Majumba ya Ufalme.

Hata hivyo, katika miaka ya karibuni, Mashahidi wa Yehova huko Taiwan wamepata Majumba mapya ya Ufalme. Mashahidi wanaendelea kutafuta viwanja vipya kwa kuwa wako tayari kulipia gharama za ujenzi kupitia michango yao ya hiari na kusitawisha ustadi wao wa ujenzi.