Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dini Ina Faida Gani?

Dini Ina Faida Gani?

Dini Ina Faida Gani?

“NINAWEZA kuwa mtu mwema bila kufuata dini!” Hayo ndiyo maoni ya watu wengi. Watu wengi wanyoofu, wenye huruma, na wanaotegemeka hawavutiwi na dini. Kwa mfano, ni watu wachache wa Ulaya Magharibi wanaoenda kanisani kwa ukawaida ingawa wengi wao husema wanamwamini Mungu. * Hata huko Amerika ya Latini, ni asilimia 15 hadi 20 tu ya Wakatoliki wanaoenda kanisani kwa ukawaida.

Kama wengine wengi, labda wewe pia unahisi kwamba dini haimsaidii mtu kuishi maisha mazuri. Huenda pia unajua kwamba miaka kadhaa iliyopita, katika siku za babu na nyanya yako, watu wengi walifuata dini sana kuliko leo. Kwa nini watu hawapendezwi tena na dini? Je, mtu anaweza kuwa mwema bila kufuata dini? Je, kuna dini inayoweza kukufaidi?

Kwa Nini Watu Wengi Wameacha Dini?

Kwa karne nyingi, watu wengi wanaodai kuwa Wakristo waliamini kwamba Mungu anataka tumtii. Walienda kanisani kupata kibali cha Mungu kupitia desturi za ibada zilizoongozwa na kasisi au kupitia mwongozo wa mhubiri. Bila shaka, wengi walijua unafiki ulio katika dini. Watu wengi walijua kwamba dini ilishiriki katika vita na walijua pia mwenendo mpotovu wa baadhi ya makasisi wao. Hata hivyo, wengi walihisi kwamba dini ni nzuri. Wengine walifurahia hali ya kifumbo iliyokuwapo, desturi, na muziki, huku wengine wakiogopa tisho la kuteswa milele katika moto, ambalo si fundisho la Kimaandiko. Baadaye, maendeleo mbalimbali yalibadili maoni ya watu kuhusu dini.

Fundisho la mageuzi lilikubaliwa. Watu fulani walianza kuamini kwamba uhai ulijitokeza tu bila Mungu. Dini nyingi zilishindwa kutoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba Mungu ndiye Chanzo cha uzima. (Zaburi 36:9) Isitoshe, kwa sababu ya maendeleo katika tekinolojia, tiba, usafiri, na mawasiliano, watu walihisi kwamba tatizo lolote linaweza kutatuliwa na sayansi. Isitoshe, watu walihisi kwamba wanasayansi wa jamii na wataalamu wa akili walitoa mwongozo bora kuliko dini. Kwa upande mwingine, dini zilishindwa kuthibitisha waziwazi kwamba kuishi kulingana na sheria za Mungu ndiyo njia bora ya maisha.—Yakobo 1:25.

Hivyo, dini nyingi zikabadili ujumbe wao. Makasisi na wahubiri wakaacha kufundisha kwamba Mungu anataka watu wamtii. Badala yake, wengi walifundisha kwamba kila mtu anapaswa kujiamulia lililo sawa na lililo kosa. Ili kujitafutia umashuhuri, baadhi ya viongozi wa dini walidai kwamba Mungu anamkubali mtu kuwa mwabudu wake haidhuru mwenendo wa mtu huyo. Mafundisho hayo yanatukumbusha unabii huu wa Biblia: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe.”—2 Timotheo 4:3.

Badala ya kuwavutia watu, mafundisho hayo yaliwachukiza. Walijiuliza hivi: ‘Ikiwa makanisa yanatilia shaka nguvu za Mungu za kuumba na hekima yake ya kutunga sheria, kuna faida gani kwenda kanisani? Kwa nini nijisumbue kuwafundisha watoto wangu mambo ya dini?’ Watu waliokuwa wakijitahidi kuishi maisha mazuri, walianza kudharau dini. Waliacha kwenda kanisani na dini haikuwa muhimu tena kwao. Kwa nini kitu kilichopaswa kuwa chenye faida kikaonwa kuwa hakifai tena? Biblia inatoa jibu lenye kusadikisha.

Dini Hutumiwa Kutimiza Makusudi Maovu

Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wa mapema kwamba watu fulani wangetumia Ukristo kwa makusudi maovu. Alisema hivi: “Mbwa-mwitu wenye kukandamiza wataingia katikati yenu nao hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:29, 30) Mwanatheolojia Mkatoliki, Augustine, ni mmoja wa wale waliosema “mambo yaliyopotoka.” Yesu aliwafundisha wafuasi wake kuwasadikisha watu kwa kujadiliana nao kupitia Maandiko. Lakini, Augustine alipotosha maana ya maneno haya ya Yesu kwenye Luka 14:23 yanayosema, ‘Washurutishe waingie,’ ili kuonyesha kwamba ni sawa kuwalazimisha watu wageuke. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 28:23, 24) Augustine alitumia dini kuwatawala watu.

Shetani, yule malaika mwasi, ndiye anayeendeleza uchafu na ufisadi katika dini. Aliwachochea watu wa dini wa karne ya kwanza ili wajaribu kuchafua makutaniko ya Kikristo. Biblia inasema hivi kuhusu watu hao: “Watu wa namna hiyo ni mitume wa uwongo, wafanyakazi wadanganyifu, wakijigeuza wenyewe kuwa mitume wa Kristo. Na si ajabu, kwa maana Shetani mwenyewe huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru. Kwa hiyo si jambo kubwa kama wahudumu wake wakiendelea pia kujigeuza wenyewe kuwa wahudumu wa uadilifu.”—2 Wakorintho 11:13-15.

Bado Shetani anatumia dini zinazojifanya kuwa za Kikristo, zinazojifanya kuwa na maadili, na zinazodai kuwa zenye kuelimisha, ili kuwafanya watu waishi kulingana na viwango vyake badala ya viwango vya Mungu. (Luka 4:5-7) Huenda umegundua kwamba makasisi wengi leo hutumia dini kujitukuza kwa kutumia majina makubwa ya cheo ili wapate pesa kutoka kwa wafuasi wao. Pia, serikali zimetumia dini kuwahimiza raia wajitolee kufa vitani.

Ibilisi hutumia dini sana kuliko vile watu wengi wanavyowazia. Huenda ukafikiri kwamba ni watu wachache tu wenye msimamo mkali wa kidini ndio wanaotumiwa na Shetani. Lakini kulingana na Biblia, ‘yule anayeitwa Ibilisi na Shetani anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ Pia, Biblia inasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Ufunuo 12:9; 1 Yohana 5:19) Mungu anahisije kuhusu dini inayotumiwa na viongozi ambao hutaka tu kuwavuta watu ili wawafuate?

“Ina Faida Gani Kwangu?”

Ikiwa unashangazwa na mwenendo fulani wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, jua kwamba zinamchukiza hata zaidi Mungu Mweza-Yote. Dini hizo zinadai kuwa zimefanya agano pamoja na Mungu; taifa la kale la Israeli lilidai hivyo pia. Taifa hilo na dini hizo zimekosa uaminifu. Yehova atazihukumu dini zinazodai kuwa za Kikristo leo kama alivyolihukumu taifa la Israeli. Yehova alisema: “Hawakuyasikiliza maneno yangu; na sheria yangu—pia waliendelea kuikataa. Ina faida gani kwangu kwamba mnaleta ubani kutoka Sheba? . . . Dhabihu zenu hazikunipendeza mimi.” (Yeremia 6:19, 20) Mungu hakuitambua ibada ya wanafiki. Hakupendezwa na desturi wala sala zao. Aliwaambia hivi Waisraeli: “Nafsi yangu imechukia . . . majira yenu ya sherehe. Zimekuwa mzigo kwangu; nimechoka kuzibeba. Nanyi mnaponyoosha mikono yenu, mimi huficha macho yangu kutoka kwenu. Hata mjapotoa sala nyingi, mimi sisikilizi.”—Isaya 1:14, 15.

Je, Yehova hufurahia sherehe ambazo makanisa huziona kuwa za Kikristo lakini ambazo hapo awali zilitukuza miungu ya uwongo? Je, yeye husikiliza sala za makasisi wanaopotosha mafundisho ya Kristo? Je, Mungu hukubali dini yoyote inayokataa sheria zake? Unaweza kuwa na hakika kwamba anaona desturi za kidini kama alivyoona dhabihu za Israeli la kale ambazo alisema hivi kuzihusu: ‘Zina faida gani kwangu?’

Hata hivyo, Yehova anajali sana ibada ya watu wanyoofu inayotolewa kwa njia ya kweli. Mungu hupendezwa watu wanapoonyesha shukrani kwa ajili ya vitu vyote wanavyopokea kutoka kwake. (Malaki 3:16, 17) Kwa hiyo, je, unaweza kuwa mtu mwema usipomwabudu Mungu? Mtu asiyefanya jambo lolote jema kwa ajili ya wazazi wake wenye upendo hawezi kusema kwamba yeye ni mwema, sivyo? Je, mtu asiyefanya jambo lolote kwa ajili ya Mungu anaweza kuwa mwema? Bila shaka, tunapaswa kupendezwa sana na Mungu wa kweli ambaye ndiye chanzo cha uzima. Katika makala inayofuata tutaona kwamba mbali na kumletea Mungu heshima, ibada ya kweli inatufaa pia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 ‘Katika nchi nyingi watu walianza kuacha kupendezwa na dini katika miaka ya 1960.’—The Decline of Christendom in Western Europe, 1750-2000.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Je, dini zimethibitisha kwamba Mungu aliumba vitu vyote?

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Je, mtu anayemwakilisha Mungu anaweza kufanya mambo haya?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mungu huionaje sherehe hii?

[Hisani]

AP Photo/Georgy Abdaladze