Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ibada Inayokufaa

Ibada Inayokufaa

Ibada Inayokufaa

MTUNGA-ZABURI Asafu alisema hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” Kwa muda fulani, alitaka kuwaiga watu wanaofuatia maisha ya raha bila kumjali Mungu. Lakini baadaye Asafu alifikiria faida za kumkaribia Mungu na akakata kauli kwamba kulikuwa kwema kwake. (Zaburi 73:2, 3, 12, 28) Je, ibada ya kweli ni njema kwako leo? Inaweza kukufaidije?

Kumwabudu Mungu wa kweli kunakusaidia kupata kitu chenye thamani sana kuliko maisha ya ubinafsi. Wale wanaofuatia mapendezi yao tu hawawezi kupata furaha kwa sababu ya jinsi ambavyo tumeumbwa na “Mungu wa upendo.” (2 Wakorintho 13:11) Yesu alifundisha ukweli wa msingi kuhusu wanadamu aliposema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Ndiyo sababu sisi hufurahia kuwafanyia mambo marafiki na watu wa familia. Lakini furaha kubwa zaidi hutokana na kufanya mambo kwa ajili ya Mungu. Anastahili upendo wetu kuliko mtu mwingine yeyote. Mamilioni ya watu kutoka matabaka mbalimbali wamegundua kwamba inaridhisha kumwabudu Mungu na kufanya mapenzi yake.—1 Yohana 5:3.

Kuwa na Kusudi Maishani

Ibada ya kweli ni njema kwako pia kwa sababu inakupa kusudi maishani. Je, umegundua jinsi mara nyingi furaha inavyohusiana na kujua kwamba unafanya jambo linalofaa? Watu wengi wana lengo maishani, liwe linahusu familia zao, marafiki, biashara, au starehe. Kwa sababu ya hali zisizotazamiwa maishani, mara nyingi mambo hayo hayawaletei furaha. (Mhubiri 9:11) Hata hivyo, ibada ya kweli hukusaidia kupata kusudi bora linaloendelea kukuridhisha hata wakati mambo mengine maishani yanapokukatisha tamaa.

Ibada ya kweli inahusisha kumjua Yehova na kumtumikia kwa uaminifu. Waabudu wa kweli humkaribia Mungu sana. (Mhubiri 12:13; Yohana 4:23; Yakobo 4:8) Huenda ukaona kuwa si rahisi kumjua Mungu vizuri sana hivi kwamba awe rafiki yako. Lakini kwa kutafakari masimulizi yanayoonyesha jinsi ambavyo ameshughulika na watu na kwa kufikiria vitu ambavyo ameumba, unaweza kuelewa utu wake. (Waroma 1:20) Isitoshe, kwa kusoma Neno la Mungu, unaweza kuelewa kusudi letu la kuwa hai, kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka, jinsi atakavyokomesha kuteseka, na labda la kupendeza hata zaidi, jinsi unavyoweza kutimiza sehemu muhimu katika kusudi lake. (Isaya 43:10; 1 Wakorintho 3:9) Kuelewa mambo hayo kunaweza kukupa kusudi maishani!

Kuboresha Utu Wako

Ibada ya kweli ni njema kwako kwa sababu inakusaidia kuboresha utu wako. Unapoabudu katika kweli, unakuza utu unaokuwezesha kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine. Unajifunza kutoka kwa Mungu na kwa Mwana wake kuwa mnyoofu, kuzungumza kwa fadhili, na kuwa mwenye kutegemeka. (Waefeso 4:20–5:5) Unapomjua Mungu vizuri sana kiasi cha kumpenda, unachochewa kumwiga. Biblia inasema hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.”—Waefeso 5:1, 2.

Je, haipendezi kushirikiana na watu wanaomwiga Mungu katika kuonyesha upendo? Inafurahisha kwamba ibada ya Mungu wa kweli si ya mtu mmoja tu. Inakuunganisha na wengine wanaopenda mema na uadilifu. Bila shaka, huenda usipendezwe na dini rasmi. Lakini, kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, tatizo la dini nyingi si kwamba hazifuati utaratibu fulani bali tatizo ni kwamba hazifuati mpangilio unaofaa na hazina makusudi yanayofaa. Dini nyingi rasmi zina makusudi yasiyopatana na Ukristo. Yehova mwenyewe amewapanga watu wake kwa utaratibu kwa ajili ya kusudi zuri. Biblia inasema hivi: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Kama wengine wengi, huenda ukagundua kwamba kushirikiana na kikundi cha Kikristo kilichopangwa kwa utaratibu kutaboresha mtazamo wako.

Tumaini la Wakati Ujao

Maandiko Matakatifu yanaonyesha kwamba Mungu anawapanga waabudu wa kweli kwa utaratibu ili waokoke mwisho wa mfumo uliopo wa mambo na kurithi dunia mpya ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13; Ufunuo 7:9-17) Hivyo, ibada inayokufaa hutoa tumaini ambalo ni muhimu ili kuwa na furaha. Matumaini ya wakati ujao ya watu wengine hutegemea serikali zilizo imara, hali ya kibiashara, afya njema, na maisha mazuri baada ya kustaafu. Lakini ni machache tu kati ya mambo hayo ambayo yanatoa msingi thabiti wa kutarajia wakati ujao wenye furaha. Kwa upande mwingine, mtume Paulo aliandika hivi: “Tumeweka tumaini letu juu ya Mungu aliye hai.”—1 Timotheo 4:10.

Ukitafuta kwa bidii, unaweza kuwapata waabudu wa kweli. Katika ulimwengu wa leo uliogawanyika, upendo na umoja huwatambulisha waziwazi Mashahidi wa Yehova. Ni watu wa mataifa mengi na malezi mbalimbali; lakini upendo walio nao miongoni mwao na kwa Yehova unawafanya wawe na umoja. (Yohana 13:35) Wanakualika ujionee mambo wanayofurahia. Asafu aliandika hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.”—Zaburi 73:28.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Unaweza kuwa rafiki ya Mungu